miércoles, 9 de septiembre de 2015

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 23 YA MWAKA-B

ALHAMISI WIKI YA 23 YA MWAKA-B
10/9/2015
Somo: Kol 3:12-17
Zab: 150:1-5
Injili: Lk 6:27-38
Nukuu:
Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi,” Kol 3:12-13
Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu,” Kol 3:13

Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye,” Kol 3:17 

Lakini nawaambia ninyi mnaosikia, Wapendeni adui zenu, watendeeni mema wale ambao wawachukia ninyi, wabarikieni wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni wale ambao wawaonea ninyi,” Lk 6:27-28 

Maana mkiwapenda wale wawapendao ninyi, mwaonyesha fadhili gani? Kwa kuwa hata wenye dhambi huwapenda wale wawapendao,” Lk 6:32

Bali wapendeni adui zenu, tendeni mema, na kukopesha msitumaini kupata malipo, na thawabu yenu itakuwa nyingi; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni mwema kwa wasiomshukuru, na waovu,” Lk 6:35

Basi, iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma,” Lk 6:36

“Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa,” Lk 6:38b

TAFAKARI: “Tunakutana na Yesu mara zote tunapopenda kweli na kusamehe kweli bila kipimo.”
Wapendwa wana wa Mungu, Ukristo wetu siyo ule wa kwenda Makanisani kila siku hata kama tendo hili lenyewe sio baya, siyo ule wa kuwa wanachama wa vikundi mbalimbali vya kitume hata kama kwa kuwafanya hivyo si vibaya, siyo ule wa kuyanena tu matakatifu bila kuyaishi, na siyo ule wa kujitoa katika Kanisa bila kuonja upendo wa sadaka zile tuzitoazo. Hakika kama ninayafanya haya kwa kuwapendezesha watu, bado sijakutana na Yesu, na inawezekana kabisa kutokukutana naye. Ukristo wetu ni pale tu tunapopenda kweli na kuishi ukweli huo, na tunaposamehe kweli na kuishi ukweli huo bila kipimo kila siku na nyakati zote.

Wapendwa, sisi sote tuliobatizwa tu wateule wa Mungu na warithi wake. Kwa upendeleo huu wa Mungu kila mmoja wetu anahesabiwa haki ya kuwa mtakatifu pale anapoishi upendo huo wa Mungu na msamaha wake. Hivyo taswira yetu kama wafuasi wake Kristo yatudai kuwa watu wa rehema, utu wema, wanyenyekevu, wapole, wavumilivu, wasamehevu, na wenye kuchukuliana kwa upendo mapungufu yetu katika kurekebishana. Mtume Paulo anatuwasa, basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi,” Kol 3:12-13. Je, ndugu yangu, una sababu yeyote ya kutokupenda na kusamehe?

Upendo kwa Mkristo ndiyo mizania ya yote hayanenayo na kuyatenda. Hivyo, zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu,” Kol 3:13. Tunakamilishwa na upendo wa Mungu, na ni kwa namna hiyo hiyo tunakamilishana tunapoishi upendo huu katika kweli yake kwa wenzetu. Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye,” Kol 3:17. Tendo hili la kuyatazama yote katika upendo wa kweli linatusukuma pasipo shaka kumtolea Mungu shukrani ya kweli. Shukrani hiyo hujeuka kuwa kielelezo cha neema na baraka za Mungu zisizo na kikomo. Ndugu yangu, moyo usiokuwa na shukrani ukausha mema yote.

Upendo wa kweli huvunja mipaka yote na kuta zote zinazotuzuia kuuona upendo wa Kristo na sadaka yake pale msalabani. Upendo huu utusukuma kupenda hata pale tunapoumia kama binadamu kwa kufanya tendo hilo kutokana na yaliyotusibu na yaliyopita na kutufanya kile tulicho. Upendo huu ujenga tena daraja Imara la kuwapenda hata wale maadui wetu. Tendo hili la upendo linatukutanisha na Yesu aliyependa hata kuutoa uhai wake kwa ajili yetu. Kwa tafsiri hii, upendo unakuwa AMRI. Hivyo Yesu anatuambia leo neno hili la uzima sisi tusiosikia, “wapendeni adui zenu, watendeeni mema wale ambao wawachukia ninyi, wabarikieni wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni wale ambao wawaonea ninyi,” Lk 6:27-28. Tendo hili ndilo linalotofautisha kati ya anayemjua Kristo na aliye mfuasi wake Kristo, Mpagani na anayeongozwa na hofu ya Mungu, na Mkristo wa kubatizwa na anayeishi ahadi za ubatizo.

Upendo wa kweli unatupa mtazamo mpya wa vitu na hasa watu wale wote unaokutakana nao na kuishi nao. Huruma huwa msukumo wetu wa ndani katika kuuona ukweli, kuutafakari, na kuutenda hata kama mazingira utuwiya vigumu kufanya hivyo. Tendo hili kimtizamo kwa yale yote tunayokutana nayo, utuweka karibu sana na Mungu. Basi, iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma,” Lk 6:36. Huruma hii ufunua undani wetu ambao huwa kielelezo sahihi cha kuona upendo wa Mungu kwa wenzetu hasa pale tunapotoa hukumu kwa wenzetu. Mzaburi anatufikirisha ukweli huu kwa kusema, “Bwana, kama wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” Zab 130:3. Ndugu yangu, hapa tunaalikwa kuwa na huruma kama Mungu alivyo na huruma nasi. Mara tulifanyapo tendo hili ndani na katika Kristo ambaye ndiye ufunuo ulio kamili wa Mungu, tendo hili huwa baraka na mizania ya kuhesabiwa haki mbele za Mungu. “Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa,” Lk 6:38b. Je, walifahamu jambo hili? Mwisho wa maisha yetu hapa duniani tuwe tayari kwa maswali haya matatu mbele ya Mungu:

1.      Ulipenda vipi katika maisha yako niliyokupa hapa duniani?
2.      Umetumiaje vipaji nilivyokupa?
3.      Je, maisha ya Mwanangu mpendwa Yesu Kristo yalikuwa na maana yoyote kwako?

Tumsifu Yesu Kristo.


EE YESU NIFANYE KUWA CHOMBO CHA UPENDO NA HURUMA YAKO POPOTE PALE NINAPOISHI. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario