JUMAMOSI WIKI YA 25 YA MWAKA-B
26/9/2015
Somo: Zek 2:1-5, 10-11a
Zab: Yer 31:10-12, 13
Injili: Lk 9:43-45
Nukuu:
“Imba, ufurahi, Ee binti Sayuni; maana, tazama, ninakuja, nami
nitakaa kati yako, asema Bwana,” Zek 2:10
“Yashikeni maneno haya
masikioni mwenu, kwa kuwa Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa katika mikono ya
watu,” Lk 9:44
“Lakini hawakulifahamu
neno lile, likafichwa kwao wasilitambue; wakaogopa kumwuliza maana yake neno
lile,” Lk 9:45
TAFAKARI: “Mungu hujifunua katika
hali zetu za mahangaiko na mateso; usipoteze Imani yako hata kama huelewi
sababu ya hali hiyo.”
Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka katika
maisha yako ushafikwa na hali ambayo huwezi ona mbele tena kutokana na kusongwa
na kila aina ya misukosuko. Wakati mwingine unapojaribu kutatua jambo fulani
mara linaibuka lingine kubwa au baya zaidi. Tukiwa katika sintofahamu hizi ni
rahisi sana kuyumba katika Imani. Ni wakati huu tunapoona na kupata shauri
mbalimbali na tusiposimama imara katika imani tunaanguka. Mungu anawaambia wana
wa Israeli na sisi pia leo hii kupitia
Nabii Zakaria kwamba, “Imba, ufurahi, Ee binti Sayuni; maana, tazama, ninakuja, nami
nitakaa kati yako, asema Bwana,” Zek 2:10. Hakuna kitu kibaya katika maisha
kama kukata tamaa. Maneno haya ya Mungu yanatuhamasisha tusikate tamaa. Hata
katika shida na mahangaiko yetu Mungu yupo nasi. Kukata tamaa ni kumkufuru Roho
Mtakatifu anayefanya kazi ndani yetu. Dhambi hii ya kumkufuru Roho Mtakatifu
haisamehewi hata kidogo. “Kwa sababu hiyo nawaambia, Kila dhambi na kila neno
la kufuru watasamehewa wanadamu, ila kwa kumkufuru Roho hawatasemehewa.” Mt
12:31. Je, walifahamu jambo hilo ndugu yangu?
Bila shaka kupitia mahangaiko haya na mateso hayo
tunaandaliwa kwa lililo kubwa zaidi mbeleni na kuwa walimu wazuri zaidi kwa
kwenye shida kama hiyo huko mbele ya safari. Kila kitu kinamakusudio yake
katika maisha. Kama tuliumbwa wa sababu na makusudi ya Mungu, basi kila jambo
ndani yetu linasababu yake na ujumbe wake hasa kuhusu imani yetu.
Bwana wetu Yesu Kristo anatujengea ujasiri wa kustahimili
mahangaiko na mateso kama anavyowaambia wanafunzi wake nyakati zile, kwamba, “Yashikeni maneno haya masikioni mwenu, kwa kuwa Mwana wa Adamu
anakwenda kutiwa katika mikono ya watu,” Lk 9:44. Ni kweli na haki kabisa kwamba ujumbe huu
kibinadamu hausikiki vizuri masikioni mwa wanafunzi wake kwa mtazamo walikuwa
nao juu ya Yesu Kristo. Maneno haya yanasikika kama jambo la kufikirika vile.
Bila shaka swali la msingi mioyoni mwa wanafunzi wake Yesu lilikuwa hivi:
maneno haya yana ukweli gani ikiwa Yesu huyu tunayemjua anaonekana kuweza vyote
na mkono wa Mungu ukifanya kazi juu yake atiwe nguvuni mikononi mwa watu?
Maandiko matakatifu yanatuambia kwamba, “hawakulifahamu neno lile,
likafichwa kwao wasilitambue; wakaogopa kumwuliza maana yake neno lile,” Lk
9:45. Kwa makusudi na nia njema kabisa ya Mungu anaweza kuuficha ukweli fulani
kwa lengo la kipimo cha Imani yetu.
Katika
maisha yetu ya kila siku yapo mazingira fulani na hata nyakati fulani kwayo
ukweli juu ya Mungu hujificha. Mara nyingi na tulio wengi nyakati za furaha na
amani huwa hatuoni uwepo wa Mungu. Hali hii hututia kiburi cha kujinyanyua na
kumweka Mungu kama hitaji la pili au la tatu katika maisha. Ni wakati wa “ponda
mali kifo chaja.” Kumbe wakati kama huu wa furaha ndiyo wakati mzuri zaidi
kumpa Mungu sifa na shukrani. Ni wakati nzuri zaidi wa kuzama katika mafumbo na
makuu ya Mungu tukijua kwamba utulivu husadifu uwepo wa Mungu.
Tumsifu
Yesu Kristo!
KAA NASI
BWANA DAIMA. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario