jueves, 10 de septiembre de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 23 YA MWAKA-B

IJUMAA WIKI YA 23 YA MWAKA-B
11/9/2015
Somo: 1Tim 1:1-2, 12-14
Zab: 15:1-2, 5-8, 11
Injili: Lk 6:39-42
Nukuu:
Nami namshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenitia nguvu kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu, akaniweka katika utumishi wake; ingawa hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri, lakini nalipata rehema kwa kuwa nalitenda hivyo kwa ujinga, na kwa kutokuwa na imani,” 1 Tim 1:12-13

“Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe, ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi kilichomo katika jicho la ndugu yako,” Lk 6:42b
TAFAKARI: “Bado unayo nafasi ya kujirudi kutoka ukengeufu wa Imana. Huko ndiko kuongoka kuliko kwa kweli.”

Wapendwa wana wa Mungu, kama wewe umebatizwa elewa kuwa unaishi ndani ya wokovu aliotupatia Bwana wetu Yesu Kristo kwa kifo chake pale msalabani. Ni jambo la kusikitisha sana kwamba tulio wengi hatuoni thamani ya wokovu huu tuliopewa bure kwa upendo wa Mungu Baba kupitia mwanaye Yesu Kristo. Tendo hili kwetu ni heshima kubwa sana, kwani tumenyanyuliwa katika udogo wetu na kuinuliwa palipo juu kabisa alipo Kristo na Mungu wetu.

Ndugu yangu, licha ya mastahili haya aliyopewa wanadamu, Mungu hakumuondolea mwanadamu huyu uhuru wake wa kuamua kutenda yaliyo mazuri au mabaya. Uhuru tuliopewa na mwenyezi Mungu ni changamoto kubwa sana katika kuiishi Imani yetu. Uhuru huu mara nyingi unatutoa katika mstari wa kuyaishi yale yampendezayo Mungu. Ni kwa kupitia uhuru huu pia tunaweza kuziacha njia zetu mbaya na kumrudia Mungu kwa toba na majuto. Hivyo basi, kila siku ya maisha yetu tunaitwa katika wongofu wa roho zetu. Siyo kuokoka, bali kuongoka kwani wokovu kesha tupatia Kristo. Wokovu ambao ni uwezekano wa kufanywa wana wa Mungu kesha tupatia Kristo mwenyewe kwa sadaka ya mateso na kifo chake pale msalabani. Hivyo yatupasa kuziishi ahadi zetu za ubatizo muda wote wa maisha yetu hapa duniani.

Kukengeuka kwetu na kunakotufanya kuwa nje ya Imani yetu kunatokana kwanza kabisa na ujinga wetu, yaani kutokujua dhamani ya Imani yetu, na lengo lake katika safari ile ielekeayo katika uzima wa milele. Mtume Paulo ni mmoja ya watu walioishi vibaya na baada ya kujitambua, hasa pale alipojeuzwa na Kristo anayasema haya kinabaugaba. Nami namshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenitia nguvu kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu, akaniweka katika utumishi wake; ingawa hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri, lakini nalipata rehema kwa kuwa nalitenda hivyo kwa ujinga, na kwa kutokuwa na imani,” 1 Tim 1:12-13. Tendo hili ndilo lijulikanalo kama KUONGOKA. Mt. Augustino ni mfano mwingine wa wale walioacha njia zao mbaya na kuongoka. Tusomapo kitabu chake cha Maungamo tunaona wazi tendo hili la kuongoka. Mt. Augustino ana fafanua kwa undani alivyoutafuta ukweli sehemu mbalimbali na kusahau kuwa ukweli huo alikuwa nao ndani yake. Alipoigusa neema ile ya wokovu wa Kristo ndani yake yote yalifunuliwa na akawa mpya ndani na katika Kristo.

Pili, kukengeuka kwetu katika Imani kunatokana na unafiki wetu. Kwa ufupi unafiki ni kuujua ukweli ulivyo lakini kutokana na mazingira au mtazamo wa watu, mhusika anaukwepa ukweli ule na kuishi kadiri na mazingira yale na mitazamo ya watu wale ili kuwapendezesha au kuwafurahisha. Kwa upande mwingine ni kuishi kile usicho na kukubali kuwa kivuli cha kitu ambacho sicho ulicho. Ili urudi katika mstari ulioukwepa, yaani Imani ya kweli, itakupasa kuurudia ukweli kama ulivyo na kwa kufanya hivyo utaweza kusonga mbele na kuwa nuru na mwanga kwa wengine. Jambo hili Yesu Kristo analikemea kwa nguvu zote na bila kupepesa macho. Wenye tabia kama hizi Yesu Kristo hana haya kutuambia hivi; “Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe, ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi kilichomo katika jicho la ndugu yako,” Lk 6:42b. Yesu amewafananisha watu wa mtindo huu kwa nyakati mbalimbali kama vipofu na makaburi yaliyopakwa chokaa. Ole kwa waandishi na mafarisayo tunasoma vizuri habari hii kutoka mwinjili Mathayo hasa ile sura ya 23 yote.

Ndugu yangu, kama wewe leo una taaluma yoyote ile na ukashindwa kutoa huduma kadiri ya taaluma yako kwa wale wanaohitaji huduma hiyo, jua kwamba tendo hilo ni mwelekeo wa ukengeufu wa kile ulichosomea, na mwisho wa siku tendo hilo litahathiri Imani yako kwa kiwango hicho hicho. Jambo hili likikutokea huwezi kukwapa tuhuma na lawama za kuwa mnafiki, na huna tofauti na waandishi na mafarisayo wa nyakati zile za Yesu. Basi kama mimi ni mwalimu wa dini, mwanasheria, Bwana afya, mwalimu, Mwanasiasa, nk, ni wakati wa kujichunguza vizuri.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU aliyeTUtia nguvu kwa sababu ULITUona kuwa waAminifu, UkaTUweka katika utumishi wakO USITUACHE TUKENGEUKE. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario