jueves, 17 de septiembre de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 24 YA MWAKA-B

IJUMAA WIKI YA 24 YA MWAKA-B
18/9/2015
Somo: 1Tim 6:2-12
Zab: 48:6-10, 17-20
Injili: Lk 8:1-3
Nukuu:
Mtu awaye yote akifundisha elimu nyingine, wala hayakubali maneno yenye uzima ya Bwana wetu Yesu Kristo, wala mafundisho yapatanayo na utauwa, amejivuna,” ITim 6:3-4b

Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu,” 1Tim 6:7 

“Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu,” 1Tim 6:9

Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” 1Tim 6:10 

Bali wewe, mtu wa Mungu, uyakimbie mambo hayo; ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole,” 1Tim 6:11

na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao,” Lk 8:2a, 3b

TAFAKARI: “Wewe mtu wa Mungu, ukafuate haki, utauwa, Imani, upendo, saburi, na upole; ndiyo uzima wa milele ulioitiwa.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, ni ukweli usiyotia shaka kwamba maisha ya kila mtu yanaongozwa na kitu fulani. Kwa mtazamo huu haijalishi wewe ni Mkleri, Mtawa au Mlei. Kila mmoja kadri ya wito wake atafakari haya kwa undani. Ndugu msafiri mwenzangu, tukirejea kidogo na hasa katika kamusi nyingi hufafanua neno "ongoza" (drive) kama "kuongoza, kutawala, kuelekeza." Kwa hiyo, unapokuwa kwa mfano unaongoza gari, unachokifanya ni kuongoza, kutawala na kuelekeza kwa wakati huo. Je, ni nguvu gani inayoongoza maisha yako? Sasa hivi unaweza kuongozwa na tatizo, msukumo fulani, au tarehe ya mwisho kwa kitu fulani. Unaweza kuongozwa na kumbukumbu ya jambo fulani linaloumiza, hofu mbaya, au imani ya ndani. Kuna mamia ya hali mbalimbali, mambo muhimu, na hisia ambavyo vyaweza kukuongoza. Hata hivyo, kuna mambo matano ambayo ni ya kawaida kwa wengi.

1. Watu tulio wengi huongozwa na hatia.
Watu hawa hutumia muda wa maisha yao yote wakiepuka lawama na kuficha aibu. Watu wanaoongozwa na hatia wanaonewa sana na kumbukumbu. Wanaruhusu mambo yaliyopita kutawala mambo yao ya usoni.Wanajiadhibu bila kujua kwa kuharibu mafanikio yao. Kaini alipotenda dhambi, hatia yake ilimtenga na Mungu, na Mungu akasema, "utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake; utakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani," Mwa 4:12. Hali hii inawaeleza jinsi watu wengi walivyo siku hizi-wanatangatanga katika maisha bila lengo. Mfano mzuri angalia katika vyama vyetu vya kitume. Wapo walio wengi huama chama kimoja cha kitume kwenda kingine na mwisho huishia katika nyumba za sala. Nyumba za sala hapa ninamaanisha vijikanisa vinavyojiibua na kujiinua kwa wachungaji wao kuwa manabii.

Ndugu yangu, sisi ni matokeo ya muda wetu uliopita lakini hatupaswi kuwa wafungwa wa muda huo. Kusudi la Mungu halifungwi na muda wako uliopita. Ona! Alimbadilisha muuaji Musa na kuwa kiongozi mzuri; akambadilisha Gidioni aliyekuwa mwoga akawa shujaa na hodari; anaweza kufanya mambo ya ajabu na maisha yako yaliyobaki. Tazama pia maisha ya Mt. Augustino wa Hippo kabla na baada ya kuongoka kwake.

Mungu ni mtaalam wa kutupa mawazo mapya. "Heri aliyesamehewa dhambi, na kusitiriwa makosa yake," Zab 32:1. Kwa maana nyingine twaweza kusema, "wana furaha kubwa wale waliosamehewa hatia zao. Na wana amani wale waliotubu dhambi zao na Mungu amefuta mashtaka yao."

2. Watu tulio wengi wanaongozwa na chuki na hasira.
Ndugu zangu, wapo wanaoshikilia maumivu (machungu) bila kuyaacha. Badala ya kutoka katika maumivu kwa kusamehe, wanaendelea kuyakumbuka katika mawazo yao tena na tena. Baadhi ya watu wanaongozwa na chuki kutunza ndani uchungu wao, na wengine huwalipukia watu wengine. Hali zote hizi si nzuri na hazisaidii maishani. Chuki mara nyingi huleta maumivu kwako kuliko yule unayemchukia. Mtu aliyekukosea anaweza kuwa amesahau lile kosa na anaendelea na maisha yake vizuri, wewe unaendelea kuumia na kuhangaika na yaliyopita.

Sikiliza ndugu yangu: Wale waliokuumiza wakati uliopita hawawezi kuendelea kufanya hivyo sasa "isipokuwa" kama utaendelea kutunza uchungu. Yaliyopita yamepita! Hakuna kitakachoyabadilisha. Unajiumiza tu na uchungu wako. Kwa ajili yako, jifunze kutokana na hilo na kisha achana nalo. Maandiko matakatifu yanatukumbusha kuwa, "kwani hasira humwua mtu mpumbavu, nao wivu humwua mjinga." Ayu 5:2.  Kuwa na hofu kiasi cha kufa kwa sababu ya uchungu ni upumbavu, ni kitu kipumbavu kukifanya. Ndugu, kwa nini wajifungia katika tanuru hili?

3. Watu walio wengi wanaongozwa na woga.
Ndugu, woga hapa unaweza kutokana na jambo baya sana lililokupata au lililowapata, matarajio yasiyotekelezeka, kukulia katika jamaa isiyo na uhuru, au hata maumbile ya asili. Bila kujua sababu, watu wanaongozwa na woga mara nyingi hupitwa na nafasi kubwa kwa sababu wanaogopa kuchukua hatua. Badala yake wanajitahidi kuwa salama, wakiepuka hasara na hivyo hujaribu kulinda hadhi yao. Woga ni kifungo ambacho mtu hujifunga mwenyewe na chaweza kukuzuia kuwa mtu yule ambaye Mungu anapenda uwe.

Unatakiwa kutoka humo kwa silaha ya IMANI na UPENDO. "Katika pendo hamna hofu; lakini pendo lililo kamili huitupa nje hofu, kwa maana hofu ina adhabu, na mwenye hofu hakukamilishwa katika pendo." 1Yoh 4:18. Kwa maneno mengine, upendo halisi huiondoa hofu kwa kuwa hofu hulemaza, maisha ya hofu-hofu ni ya kifo, hofu ya hukumu- ni maisha ambayo hayajakamilika katika upendo.

4. Watu wengi wanaongozwa na mali
Wapendwa tupo pamoja? Tamaa yao ya kupata vitu linakuwa ndilo lengo la maisha yao yote. Jambo hili haijalishi upo utawani au kwenye maisha ya ndoa. Msukumo huu wa kutaka zaidi kila siku una misingi yake katika udanganyifu wa kuwa nikiwa na vingi nitakuwa na furaha zaidi, nitakuwa wa muhimu, na nitakuwa salama; lakini mawazo hayo yote matatu si ya kweli. “Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu,” 1Tim 6:9. Mali huleta furaha ya "muda mfupi tu." Na sababu kubwa ndugu yangu, vitu havibadiliki, hivyo vinatuchosha na tunataka vipya, vikubwa, na bora zaidi.

Kuna imani pia kwamba nitapata mali nyingi nitakuwa wa muhimu. Umuhimu wako na umuhimu unaotegemea ulivyo navyo ndugu yangu ni vitu viwili tofauti. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” 1Tim 6:10. Thamani yako haitegemei mali zako, Mungu anasema kitu cha muhimu maishani mwako si vitu! Imani ya watu wengi kuhusu fedha ni kwamba kuwa nazo nyingi kutanipa usalama. Huwezi! Tulio utawani hatuchoki kuwa na tumiradi binafsi twa siri twingiiii. Usicheke ndiyo ukweli kwa baadhi yetu. Mambo yanapokwenda vibaya kwenye huto tumiradi tupresha twa kupanda na kushuka hatukomi.

Ndugu yangu, utajiri unaweza kupotezwa mara moja kwa sababu zisizozuilika. Usalama halisi unaweza kupatikana katika kile ambacho huwezi kunyang'anywa yaani uhusiano wako na Mungu. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu,” 1Tim 6:7. Mt. Augustino anatuwasa kutoka kwenye kanuni yake, "kuna furaha kubwa kuwa na vichache kuliko kuwa na vingi." Hata hivyo tatizo hapa ni kipimo cha huo uchache na huo wingi.

5. Watu wengi wanaongozwa na kutaka sifa
Ndugu yangu, wakati mwingine watu hawa wanaruhusu matarajio ya wazazi, waume, au wake, watoto, waalimu au rafiki zao kutawala maisha yao. Watu wazima bado wanajaribu kupata sifa kwa wazazi wao ambao hawajafurahi kamwe. Wengine wanasukumwa na vikundi vya marafiki, wanahofu wenzao watawafikiriaje. Kwa bahati mbaya, wale wafuatao kundi au maoni ya mtu binafsi hupotea ndani yake. Ndugu yangu, kwa nini kujifungia katika gereza hili la fikra na maoni? Mtu awaye yote akifundisha elimu nyingine, wala hayakubali maneno yenye uzima ya Bwana wetu Yesu Kristo, wala mafundisho yapatanayo na utauwa, amejivuna,” ITim 6:3-4b. Sifa yetu kubwa ni kulitenda lile alilofundisha Bwana wetu Yesu Kristo kwani ndilo lenye uzima wa milele.

Ndugu yangu, sijui funguo zote za mafanikio, lakini ufunguo mmoja wa kushindwa ni kujaribu kumpendeza kila mtu. Kutawaliwa na maoni ya watu wengine ni njia wazi ya kukosa makusudi ya Mungu katika maisha yako. Bwana wetu Yesu Kristo anatupa angalisho kwa jambo hili, "hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu, ama atashindana na huyu na kumdharau huyu: hamwezi kumtumikia Mungu na mali." Mt 6:24.

Kuna nguvu nyingi zinazoweza kuongoza maisha yako lakini zote mwisho wake ni mfu: kutotumia vipawa ulivyo navyo, mahangaiko ya moyo, na maisha yasiyo ya utoshelevu. Bali wewe, mtu wa Mungu, uyakimbie mambo hayo; ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole,” 1Tim 6:11. Kuishi katika mfumo huu ndiko kutakako kupa amani ya kweli na utulivu wa ndani.

Ndugu yangu, kuishi maisha yanayoongozwa na malengo, ni kutawaliwa, na kuelekezwa na makusudi ya Mungu. Hakuna kitu cha muhimu zaidi kama kujua malengo ya Mungu kwa maisha yako, na hakuna mbadala kwa hilo-siyo mafanikio, utajiri, kujulikana, au anasa. Bila malengo, maisha ni mwendo usio na maana, shughuli bila mwelekeo, na matukio bila sababu. Bila malengo, maisha ni kitu duni, kidogo sana, kisicho na umuhimu wowote.

Wapendwa wana wa Mungu, Injili ya leo inatufundisha jambo la muhimu sana kuhusu maisha yetu ya kiroho na mali tulizonazo. Ukweli ni kwamba, waliokwisha kupata neema, baraka na uponyaji ni wale tu walijinyenyekesha kwa Kristo mwanakondoo wa Mungu, na kumtumikia kwa mali zao. Na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao,” Lk 8:2a, 3b. Je, kuna uhusiano wa namna gani kati ya maisha yako ya kiroho na mali ulizokuwa nazo?

Tumsifu Yesu Kristo!

EE YESU KWETU WATOSHA. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario