IJUMAA
KUU
Somo
I: Isa 52:13-53:12
Zab:
30:2, 6, 12-17,25
Somo
II: Ebr 4:14-16, 5:7-9
Injili:
Yoh 18:1-19, 42
Nukuu:
“Alidharauliwa
na kukataliwa na watu, mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; na kama mtu
ambaye watu humficha nyuso zao, alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu.”
Isa 53:3
“Alionewa, lakini
alinyenyekea, wala hakufunua kinywa chake; kama mwanakondoo apelekwaye
machinjoni, na kama vile kondoo anyamazavyo mbele yao wakatao manyoya yake;
naam, hakufunua kinywa chake,” Isa 53:7
“Kwa kuwa hatuna kuhani
mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye
alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi,” Ebr 4:15
“Basi Yesu, hali akijua
yote yatakayompata, akatokea, akawaambia, “Ni nani mnayemtafuta?” Yoh 18:4
“Yesu akawaambia, “Ni
mimi.” Yoh 18:5
“Nimekwisha kuwaambieni
ya kwamba ni mimi; basi ikiwa mnanitafuta mimi, waacheni hawa waende zao.” Yoh 18:8
“Rudisha upanga alani
mwake; je! Kikombe alichonipa Baba, mimi nisikinywee?” Yoh 18:11
“Mimi nimesema na
ulimwengu waziwazi; sikuzote nalifundisha katika sinagogi na katika hekalu,
wakusanyikapo Wayahudi wote; wala kwa siri mimi sikusema neno lo lote. Ya nini kuniuliza mimi? Waulize wale
waliosikia ni nini niliyowaambia; wao wanajua niliyoyanena.” Yoh 18:20-21
“Kama nimesema vibaya, ushuhudie
ule ubaya; bali kama nimesema vema, wanipigia nini?” Yoh 18:23
“Wewe wasema hivi kwa
nafsi yako, au watu wengine walikuambia habari zangu?” Yoh 18:34
“Ufalme wangu sio wa
ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu
wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio
wa hapa.” Yoh 18:36
“Wewe wasema, kwa kuwa
mimi ni mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi
nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia
sauti yangu.” Yoh 18:37
“Wewe
hungekuwa na mamlaka yo yote juu yangu, kama usingepewa kutoka juu; kwa hiyo
yeye aliyenitia mikononi mwako yuna dhambi iliyo kubwa zaidi.” Yoh 19:11
“Mama,
tazama, mwanao.” Yoh 19:26
“Tazama,
mama yako.” Yoh 19:27
“Naona
kiu.” Yoh 19:28
“Imekwisha.”
Yoh 19:30
TAFAKARI: “Mateso na kifo cha
aibu cha Bwana yetu Yesu Kristo, ni ushindi wa wema dhidi ya uovu, kuinuliwa
kwa wanyonge na wanyofu wa moyo, uponyaji wa maumivu ya ndani, na ni njia pekee
ya kujipatia Utukufu.”
Wapendwa wana wa Mungu leo tunatafakari
fumbo zima la mateso, na kifo cha msalaba cha Bwana wetu Yesu Kristo. Hapa
ndipo kwenye hitimisho zima la safari yetu ya Ukombozi. Hapa ndipo kwenye
ushindi dhidi ya umauti na mwelekeo wa umilele. Hapa ndipo sote kwa utofauti
wetu twafanywa upya na kuwa wana pekee na wapendwa wa Mungu. Hapa ndipo mimi na
wewe kama wafuasi wa Kristo twajivunia Ukristo wetu kwa sababu kuna maisha tena
ya umilele baada ya kifo kilichopigwa mwereka na ushindi wa Yesu Kristu dhidi
ya dhambi.
Ndugu yangu mpendwa
unayesafiri nami katika tafakari hii, naona ni vyema tuzame katika neno hili, “Mateso na kifo
cha aibu cha Bwana yetu Yesu Kristo, ni ushindi wa wema dhidi ya uovu,
kuinuliwa kwa wanyonge na wanyofu wa moyo, uponyaji wa maumivu ya ndani, na ni
njia pekee ya kujipatia Utukufu.” Yesu Kristo anayeyakubali mateso haya na aibu
hii kubwa dhidi ya dhambi zangu na zako, anakubali kuyabeba yote kwa
unyenyekevu na ustahimilivu uliotukuka. Nabii Isaya anatoa wasifu wa huyu abebaye
kadhia hii, yaani kwa unabii huo, Yesu
ndiyo mtazamo na kwelekeo wake wa kuyapokea mateso na karaha hizi. “Alidharauliwa na kukataliwa na watu,
mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; na kama mtu ambaye watu humficha nyuso
zao, alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu.” Isa 53:3.
Pamoja na karaha na
kadhia hizi, na hasa kukataliwa na watu waliomfahamu, Yesu Kristo bado
anajinyenyekesha na kuwa tayari kutaabika kwa faida yako na yangu, na tendo hili
linakunifanya mimi na wewe tuwe huru mwili na roho. Kukombolewa huku na
kufanywa huru mwili na roho kumemgharimu sana Mwokozi wetu. Mtume Petro
anasema, “Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikiavyo, kwa
fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba
zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na
waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19. Hakika mateso ya Yesu ni huzuni kubwa
hasa tunapotenda dhambi tukilinganisha na majitoleo yake ya kutupatanisha na
Mungu Baba. “Alionewa, lakini alinyenyekea, wala hakufunua kinywa chake; kama
mwanakondoo apelekwaye machinjoni, na kama vile kondoo anyamazavyo mbele yao
wakatao manyoya yake; naam, hakufunua kinywa chake,” Isa 53:7
Wapendwa katika Kristo,
kwa mwono huu wa Yesu Kristo mbele ya watesi wake, ni vyema tuyatafakari maneno
yale aliyoyatamka Yesu Kristo tangu kukamatwa kwake alfajiri na mapema hadi
pale alipoitwa roho yake. Kila alilolitamka Kristo ni fundisho la kina kwetu.
Alfajiri na mapema siku ya Ijumaa, kundi kubwa la askari wa kirumu wakiongozwa
na Msaliti Yuda Iskariote, hawakumjua Yesu mpaka pale alipojitambulisha
mwenyewe. “Basi Yesu, hali akijua yote yatakayompata, akatokea, akawaambia, “Ni
nani mnayemtafuta?” Yoh 18:4. Kwa swali hili
laonyesha wazi Yesu anafanyiwa hujuma iliyo wazi. Kama angekuwa mwovu kwa
matendo yake, basi kusingalikuwa na ulazima wa kujitambulisha. Mara nyingi na
walio wengi wamejikuta magerezani kama ndoto vile na wakati mwingine wakijikuta
wanasomewa mashitaka wasiyo yajua na hata kuhukumiwa kifo. Jambo kama hili mara
nyingi linakuwa ni agizo kutoka kwa wakubwa na wenye pesa hasa kwenye utawala
dhalimu. Pamoja na dhulima hii, Yesu hakimbii wala kujificha. Badala yake
anajisalimisha mwenyewe pasipo hofu. Anawaambia, “Ni mimi.” Yoh 18:5.
Tendo hili la kujitambulisha Kristo kuwa ni yeye, mara unatokea muujiza wa
kwanza, ‘wote wanadondoka chini.’
Hata katika muujiza
huu, bado wanashindwa kugundua usafi na wema wa Yesu. Wakiwa katika hali ya
sintofahamu, Yesu anawasaidia kwa kujitambulisha tena, na hapa akiwakingia
kifua wanafunzi wake. “Nimekwisha kuwaambieni ya kwamba ni mimi; basi ikiwa
mnanitafuta mimi, waacheni hawa waende zao.” Yoh
18:8. Yesu akiwa Baba wa Familia mwenye kujali na kuwajibika, anajitoa muhanga mwenyewe
ili wamtende yeye tu, na familia yake iwe salama. Huyu ni mzazi anayejali
familia yake hata nyakati za kiza kinene. Leo wazazi wengi wamezitelekeza
familia zao kwa ulevi, ukahaba, kuwa na nyumba ndogo, na wakati mwingine
kupenda anasa na tafrija kulikopindukia.
Wapendwa,
ule msemo wetu kwamba damu nzito kuliko maji, anautumia Mtume Petro kwa
kujaribu kumnusuru Yesu Kristo, kwa kumkata sikio mmoja wa vibaraka
aliyetambulika kwa jina la Malko. Mara Yesu anazuia damu kumwagika, na kutoa
onyo kwa Petro. “Rudisha upanga alani mwake; je! Kikombe
alichonipa Baba, mimi nisikinywee?” Yoh 18:11. Kristo anatufundisha tusiwe
wepesi wa kulipa baya kwa baya. Hayo siyo malengo na mtazamo wa Mungu na hata
wa Ukristo wetu. Ingalikuwa hivyo, basi hata yeye Kristo angeweza hata
kuwashushia moto kutoka mbinguni wakaungua wote waliotumwa kumkamata. Je, ni
mara ngapi nimekuwa mtu wa visasi hata kuishi kwa visasi muda wote? Kuonyesha
kuwa Yeye, yaani, Yesu Kristo hayupo katika lolote lililo ovu, anafanya muuza
mwingine kwa kulirudisha sikio pale lilipoondolewa kwa upanga. Kristo bado
anatenda wema hata pale ambapo mazingira yangemshawishi kutokufanya hivyo. Kwa
upande wa watesi wake hata hili hawalioni. Hakika sikio la kufa alisikii dawa!
Ndugu yangu, kukamatwa
kwa Yesu Kristo hakukua kwa haki na uhalali wowote, na hata mashitaka yake
yalikuwa ya kuokoteza okoteza tu. Kitu cha ajabu ni kwamba waliomkamata
hawakujua sawa sawa kisa cha kufanya hivyo. Na badala yake wanataka Yesu
Mwenyewe ayaseme makosa yake. Huu ni uonevu uliokithiri. Hata katika hali hii
Yesu hajitetei kwa yale mema aliyoyafanya badala yake anashauri waulizwe wale
alioishi nao na kuwafundisha kweli. Yesu anawaambia, “Mimi nimesema na
ulimwengu waziwazi; sikuzote nalifundisha katika sinagogi na katika hekalu, wakusanyikapo
Wayahudi wote; wala kwa siri mimi sikusema neno lo lote. Ya nini kuniuliza mimi? Waulize wale
waliosikia ni nini niliyowaambia; wao wanajua niliyoyanena.” Yoh 18:20-21. Ni mara ngapi tunasikia watu
wamebambikiziwa kesi za mauaji? Wapo wengi hata leo hii wanateseka kama Kristo
magerezani bila kujua hatma yao. Ni mara ngapi nimetoa ushahidi wa uongo, na
hata kushuhudia uongo? Leo mtu kuporwa haki yake umekuwa utamaduni na wenye
kuhalalishwa katika jamii yetu. Mfano; si ajabu kuona na kusikia aliyeshinda
ndiye kashindwa, na aliye shindwa ndiye kashinda. Mbaya zaidi jamii yetu leo
imeanza kujijengea utamaduni huu mwovu.
Ndugu
yangu, hata kwa ukweli aliousema Yesu, bado anaonekana mkosefu, na hivyo
anachapwa vibao. Wapo watu wengi kati yetu wanaoteseka katika mateso ya
kimfumo. Mateso ya kimfumo ni pale wachache na wenye uwezo wanapokandamiza haki
za wanyonge na hasa wale wanoonekana kuwa mwiba katika maslahi yao. Leo
tunashuhudi baadhi ya watu wakiuwawa kwa vile tu wamesimama katika kweli. Wapo
wengine wanauwawa kwa vifo nyamavu kwa kulishwa sumu ya muda mrefu. Wapo wengi
wanaofukuzwa kazi na hata kufunguliwa kesi lukuki kwa vile tu hakubaliani na
uovu wa kimfumo. Haya yote Yesu anakabiliana nayo. Katika hali hii Yesu jibu
lake ni hili, “Kama nimesema vibaya, ushuhudie ule
ubaya; bali kama nimesema vema, wanipigia nini?” Yoh 18:23. Kwa kweli Kristo hakufanyiwa haki
hata kidogo. Wapo pia wengine wanateswa na kunyanyaswa kama Kristo kwa
kutosikilizwa na hata kujitetea. Leo polisi si mahali salama tena ambapo
unaweza kupakimbilia ili upate msaada.
Yesu
Kristo ni Mfalme wa amani, upendo, haki, upole, unyenyekevu, na hivi ndivyo
vinavyompa nguvu ya maadili kusema na kusimama katika kweli. Anapoulizwa kama
yeye ni mfalme, Yesu Kristo anashangazwa na swali hili kutokana na kutokufahamu
kwao. “Wewe wasema hivi kwa nafsi yako, au watu wengine
walikuambia habari zangu?” Yoh 18:34. Maisha ya Yesu ni somo tosha la kile
asemacho na akiishicho. Kwa kuulizwa kama yeye ni mfalme, Yesu anaandaliwa kesi
ya kubambikiziwa. Leo pia wapo watu wengi wanasota maabusi na wengi magerezani
kwa kubambikiziwa kesi za uongo. Katika hali hii, Yesu anawafundisha na
kutufundisha tena, ili waelewe na tuelewe sababu ya maisha yake hapa duniani.
“Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu
huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi.
Lakini ufalme wangu sio wa hapa.” Yoh
18:36. Yesu Kristo ni mfalme wa Amani. Na utimilifu wa ufalme huu ni maisha ya
umilele.
Ndugu
yangu, sababu kubwa ya Yesu kuwa kile alicho ni kumkomboa mwanadamu kutoka
utumwa wa dhambi, na kuokoa kile kilichoumbwa na Mungu na kwa njia ya Mwanaye,
yaani Yesu Kristo, Yoh 1:3. Yesu Kristo hasiti kusema yeye ni mfalme kwa maana
ya ufalme wa haki, amani, upendo, unyenyekevu na upole. “Wewe
wasema, kwa kuwa mimi ni mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa
ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa
hiyo kweli hunisikia sauti yangu.” Yoh
18:37. Ni katika kuishi kweli na kutafuta kweli tunakuwa huru ndani na katika
Kristo. Kwa mantiki hii hakuna mwenye mamlaka ya mwisho kuhusu uhai wa mtu,
isipokuwa Mungu mwenyewe, ambaye kwa namna ya pekee ameyafunua hayo kwa mwanaye
mpendwa Yesu Kristo. Katika jambo hili Yesu anatoa onyo kwa Pilato na tawala
zote zile kandamizi. “Wewe hungekuwa na
mamlaka yo yote juu yangu, kama usingepewa kutoka juu; kwa hiyo yeye aliyenitia
mikononi mwako yuna dhambi iliyo kubwa zaidi.” Yoh 19:11. Ndugu yangu uliyejaliwa kuwa na
mamlaka na dhamana pale ulipo, je, wayatumiaje madaraka hayo?
Kanisa leo yaani; Moja, Takatifu, Katoliki, na la Mitume,
ni taswira ya Yesu Kristo mwenyewe ambao ni
mwili wake, na sisi waamini ni viungo vya mwili huo. Katika mantiki hii,
mafundisho na matendo ya Kanisa lazima yawe na mwono na ufanyisi wa Kristo
mwenyewe. Jambo hili Yesu Kristo akiwa katika hatua zake za mwisho kabla ya
kutwaa roho yake, analikabidhi Kanisa kwa Mama yake Mzazi, katika maana ya
uangalizi na ulezi, na lenye mamlaka fundishi. “Mama, tazama, mwanao.” Yoh
19:26. Na ni kwa namna hiyo pia Kanisa linajikabidhi katika mikono ya Mama
Maria. Mwana “Tazama, mama yako.” Yoh 19:27.
Ndugu
yangu, Yesu anasema, “Naona kiu.” Yoh
19:28. Kiu ya Yesu kwangu na kwako, ni kuwa na upendo wa kweli kwako binafsi,
sisi kwa sisi, na Mungu. Kiu yake ni kuona tunakuwa jumuiya inayoongozwa na
upendo, yenye kuhurumiana na kutaabikiana. Kwa maana hiyo, tunapoutazama
msalaba tuone upendo huo ambao kwa sauti ya ukimya inasikika kutoka kwenye
mikono yake licha ya kufungwa kwa misumari ikisema “embu ona nilivyokupenda na
ninavyokupenda, njoo kwangu na nitakupokea kama ulivyo. Nimeutoa uhai wangu kwa
sababu nakupenda upeo. Na kwa sababu hiyo nakupenda kama ulivyo.”
Ndugu yangu, neno la mwisho la Yesu, ni hili, “Imekwisha.” Yoh 19:30. Safari ya kukukomboa na kunikomboa
imefikia kilele chake hapa msalabani. Hapa ndiyo mwisho wa yote pale tunapokuwa
ndani na katika Kristo. Kwa maneno haya, ninaona mambo haya niutazamapo msalaba
mtakafifu; Ninaona kiti chake cha hukumu yaani boriti lile alilowambwa mwokozi
wangu. Kiti hiki mahudhui yake ni UPENDO NA HURUMA YA MUNGU. Hapa ndipo sehemu
salama na ndipo penye uponyaji wa ndani wa maumivu yetu kila mmoja kadiri ya
historia yake na makuzi yake. Kwenye huu msalaba ninaona kofia yake ya kifalme
iliyosukwa kwa taji la miba. Ufalme na utawala wake niwakufikika na kila mmoja
wetu. Ni ufalme wa amani. Ni hapa tu ninapoweza kuyatafakari makuu ya Mungu na
mapito ya maisha yangu na kupata faraja ya moyo wangu kwa sababu najua ninaye
jemedari aliyeshinda uovu kwa wema, bila fujo wala vita.
Ndugu yangu, ni ukweli usiotia shaka kwamba uponyaji kutoka
kwa Mungu tunaupata hasa katika sehemu kubwa mbili:-
Msalabani alipowabwa Yesu. Hapa Yesu alichukuwa magonjwa
yetu, taabu, maumivu, hofu, dhambi na hata umaskini wetu. Yesu aliteseka kiroho
kwa kubeba dhambi tulizotenda na kuhukumiwa pasipo kosa lolote. Pia aliteseka
kihisia kwa aibu aliyopata kwa kuwambwa uchi msalabani. “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye
sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala
hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika
ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa
amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa,” Isa 53:3-4. Mateso ya Yesu ni kama
ifuatavyo:-Alikuja kwa wale aliowapenda sana lakini walimkataa, pale msalabani
alipoteza kila kitu, Mitume, Heshima yake, na Utu wake. Kutokana na Yesu kubeba
huzuni, fadhaa na masikitiko yetu ndiyo maana sisi tunapona kwa kupigwa kwake
na tunapona mwili, nafsi, na roho. “Kwa kuwa hatuna kuhani
mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye
alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi,” Ebr 4:15
Uponyaji wa Roho Mtakatifu. Uponyaji huu tunaupata kupitia
Roho Mtakatifu katika wakati huu wetu na tangu wakati wa Yesu alipoanza huduma
yake. “Roho ya Bwana MUNGU i juu yangu; kwa sababu Bwana amenitia
mafuta niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga
waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za
kufunguliwa kwao,”
Isa 61:1. Ili tupate uponyaji ni lazima tumruhusu Roho Mtakatifu atuponye.
Tujiachie kwake naye atatenda.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mimi nimesema na ulimwengu
waziwazi; sikuzote nalifundisha katika sinagogi na katika hekalu, wakusanyikapo
Wayahudi wote; wala kwa siri mimi sikusema neno lo lote. Ya nini kuniuliza mimi? Waulize wale
waliosikia ni nini niliyowaambia; wao wanajua niliyoyanena.” Yoh 18:20-21
Ee Yesu na Bwana wangu, mimi ni nani basi nisiyesamehe?
No hay comentarios:
Publicar un comentario