sábado, 12 de septiembre de 2015

TAFAKARI: JUMAPILI YA 24 YA MWAKA-B

JUMAPILI YA 24 YA MWAKA-B
13/9/2015
Somo I: Isa 50:5-9a
Zab: 114:1-9
Somo II: Yak 2:14-18
Injili: Mk 8:27-35
Nukuu:
Naliwatolea wapigao mgongo wangu, na wang'oao ndevu mashavu yangu; sikuficha uso wangu usipate fedheha na kutemewa mate,” Isa 50:6 

Maana Bwana MUNGU atanisaidia; kwa sababu hiyo sikutahayari, kwa sababu hiyo nimekaza uso wangu kama gumegume, nami najua ya kuwa sitaona haya,” Isa 50:7 

Lakini mtu atasema, Wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu,” Yak 2:18

Naye akawauliza, Na ninyi mnasema ya kuwa mimi ni nani? Petro akamjibu, akamwambia, Wewe ndiwe Kristo,” Mk 8:29

Akawaita mkutano pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, Mtu ye yote akitaka kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate,” Mk 8:34

Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha,” Mk 8:25

TAFAKARI: “Ni mtu yule tu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha dominika ya 24 ya mwaka ‘B’wa Kanisa. Dominika ya leo tunaalika tumtafakari kwa undani ‘mtu wa ndani’, hasa NAFSI ili kuisalimisha katika mema na yaliyo makusudi ya Mungu. Mtu kamili anakuwa katika sehemu kuu tatu:- Nafsi, Roho, na Mwili. “Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi Nafsi zenu na Roho zenu na Miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.” I The 5:23

Katika hili Roho na Nafsi huwa pamoja na ndizo wewe mwenyewe. Mwili ni nyumba ya roho na nafsi. Katika uumbaji Mungu aliumba mwili kwa udongo halafu akapulizia pumzi puani ambayo ni roho yake ndipo mtu huyo akawa nafsi iliyo hai. “Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Mwa. 2:7. Miili tuliyonayo ni nyumba ya Nafsi na Roho. Kwa hali hii sisi binadamu ni wawili. Kuna mtu wa ndani na mtu wa nje. Mtu wa ndani ni Nafsi na Roho, na mtu wa nje ni Mwili lakini watu hawa wapo pamoja hatuwezi kuwatenganisha wala kumwona kwa macho ya nyama huyu mtu wa ndani, ila yupo.

Katika hili twaona haya yafuatayo:- Huyu mtu wa nje hukua, kuzeeka na kufa. Mtu wa ndani hakui, hazeeki, wala hafi. Mtu wa ndani hubadilika kwa kuchakaa kunakotokana na kujeruhiwa na kuumizwa kunakosababishwa na dhambi na matukio mbalimbali yanayomsibu binadamu. Mtu wa ndani alianza tangu pale kutungwa mimba siku ya kwanza wakati yai na mbegu na pumzi ya Mungu alipoweka roho yake. Mtu huyu wa ndani hakui wala haongezeki ila hufanywa upya. “Kwa hiyo hatulegei, bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku,” 2Kor 4:16. Kwa hiyo huyu mtu wa nje akifa mtu wa ndani huenda mahali atakapokuwa amejiandalia ama Mbinguni au motoni.

Wapendwa wana wa Mungu, kwenye Nafsi ndipo penye tatizo lenyewe kwani ni katikati ya Roho na Mwili. Nafsi hutawaliwa na Hisia, mfano:- Hofu, Chuki, Hasira, Kujihukumu, Kujikataa, Kukosa furaha, Kukosa upendo, Kukosa amani, n.k. Ni muhimu sana mtu atawale hisia zake. Nafsi ikiegemea rohoni huleta matunda mzuri. “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.” Gal. 5:22-23. Ila nafsi inapoingia katika Mwili mambo huwa mabaya kwani ufanya matendo ya mwili kama tusomavyo katika maandiko matakatifu, “basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo; katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” Gal.5:19-21. Ni vizuri kujua nafsi yako imeegemea wapi. Ikiegemea rohoni utaenda Mbinguni, ikiegemea mwilini utaenda motoni.

Ndugu yangu unayesafari nami katika tafakari hii hatutaweza kumfuata Kristo katika mwelekeo ule ule alioufuata, yaani wokovu kupitia msalaba na kuufikia utukufu kama hatujui Nafsi yetu imeegemea wapi. Kuhusu jambo hili Yesu analiweka wazi kabisa na kusema, Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha,” Kuiponya Nafsi ni kuiridhia nafsi kwa kuyapenda na kuyaegemea matendo ya mwili. Kwa mantiki hii ni kuingamiza nafsi kwa kujua kabisa. Na kuiangamiza nafsi kwa ajili ya Kristo na Injili-habari njema, ni kuyapenda na kuyaegemea matendo ya Rohoni. Huku ndiko kuisalimisha Nafsi kuliko kwema na mpango wa Mungu.

Nafsi husalimika kwa kuyapenda na kuyaegemea matendo ya Rohoni pale tu tunapokuwa tayari kumfuata Kristo, kujikana nafsi, na kujitwika msalaba wetu daima na kwa hiari bila shuruti. Yesu akawaita mkutano pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, Mtu ye yote akitaka kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate,” Mk 8:34. Tukijua aliyekamkamilifu ni Mungu tu, basi kila mwanadamu ili aufikie ukamilifu na kumwona Mungu kama alivyo itampasa kujisafisha kwa kile ambacho kwa tafsiri ya ndani ni ‘msalaba wa kila mmoja wetu.’ Msalaba katika tafsiri hii twaweza kusema ni mapungufu aliyokuwa nayo kila mmoja wetu karidi ya maisha na wito wake. Madhaifu na mapungufu yetu huponywa pale tu tunapoyapokea ndani na katika Kristo. Hivyo, “tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu,” Ebr 12:2-3

Ukweli wa maisha na tafsiri ya ‘Msalaba,’ katika mwono wa Injili ya leo unatupeleka ndani zaidi kuijua Imani yetu na yule tunayemwamini na kumfuata. Kumjua ni nani tunayemfuata, Yesu anauliza swali la uchokozi kwa wanafunzi wake na Petro anatoa jibu, tena jibu lililo sahihi kabisa. Naye akawauliza, Na ninyi mnasema ya kuwa mimi ni nani? Petro akamjibu, akamwambia, Wewe ndiwe Kristo,” Mk 8:29. Kristo yaani, aliyewekwa kwa sababu hiyo, yaani wokovu wa mwanadamu. Huyu ndiye Masiha kwa ajili ya wokovu wetu.

Imani ya kweli huwezi itofautisha na matendo ya kweli yanayoambatana na kile mtu anachoamini. Na wakati mwingine matendo (ya upendo na huruma) husema zaidi ya kila kilicho ndani ya mtu yaani Imani (yanayoonekana na yasiyoonekana). Lakini mtu atasema, Wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu,” Yak 2:18. Nabii Isaya yupo tayari kupokea kadhia zote kwa sababu anayo Imani na Mungu anayemwamini kuwa ndiye msaada na kweli katika yote. Naliwatolea wapigao mgongo wangu, na wang'oao ndevu mashavu yangu; sikuficha uso wangu usipate fedheha na kutemewa mate,” Isa 50:6. Nabii Isaya yupo tayari kupokea fedheha zote akijua mwisho wa siku mateso yake si bure kwani anaye mtetezi wa kweli yaani, Mungu. Maana Bwana MUNGU atanisaidia; kwa sababu hiyo sikutahayari, kwa sababu hiyo nimekaza uso wangu kama gumegume, nami najua ya kuwa sitaona haya,” Isa 50:7. Je, mateso uliyonayo yanakupa mwanga zaidi kuhusu Imani yako? Tunapozungukwa na mateso na hali ya kukata tamaa tujifunze kutoka kwa Mtume Paulo na kusema,  “Lakini mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu,” Gal 6:14.

Kijana Humphrey mcha Mungu na mwenye akili sana darasani hakuwahi kumjua Baba yake mzazi licha ya kwamba anamjua mama yake mzazi ambaye ni kichaa. Humphery ambaye kwa sasa ni Mwalimu katika Chuo Kikuu Kimoja Nchini, anampenda sana Mama yake licha ya hali aliyokuwa nayo.

Jambo la ajabu na muujiza kwake ni pale anapotafakari ilikuwaje Mama yake kumzaa na kumtunza hasa katika uchanga wake bila kupata matatizo yoyote yale. Hakika kwa tendo hili Humphrey umwona Mungu katika mpango mzima wa maisha yake. Licha ya ukali alikuwanao Mama yake huku akibeba vitu vya hatari kama visu na misumari, makopo na chupa,  hakuweza kumdhuru katika uchanga wake.

Kwa upande mwingine Humphrey amekuwa faraja kubwa sana na ulinzi wa kutosha kwa mama yake mzazi licha ya usumbufu mkubwa anaoupata kwa kupotea mara kwa mara nyumbani anapoishi na mwanaye huyu. Watu wengi na hasa marafiki zake Humphrey humshawishi na kumwambia, ni wakati mwafaka angeoa ili apate msaada zaidi katika kumtunza Mama yake. “Nitao siku ambayo Mungu atamchukua Mama yangu kutoka dunia hii. Kama aliweza kunizaa na kunitunza katika uchanga wangu bila kunidhuru, kamwe sintoshindwa kumtunza kwa hali hii aliyonayo sasa,” mara zote hili ndilo jibu la Humphrey wa marafiki zake. Bila shaka Humphrey angependa kuleta maneno na manung’uniko kwa yule ambaye angemwoa na kuwa mke wake.

Humphrey hata mara moja haoni aibu juu ya hali ya Mama yake mzazi. Angeweza kufanya anachoweza kuikwepa aibu hii kwa sababu elimu anayo na maisha mazuri Mungu kamjalia. Humphrey yupo tayari kuubeba msalaba huu hadi mwisho, tena kwa fuhara bila shuruti.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUJALIE NEEMA NA UJASIRI WA KUIBEBA MISALABA YETU NAWE HADI MWISHO. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario