JUMAMOSI
WIKI YA 5 YA KWARESMA
19/3/2015
Mt. Yosefu, Mume wa Bikira
Maria
Somo I: 2 Sam 7:4-5, 12-14, 16
Zab: 89:2-3, 4-5, 29, 29
Somo II: Rum 4:13, 16-18, 22
Injili: Mt 1:16, 18-21, 24
Nukuu:
“Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha
ufalme wake nitakifanya imara milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa
mwanangu,” 2 Sam 7:13-14
“Kwa maana ahadi ile ya kwamba atakuwa mrithi wa ulimwengu alipewa
Ibrahimu na uzao wake, si kwa sheri bali kwa haki aliohesabiwa kwa imani. Kwa
hiyo ilitoka katika imani, iwe kwa njia ya neema, ili kwamba ile ahadi iwe
imara kwa wazao wote; si kwa wale wa torati tu, ila na kwa wale wa imani ya
Ibrahimu; aliye baba yetu sisi wote,” Rum 4:13, 16
“Naye Yusufu mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake
kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri,” Mt 1:19
TAFAKARI: “Utabiri juu ya Yesu Kristo, na kuhesabiwa haki kwa Yusufu/Yosefu Baba
Mlezi wa Kristo.”
Wapendwa wana wa Mungu, karibu katika tafakari yetu ya leo, ambapo Mama
Kanisa anafanya Sikukuu ya Mtakatifu Yusufu/Yosefu Baba Mlezi wa Yesu Kristo,
na kuadhimisha pia miaka mitatu ya Uongozi wa Baba Mtakatifu wetu Fransisco.
Tafakari yetu ya leo imejikita katika wazo kuu hili, “utabiri juu ya Yesu
Kristo, na kuhesabiwa haki kwa Yusufu/Yosefu Baba Mlezi wa Yesu Kristo.”
Somo letu la kwanza na la pili katika siku hii maalumu, yanatupatia
utabiri wa Yesu Kristo na kazi yake katika utimilifu ulio wazi wa historia ya
wokovu wetu. Somo la kwanza limetupa kwa ufupi utabiri huo wa Yesu Kristo kwa
maneno haya, “Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha
enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye
atakuwa mwanangu,” 2 Sam 7:13-14. Kazi kubwa atakayokuwa nayo Kristo ni
kuijenga nyumba ya Mungu kwa jina la Mungu, na kiti cha ufalme wake kitafanywa
kuwa imara Milele. Je, nyumba ya Mungu ni nini? Na, kiti
chake cha ufalme ni kipi?
Ndugu yangu, nyumba ya
Mungu ni Kanisa lake kama jengo, na wafuasi wa Kristo, yaani wale wote
waliobatizwa kwa jina lake, na kuyaishi yale yote aliyoyafundisha kama
mwendelezo wa ufunuo wa aliye yote katika yote na utimilifu wote. Kanisa hili
la wabatizwa ni hili linalotembea, yaani Kanisa la hija, Kanisa la Watakatifu
Mbinguni, na Kanisa linaloteseka Toharani ambalo kwalo, lahitaji sala na maombi
ya Kanisa la hija na Kanisa la Watakatifu Mbinguni.
Kanisa hili la hija ni
mchanganyiko wa Watakatifu na wadhambi. Ni Kanisa linaloendelea kutakatifuzwa
kwa neema zipatikanazo katika Kanisa kwa njia ya Masakramenti yake. Mimi na wewe
tupo katika Kanisa hili la hija. Tunaitaji maelekezi na mwongozo wa Kristo na
Kanisa la Watakatifu katika wongofu wetu wa kila siku ya maisha yetu hapa
duniani. Ni Kanisa lililojaa Huruma ya Mungu, na kuongozwa kwa unyenyekevu
katika kujiachia katika Kristo na ndani ya Kristo, kama asemavyo Mtume Paulo,
“Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; Bali nakaza mwendo
ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu.
Nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo
Yesu.” Flp 3:12,14. Wito wetu mkuu tulio wafuasi wa Kristo ni kuwa WATAKATIFU.
Kiti cha Ufalme wake
Kristo ni Mamlaka “Authority” yake. Mamlaka ya Kristo si Nguvu “Power” katika
mtazamo wa kiutawala wa leo na kisiasa, bali ni mamlaka katika Maadili “Moral.”
Kwa hiyo ni kiti cha nguvu ya Mamlaka ya kimaadili “Moral Authority,” ambayo
kiundani inanguvu kuliko nguvu ya siasa katika utawala “Political Authority.”
Nguvu hii ya kiutawala kwa mtazamo wa Kanisa na Kristo imelindwa na kuachwa
katika mambo makuu matatu; Maandiko
Matakatifu “Scriptures”; Mapokea ya Mitume kuanzia Kristo mwenyewe hadi leo
katika umoja wa Maaskofu “Tradition; na Mamlaka fundishi ya Kanisa
“Magisterium.” Mambo haya matatu kwa mtazamo wa leo Kikanisa ndiyo kiti cha
ufalme wa Kristo. Ni mwendelezo wa yale aliyokuwa akiyafanya na anaendelea
kuyafanya hadi mwisho wa nyakati. Hapa ndipo tunapouona umoja wa waamini ndani
na katika Kristo. Misingi hii na miimili hii mitatu yapaswa kuwa Imara muda
wote na kutosigana. Yote hufanywa kwa unyenyekevu mkubwa, kwa kila mmoja watu
kujua nafasi yake katika safari hii ya wokovu.
Mpendwa wana wa Mungu,
somo letu la pili, laufunua utabiri huo wa Kristo na mwendelezo wake katika
kuyaishi, kwa maneno haya, “Kwa maana ahadi ile ya kwamba atakuwa mrithi wa
ulimwengu alipewa Ibrahimu na uzao wake, si kwa sheri bali kwa haki
aliohesabiwa kwa imani. Kwa hiyo ilitoka katika imani, iwe kwa njia ya neema,
ili kwamba ile ahadi iwe imara kwa wazao wote; si kwa wale wa torati tu, ila na
kwa wale wa imani ya Ibrahimu; aliye baba yetu sisi wote,” Rum 4:13, 16.
Hapana shaka ye yote
ndugu yangu, kwamba, mpango wa Mungu katika wokovu licha kwamba ulianza kwa mtu
mmoja kama Ibrahimu, na tena kwa kundi la watu yaani Waisraeli (Torati),
utimilifu wake ni kwa watu wote kwa sababu, Ibrahimu alihesabiwa haki ya kuwa
Baba wa sisi sote. Yesu Kristo katika mateso, kifo na ufufuko wake kaliweka
jambo hili wazi na kwa uelewa mkubwa sana. Kwa sababu hiyo, “Hakuna aliye na
upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,”
Yoh 15:13. Katika kifo chake sisi sote kama wafuasi wa Kristo tumehesabiwa haki
kwa damu yake Msalabani kwa upendo wake huu mkuu. Sisi si watumwa tena, bali ni
rafiki zake na ndugu zake Kristo. Kwa maana hiyo, “Siwaiti tena watumwa; kwa
maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa
yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.” Yoh 15:15. Litendwalo ndani na katika
Kristo ni lile tu liufunualo; upendo wake, unyenyekevu wake, uaminifu wake,
upole wake, utii wake, amani yake, na utakatifu wake.
Injili yetu ya leo, na
hasa siku hii kuu ya Mtakatifu Yusufu/Yosefu, imelenga katika kuhesabiwa haki
Yosefu kama Baba Mlezi wa Yesu Kristo. Kibinadamu ni vigumu sana kupokea hali
iliyomkuta Yosefu. Ni ukweli ulio wazi kwamba kwa vile Yosefu alimpenda sana
Mama Bikira Maria, hakutaka kumwaibisha. Unyenyekevu wake huu unamfanya Yosefu
achukue hatua ya busara kwa kufanya hivi: “Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa
na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uwezo wa Roho
Mtakatifu. Naye Yusufu mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake
kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri,” Mt 1:18b-19. Je, ni aibu gani
ingempata Mama Bikira Maria kama Yosefu angeamua kuliweka wazi?
Ndugu yangu, kadiri ya
Sheria za kiyahudu na utaratibu wao kuhusu mahusiano, Bikira Maria ilimpasa
adhabu ya Kifo. Kuwa na ujauzito kabla ya ndoa halisi ya Kiyahudi lilikuwa kosa
kubwa sana. Si aibu kwa Bikira Maria tu, bali hata kwa familia yake kwa kukosa
malezi mazuri ya Binti yao. Kwa kosa hili adhabu yake ilikuwa hivi. “Lakini
ikiwa ni kweli neno hili, la kutoonekana kwake yule kijana alama za ubikira; na
wamtoe nje yule kijana mlangoni pa nyumba ya baba yake, na waume wa mji wake
wampige kwa mawe hata afe; kwa vile alivyofanya upumbavu katika Israeli, kwa
kufanya ukahaba katika nyumba ya baba yake; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati
yako.” Kumb 22:20-21.
Kwa mantiki hii, Yosefu
alijua wazi kitakacho mpata Bikira Maria hivyo anaamua kumwacha kwa siri. Na
kwa vile kadiri ya uchumba na maandalizi ndoa ya kiyahudi huchukua si chini ya
miezi sita, bila shaka Yosefu alijua uaminifu wa Bikira Maria, kuwa ni binti
aliyekuwa na malezi mazuri. Ujauzito huu ulimchanganya sana Yosefu. Hivyo
kutohusika na jambo hili ambalo kwake lilikuwa ni fumbo, anaamua kutoshiriki
kumwaka damu yake. Hapa ndipo anapohesabiwa haki Mtakatifu Yosefu kwa
uthibitisho wa maneno haya ya Malaika, “Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu
kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu,” Mt
1:20. Malaika wa Mungu anafunua ukweli wa kitakachozaliza kuwa kina mkono wa
Mungu na ni kwa ajili ya wokovu wa dunia nzima. “Naye atazaa mwana, nawe
utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi
zao,” Mt 1:21. Je, akina baba katika ndoa zenu mna kifua kizito kama cha
Mt.Yosefu?
Ndugu yangu,
yakujifunza kutoka kwa Mt.Yosefu yapo mengi sana kwa Kanisa katika ujumla wake
na kwa kila mmoja wetu. Kwa upande wa Kanisa na hasa wale waliopewa dhamana
katika utumishi wa Kristo, yatupasa kuwa na subira na unyenyekevu kama wa Mt.
Yosefu katika kuona, kufikiri, kuamua, na kutenda. Msingi wa haya yote ni
unyenyekevu. Kwa kila mmoja wetu, na hasa wana familia ya Mungu, yatupasa
kusikiliza sana sauti iliyopo ndani
mwetu na kuamua lililo jema zaidi, na sio ushindi wa haraka usio na tija. Pili,
hatujihesabii haki hata kama tunayomastahili katika yale yatuhusuyo kisheria,
kimtazamo, na hata kimila na desturi
zetu. Tumpe kwanza nafasi Roho Mtakatifu atuelekeze namna ya kufanya pale
tunapokabiliwa na giza nene katika maamuzi.
Mwisho wapendwa,
tuliombee Kanisa lote kiulimwengu, na hasa maeneo yale ambayo Wakristo wenzetu
wanateseka na kuuwawa kikatili kwa sababu ya Imani yao juu ya Kristo na Mungu
aliye hai. Tuliombee Kanisa na hasa leo ambapo Baba Mtakatifu anapoadhimisha
miaka mitatu ya uzinduzi wa ofisi yake ya Kipapa kama Baba Mtakatifu. Tuliombee
pia Kanisa letu mahalia la Tanzania hasa katika kipindi hiki cha sintofahamu
nyingi za kiimani.
Tumsifu Yesu Kristo
“Naye Yusufu mumewe, kwa vile
alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri,” Mt
1:19
Ee Yesu, tuhesabie haki kwa kile
tulicho kila mmoja kadiri ya wito wake.
No hay comentarios:
Publicar un comentario