JUMATATU WIKI YA 26 YA MWAKA-B
28/9/2015
Somo: Zek 1:1-8
Zab: 101:16-23, 29
Injili: Lk 9:46-50
Nukuu:
“Bwana
amewakasirikia sana baba zenu,” Zek 1:2
“Basi, uwaambie,
Bwana wa majeshi asema hivi, Nirudieni mimi, asema Bwana wa majeshi, nami
nitawarudia ninyi, asema Bwana wa majeshi,” Zek 1:3
“akawaambia, Ye yote
atakayempokea mtoto huyu kwa jina langu anipokea mimi; na ye yote
atakayenipokea mimi ampokea yeye aliyenituma. Kwa kuwa aliye mdogo miongoni
mwenu nyote huyo ndiye mkubwa,” Lk 9:48
“Yesu akamwambia,
Msimkataze, kwa kuwa yeye ambaye si kinyume chenu yu upande wenu,” Lk 9:50
TAFAKARI: “Wakati ndiyo sasa.”
Wapendwa
wana wa Mungu, hakuna mtihani mgumu kwa mwanadamu kama kufanya maamuzi ya kina
kuhusu mwelekeo mzima wa maisha yake. Mara zote binadamu amekuwa na uhakika wa
jana kuliko kesho ambayo bado kufikika. Ila ukweli ni kwamba hatuwezi kuwa na
kesho nzuri kama hatuna leo nzuri. Hivyo kama jana haikuwa nzuri basi
itakulazimu ufanye maamuzi mazuri na ya kina leo ili kesho yako iwe nzuri.
Wakati ndio sasa! Kama sijui cho chote kuhusu uhai wangu dakika chache kuanzia
sasa, hivyo muda ninaoishi sasa ni muhimu sana kufanya maamuzi ya kina kwa kile
ambacho kipo chini ya uwezi wangu kwa maisha yangu na vizazi vijavyo.
Mungu
aliye UPENDO na kwenye kututakia MEMA daima, anakuwa sababu ya kuwafanya
Waisraeli wafanye maamuzi ya kina kuhusu maisha yao na vizazi vijavyo
anapowaambia kupitia Nabii Zekaria akisema, “Bwana
amewakasirikia sana baba zenu,” Zek 1:2. Ndugu yangu, sababu ya kufanya maamuzi
hayo ni pale tunapokuwa nje ya mpango mzima wa maisha yetu na mahusiano yetu na
Mungu. Hivyo wito wa Mungu kwetu ni kumrudia na kuwa na hofu hiyo ya Kimungu.
Zekaria Nabii anawaambia ujumbe huu wa Mungu kwa wana wa Israeli, “Bwana wa
majeshi asema hivi, Nirudieni mimi, asema Bwana wa majeshi, nami nitawarudia
ninyi, asema Bwana wa majeshi,” Zek 1:3. Hakuna njia nyingine ya kuwa karibu na
Mungu kama hautajisalimisha kwake. Kujisalimisha kuliko kweli ni tendo la
Ibada. Tendo hili la Ibada linajulikana kama ‘kuabudu.’ Tunapofanya maabudu
tunajisalimisha kwa Mungu, na kwa namna hiyo tunamrudia Mungu naye anaturudia
kwa kutuneemesha upendo wake.
Wapendwa wana wa Mungu, tendo zima la kujisalimisha na
kutupeleka katika maabudu kama Ibada, linatualika kwa namna ya pekee kujishusha
na kujinyenyekeza mbele ya kile kilicho kikuu zaidi na chenye kusema yote
kuhusu uhai wetu. Tunajinyenyekesha chini ya Mamlaka ya Mungu si kwa unyonge,
bali ndiyo njia pekee ya kuwa kile tulicho na mpango wa Mungu. Kujishusha na
kujinyenyekeza ndiko tunapokufanya kuwa binadamu halisi kadiri ya mpango wa
Mungu na lengo la uumbaji wako. Huku ndiko kujipokea kama ulivyo. Kujipokea
kama ulivyo ndiyo njia pekee ya kuanza kufanya mabadiliko ya kina kuhusu maisha
yako. Mabadiliko yote yale lazima yaanze sehemu fulani. Hivyo mabadiliko ya
kimwili na kiroho kumwelekea Mungu wetu, huanza pale tu tunapojipokea kama
tulivyo, yaani, kujishusha, na kujinyenyekeza mbele yake aliye uhai, uzima, na
umilele wetu.
Bila kufahamu ukweli huu, tunaona katika somo la injili
njinsi ambavyo wanafunzi wa Yesu wakibishana njiani kuhusu ‘nani aliyemkubwa
kati yao.’ Kutafuta ukubwa na ukuu bila kujua mapaswa na matakwa yake, ni
chanzo kikubwa sana cha kwenda kinyume na mpango wa Mungu na watu wake. Yesu
baada ya kutambua ukweli huu ndani ya mioyo ya wanafunzi wake, anawapa
angalisho ya kile wanachokitamani. Naye Yesu anawaambia wanafunzi wake kwa
mfano, “Ye yote atakayempokea mtoto huyu kwa jina langu anipokea mimi;
na ye yote atakayenipokea mimi ampokea yeye aliyenituma. Kwa kuwa aliye mdogo
miongoni mwenu nyote huyo ndiye mkubwa,” Lk 9:48. Udogo anauongelea Yesu ni ule utayari wa
kujifunza, kumtegemea Mungu pasipo shaka kama afanyavyo mtoto kwa mzazi wake,
kujishusha na kujinyenyekeza hasa tutoapo huduma kwa wengine pasipo kujiinua
binafsi zetu.
Wapendwa wana wa Mungu, ye
yote atakaye fanya tendo lo lote la upendo, matumaini, na imani hata kama si
mmoja katika mtazamo wa kundi unaloishi na jumuiya unayoshirikiana nayo, mtu
huyo hayupo kinyume cha matamanio ya Mungu kwetu. Jambo hili Yesu analiweka
sawa anapopata taarifa ya wanafunzi wake walipomkataza mtu mmoja kutenda
lililojema eti kwa vile tu hakuwa mmoja wao. “Yesu akamwambia,
Msimkataze, kwa kuwa yeye ambaye si kinyume chenu yu upande wenu,” Lk 9:50.
Kuwa kinyume na mpango wa Mungu ni pamoja na kule kutojisalimisha kwa mtu huyo
katika mpango mzima wa wokovu wa Mungu. Ni pale pia tunajiinua nafsi zetu na
kusahau hatma ya maisha yetu. Ni pale pia kwa uhakika tunapojitanguliza mbele
zaidi na kusahau usalama wetu upo chini na jemedari wetu Mkuu Yesu Kristo.
Tumsifu
Yesu Kristo!
EE
YESU NASI TUNAKUBALI KUWA WAKATI NDIYO SASA. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario