martes, 8 de marzo de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 4 YA KWARESMA

JUMATANO WIKI YA 4 YA KWARESMA

Somo: Isa 49:8-15
Zab: 145:8-9, 13cd-14, 17-18
Injili: Yoh 5:17-30
Nukuu:
“Je, mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe,” Isa 49:15

“Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani,” Yoh 5:24

TAFAKARI: Usikivu wa Upendo wa Mungu Baba na Mwana, hu na uzima wa milele ndani yake.

Wapendwa wana wa Mungu, “Usikivu wa Upendo wa Mungu Baba na Mwana, hu na uzima wa milele ndani yake.” Yesu Kristo anaudhihirisha upendo wa Mungu Baba kwetu, na ni kwa njia yake twaweza kumjua Baba Mungu. Hili ndiyo fumbo kubwa la kumwilishwa kwa neno wa Mungu na kuwa mwanadamu.

Ahadi ya Mungu kwetu ni kutokutusahau katika hali zote hata kama kibinadamu jambo hilo linawezekana. Mungu hawezi kutusaha. “Je, mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe,” Isa 49:15

  Maisha yetu ni mpango wa Mungu na kwa malengo ya Mungu. Mpango huu unarahisishwa kwa uwepo wa Mwanaye Yesu Kristo, ambaye hajifanyii mambo yake pasipo Mungu Baba aliyempeleka. “Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka,” Yoh 5:30

Wayahudi wanapinga ufundishi na utendaji wa Yesu, hasa kwenye uelewa wa Mungu mmoja tu, na si katika nafsi tatu. Kadiri ya uelewa na mtazamo wa Kiimani wa Kiyahudi, kama ilivyopia kwa dini nyingine kama Waislamu, Mungu hawezi kuwa na mtoto, na Yesu kusema yeye ni Mwana wa Mungu, wakati wanajua yeye binafsi na wazazi wake, ni kufuru kubwa sana. Lakini ukweli ni kwamba, nafsi hizi tatu hujitofautisha katika utendaji. Na katika utendaji huu wa nafsi mojawapo, hauondoi uwepo na ushirikiano wa nafsi nyingine.

Ndugu yangu, yawezekana kupenda bila kujua na wakati mwingine kutokufanya chochote, ila huwezi kujua ukaacha kufanya na kupenda. Mbali zaidi ni kwamba, kupenda na kufanya huku msingi wake ni kuamini yale ayafanyayo Yesu Kristo pamoja na uelewa wetu kibinadamu kutotosheleza kuzama kabisha katika fumbo la Utatu Mtakatifu. Tuanze na kuyaamini haya ayasemayo na kuyafanya Yesu Kristo, na katika safari hiyo tutajua taratibu siri ya fumbo hili la Utatu Mtakatifu na kupenda.

Ahadi ya kuyafanya hayo yote, Yesu Kristo anaweka wazi jambo hili, na kusema, “Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani.” Yoh 5:24. Jambo hili la kusikia neno na kumwamini Yesu Kristo liongoze dira nzima ya maisha yetu ya kiroho. Mpendwa kuwa na uzima ndani ya Kristo na katika Kristo ni kumfanya Kristo kuwa pumzi ya maisha yako kila siku; katika kufikiri, kutenda, na kuishi.

Tumsifu Yesu Kristo!

Tena Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote; ili watu wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba,” Yoh 5:22-23


Bwana Yesu, uwe pumzi na uhai wangu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario