miércoles, 16 de marzo de 2016

TAFAKARI: JUMATATU YA WIKI KUU

JUMATATU YA WIKI KUU
Somo: Isa 42:1-7
Zab: 27:1, 2, 3, 13-14
Injili: Yoh 12:1-11
Nukuu:
“Mimi, Bwana, nimekuita katika haki, nami nitakushika mkono, na kukulinda, na kukutoa uwe agano la watu, na nuru ya mataifa; kuyafunua macho ya vipofu, kuwatoa gerezani waliofungwa, kuwatoa wale walioketi gizani katika nyumba ya kufungwa,” Isa 42:6-7

“Mwache aiweke kwa siku ya maziko yangu. Kwa maana maskini mnao sikuzote pamoja nanyi, bali mimi hamnami sikuzote.” Yoh 12:7-8

TAFAKARI: “Utulivu, amani, na upendo wa Bwana Yesu Kristo katika kujitoa sadaka; na unafiki wa Yuda Iskariote.”

Wapendwa wana wa Mungu, tuone katika tafakari yetu ya leo “utulivu, amani, na upendo wa Bwana Yesu Kristo katika kujitoa sadaka, na kwa upande wa pili tuone unafiki wa Yuda Iskariote.” Muonekano huu wa utulivu, amani, na upendo wa Bwana wetu Yesu Kristo kukijongea kifo unajionyesha kwanye masomo yetu, yaani somo la leo, na injili.

Nabii Isaya anatupa taswira na picha ya huyo ambaye anayejitoa sadaka kwa ajili ya wokovu wa wengi. Sifa ya kwanza kabisa Roho wa Mungu yu juu yake. Kwa maana hii, yote ayafanyayo yana baraka ya Mungu na ni kwa ajili ya ushirika wake na Mungu. Kwa kuwa na sifa hii, Mtarajiwa huyu, atakuwa na mamlaka ya kutoa hukumu kwa mataifa. Na kwa vile yote yana mkono wa Mungu, kujitoa kwake sadaka hakuna makeke, ila ujasiri uliojijenga katika misingi wa unyenyekevu.

Licha ya kuwa na sifa hizo hapo juu, mteule huyu, kutokana na upole na unyenyekevu wake, umempatia utukufu na uzima. Atakuwa uzima kwa mwenye kuitaji uzima huo. Atawaponya watu kadiri ya mahangaiko yao; vipofu wataona, wafungwa watafunguliwa na kuwa huru. Uthibitisho huu watoka kwa Mungu mwenyewe. “Mimi, Bwana, nimekuita katika haki, nami nitakushika mkono, na kukulinda, na kukutoa uwe agano la watu, na nuru ya mataifa; kuyafunua macho ya vipofu, kuwatoa gerezani waliofungwa, kuwatoa wale walioketi gizani katika nyumba ya kufungwa,” Isa 42:6-7

Ndugu yangu, utabiri huu umekuwa kweli ndani na katika Kristo. Na sasa mwanakondoo huyu asiye na doa anajongea kifo chake kwa ujasiri kujichukulia taji la ushindi. Wakati ndiyo sasa, na yampasa kujongea Yerusalemu kuyatimiza yale yote yaliyotabiriwa juu yake. Huyu ndiye Yesu Kristo atuambiaye, “nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu,” Yoh 10:28

Pamoja na kutuhakikishia uzima huo usiopokonywa ndani na katika mikono yake, binadamu tumekuwa tukitenda kinyume na mara nyingine kile tusemacho sicho tunacho amini na kumaanisha. Huku ni kumsaliti Kristo kuliko wazi kama anavyofanya Yuda Iskariote anapoona Yesu akinawishwa kwa Marhamu. Yuda Iskariote anawaonea huruma Maskini kwa kuona tendo lile la upendo analofanyiwa Yesu. Huu ni unafiki mkubwa sana wetu sisi wanadamu.

Kwa hiyo, tunashauriwa kufanya lililo jema  kila wakati tunapowajibika kufanya hivyo. Kwa maana hiyo, Yesu anasisitiza, “Mwache aiweke kwa siku ya maziko yangu. Kwa maana maskini mnao sikuzote pamoja nanyi, bali mimi hamnami sikuzote.” Yoh 12:7-8

Ndugu yangu, unafiki ni saratani mbaya sana hasa katika ufuasi wetu. Mwisho wa siku hutojua ulikuwa unamtumikia nani hapa duniani. Ni ukweli usiotia shaka kwamba, kutokana na hali ya kutokukamilika kwetu kama wanadamu, huwezi kuwaridhisha watu wote kwa nyakati zote. Yakupasa kuchagua njia moja na yenye kufaa. Katika uchaguzi huu ni wazi utakugharimu kama unavyomgaribu Bwana wetu Yesu Kristo. Kwa upande wake, anapokea changamoto hiyo kwa amani, upole, utulivu na upendo kwa sababu amefanya uchaguzi mwenyewe na ulio bora. Na wewe Je?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Mwache aiweke kwa siku ya maziko yangu. Kwa maana maskini mnao sikuzote pamoja nanyi, bali mimi hamnami sikuzote.” Yoh 12:7-8


Ee Yesu, nijalie neema ya kuishi kile nilicho na kujitoa sadaka kila siku bila kujibakiza. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario