JUMATANO WIKI YA 26 YA MWAKA-B
30/9/2015
Somo: Neh 2:1-8
Zab: 136:1-6
Injili: Lk 9:57-62
Nukuu:
“Nikamwambia mfalme, Mfalme akiona vema, na ikiwa mimi,
mtumishi wako, nimepata kibali machoni pako, tafadhali unipeleke mpaka Yuda,
niuendee mji wa makaburi ya baba zangu, nipate kuujenga,” Neh 2:5
“Yesu akamwambia, Mbweha
wana pango, na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa
kujilaza kichwa chake,” Lk 9:58
“Akamwambia Waache
wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu,” Lk 9:60
“Yesu akamwambia, Mtu
aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu,”
Lk 9:62
TAFAKARI: “Ni heri ukawa
baridi au joto kuliko kuwa vuguvugu katika Imani.”
Wapendwa
wana wa Taifa la Mungu, Imani ya mtu husema yote kuhusu maisha ya mtu. Imani
siyo kitu tunwezacho kukiona kwa macho yetu ya nyama, na kukipima ukubwa na
upana wake, bali Imani huonekana katika maisha mazima ya mtu ikiwa ni pamoja na
changamoto zinazobeba maisha hayo ya kila siku. Nathubutu kusema kwamba sisi
tulio wengi kama Wakristo na Wakatoliki kwa kiasi kikubwa tu wakristo wa majina
tu, na wakati mwingine wakristo wa jumapili. Tunafika mahali na kumfanya Mungu
wetu kama kituo cha msalaba mwekundu. Tunamwitaji Mungu pale tu tunapobanwa na
matatizo. Hata katika hali ya matatizo tunajitoa kwake kwa masharti fulani.
Wapendwa
katika Kristo, masomo yetu ya leo yanagusia kwa kiasi kikubwa nini maana ya
imani na kuishi imani hiyo. Yapo mambo makuu manne tunayoweza kujifunza kuhusu
Imani kutoka kwenye masomo yetu ya leo. Kwanza kabisa Imani ya kweli siyo kuwa
waaminifu kwa tamaduni zetu kwa vile tu zilishikiliwa vizuri na wazee wetu
kiupofu. Wakati mwingine mila zetu na desturi ni mkusanyiko wa viaminika
kimazoea ambavyo mwisho wa siku havina uhalisia na uhusiano wo wote na hali
halisi ya ukweli huo. Mazingira kama haya wakati mwingine yanakufanya
kuwajibika kulipopita kiasi pasipo kujielewa. Mwisho wa siku tunakuwa watumwa
na siyo huru tena. Hali hii tunaiona katika somo la kwanza. “Nikamwambia mfalme, Mfalme akiona vema, na
ikiwa mimi, mtumishi wako, nimepata kibali machoni pako, tafadhali unipeleke
mpaka Yuda, niuendee mji wa makaburi ya baba zangu, nipate kuujenga,” Neh 2:5.
Tunaona jinsi gani mtu huyu anavyokuwa na shauku ya kuujenga mji wa makaburi.
Lakini tukumbuke kwamba mara baada ya kufufuka Yesu, malaika
wanawapa ujumbe muhimu wanawake wale waliokwenda kaburini na kumkosa Yesu. “Malaika akajibu, akawaambia wale wanawake, Msiogope ninyi; kwa
maana najua ya kuwa mnamtafuta Yesu aliyesulibiwa. Hayupo hapa; kwani amefufuka kama
alivyosema. Njoni, mpatazame mahali alipolazwa. Nanyi nendeni upesi, mkawaambie
wanafunzi wake, Amefufuka katika wafu. Tazama, awatangulia kwenda Galilaya;
ndiko mtakakomwona. Haya, nimekwisha waambia,” Mt 28:5-7. Hivyo ndugu zangu
Imani yetu leo inatuelekeza kuwa, Yesu huyu aliye shauku yetu tunakutana naye
Galilaya na siyo kaburini. Galilaya yako ni hapo ulipo kadiri ya wito na utume
wake. Ishi vyema hapo ulipo na timiza yote na hasa yale madogo madogo kwa
upendo na unyenyekevu mkubwa. Hapo utakutana na Yesu.
Jambo la
pili tunalofundishwa leo kuhusu Imani, ni namna tunavyochukulia ufuasi wetu.
Je, ninakiri kumfuata Yesu popote atakapo kuwa kama upepo na bendera? Je,
katika ufuasi huo natambua mapaswa yake? Je, nipo imara na nitakuwa imara
katika nyakati zote na hasa zile nyakati za sintofahamu? Yesu anampa angalisho
mtu yule aliyekutana naye njiani na kusema yupo tayari kufuatana naye ko kote
atakapokwenda. “Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana
viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake,” Lk 9:58. Kwa maneno
mengine Yesu anatuambia hakuna maslahi yo yote kibinadamu zaidi ya maisha ya
umilele kutoka kwake. Kama ni swala la utajiri na kuwa na maisha mazuri siyo
kipaumbele katika ufuasi wetu kwake. “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na
haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:9. Kazi yetu ya kwanza ni kuutafuta
kwanza ufalme wa mbinguni na mengine yote tutapewa kwa ziada.
Jambo la
tatu tunalofundishwa leo kuhusu Imani ya kweli ni utambuzi wa kweli na kujua
nafasi ya Mungu katika maisha yako. Bila shaka hakuna asiyekuwa na hofu ya
kifo. Ila kifo kipo tupende au tusipende. Na kama umezaliwa basi ipo siku
utakufa. Kwa hiyo katika uhalisia wa kifo hatupaswi kukiogopa. Yatupasa
kuishinda hofu ili tuwe tayari kukipokea kifo kama njia pekee ya kuishi umilele
tunaojiandaa leo hapa duniani. Hakutakuwa na maisha baada ya umilele baadaye
bila kupita katika fumbo hili la kifo. Hivyo Yesu anamtoa hofu ndugu yule
aliyetoa hoja ya kwenda kwanza kumzika Baba yake ndipo amfuate. Naye Yesu
anamwambia, “Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme
wa Mungu,” Lk 9:60. Je, Yesu anatukataza kuwazika wazazi wetu? La hasha!
Kufanya hivyo atakuwa anaenda kinyumbe na ile amri ya nne ya Mungu, “waheshimu
baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na
Bwana, Mungu wako,” Kut 20:12. Yesu anachotaka kutuambia ni kwamba kifo ni
ukweli usiopingika na hivyo shughuli zake zisiwe sababu ya kutokupokea ujumbe
wake wa uzima wa milele.
Na jambo
la nne na la mwisho tunalofundishwa leo kuhusu Imani ni kule kuwa na msimamo
thabiti wa wito tulio nao na kile tulichoitiwa. Hii ni pamoja na kutokuwa na
kigeugeu na kutazama nyumba tulipotoka kwa malengo ya kujaribu tena. Wengi wetu
baada ya kubatizwa tumerudi kuishi maisha ya kipagani kabida. Wengi wamekuwa
washirikina wa kupindukia na kuongozwa na nguvu za giza ili hali tumejivika
visakramenti mwili mzima. Katika hili Yesu anatupa angalisho, na kusema, “Mtu
aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu,”
Lk 9:62. Kwa maneno mengine ni heri kuwa baridi au joto, kuliko kuwa vuguvugu
katika Imani.
Tumsifu
Yesu Kristo!
EE
YESU TUPE NGUVU YA KUINUKA PALE TUNAPODONDOKA. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario