domingo, 27 de septiembre de 2015

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 26 YA MWAKA-B

JUMATATU WIKI YA 26 YA MWAKA-B
28/9/2015
Somo: Zek 1:1-8
Zab: 101:16-23, 29
Injili: Lk 9:46-50
Nukuu:
Bwana amewakasirikia sana baba zenu,” Zek 1:2

Basi, uwaambie, Bwana wa majeshi asema hivi, Nirudieni mimi, asema Bwana wa majeshi, nami nitawarudia ninyi, asema Bwana wa majeshi,” Zek 1:3

akawaambia, Ye yote atakayempokea mtoto huyu kwa jina langu anipokea mimi; na ye yote atakayenipokea mimi ampokea yeye aliyenituma. Kwa kuwa aliye mdogo miongoni mwenu nyote huyo ndiye mkubwa,” Lk 9:48 

Yesu akamwambia, Msimkataze, kwa kuwa yeye ambaye si kinyume chenu yu upande wenu,” Lk 9:50

TAFAKARI: “Wakati ndiyo sasa.”

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna mtihani mgumu kwa mwanadamu kama kufanya maamuzi ya kina kuhusu mwelekeo mzima wa maisha yake. Mara zote binadamu amekuwa na uhakika wa jana kuliko kesho ambayo bado kufikika. Ila ukweli ni kwamba hatuwezi kuwa na kesho nzuri kama hatuna leo nzuri. Hivyo kama jana haikuwa nzuri basi itakulazimu ufanye maamuzi mazuri na ya kina leo ili kesho yako iwe nzuri. Wakati ndio sasa! Kama sijui cho chote kuhusu uhai wangu dakika chache kuanzia sasa, hivyo muda ninaoishi sasa ni muhimu sana kufanya maamuzi ya kina kwa kile ambacho kipo chini ya uwezi wangu kwa maisha yangu na vizazi vijavyo.

Mungu aliye UPENDO na kwenye kututakia MEMA daima, anakuwa sababu ya kuwafanya Waisraeli wafanye maamuzi ya kina kuhusu maisha yao na vizazi vijavyo anapowaambia kupitia Nabii Zekaria akisema, Bwana amewakasirikia sana baba zenu,” Zek 1:2. Ndugu yangu, sababu ya kufanya maamuzi hayo ni pale tunapokuwa nje ya mpango mzima wa maisha yetu na mahusiano yetu na Mungu. Hivyo wito wa Mungu kwetu ni kumrudia na kuwa na hofu hiyo ya Kimungu. Zekaria Nabii anawaambia ujumbe huu wa Mungu kwa wana wa Israeli, “Bwana wa majeshi asema hivi, Nirudieni mimi, asema Bwana wa majeshi, nami nitawarudia ninyi, asema Bwana wa majeshi,” Zek 1:3. Hakuna njia nyingine ya kuwa karibu na Mungu kama hautajisalimisha kwake. Kujisalimisha kuliko kweli ni tendo la Ibada. Tendo hili la Ibada linajulikana kama ‘kuabudu.’ Tunapofanya maabudu tunajisalimisha kwa Mungu, na kwa namna hiyo tunamrudia Mungu naye anaturudia kwa kutuneemesha upendo wake.

Wapendwa wana wa Mungu, tendo zima la kujisalimisha na kutupeleka katika maabudu kama Ibada, linatualika kwa namna ya pekee kujishusha na kujinyenyekeza mbele ya kile kilicho kikuu zaidi na chenye kusema yote kuhusu uhai wetu. Tunajinyenyekesha chini ya Mamlaka ya Mungu si kwa unyonge, bali ndiyo njia pekee ya kuwa kile tulicho na mpango wa Mungu. Kujishusha na kujinyenyekeza ndiko tunapokufanya kuwa binadamu halisi kadiri ya mpango wa Mungu na lengo la uumbaji wako. Huku ndiko kujipokea kama ulivyo. Kujipokea kama ulivyo ndiyo njia pekee ya kuanza kufanya mabadiliko ya kina kuhusu maisha yako. Mabadiliko yote yale lazima yaanze sehemu fulani. Hivyo mabadiliko ya kimwili na kiroho kumwelekea Mungu wetu, huanza pale tu tunapojipokea kama tulivyo, yaani, kujishusha, na kujinyenyekeza mbele yake aliye uhai, uzima, na umilele wetu.

Bila kufahamu ukweli huu, tunaona katika somo la injili njinsi ambavyo wanafunzi wa Yesu wakibishana njiani kuhusu ‘nani aliyemkubwa kati yao.’ Kutafuta ukubwa na ukuu bila kujua mapaswa na matakwa yake, ni chanzo kikubwa sana cha kwenda kinyume na mpango wa Mungu na watu wake. Yesu baada ya kutambua ukweli huu ndani ya mioyo ya wanafunzi wake, anawapa angalisho ya kile wanachokitamani. Naye Yesu anawaambia wanafunzi wake kwa mfano, “Ye yote atakayempokea mtoto huyu kwa jina langu anipokea mimi; na ye yote atakayenipokea mimi ampokea yeye aliyenituma. Kwa kuwa aliye mdogo miongoni mwenu nyote huyo ndiye mkubwa,” Lk 9:48. Udogo anauongelea Yesu ni ule utayari wa kujifunza, kumtegemea Mungu pasipo shaka kama afanyavyo mtoto kwa mzazi wake, kujishusha na kujinyenyekeza hasa tutoapo huduma kwa wengine pasipo kujiinua binafsi zetu.

Wapendwa wana wa Mungu, ye yote atakaye fanya tendo lo lote la upendo, matumaini, na imani hata kama si mmoja katika mtazamo wa kundi unaloishi na jumuiya unayoshirikiana nayo, mtu huyo hayupo kinyume cha matamanio ya Mungu kwetu. Jambo hili Yesu analiweka sawa anapopata taarifa ya wanafunzi wake walipomkataza mtu mmoja kutenda lililojema eti kwa vile tu hakuwa mmoja wao. Yesu akamwambia, Msimkataze, kwa kuwa yeye ambaye si kinyume chenu yu upande wenu,” Lk 9:50. Kuwa kinyume na mpango wa Mungu ni pamoja na kule kutojisalimisha kwa mtu huyo katika mpango mzima wa wokovu wa Mungu. Ni pale pia tunajiinua nafsi zetu na kusahau hatma ya maisha yetu. Ni pale pia kwa uhakika tunapojitanguliza mbele zaidi na kusahau usalama wetu upo chini na jemedari wetu Mkuu Yesu Kristo.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU NASI TUNAKUBALI KUWA WAKATI NDIYO SASA. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario