lunes, 21 de septiembre de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 25 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 25 YA MWAKA-B
22/9/2015
Somo: Ezr 6:7-8, 12, 14-20
Zab: 121:1-5
Injili: Lk 8:19-21
Nukuu:
Iacheni kazi hii ya nyumba ya Mungu, msiizuie; waacheni liwali wa Wayahudi, na wazee wa Wayahudi, waijenge nyumba hii ya Mungu mahali pake,” Ezr 6:7

Na Mungu huyu, aliyelifanya jina lake likae pale, na aangamize wafalme wote, na watu wote, watakaonyosha mikono yao kulibadili neno hili, na kuiharibu nyumba hii ya Mungu, iliyoko Yerusalemu,” Ezr 6:12

Nao wazee wa Wayahudi wakajenga, wakafanikiwa, kwa msaada wa kuhubiri kwao Hagai nabii, na Zekaria mwana wa Ido. Wakajenga, wakaimaliza kazi yao, kwa maagizo ya Mungu wa Israeli, na kwa amri ya Koreshi, na Dario, na Artashasta mfalme wa Uajemi,” Ezr 6:14

Wakawaweka makuhani katika kura zao, wakawaweka na Walawi katika zamu zao, kwa ajili ya huduma ya Mungu, iliyokuwako Yerusalemu; vile vile kama vilivyoandikwa katika chuo cha Musa,” Ezr 6:18

Kwa maana makuhani na Walawi walikuwa wamejitakasa wote pamoja; wote walikuwa hali ya tohara; wakachinja Pasaka kwa ajili ya wana wote wa uhamisho, na kwa ajili ya ndugu zao makuhani, na kwa ajili ya nafsi zao,” Ezr 6:20

Akawajibu akasema, Mama yangu na ndugu zangu ndio hao walisikiao neno la Mungu na kulifanya,” Lk 8:21

TAFAKARI: “Wale wote wenye hofu ya Mungu hubarikiwa katika mambo yao.”

Wapendwa wana wa Mungu, mwanadamu ye yote asiyekuwa na hofu ya Mungu ni hatari sana kwake yeye mwenyewe, kwa wenzake, na mazingira yake. Mwenye hofu ya Mungu hutambua mafanikio yake na madhaifu yake. Mizania hii umwongoza katika kweli na haki. Ukweli utakuwa maisha yake kwa sababu anajijua udhaifu wake na mazuri yake. Haki itakuwa kielelezo chake cha kutenda akiongozwa na upendo usiobagua kwa wale wote wanaomzunguka.

Wapendwa wana wa Mungu, faida ya kuwa na hofu ya Mungu ni kuyawaza na kuyatenda yale ya Mungu. Hofu hii hutuinua na  kuyatafuta yale yaliyo juu kule Kristo na Mungu walipo. Hatuwezi kamwe kuridhika na haya ya leo na kesho tu. Hofu ya Mungu hutusukuma kuelekea umilele. Mtume Paulo anatuwasa na kusema, “basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1. Hofu hii ya Mungu utufanya kutafuta zaidi yale yaliyo ya Mungu.

Wapendwa katika Kristo, tunaona hofu hii ya Mungu ikimsukuma Mfalme Dario katika uhamasishaji wa kujenga nyumba ya Mungu. Naye anawaambia watu wake, iacheni kazi hii ya nyumba ya Mungu, msiizuie; waacheni liwali wa Wayahudi, na wazee wa Wayahudi, waijenge nyumba hii ya Mungu mahali pake,” Ezr 6:7. Uwepo wa Hekalu kwa kumwabudu Mungu na kumtolea shukrani, uwepo wa ardhi kwa kujipatia mahitaji yao ya mwili, na uwepo wa uongozi imara, vilikuwa vithibitisho vya uwepo wa Mungu katika maisha ya Wayahudi. Hivyo kulikuwa na hitaji kubwa sana ya kuiisimamisha nyumba ya Mungu-Hekalu. Ilikuwa ni kosa kubwa na laana kwa Mungu kwa ye yote atakaye zuia mpango huu Mtakatifu. Hivyo Mfalme Dario anatoa angalisho kwa ye yote atakayezuia mpango huu.Na Mungu huyu, aliyelifanya jina lake likae pale, na aangamize wafalme wote, na watu wote, watakaonyosha mikono yao kulibadili neno hili, na kuiharibu nyumba hii ya Mungu, iliyoko Yerusalemu,” Ezr 6:12. Hofu ya Mungu utupeleka pale alipo Mungu.

Ni ukweli kwamba tunapoliona tatizo kwa pamoja ni kwa njia hiyo hiyo tatizo hilo hutatuliwa kwa wepesi zaidi. Kiongozi Imara kama Dario alikuwa kielelezo cha umoja ule Mungu aliokuwa anautaka kwa watu wake. Hivyo tamko la Mfalme Dario linapokelewa na wote na kazi ya Mungu inafanyika. Nao wazee wa Wayahudi wakajenga, wakafanikiwa, kwa msaada wa kuhubiri kwao Hagai nabii, na Zekaria mwana wa Ido. Wakajenga, wakaimaliza kazi yao, kwa maagizo ya Mungu wa Israeli, na kwa amri ya Koreshi, na Dario, na Artashasta mfalme wa Uajemi,” Ezr 6:14. Hapa tunaona mafanikio tuyapatayo tunapoongozwa na hofu ya Mungu. Wale wote wenye hofu ya Mungu hubarikiwa katika mambo yao.

Ndugu zangu, hofu ya Mungu utujengea utaratibu wa namna ya kufanya. Hapa ukweli na haki katika kuona na kutenda ujidhihirisha. Dhamiri zetu ndani utusukuma kwa lile la kweli na haki. Kila mmoja kadiri ya nafasi, uwezo, na wito wake atafanya kwa ajili ya wengine. Matokeo ya tendo hili uzaa hali ya kufaidiana kuliko kweli na haki. Hivyo, wakawaweka makuhani katika kura zao, wakawaweka na Walawi katika zamu zao, kwa ajili ya huduma ya Mungu, iliyokuwako Yerusalemu; vile vile kama vilivyoandikwa katika chuo cha Musa,” Ezr 6:18. Huku pia ndiko kuongozwa kwa ufunuo wa Roho na mapendo ya kweli. Ni kwa namna hii, “kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yule yule,” 1Kor 12:7-8. Kwa maana nyingine kila mmoja wetu atakuwa kile alicho na makusudi na Mungu katika kuumbwa kwake, yaani, kumjua Mungu, kumpenda Mungu, kumtumikia Mungu, na mwisho turudi kwake mbinguni kwenye umilele.

Wapendwa wana wa Mungu, tunapokuwa kweli kile tulicho, kikiambatana na makusudi ya Mungu katika uumbaji wetu, maisha huwa tendo la shukrani kwa Mungu kila tuivutapo pumzi yake. Shukrani azitoazo mwanadamu kwa muumba wake ni tendo la kusadifu yale yote ayapatayo kuwa si kwa nguvu na uweza wake mwanadamu, bali ni Mungu mwenyewe. Ni kujua kwamba yote tuyapatayo ni kwa neema zake Mungu. Kwa kutambua ukweli huu, makuhani na Walawi walikuwa wamejitakasa wote pamoja; wote walikuwa hali ya tohara; wakachinja Pasaka kwa ajili ya wana wote wa uhamisho, na kwa ajili ya ndugu zao makuhani, na kwa ajili ya nafsi zao,” Ezr 6:20. Sifa na shukrani ni kwa Mungu peke yake kwani matendo yake kwetu ni makubwa sana.

Wapendwa katika Kristo, hofu hii ya Mungu licha ya kutuongoza katika kweli, haki na upendo wa dhati, utuunganisha kuwa kitu kimoja katika Kristo. Sote huwa ndugu katika Kristo si kwa njia hii ya kibailojia, bali ufanywa ndugu kiroho na kutuvusha katika mitizamo ya kibinadamu isiyo beba umilele ule tunaoutamani. Hivyo Yesu analisema jambo hii akifafanua maana ya ndugu pale alipoletewa taarifa  ya uwepo wa Mama yake na ndugu zake wakimsubiri nje ya Hekali. Naye anasema, Mama yangu na ndugu zangu ndio hao walisikiao neno la Mungu na kulifanya,” Lk 8:21. Ni kwa hofu ya Mungu tu twaweza lisikia neno la Mungu na kulifanya. Na tunapolisikia na kulifanya neno hili la Mungu bila mawaa, baraka na neema huwa matunda yake.

Tumsifu Yesu Kristo!


Basi sasa hofu ya Bwana na iwe juu yenu; angalieni mkaifanye; kwa maana kwa Bwana, Mungu wetu, hapana uovu, wala kujali nafsi za watu, wala kupokea zawadi,” 2Nya 19:7

No hay comentarios:

Publicar un comentario