lunes, 14 de septiembre de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 24 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 24 YA MWAKA-B
15/9/2015
Somo: 1Tim 3:1-13
Zab: 100:1-3, 5, 6
Injili: Lk 7:11-17
Nukuu:
Na alipolikaribia lango la mji, hapo palikuwa na maiti anachukuliwa nje, ni mwana pekee wa mamaye ambaye ni mjane, na watu wa mjini wengi walikuwa pamoja naye,” Lk 7:12

Bwana alipomwona alimwonea huruma, akamwambia, Usilie,” Lk 7:13 

Akakaribia, akaligusa jeneza; wale waliokuwa wakilichukua wakasimama. Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka. Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. Akampa mama yake,” Lk 7:14-15

Hofu ikawashika wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, Nabii mkuu ametokea kwetu; na, Mungu amewaangalia watu wake,” Lk 7:16

Ni neno la kuaminiwa; mtu akitaka kazi ya askofu, atamani kazi njema,” 1Tim 3:1

Basi imempasa askofu awe mtu asiyelaumika, mume wa mke mmoja, mwenye kiasi na busara, mtu wa utaratibu, mkaribishaji, ajuaye kufundisha,” 1Tim 3:2

Vivyo hivyo mashemasi na wawe wastahivu; si wenye kauli mbili, si watu wa kutumia mvinyo sana, si watu wanaotamani fedha ya aibu,” 1Tim 3:8

Kwa maana watendao vema kazi ya shemasi hujipatia daraja nzuri, na ujasiri mwingi katika imani iliyo katika Kristo Yesu,” 1Tim 3:13

TAFAKARI: “Huwezi kuwatumikia watu kama huwapendi.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, ni ukweli usioshaka kwamba huwezi kuwatumikia watu kama huwapendi. Hata hivyo, katika hali ya kawaidi inawezekana ukatoa bila kupenda, ila huwezi kupenda bila kutoa. Kwa kusumbuliwa, mfano, mtu anayekuomba kila siku unaweza kumpa anachokuomba kuepukana na usumbufu. Ila kama unapenda kweli utajikuta unatoa hata kama hujaombwa. Ukweli huu ndio anatufundisha Mtume Paulo kwamba, yote yatafika wisho yaani, MATUMAINI, NA IMANI, ila UPENDO utadumu daima. “Basi, sasa inadumu Imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo,” IKor 13:13.

Upendo aliokuwa nao Bwana Yetu Yesu Kristo ni kama kikohozi, kwamba huwezi kuzuiya kinapokujia. Hivyo Yesu akiwa safarini kuelekea mipaka ya Naini, anakutana na tukio la kuhuzunisha, yaani kifo. Akiwa Bwana wa wazima na wafu, Yesu anashindwa kujizui katika PENDO la kweli. Na alipolikaribia lango la mji, hapo palikuwa na maiti anachukuliwa nje, ni mwana pekee wa mamaye ambaye ni mjane, na watu wa mjini wengi walikuwa pamoja naye,” Lk 7:12. Yesu anapokutana na hali hii anakuwa mfariji wa kwanza kabisa kwa wale wote wanaoomboleza. Kwanza kabisa anatutoa hofu. Bwana alipomwona alimwonea huruma, akamwambia, Usilie,” Lk 7:13. Huyu ndiye Yesu, mwalimu na kiongozi. Yupo tayari kufanya yote kwa sababu anatupenda kama tulivyo na mapungufu yetu. Yupo tayari kuyafuta machozi yetu na kuwa tumaini jipya na lenye heri. Yesu anatufundisha kwamba bado tumaini lipo ndani yake tunapomwamini licha ya matatizo tunayokabiliana nayo kwa sasa. Matatizo siyo mwisho wa tumaini jipya ndani na katika Kristo.

Wapendwa katika Kristo, tunaye Jemedari wa kweli na hai kila siku ya maisha yetu. Je, bado unamashaka ya kuambatana na Jemedari huyu? Yesu ndiye kimbilio yetu na yetu yote matumaini. Kamwe ndani ya uongozi wake hatuwezi kuwa mateka tena. Kwa Yesu kuna uhuru wa kweli na tunaona upendo wa kweli. Yesu hutenda makuu kwetu siyo kwamba ni mastahili yetu, bali hawezi kuacha kufanya hivyo kwa sababu anatupenda upeo. Kwa upendo huo, Yesu akakaribia, akaligusa jeneza; wale waliokuwa wakilichukua wakasimama. Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka. Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. Akampa mama yake,” Lk 7:14-15. Kwa upendo wa Kristo sote unainuliwa kutoka hali yetu ya kufa na kukata tamaa. Ndugu yangu elewa kila unapokosa mwelekeo wa maisha Yesu anakuambia INUKA!

Wapendwa wana wa Mungu, upendo huu wa Yesu unapokuwa sehemu ya maisha yetu kila siku, kamwe hatubaki kama tulivyokuwa mwanzo. Upendo huu hujenga hofu ya Mungu ndani mwetu na kuzidi kuyaona yote katika Kristo Mfufuka na hali. Upendo huu unatuwajibisha kuwa kama Kristo mwenyewe, yaani, kuwa habari njema kwa watu wote. Hivyo wakazi wa Naini hofu ikawashika wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, Nabii mkuu ametokea kwetu; na, Mungu amewaangalia watu wake,” Lk 7:16. Huyu ndiye Kristo Kiongozi mwenye upendo wa kweli, na anatutaka mara zote tuwe kielelezo cha upendo huo, kila mmoja kadiri ya hali na ngazi yoyote ya uongozi aliyopewa kama dhamana, ikiendana na wito wake.

Katika hali ya wito, Mtume Paulo anawazungumzia watu wawili, yaani mwenye hadhi ya Askofu na Shemasi. Mtume Paulo anawazungumzia watu hawa kutokana na nafasi zao katika utume na jamii wanayoishi, ikiambatana na mapasa yao. Sifa kuu ya watu hawa ni kutumika ipasavyo na bila kujibakiza kwa wote, ili Kristo aonekane kwa wote aliowafia kwa UPENDO. Hivyo basi, Askofu ili ambebe Kristo katika ukamilifu wote yampasa “awe mtu asiyelaumika, mume wa mke mmoja, mwenye kiasi na busara, mtu wa utaratibu, mkaribishaji, ajuaye kufundisha,” 1Tim 3:2. Kadiri ya mapokea ya Kanisa la zamani Askofu aliruhusiwa kuoa. Ila kadiri ya mahitaji ya nyakati mbali mbali katika Kanisa lililokuwa na kuongezeka, ilionekana ni vyema kwa makleri kutokuoa ili wasijigawe katika upendo wa Kristo kwenye huduma zao Kikanisa. Mashemasi pia iliwapasa “wawe wastahivu; si wenye kauli mbili, si watu wa kutumia mvinyo sana, si watu wanaotamani fedha ya aibu,” 1Tim 3:8. Kadiri ya mang’amuzi ya uongozi na maisha ya wito, kupenda fedha  ni “shina moja la mabaya ya kila namna; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” 1Tim 6:10. Ila  “watendao vema kazi ya shemasi hujipatia daraja nzuri, na ujasiri mwingi katika imani iliyo katika Kristo Yesu,” 1Tim 3:13. Yote huwa sawa katika upendo, na ndiyo dira ya kila kitu tukifanyacho. Kwani “ukipenda utafanya yote,” Mt. Augustino wa Hippo.
Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUJALIE UPENDO WAKO, NA TUYAFANYE YOTE KWA UPENDO. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario