lunes, 28 de marzo de 2016

TAFAKARI: JUMANNE YA OKTAVA YA PASAKA

JUMANNE YA OKTAVA YA PASAKA
Somo: Mdo 2:36-41
Zab: 33:4-5, 18-19, 20, 22
Njili: Yoh 20:11-18
Nukuu:
Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu,” Mdo 2:38

Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie,”  Mdo 2: 39 

Akawashuhudia kwa maneno mengine mengi sana na kuwaonya, akisema, Jiokoeni na kizazi hiki chenye ukaidi,” Mdo 2:40

Yesu akamwambia, Mama, unalilia nini? Unamtafuta nani? Naye, huku akidhania ya kuwa ni mtunza bustani, akamwambia, Bwana, ikiwa umemchukua wewe, uniambie ulipomweka, nami nitamwondoa,” Yoh 20:15

Yesu akamwambia, Mariamu. Yeye akageuka, akamwambia kwa Kiebrania, Raboni! (Yaani, Mwalimu),” Yoh 20:16

Yesu akamwambia. Usinishike; kwa maana sijapaa kwenda kwa Baba. Lakini enenda kwa ndugu zangu ukawaambie, Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu,” Yoh 20:17 

TAFAKARI: “Kwa Ufufuko wa Yesu Kristo sote twahesabiwa haki kwa kufanya toba ya kweli; Naam, sote kwa upendo wa Mungu twaitwa wana wake na yeye ni Mungu wetu.”

Wapendwa wana Mungu, tendo la ufufufuko wa Bwana Wetu Yesut Kristo, linatuwezesha na linakuwa neema na baraka kwetu, hasa ule uwezo wa kupokea vipawa vya Roho Mtakatifu pale tu tunapofanya toba ya kweli. Ni kwa dhambi zetu imekua sababu ya kifo cha Bwana wetu Yesu Kristo, na ni kwa kupitia toba ya kweli kwa dhambi zetu twapokea neema na baraka, na kuhesabiwa tena haki kuwa warithi na wana wa Mungu. Ni kwa sababu hii, leo kwa namna ya pekee tutafakari juu ya neno hili, “Kwa Ufufuko wa Yesu Kristo sote twahesabiwa haki kwa kufanya toba ya kweli; Naam, sote kwa upendo wa Mungu twaitwa wana wake na yeye ni Mungu wetu.”

Mtume Petro, kwa kujaliwa ujasiri na nguvu ya Kristo Mfufuka, haoni haya kuwaambia Wayahudi ukweli kuhusu wokovu wao baada ya kufanya kosa la kumwua mwenye haki-Yesu Kristo. Hata sasa Mtume Petro ananiambia mimi na wewe ambao twahitaji huruma na neema ya Mungu. Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu,” Mdo 2:38. Ndugu yangu, ni kwa jina la Yesu Kristo tu twaweza kupata msamaha wa dhambi, na kupatanishwa tena na Mungu Baba. Na ni kwa njia ya ubatizo tunafia dhambi na kuzaliwa wapya kama ishara halisi ya Ufufuko wa Yesu Kristo. “Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi; naye ni mfano wa Mungu alisiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” Kol 1:13-15. Ili tufaidi neema za Ufufuko wa Bwana Yesu Kristo, ikiwa pamoja na vipawa vya Roho Mtakatifu, yatupasa kufanya toba ya kweli, ikiambatana na kuzaliwa upya kwa njia ya Roho Mtakatifu.

Toba ya kweli ni kutambua kule kujikwaa kwetu, na kuyaacha maanguko hayo, huku tukifuata njia iliyo sahihi. Yesu Kristo pasipo shaka yeyote, ndiye njia sahihi ya kufuata, kwani kwa Ufufuko wake, yaliyo ya kale, na yasasa, na yajayo yamekwisha eleweka. Tuendako sasa twakujua. Yesu akamwambia. Usinishike; kwa maana sijapaa kwenda kwa Baba. Lakini enenda kwa ndugu zangu ukawaambie, Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu,” Yoh 20:17. Ili tupate mastahili ya kumshika Kristo Mfufuka, yatupasa kufanya toba ya kweli kama nilivyokwisha kusema. Yesu anamwambia Mariamu na kumbumbusha toba ya kweli. Huu ni wito wa kujitakasa kwa yale mambo yanayotukwamisha kuiona sura ya Mungu. Mastahili yetu baada ya kuhesabiwa haki kwa kufanya toba ya kweli, ni maisha ya utakatifu.

Maisha mapya baada ya Ufufuko, ni maisha ya Utakatifu kwa wote wanaoridhia njia ya Kristo. Kuridhia njia hii ni kufanya toba ya kweli. Tendo hili la toba ya kweli ndani na katika Kristo, linatupa mastahili sawa bila kujali historia zetu mbaya, makabila yetu, na hata utaifa wetu. Tendo hili linatupa uhalali wa kuwa wana wa Mungu. Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie,”  Mdo 2: 39. Tendo hili ni upendeleo mkubwa sana kwetu, na upendo wa Mungu wa ajabu. Je, watambua jambo hilo? Je, wayajua mapungufu yako? Je, waona umuhimu wa kupatanishwa na Mungu Baba kupitia ushindi wa Mwanae dhidi ya uovu na dhambi?

Njia na namna yetu ya kuishi baada ya Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo inatusukuma kuishi upya katika kutenda na kunena. Ni maisha ya ushuhuda wa kweli. Kwa maana hii, Mtume Petro anasema, “Jiokoeni na kizazi hiki chenye ukaidi,” Mdo 2:40. Leo tunaisha katika kizazi chenye ukaidi uliokithiri. Leo walio wengi siyo kwamba tu hawaamini, ila pia hawaoni umaana wa maisha yenye uhusiano na Mungu. Wengi wamefiki hatua ya kuona historia nzima ya wokovu wetu kama hadithi za kufikirika tu. Tupo kwenye wakati wa “ponda mali kifo chaja.” Kwa mtu yeyote na hasa kiongozi akikosa hofu ya Mungu ndani yake, maisha na utu wa binadamu hauna tofauti na bidhaa rahisi na isiyodumu kuwahi kutokea. Leo tunashuhudia mauaji ya wazi na kikatili kuwahi kutokea.

Jambo muhumu la kujiuliza katika maisha yako, “unatafuta nini, na kwa sababu gani?” Mariamu anamtafuta Yesu Kristo kaburini akiwa analia, ili hali Yesu Kristo keshafufuka. Yesu akamwambia, Mama, unalilia nini? Unamtafuta nani? Naye, huku akidhania ya kuwa ni mtunza bustani, akamwambia, Bwana, ikiwa umemchukua wewe, uniambie ulipomweka, nami nitamwondoa,” Yoh 20:15. Mariamu bado yupo kwenye fikra za umauti wa Yesu.

Ndugu yangu, Mariamu mara baada ya kumtambua Kristo, anaanza maisha mapya. Yesu anakuwa mwalimu wa maisha mapya. Mariamu analisema jambo hili toka ndani ya moyo wake. Yesu akamwambia, Mariamu. Yeye akageuka, akamwambia kwa Kiebrania, Raboni! (Yaani, Mwalimu),” Yoh 20:16. Mwalimu ndiye ajuaye yale tunayotaka kujifunza. Mwalimu ndiye ajuaye siri ya kile tunachotaka kukijua. Mwalimu hutuongoza, kutuelekeza, na kutuonyesha kuona kile anachokiona yeye ambacho ndiyo makusudia ya yale tunayojifunza.

Ndugu yangu, hatuwezi kuona na kujua siri ya maisha ya umilele, bila kuwa na Mwalimu wetu Yesu Kristo. Tutaona yale ayaonayo Kristo endapo tu tanamwamini. Yesu anasema, “mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe,” Yoh 6:35. Kupata neema na baraka yatupasa kumwamini Kristo. Naye anasema, “aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji hai itatoka ndani yake,” Yoh 7:38. Kuishi maisha ya ufufuo na uzima yatupasa kumwamini Kristo. Naye anatupa hakikisho hilo kwa kusema, “mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi,” Yoh 11:25. Kumwamini Yesu Kristo ni kumwamini Mungu Baba aliyempeleka na kumwamuru kuyafanya yote. “Naye Yesu akapaza sauti, akasema, Yeye aniaminiye mimi, haniamini mimi bali yeye aliyenipeleka,” Yoh 12:44. Tunapomwamini Kristo, tunafunuliwa makusudi yake hapa duniani na kufanywa kila mara kuishi katika nuru yake. “Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye mimi asikae gizani,” Yoh 12:46. Na mwisho tunaweza kujua na kuzifanya kazi alizozifanya Kristo endapo tunamwamini. “Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba,” Yoh 14:12. Ndugu yangu, Yesu ni nani kwako? Je, unayoimani thabiti kwa hayo unayoishi ndani na katika Kristo?

Tumsifu Yesu Kristo!

Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu,” Mdo 2:38


Ee Yesu, tuwezeshe kufanya toba ya kweli. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario