JUMAPILI
YA 26 YA MWAKA-B
27/9/2015
Somo
I: Hes 11:25-29
Zab:
18:8, 10, 12-14
Somo
II: Yak 5:1-6
Injili:
Mk 9:38-43, 45, 47-48
Nukuu:
“Yoshua mwana wa Nuni,
mtumishi wa Musa tangu ujana wake, akajibu akasema, Ee bwana wangu Musa,
uwakataze,” Hes 11:28
“Musa akamwambia, Je! Umekuwa
na wivu kwa ajili yangu; ingekuwa heri kama watu wote wa Bwana wangekuwa
manabii na kama Bwana angewatia roho yake,” Hes 11:29
“Yohana akamjibu,
akamwambia, Mwalimu, tulimwona mtu akitoa pepo kwa jina lako, ambaye hafuatani
nasi; tukamkataza, kwa sababu hafuatani nasi,” Mk 9:38
“Yesu akasema,
Msimkataze, kwa kuwa hakuna mtu atakayefanya mwujiza kwa jina langu akaweza
mara kuninenea mabaya; kwa sababu
asiye kinyume chetu, yu upande wetu,” Mk 9:39-40
“Na ye yote
atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la
kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini,” Mk 9:42
“Na mkono wako
ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima u kigutu, kuliko kuwa na
mikono miwili, na kwenda zako jehanum, kwenye moto usiozimika,” Mk 9:43
“Na mguu wako
ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima, u kiwete, kuliko kuwa na
miguu miwili, na kutupwa katika jehanum,” Mk 9:45
“Na jicho lako
likikukosesha, ling'oe, ulitupe; ni afadhali kuingia katika ufalme wa Mungu,
una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum,” Mk 9:47
“Dhahabu yenu na fedha
yenu zimeingia kutu, na kutu yake itawashuhudia, nayo itakula miili yenu kama
moto. Mmejiwekea akiba katika siku za mwisho,” Yak 5:3
“Mmefanya anasa katika
dunia, na kujifurahisha kwa tamaa; mmejilisha mioyo yenu kama siku ya
machinjo,” Yak 5:5
TAFAKARI:
“Na tuwe wafadhili sisi kwa sisi, tuone mazuri kwa
wenzetu na vipaji vyao, tuwe wenye huruma, tukisameheana kama na Mungu katika
Kristo alivyotusamehe sisi.”
Wapendwa wana wa Mungu,
karibuni katika tafakari yetu ya leo. Leo Mama Kanisa katika dominika hii ya 26
ya mwaka “B,” anatualika tutafakari kwa undani mahusiano yetu na wenzetu hasa
akitutaka tuyaone mazuri kwa wenzetu ikiwa ni pamoja na vipaji na karama zao,
tuwe wafadhili sisi kwa sisi, tuwe wenye huruma, na tusameheane kama na Mungu
katika Kristo alivyotusamehe sisi.
Mara nyingi kwa
wasioongozwa na hofu ya Mungu ni vigumu kuona mazuri kutoka kwa wengine. Ni
katika mazingira haya tunapozungumzia swala zima la mtu kuwa na wivu. Wivu kama
wivu siyo kitu kibaya. Wivu ikiwa ni tokeo la nafsi kutawaliwa na hisia, ni
kama kioo cha kujitazama na kujiona vizuri mara baada ya kuona utofauti wa
kweli kati yako na wenzako na mazingira yanayokuzunguka. Hivyo tendo hilo
huweza kukuongoza kuliko kwema na haki, kujipima uwezo wako, na fursa zote
zinazokuzunguka ikiwa ni kiashirio cha kufanya vizuri zaidi endapo nafsi hivyo
itaegemea roho. Wivu katika maana hii utuelekeza katika maendeleo. Na huu ndio
wivu wa maendeleo. Wivu huwa shahuku ya kufanya vizuri zaidi bila kumdhuru
mwenzako kwa hali yoyote ile, na mazingira yanayokuzunguka unapoyachukulia kama
fursa ya kufika pale mazuri na pema zaidi.
Ni hatari sana wivu
unapotupeleka katika hali ya chuki na hasira kwa wengine na mazingira yanayotuzunguka.
Wivu huu ni tokea la nafsi inapoegemea mwili na matendo yake. Tatizo kubwa hapa
ni pale tunaposhindwa kujipokea kama tulivyo na kuanza hapo tulipo kuzonga
mbele. Hata kama chumba hakina mwanga haitoshi kulalamika tu kwa ukweli huo
bila kufanya cho chote kadiri ya mazingira uliyonayo kama fursa pekee. Kama
hakuna umeme basi uwashe angalao mshumaa. Na kama hakuna mshumaa washa basi
hata kijinga cha moto. Na kama hakuna mshumaa na kijinga cha moto, fungua basi
hata madirisha uweze kunufaika na mwanga wa mbalamwezi kutoka nje.
Wivu wa kubomoa, yaani
unaoongozwa na chuki na hasiri kwa vile tu mwenzangu anafanya vizuri kuliko
mimi, ni hatari sana kwani hali hiyo itakudumaza mwili, akili, na roho. Somo
letu la kwanza kutoka kitabu cha hesabu, na Injili yanaongelea vizuri sana
kuhusu wivu na athari zake. Kila mmoja wetu amejaliwa kwa namna ya pekee vipawa
mbalimbali. Tatizo letu kubwa ni pale tunapopoteza muda mwingi kunakili vipaji
vya wengine na kuacha kuendeleza vile alivyotupatia Mungu. Tunapenda sana kuwa
vivuli vya wengine. Hakika kwa hali hii lazima uwe tayari kudumaa mwili, akili,
na roho. Tunaona katika somo la kwanza kwamba Mungu mwenye uwezo wote, na
mwenye kumpa kila mmoja wetu kadiri apendavyo, anashuka na kutoa sehemu ya roho
iliyokuwa juu ya Musa na kuwapa watu wengine kwa muda fulani tu kadiri
alivyoona inampendeza. Hata baada ya muda huo kwisha, walionekana watu wawili
hemani, Eldadi na Medadi wakiwa bado wana upako wa kutabiri. Jambo hili
linakuwa chukizo kwa Yoshua, na anamkaripia Musa kwa kusema, “Ee bwana wangu Musa, uwakataze,” Hes 11:28. Musa kwa
kuelewa sisi sote katika umoja na
utofauti wetu ndio uzuri wa Mungu, anamjibu Yoshua na kumwambia, “Je!
Umekuwa na wivu kwa ajili yangu; ingekuwa heri kama watu wote wa Bwana
wangekuwa manabii na kama Bwana angewatia roho yake,” Hes 11:29. Ndugu yangu
kwa nini basi mara kwa mara unajisikia vibaya mwenzako anavyofanya vizuri?
Wapendwa
wana wa Mungu, tunaona tukio kama hili kwenye somo la injili. Tunaona Yohana
anamkataza mtu mmoja aliyekemea pepo kwa kutumia jina la Yesu. Wakati mwingine
tunapoongozwa na roho ya wivu hujikuta tunajihesabia haki pasipo haki yo yote.
Naye anamwambia Yesu, “Mwalimu, tulimwona mtu akitoa pepo kwa jina lako, ambaye
hafuatani nasi; tukamkataza, kwa sababu hafuatani nasi,” Mk 9:38. Yohana
anapotoa taarifa hii mbele ya Yesu, anakutana na karipio zito kutoka kwa Yesu. Yesu anajibu na kuwaambia, “Msimkataze,
kwa kuwa hakuna mtu atakayefanya mwujiza kwa jina langu akaweza mara kuninenea
mabaya; kwa sababu asiye kinyume chetu,
yu upande wetu,” Mk 9:39-40. Hapa Yesu anatufundisha uzuri wa umoja wetu katika
utofauti wetu kama wana wa Mungu. Hivyo yatupasa kutakiana mema na hasa
kutambua vipaji vya wenzetu kwa ajili ya manufaa ya wote. Huu ndio utendaji wa
Mungu. Hivyo tunawaswa kujihadhari sana na ile dhambi ya kuwakwaza wengine
wafanyapo mema. Hivyo Yesu anasema, “Na ye yote
atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la
kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini,” Mk 9:42. Kufungiwa jiwa shingoni
na kutupwa haharini kulimaanisha kwamba kwa kosa hilo la kukwaza ilitosha
kutokuonekana katika sura ya dunia na hata masalia ya mwili wako. Tunajua wazi
kwamba mtu akifa maji huzama na mwisho wa siku mwili wake uelea juu. Kwa
kufungiwa jiwe shingoni kusinge ufanya mwili uelee juu ya maji.
Wapendwa
wana wa Mungu, Bwana wetu Yesu Kristo anaenda mbali zaidi akigusia dhambi zile
ambazo huwa vichocheo vya kuwa na wivu na kuzama zaidi katika dhambi. Hivyo ili
tuwe mikono salama yatupasa kuachana na mizizi hiyo ya dhambi. Hivyo kama mkono
wako ndio sababu ya kuikosa mbingi afadhali usiwe na mkono huo. “Na mkono wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika
uzima u kigutu, kuliko kuwa na mikono miwili, na kwenda zako jehanum, kwenye
moto usiozimika,” Mk 9:43. Mkono hapa unaweza kutafsiriwa kama ukarimu wetu kwa
wenzetu. Hivyo uchoyo ukiwa ndio sababu ya kukosa mbingu ni fadhali kuachana na
tabia hiyo. Tuwe wakarimu kwa watu wote bila kubaguana.
Na endapo
mguu wako unakuwa sababu yakutokuiona mbingu ni aheri kutokuwa na mguu huu. “Na mguu wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika
uzima, u kiwete, kuliko kuwa na miguu miwili, na kutupwa katika jehanum,” Mk
9:45. Kwa kutumia miguu yetu twaweza kuwafikia watu na kuhubiri habari njema
kwao. Hivyo tendo hili twaweza kuwa wawakilishi wazuri wa Kristo kama
wamisionari. Vile vile kwa miguu yetu twaweza kuwa waenezaji wabaya sana wa
habari mbaya kama umbea na hivyo kule machafuko na kutokuelewana katika jamii.
Kama hili linajitokeza twatupasa kuwa makini sana. Yatupasa kuwa chombo cha
amani ya Bwana kama asemavyo Mt. Franscisko wa Assis.
Ndugu
yangu, na endapo jicho lako litakuwa sababu ya kutokuurithi ufalme wa mbinguni,
ni aheri ukawa chongo. “Na jicho lako likikukosesha, ling'oe, ulitupe; ni afadhali kuingia
katika ufalme wa Mungu, una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa
katika jehanum,” Mk 9:47. Kupitia jito tunaona na kutamani. Kupitia jicho
tunaona na kuongoka. Kupitia jicho tunaona na kumtukuza Mungu kwa uzuri wa
uumbaji wake. Lakini jicho lako likiwa sababu ya wivu na chuku kwa wengine,
basi jicho hilo halikufai. Jicho hili litusaidie kuona mahangaiko na shida za
watu wengine pia. Hatupaswi kufumba macho tunapoona haki za watu zinakanyagwa.
Mtume
Yakoba katika somo letu la pili anaongelea sana kuhusu kutokutaabikiana sisi
kwa sisi. Ni vyema kuona uhalisia wa maisha ya watu na kuwapa kadiri ya mapato
yao alisi na staha zao za kazi. Matajiri wengi na watu wenye uwezo hawachoki
kuwanyonya wanyonge. Wanyonge hutumikishwa kazi ngumu na kwa muda mrefu na
mwisho wa siku wanalipwa kidogo sana na kisichoweza kukidhi mahitaji yao
halisi. Hivyo Yakobo anawapa onyo matajiri na makabaila, “Dhahabu yenu na fedha yenu zimeingia kutu, na kutu yake
itawashuhudia, nayo itakula miili yenu kama moto. Mmejiwekea akiba katika siku
za mwisho,” Yak 5:3. Utajiri wo wote ule unaotokana na dhuluma hakika ni laana
kubwa sana kwa Mungu. Katika mazingira ya kawaida, watetezi wa wanyonge ni
viongozi wale tuliowapa dhamana katika uongozi. Lakini kitu cha kushangaza ni pale
tunapoona viongozi wakijinufaisha wenyewe na kuwadhulumu wanyonge wakiungana na
matajiri na makabaila ndani na nje ya nchi. “Mmefanya anasa katika
dunia, na kujifurahisha kwa tamaa; mmejilisha mioyo yenu kama siku ya
machinjo,” Yak 5:5. Je, leo katika Taifa letu wanyonge wana heri yo yote? Je, nina mchango
gani katika ukweli huu? Yatupasa tufika mahali na kuona ukweli kama ulivyo na
daima tutende kwa haki bila kubaguana. Ili kutoka kwenye ombwe hili la uongozi
na mfumo mbaya wa kuwanyonya wanyonge yatupasa kila mmoja wetu kutambua ukweli
wa tatizo kama jamii moja, na pia kutambua uwezo, vipaji na karama za wengine.
Hivyo kwa umoja wetu tunaweza kuurekebisha na kuutoa kabisa mfumo kandamizi
katika jamii yetu. Uovu hauwezi kudumu milele.
Na mwisho wa uovu ni aibu.
Devotha
ni binti mwenye akili na karama nyingi.
Kutokana na karama zake hizo aliona inafaa na kumpendeza Mungu kama angejiunga
na maisha ya kitawa ili awe na nafasi nzuri zaidi kuvitoa vipaji vyake kwa
wengi. Hakika aliona kwa njia hii anaweza kufikika kwa wengi na ni kwa namna
hiyo Kristo angejulikana kwa wengi.
Baada ya
kumaliza kidato cha sita akiwa amefaulu vizuri masomo yake ya sayansi (PCB),
alishauriana na wazazi wake kuhusu nia yake hiyo na kupata baraka zote kwa kile
alichopenda kuwa katika maisha yake. Kwa upande wa Devotha alifarijika sana na
uelewa wa wazazi wake. Hivyo Devotha alijiunga na shirika moja la kitawa ambalo
karama na huduma zao huwa mashuleni na mahospitalini.
Dada
Devotha alipita vizuri katika hatua za mwanzo, yaani, ukandidati na
upostulanti, hivyo akachaguliwa kuendelea na unovisi. Unovisi ni hatua muhimu
sana kwa maisha ya kitawa, na baada ya hatua hii ilimpasa kuweka nadhiri za
mwanzo kwa muda wa mwaka mmoja. Hatua hii ilikuwa na changamoto sana kwa
Devotha. Devotha hakukata tamaa licha ya kutoelewana vizuri na Mlezi wake.
Hofu ya
Mlezi wake ilikuwa kwamba kwa uwezo wa akili na karama alizokuwa nazo Devotha
vingeweza kumtia kiburi na baadaye kutokuendelea na maisha ya kitawa.
Kilichompoza Devotha ni kule kuwa wazi na kusema alichoona ni kweli na haki
bila kumkwaza ye yote. Hivyo hali hii ilimletea shida sana Devotha. Wiki moja
kabla ya kufunga nadhiri wakiwa jumla ya wanovisi saba, Devotha alitwa na
kupewa ujumbe huu na mlezi wake: “Devotha, baada ya mashauriano na wengine
katika nyumba hii yetu ya unovisi, nimeonelea kwa dhamiri yangu safi kwamba
huwezi kuendelea na maisha haya ya kitawa. Hivyo, unaweza kuwa mama mzuri tu
katika Taifa la wana wa Mungu. Kwa maana hiyo, hutakuwa mmoja ya wale wenzako
sita watakao funga nadhiri wiki ijayo. Mungu anguangazie zaidi katika maisha
yako. Kwaheri na wasalimie wazazi wako.”
Devotha
alipokea kwa masikitiko makubwa sana habari ile. Hata hivyo alijipa moyo sana na
kusema, “Ee Bwana wafahamu nia yangu tangu nikiwa mdogo. Hata sasa sijabadili
nia yangu na ninaona maisha haya ndiyo ninayoweza kutimiza ndoto yangu. Ee Mama
Bikira Maria na Mwanao Yesu Kristo msiniache.” Sala hii ilimpa ujasiri sana
Devotha. Hivyo siku iliyofuata Devotha aliondoka utawani.
Miaka
kumi na nane baadaye, Devotha alikwisha maliza masomo yake ya udaktari na kuwa
Dactari bingwa wa upasuaji na magonjwa ya watoto na akina mama. Akiwa
anajiandaa kuelekea uwanja wa ndege majira ya saa saba mchana kwa ajili ya
safari ya saa kumi na moja jioni kuelekea Marekani kwa semina ya wiki moja,
Devotha alipigiwa simu na kuitajika haraka sana katika chumba cha upasuaji.
Basi Dr.
Devotha alikimbia haraka na kuingia moja kwa moja katika chumba cha upasuaji
alipokuwa ameandaliwa mgonjwa yule. Basi baada ya upasuaji ule uliochukua
takribani masaa mawili na kufanikiwa, ndipo Devotha alipopewa yaliyojiri
kuhusua mgonjwa yule. Kwa ufupi hapakuwa na dactari mwingine wa kufanya
upasuaji wa ugonjwa ule isipokuwa Dr. Devotha. Ni yeye tu aliyekuwa na uwezo wa
kufanya upasuaji ule, na kama isingekuwa hivyo mgonjwa yule angefariki masaa
machache baadaye.
Baada ya
maelezo yale kutoka kwa madaktari wasaidizi,
Dr. Devotha alipenda kumjua mgonjwa yule. Jambo la furaha na kusikitisha
mgonjwa yule alikuwa Mlezi wake wa unovisi miaka 18 iliyopita. Mkuu wa shirika
lile akiwa na masista wengine alitoa shukrani zake kwa niaba ya Sista aliyepata
upasuaji ule, kwa kusema, “tunajisikia furaha sana kwa uwepo wako na vipaji
vyako Mungu alivyokujalia. Kwa upande wetu kama shirika tunachoweza kusema leo
labda lilikuwa kosa lenye bahati kukuondoa utawani. Tunaomba utusamehe kwa
yaliyokwisha tokea na Mungu akutumie vizuri zaidi kwa wengine wenye shida kama
hii iliyompata sista wetu.” “Nami najisikia furaha kubwa sana kutoa huduma kwa
Mlezi wangu. Haya yote nayaona kama mpango wa Mungu kunikutanisha na Mlezi
wangu ambaye hakuweza kunifahamu vizuri. Nami nilishayasamehe yote miaka 18
iliyopita. Nimeweka nadhiri mbele ya Mungu kuwa mlei mmisionari maisha yangu
yote. Asanteni masista yanipasa kusafiri hapo saa kumi na moja jioni hii
kuelekea Marekani. Tutaonana tena Mungu akipenda. Kwa herini,” Dr. Devotha
aliwaaga masista wale kwa furaha na tabasamu la afya.
Wapendwa
wana wa Mungu, mwisho wa chuki, wivu, ubaya na uovu ni AIBU. Usiacha
kutenda mema daima.
Tumsifu
Yesu Kristo!
EE
YESU TUFANYE VYOMBO VYA AMANI YAKO DAIMA. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario