jueves, 24 de septiembre de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 25 YA MWAKA-B

ijumaa wiki ya 25 ya mwaka-b
25/9/2015
Somo: Hag 1:15-2:9
Zab: 42:1-4
Injili: Lk 9:18-22
Nukuu:
Fedha ni mali yangu, na dhahabu ni mali yangu, asema Bwana wa majeshi, Hag 2:8 

Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema Bwana wa majeshi; na katika mahali hapa nitawapa amani, asema Bwana wa majeshi,” Hag 2:9

Akawaambia, Nanyi mwasema ya kwamba mimi ni nani? Petro akamjibu akasema, Ndiwe Kristo wa Mungu,” Lk 9:20

akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka,” Lk 9:22

TAFAKARI: Utajiri wa kweli ni kuwa na Kristo aliyekubali kuwa maskini ili uwe tajiri.”

Wapendwa wana wa Mungu, wengi wetu tunafikiri furaha ya kweli na amani ndani mwetu ni kuwa na mali au vitu au utajiri fulani. Ukweli ni kwamba ni vyema kuwa na yule anayeutoa utajiri huo na amani ya kweli ndani ya mioyo yetu, kuliko kuridhika na haya ya leo na kesho tu. Yesu Kristo amejitoa sadaka na kufa pale msalabani ili mimi na wewe tuwe matajiri wa kudumu. “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9

Wapendwa tupo pamoja?  Kwa hiyo si vyema hata kidogo tukasukumwa na tamaa ya kupata vitu na jambo hili kuwa ndilo lengo la maisha yetu hapa duniani. Tamaa ya kuwa na kitu haijalishi upo utawani au kwenye maisha ya ndoa. Msukumo huu wa kutaka zaidi kila siku una misingi yake katika udanganyifu wa kuwa nikiwa na vingi nitakuwa na furaha zaidi, nitakuwa wa muhimu, na nitakuwa salama; lakini mawazo hayo yote matatu si ya kweli. “Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu,” 1Tim 6:9. Mali huleta furaha ya "muda mfupi tu." Na sababu kubwa ndugu yangu, vitu havibadiliki, hivyo vinatuchosha na tunataka vipya, vikubwa, na bora zaidi. Ukweli ni kwamba tunasahau kuwa, fedha ni mali yangu, na dhahabu ni mali yangu, asema Bwana wa majeshi, Hag 2:8. Ukiwa na vitu hivi elewa kwamba wewe ni mtunzaji tu kwa muda fulani, na ipo siku utaviacha vyote hapa hapa duniani na mwingine atapewa kuvitunza kama wewe ulivyopewa leo na kesho. 

Kuna imani pia kwamba nitapata mali nyingi nitakuwa wa muhimu. Umuhimu wako na umuhimu unaotegemea ulivyo navyo ndugu yangu ni vitu viwili tofauti. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” 1Tim 6:10. Thamani yako haitegemei mali zako, Mungu anasema kitu cha muhimu maishani mwako si vitu! Imani ya watu wengi kuhusu fedha ni kwamba kuwa nazo nyingi kutanipa usalama. Huwezi! Tulio utawani hatuchoki kuwa na tumiradi binafsi twa siri twingiiii. Usicheke ndiyo ukweli kwa baadhi yetu. Mambo yanapokwenda vibaya kwenye huto tumiradi tupresha twa kupanda na kushuka hatukomi.

Ndugu yangu, utajiri unaweza kupotezwa mara moja kwa sababu zisizozuilika. Usalama halisi unaweza kupatikana katika kile ambacho huwezi kunyang'anywa yaani uhusiano wako na Mungu. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu,” 1Tim 6:7. Mt. Augustino anatuwasa kutoka kwenye kanuni yake, "kuna furaha kubwa kuwa na vichache kuliko kuwa na vingi." Hata hivyo tatizo hapa ni kipimo cha huo uchache na huo wingi. Mungu anaufunua ukweli halisi wa sisi kushikamana nao kupitia kinywa cha Nabii Haggai, na kusema, Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema Bwana wa majeshi; na katika mahali hapa nitawapa amani, asema Bwana wa majeshi,” Hag 2:9. Utukufu huu na amani hii ya kweli tunaipata kwa Kristo mwenyewe.

Hata hivyo yatupasa kumjua huyu Yesu ni nani kwetu. Yesu alitaka kujua kutoka kwa watu na hata kwa wanafunzi wake wa karibu kabisa wanamtazamo gani juu yake. Mtume Petro anatoa jibu sahihi kuhusu Yesu, na lile lililo mpasa Kristo katika ulimwengu huu. Akawaambia, Nanyi mwasema ya kwamba mimi ni nani? Petro akamjibu akasema, Ndiwe Kristo wa Mungu,” Lk 9:20.

Mpendwa unayesafiri nami katika tafakari hii nikuulize swali la msingi; pamoja na majibu ya wengine, na hasa jibu alilolitoa Petro kuhusu swali alilouliza Yesu, wewe binafsi Yesu kwako ni nani? Jibu la Petro kwa tafsi, Kristo yaani Masiha wa Mungu, ndiye yeye tu aliyewekwa katika mpango mzima wa ukombozi wa mwanadamu. Hivyo tutaiona mbingu na kuufurahia uhuru wa kweli endapo tu tutakuwa tayari kushikamana na mwana huyu wa Mungu. “Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:11-12. Hivyo kufikia hatua hii la kuokolewa kwetu kupitia jina hili hatunabudi kushiriki njia ile aliyopitia Bwana wetu Yesu Kristo kama anavyowanong’onozea wanafunzi wake siri hii na kusema, “Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka,” Lk 9:22. Ndugu yangu hakuna PASAKA PASIPO IJUMAA KUU. Ndivyo hivyo kwetu kama wafuasi wake Kristo tulio hai kwamba hakuna UTUKUFU PASIPO MSALABA.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU WEWE NDIYE FURAHA YETU YA KWELI. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario