miércoles, 30 de septiembre de 2015

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 26 YA MWAKA-B

ALHAMISI WIKI YA 26 YA MWAKA-B
1/10/2015
Somo: Neh 8:1-12
Zab: 18:8-11
Injili: Lk 10:1-12
Nukuu:
“Siku hii ni takatifu kwa Bwana, Mungu wenu; msiomboleze wala msilie. Maana watu wote walilia, walipoyasikia maneno ya torati,” Neh 8:9

“Enendeni zenu, mle kilichonona, na kunywa kilicho kitamu, tena mpelekeeni sehemu yeye asiyewekewa kitu; maana siku hii ni takatifu kwa Bwana wetu; wala msihuzunike; kwa kuwa furaha ya Bwana ni nguvu zenu,” Neh 8:10 

Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake,” Lk 10:2

Basi, kaeni katika nyumba iyo hiyo, mkila na kunywa vya kwao; maana, mtenda kazi amestahili kupewa ujira wake. Msihame-hame kutoka nyumba hii kwenda nyumba hii,” Lk 10:7

Na mji wo wote mtakaouingia, wakiwakaribisha, vileni vyakula viwekwavyo mbele yenu; waponyeni wagonjwa waliomo, waambieni, Ufalme wa Mungu umewakaribia,” Lk 10:8-9

TAFAKARI: “Furaha na Amani ya kweli tunapojitoa bila kujibakiza ndani na katika Kristo Yesu kuuishi na kuuhubiri Ufalme wa Mungu.”

Wapendwa katika Kristo, neno furaha au amani la weza kuwa na maana tofauti tofauti kati ya mtu mmoja na mwingine. Ni kweli pia kati yetu tunamwelekeo wa kuona furaha yetu au amani yetu hutokana na “vitu.” Tulivyonavyo. Hivyo vitu fulani katika maisha vinakuwa vigezo vya furaha na amani ya mtu. Kabla ya kuzama katika tafakari hii ni vyema tuyatafakari maswali matatu ya Mhubiri.
Swali la kwanza la muhubiri kuhusu “faida” anauliza kama ifuatavyo, “Mtu ana faida gani ya kazi yake yote aifanyayo chini ya jua?” Ndugu yangu yawezekana kabisa kazi yako ikawa sababu ya furaha na amani yako. Ni kweli kwamba sana unafanya kazi na una nguvu za kufanya hivyo. Je, nguvu hizo zikikuishia na uzee ukakunyemelea, kazi yako itaendelea kuwa sababu ya furaha na amani yako? Tafakari sana jambo hili ndugu yangu.

Mhubiri anaendelea kuuliza swali yake la pili na kusema, Je! Mtendaji anayo faida gani katika yale anayojishughulisha nayo?” Mhu 3:9. Yawezekana furaha na amani yako imejikita katika shughuli zako za kila siku kama vile biashara, maswala ya siasa, ufundishaji, uimbaji, na tume mbalimbali kila mmoja kadiri ya nafasi na wito wake. Je, hiyo tu ndiyo sababu ya furaha na amani yako? Je, utadumu katika shughuli hiyo kwa muda gani? Umejaribu kujiuliza mwisho wa shughuli hiyo utakuwaje? Je, utahimili ushindani wa shughuli hiyo daima? Bila shaka furaha na amani katika swali hili la Mhubiri ipo hatiani.

Mhubiri anatuuliza swali la tatu kuhusu faida na kusema, Kwa maana mwenye hekima hupata faida gani kuliko mpumbavu? Au Maskini ana nini kuliko yeye ajuaye kwenda mbele ya walio hai?” Mhu 6:8. Wapendwa, mwenye hekima ni yule mwenye uwezo wa kuona ukweli na uhalisia wa jambo kama ulivyo. Pili ni yule ambaye kwa kupitia mang’amuzi ya maisha yake anakuwa tayari kuyatafutia suluhisho matatizo anayokumbana nayo na hasa jamii ile anamoishi. Katika mwono huu, mtu mwenye hekima huweza kuzisoma alama za nyakati za wakati wake na kuona mbali zaidi kule anapoelekea licha ya kwamba bado hajaishi hali hiyo. Je, mtu mwenye hekima kwa kuyajua hayo yote ndiyo msingi wa furaha na amani yake?

Mtu mpumbavu ni yule ajifanyaye mwelewa kumbe si mwelewa katika uhasilia wa mambo kama yalivyo. Ni mtu yule anayeshupalia ujinga kwa kiwango cha juu. Je, msimamo huu kimaisha ndiyo sababu ya furaha yako? Na siku basi utakapotambua ukweli kama ulivyo ndiyo itakuwa mwisho wa furaha na amani yako? Masikini ni ye yote yule mwenye uhitaji. Kama sote ni wahitaji, basi sote ni maskini wa viwango tofauti. Mbele ya walio hai ni wale wote wanaoishi katika umilele. Hawa ni watakatifu wa Mungu. Bila shaka hawa wana furaha na amani ya kweli kwa sababu wanamwona Mungu kama alivyo na wanaishi si tena katika imani na matumaini, bali katika umilele wa upendo wa Mungu. “Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo,” 1Kor 13:13.

Wapendwa wana wa Mungu, Mhubiri natupatia jibu la maswali hayo matatu na kusema, Kisha nikaziangalia kazi zote zilizofanywa kwa mikono yangu, na taabu yote niliyotaabika katika kuzitenda; na tazama, yote ni ubatili na kujilisha upepo, wala faida hakuna chini ya jua,” Mhu 2:11. Je, kama hakuna faida yo yote chini ya jua, furaha na amani yangu ya kweli naipata wapi? Yesu anatuambia jambo hili wazi, “kuwa itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake?” Mk 8:36. Ndugu yangu unayesafiri nami kati tafakari hii, furaha ya kweli tunaipata pale tunapokuwa watu wa kiasi, yaani kuishi kwa uchache. Jambo hili tunaliona katika mfano ule wa talanta. “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako,” Mt 25:23. Furaha ya kweli tunaipata pale tunaposhiriki mateso yetu kikamilifu na Kristo. Ni pale tunapoisha kweli na haki bila kumwonea aibu Kristo. Ni pale tunapotesaka kwa ajili ya Kristo na hasa kuwa sauti za wasiokuwa na sauti katika jamii dhalimu na ovu. Yesu anasema hivi, “Basi ninyi hivi sasa mna huzuni; lakini mimi nitawaona tena; na mioyo yenu itafurahi, na furaha yenu hakuna awaondoleaye,” Yoh 16:22.

Wapendwa wana wa Mungu, amani ya kweli ni ile tuipewayo na Kristo mwenyewe, yaani tunapokuwa ndani na katika yeye. Amani hiyo siyo ile tuipewayo na ulimwengu huu. Tukiwa ndani na katika Kristo hatuwezi kuishi katika mifadhaiko wala woga. Yesu anatuambia, “Amani nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga,” Yoh 14:27. Na tunaipata amani hii tunapotenda kadiri anavyotufundisha Kristo. Kuyatenda yale yampendezayo Mungu siyo yale yafaidishayo nafsi na mwili tu. “Maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu,” Rum 14:17. Kuna faida kubwa kuteswa kwa kutenda mapenzi ya Mungu kuliko kutenda mabaya. “Maana ni afadhali kuteswa kwa kutenda mema, ikiwa ndiyo mapenzi ya Mungu, kuliko kwa kutenda mabaya,” 1Pet 3:17.

Hivyo wapendwa wana wa Mungu furaha yetu na amani yetu ya kweli ni kutenda kadiri ya Mungu apendavyo, na kufanya hivyo bila kujibakiza. Tunapoikubali hali hii tuwe tayari kupokea mateso na kadhia zote ndani na katika Kristo. Hatuna sababu ya kuendelea kuomboleza na kusikitika kama tunaye Mungu ndani yetu. Wana wa Israeli walipoipokea torati haikuwapasa tena kuendelea kuomboleza na kufia masikitiko yao. Nabii Nehemia anawaambia Waisraeli, “Siku hii ni takatifu kwa Bwana, Mungu wenu; msiomboleze wala msilie. Maana watu wote walilia, walipoyasikia maneno ya torati,” Neh 8:9. Kama kweli ninayo imani na neno la Mungu, na Kristo aliyekufa kwa ajili yangu, sina sababu ya kuwa na mashaka wala hofu juu ya maisha yangu na Kristo.

Wapendwa katika Kristo, furaha ya Bwana ni nguvu yetu. Tunapojazwa amani na furaha ya Bwana ndani yetu hakuna cho chote tutakachofanya bila kufanikiwa. Maisha yetu yatakuwa yanaongozwa kwa malengo ya Mungu mwenyewe. Hivyo Nabii Nehemia anawaambia watu wake kwamba, “Enendeni zenu, mle kilichonona, na kunywa kilicho kitamu, tena mpelekeeni sehemu yeye asiyewekewa kitu; maana siku hii ni takatifu kwa Bwana wetu; wala msihuzunike; kwa kuwa furaha ya Bwana ni nguvu zenu,” Neh 8:10. Je, ni nani atakaye kuwa na nguvu juu yetu kama Mungu yu upande wetu? Hivyo mimi na wewe ni sababu tosha ya kuuleta ujumbe wa amani na furaha ya Mungu kwa watu. Na pale ambapo haipo furaha na amani hiyo, yatupasa kuiomba kwa Mungu, naye atatoa kadiri ya mahitaji yetu. Kama jumuiya ya wenye hofu ya Mungu, Yesu anatualika kuliomba hili kadiri ya maitaji ya kanisa lake, na kusema, “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake,” Lk 10:2. Hili ni jukumu la kila mbatizwa.

Kufikia lengo la kuutangaza ufalme wa Mbinguni kwa wengine, sisi tuliopata habari hii ya wokovu yatupasa kulisimamia jambo hilo kwa weledi mkubwa, kwa kuwa waaminifu kwalo, na kuushikila ukweli huu bila kutetereka. Yesu anatutaka kuwa makini sana huko tuendako kuupeleka ujumbe wa wokovu. Naye anasema, Basi, kaeni katika nyumba iyo hiyo, mkila na kunywa vya kwao; maana, mtenda kazi amestahili kupewa ujira wake. Msihame-hame kutoka nyumba hii kwenda nyumba hii,” Lk 10:7. Na lifanyike jambo moja kwa wakati. Hii ni pamoja na kuwa makini kwa jambo lile lile tu. Tusibebe ajenda nyingi katika safari hii ya uinjilishaji. Mambo hayo {mfuko, mkoba, viatu na wala kuwaamkie mtu njiani} tukiambatana nayo yatatuchanganya na kutufanya tupoteze mwelekeo. Tuambatane na kubeba yale tu tunayohitaji kwa utume huo. Tusipokuwa na uchache wa vitu furaha na amani ya kweli hutoweka. Tusiuzunike pale ambapo tunaona mambo hayakwenda kama tulivyotarajia. Kufanya hivyo ni kupoteza muda bure kwani muda hautungoji hata kidogo.

Katika jambo hili Yesu anasema, “Na mji wo wote mtakaouingia, nao hawawakaribishi, tokeni humo, nanyi mkipita katika njia zake semeni, Hata mavumbi ya mji wenu yaliyogandamana na miguu yetu tunayakung'uta juu yenu. Lakini jueni hili, ya kuwa Ufalme wa Mungu umekaribia,” Lk 10:10-11. Jambo la msingi la kuzingatia ni kufanya yale tu tuliyotarajia kuyafanya na kuwa na mahusiano mazuri na wale tuliokusudia kuwainjilisha neno la Mungu. Na mji wo wote mtakaouingia, wakiwakaribisha, vileni vyakula viwekwavyo mbele yenu; waponyeni wagonjwa waliomo, waambieni, Ufalme wa Mungu umewakaribia,” Lk 10:8-9. Tuyafanyapo haya kwa unyenyekevu bila kujibakiza huwa msingi wa furaha na Amani yetu.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUFANYE VYOMBO VYA FURAHA NA AMANI YAKO. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario