martes, 29 de septiembre de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 26 YA MWAKA-B

JUMATANO WIKI YA 26 YA MWAKA-B
30/9/2015
Somo: Neh 2:1-8
Zab: 136:1-6
Injili: Lk 9:57-62
Nukuu:
Nikamwambia mfalme, Mfalme akiona vema, na ikiwa mimi, mtumishi wako, nimepata kibali machoni pako, tafadhali unipeleke mpaka Yuda, niuendee mji wa makaburi ya baba zangu, nipate kuujenga,” Neh 2:5 

Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake,” Lk 9:58

Akamwambia Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu,” Lk 9:60  

Yesu akamwambia, Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu,” Lk 9:62

TAFAKARI: “Ni heri ukawa baridi au joto kuliko kuwa vuguvugu katika Imani.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, Imani ya mtu husema yote kuhusu maisha ya mtu. Imani siyo kitu tunwezacho kukiona kwa macho yetu ya nyama, na kukipima ukubwa na upana wake, bali Imani huonekana katika maisha mazima ya mtu ikiwa ni pamoja na changamoto zinazobeba maisha hayo ya kila siku. Nathubutu kusema kwamba sisi tulio wengi kama Wakristo na Wakatoliki kwa kiasi kikubwa tu wakristo wa majina tu, na wakati mwingine wakristo wa jumapili. Tunafika mahali na kumfanya Mungu wetu kama kituo cha msalaba mwekundu. Tunamwitaji Mungu pale tu tunapobanwa na matatizo. Hata katika hali ya matatizo tunajitoa kwake kwa masharti fulani.

Wapendwa katika Kristo, masomo yetu ya leo yanagusia kwa kiasi kikubwa nini maana ya imani na kuishi imani hiyo. Yapo mambo makuu manne tunayoweza kujifunza kuhusu Imani kutoka kwenye masomo yetu ya leo. Kwanza kabisa Imani ya kweli siyo kuwa waaminifu kwa tamaduni zetu kwa vile tu zilishikiliwa vizuri na wazee wetu kiupofu. Wakati mwingine mila zetu na desturi ni mkusanyiko wa viaminika kimazoea ambavyo mwisho wa siku havina uhalisia na uhusiano wo wote na hali halisi ya ukweli huo. Mazingira kama haya wakati mwingine yanakufanya kuwajibika kulipopita kiasi pasipo kujielewa. Mwisho wa siku tunakuwa watumwa na siyo huru tena. Hali hii tunaiona katika somo la kwanza. Nikamwambia mfalme, Mfalme akiona vema, na ikiwa mimi, mtumishi wako, nimepata kibali machoni pako, tafadhali unipeleke mpaka Yuda, niuendee mji wa makaburi ya baba zangu, nipate kuujenga,” Neh 2:5. Tunaona jinsi gani mtu huyu anavyokuwa na shauku ya kuujenga mji wa makaburi.

Lakini tukumbuke kwamba mara baada ya kufufuka Yesu, malaika wanawapa ujumbe muhimu wanawake wale waliokwenda kaburini na kumkosa Yesu. Malaika akajibu, akawaambia wale wanawake, Msiogope ninyi; kwa maana najua ya kuwa mnamtafuta Yesu aliyesulibiwa. Hayupo hapa; kwani amefufuka kama alivyosema. Njoni, mpatazame mahali alipolazwa. Nanyi nendeni upesi, mkawaambie wanafunzi wake, Amefufuka katika wafu. Tazama, awatangulia kwenda Galilaya; ndiko mtakakomwona. Haya, nimekwisha waambia,” Mt 28:5-7. Hivyo ndugu zangu Imani yetu leo inatuelekeza kuwa, Yesu huyu aliye shauku yetu tunakutana naye Galilaya na siyo kaburini. Galilaya yako ni hapo ulipo kadiri ya wito na utume wake. Ishi vyema hapo ulipo na timiza yote na hasa yale madogo madogo kwa upendo na unyenyekevu mkubwa. Hapo utakutana na Yesu. 

Jambo la pili tunalofundishwa leo kuhusu Imani, ni namna tunavyochukulia ufuasi wetu. Je, ninakiri kumfuata Yesu popote atakapo kuwa kama upepo na bendera? Je, katika ufuasi huo natambua mapaswa yake? Je, nipo imara na nitakuwa imara katika nyakati zote na hasa zile nyakati za sintofahamu? Yesu anampa angalisho mtu yule aliyekutana naye njiani na kusema yupo tayari kufuatana naye ko kote atakapokwenda. Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake,” Lk 9:58. Kwa maneno mengine Yesu anatuambia hakuna maslahi yo yote kibinadamu zaidi ya maisha ya umilele kutoka kwake. Kama ni swala la utajiri na kuwa na maisha mazuri siyo kipaumbele katika ufuasi wetu kwake. “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:9. Kazi yetu ya kwanza ni kuutafuta kwanza ufalme wa mbinguni na mengine yote tutapewa kwa ziada.

Jambo la tatu tunalofundishwa leo kuhusu Imani ya kweli ni utambuzi wa kweli na kujua nafasi ya Mungu katika maisha yako. Bila shaka hakuna asiyekuwa na hofu ya kifo. Ila kifo kipo tupende au tusipende. Na kama umezaliwa basi ipo siku utakufa. Kwa hiyo katika uhalisia wa kifo hatupaswi kukiogopa. Yatupasa kuishinda hofu ili tuwe tayari kukipokea kifo kama njia pekee ya kuishi umilele tunaojiandaa leo hapa duniani. Hakutakuwa na maisha baada ya umilele baadaye bila kupita katika fumbo hili la kifo. Hivyo Yesu anamtoa hofu ndugu yule aliyetoa hoja ya kwenda kwanza kumzika Baba yake ndipo amfuate. Naye Yesu anamwambia, “Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu,” Lk 9:60. Je, Yesu anatukataza kuwazika wazazi wetu? La hasha! Kufanya hivyo atakuwa anaenda kinyumbe na ile amri ya nne ya Mungu, “waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na Bwana, Mungu wako,” Kut 20:12. Yesu anachotaka kutuambia ni kwamba kifo ni ukweli usiopingika na hivyo shughuli zake zisiwe sababu ya kutokupokea ujumbe wake wa uzima wa milele.

Na jambo la nne na la mwisho tunalofundishwa leo kuhusu Imani ni kule kuwa na msimamo thabiti wa wito tulio nao na kile tulichoitiwa. Hii ni pamoja na kutokuwa na kigeugeu na kutazama nyumba tulipotoka kwa malengo ya kujaribu tena. Wengi wetu baada ya kubatizwa tumerudi kuishi maisha ya kipagani kabida. Wengi wamekuwa washirikina wa kupindukia na kuongozwa na nguvu za giza ili hali tumejivika visakramenti mwili mzima. Katika hili Yesu anatupa angalisho, na kusema, “Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu,” Lk 9:62. Kwa maneno mengine ni heri kuwa baridi au joto, kuliko kuwa vuguvugu katika Imani.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUPE NGUVU YA KUINUKA PALE TUNAPODONDOKA. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario