miércoles, 2 de marzo de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 3 YA KWARESMA

JUMAMOSI WIKI YA 3 YA KWARESMA
Somo: Hos 6:1-6
Zab: 51:3-4, 18-19, 20-21
Injili: Lk 18:9-14
Nukuu:
“Maana nataka fadhila wala si sadaka, na kumjua Mungu kuliko sadaka za kuteketezwa,” Hos 6:6

“Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipigapiga kifua akisema, ‘Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi,” Lk 18:13

TAFAKARI: “Majuto ya dhambi ya kweli, na Msamaha dhambi.”

Wapendwa wana wa Mungu, na tutafakari leo, “Majuto ya dhambi ya kweli, na Msamaha wa dhambi.” Toba na majuto ya kweli ni kumrudia Mungu bila kujibakiza. Mungu hujua yote katika maisha yetu na hata yale ambayo yapo mbele yetu. “Je! Mashomoro watano hawauzwi kwa sentí mbili? Wala hasahauliwi hata mmojawapo mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi, bora ninyi kuliko mashomoro wengi,” Lk 12:6-7.

Somo la kwanza linatupa picha hiyo na mwono huo wa Mungu. Anachoitaji kwako, ni wewe wenyewe na siyo yale uyafanyayo. Yakupasa kumjua Mungu, na hii ndiyo fadhila mbele za macho yake. “Maana nataka fadhila wala si sadaka, na kumjua Mungu kuliko sadaka za kuteketezwa,” Hos 6:6.

Ndugu yangu, huyafuti makosa yako mbele za Mungu kwa wingi wa sadaka za kuteketezwa uzifanyazo au uzitoazo. Leo hii katika jamii na makabila yetu, bado tupo na tunaendelea kutoa sadaka za kuteketezwa. Mitambiko isiyokoma, na kwa mitindo mbalimbali. Sadaka za mbuzi, na kuvishwa ngozi na mabangili ya shaba kwa kushikamanishwa na sadaka hizo. Wingi wa matendo na sadaka hizi, hauondoi kosa letu mbele za Mungu. Tunachofanya ni kujiongezea hofu pasipo hofu.

Kukiri na kufanya toba ya kweli ndiyo salama ya maisha yetu. Sadaka hizi hazimpendezi Mungu. Ni chukizo mbele ya Mungu. “Dhabihu na matoleo na sadaka za kuteketezwa na hizo za dhambi hukuzitaka, wala hukupendezwa nazo (zitolewazo kama ilivyoamuru torati), ndipo aliposema, Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako. Aondoa la kwanza, ili kusudi alisimamishe la pili,” Ebr 10:8-9. La pili limeshasimamishwa na sadaka ya mwanaye Mpenzi Yesu Kristo. Kasadaka kako na matambiko yako yananafasi gani mbele ya Kristo? Acha maigizo hayo!

Habari Njema-Injili yetu ya leo yatufundisha namna ya kufanya toba ya kweli na mkao wetu mbele ya Mungu kwenye kiti chake cha Huruma na Msamaha. Ndugu yangu, tuwapo mbele ya Kiti cha huruma na Msamaha wa Mungu, Yeye haitaji historia ya mema yetu tufanyayo kwa sababu wema na uzuri ni asili na ni tabia ya Mungu. Haitaji kusikia ubaya wa wengine, ila makosa yako. Mfarisayo anatoa historia ya mazuri yake na namna afanyavyo mfungo wake. “Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang’anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote,” Lk 18:11-12.

Ndugu yangu, mbele za Mungu hatujihesabii haki, bali tunapewa haki hiyo baada ya kufanya yampendezayo Mungu. Tunachohitaji mbele ya Mungu ni Huruma na Msamaha wake.  Tukiwa mbele ya kiti hiki cha Huruma ya Mungu, hatufanyi malinganisho ya dhambi wala uhalalishaji wa dhambi, ila makosa yetu tuliyoyafanya kwa kujua au kutokujua. Labda nitoe mfano: Huwezi kwenda kuungama na kusema hivi; “nimechukua pesa ya mume wangu na kulipa zaka kwa sababu yeye hapendi kulipa zaka.” Kosa la wizi lipo pale pale, licha ya kwamba nia yako ilikuwa nzuri, yaani kulipa zaka kwa niaba ya mume wako. Njia mbovu na ovu, haziwezi kamwe kuhalalisha tendo lolote lile hata kama malengo yake ni mazuri.

Mfano wa kuigwa ni wa Mtoza ushuru. Mtoza ushuru anajiachia kwenye kiti hiki cha Huruma na Msamaha wa Mungu kama alivyo na kama alivyoyatenda makosa yake. “Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi,” Lk 18:13. Kwa maneno haya yanatosha kupewa dhawabu na kuinuliwa katika hali yake ya unyonge iliyotokana na dhambi zake. Mtoza ushuru alikuwa amejawa na hofu ya Mungu kiasi kwamba hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifuani mwake. Hii ndiyo toba ya kweli na aibu juu ya dhambi. Ndugu yangu, uwapo kwenye kiti cha Huruma na Msamaha wa Mungu, unachoitaji ni uponyaji wa mwili na roho. Mponyaji wetu ni Mungu anayejua makandokando yetu yote. Kamwe usione aibu kuziungama dhambi zako, na tena kwa uwazi kabisa.

Ndugu yangu, mara nyingine waona baadhi ya dhambi zako ni kubwa sana, na mbele ya kiti hiki cha Huruma na Msamaha, unaishia kusema na “nyingine nilizosahau,” ili hali unajua hujazisahau. Huku ni kuchezea Kiti hiki cha Huruma ya Mungu na Msamaha, na zaidi, kumkufuru Roho Mtakatifu. “Na kila mtu atakayenena neno juu ya Mwana wa Adamu atasamehewa, bali aliyemkufuru Roho Mtakatifu hatasamehewa,” Lk 12:10. Hakuna dhambi kubwa mbele ya Mungu ambayo atashindwa kukusamehe, na hakuna dhambi ndogo mbele ya Mungu ambayo hata ichukulia maanani. Neema na huruma ya Mungu ni KUBWA kuliko dhambi zako. Ikiwa dhambi ni ukosefu wa kutenda mema na kwenda kinyume cha upendo wa Mungu, basi hakuna uzito wa dhambi kubwa wala ndogo mbele ya Mungu kwa kusamehe. Tuziungame zote bila aibu.

Kwa kuziungama dhambi hizo kama alivyofanya Mtoza ushuru, unahesabiwa haki, na kukwezwa mbele za Mungu. “Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule (Mfarisayo); kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,” Lk 18:14.

Ndugu yangu, mali yako halali mbele ya Mungu ni dhambi zako. Vingine vyote ni mali na uzuri wa Mungu. Kuviishi kwa amani na uhuru alivyokupa Mungu kama sehemu ya uzuri wake, yakupasa kusalimisha mali zako kwake, yaani dhambi zako. Hivyo, twende muda na wakati wo wote kupatanishwa naye kwenye kiti chake hiki cha Huruma, Msamaha, na Upendo.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi,” Lk 18:13b


Ee Yesu, nijalie neema ya kuziona na kuziungama dhambi zangu zote bila aibu mbele ya kiti chako cha Huruma, Msamaha, na Upendo. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario