martes, 22 de septiembre de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 25 YA MWAKA-B

jumatano wiki ya 25 ya mwaka-b
23/9/2015
Somo: Ezr 9:5-9
Zab: Tob 13:2-4, 6-8
Injili: Lk 9:1-6
Nukuu:
Tangu siku za baba zetu tumekuwa na hatia kupita kiasi hata leo; na kwa sababu ya maovu yetu sisi, na wafalme wetu, na makuhani wetu, tumetiwa katika mikono ya wafalme wa nchi hizi, tumepigwa kwa upanga, tumechukuliwa mateka, tumenyang'anywa mali zetu, tumetiwa haya nyuso zetu, kama hivi leo,” Ezr 9:7 

Na sasa kwa muda kidogo tumeneemeshwa na Bwana, Mungu wetu, hata akatuachia mabaki yaokoke, akatupa msumari katika mahali pake patakatifu. Mungu wetu atutie nuru machoni mwetu, tuburudike kidogo katika kufungwa kwetu,” Ezr 9:8 

Maana sisi tu watumwa; lakini Mungu wetu hakutuacha katika utumwa wetu, bali ametufikilizia rehema zake, mbele ya wafalme wa Uajemi, ili kutuburudisha, kuisimamisha nyumba ya Mungu wetu, na kuitengeneza palipobomoka, atupe ukuta katika Yuda na Yerusalemu,” Ezr 9:9

Akawatuma wautangaze ufalme wa Mungu, na kupoza wagonjwa,” Lk 9:2 

Akawaambia, Msichukue kitu kwa safari yenu, fimbo, wala mkoba, wala mkate, wala fedha, wala mmoja wenu asiwe na kanzu mbili,” Lk 9:3 

Na nyumba yo yote mtakayoingia kaeni humo, mpaka mtoke mjini,” Lk 9:4 

Na wale wasiowakaribisha, mtokapo katika mji huo, yakung'uteni hata mavumbi ya miguuni mwenu, kuwa ushuhuda juu yao,” Lk 9:5 

TAFAKARI: “Yote yanamwisho ndani na katika Kristo Yesu. AMINI pasipo SHAKA.”

Wapendwa wana wa Mungu, napolitazama Taifa letu leo linanifikirisha sana na Taifa la wana wa Israeli katika nyakati mbalimbali wakionja mateso ya utumwani na kabla na baada ya kuwa huru katika inchi ile ya ahadi waliyopewa na Mungu. Furaha ya wana wa Israeli haijawa ya kudumu hata hivi leo. Vita na machafuko havijafikia ukomo wake. Tofauti iliyopo leo na zama zile ipo kwenye ukweli wa tafsiri na maana nzima iliyobeba historia ya wokovu wetu.

Kama ilivyo kwa upande wa kifo kabla na baada ya Kristo, ndivyo hivyo ilivyokuwa hata sasa, ila kifo hiki cha sasa kina uelewa mpana kuliko ilivyokuwa kabla ya Kristo. Ndani na katika Kristo kifo hakina nguvu tena, kwani kwa mateso na kifo chake Bwana wetu Yesu Kristo hukumu ya kifo imebatilishwa. Sote tu huru na warithi wa ufalme wa Mungu kwa sadaka yake pale msalabani. Yatupasa kufa na kufufuka nale kila siku tunapoishi kweli ahadi zetu za ubatizo.

Taifa letu leo linapita kipindi kigumu zaidi kuliko ilivyokuwa siku zile za mwanzo wa uhuru wetu. Ni kweli yapo mambo mengi mazuri tuliyoyaonja mara baada ya uhuru wetu kama Taifa kutoka mikononi mwa Waingereza na yapo mabaya zaidi ambayo kama Taifa hatukujali kuyapa msisitizo na sasa yamekuwa shumiri kwetu. Je, Mungu wetu yule mwenye huruma amebadilika? La hasha! Mungu anasema hivi; Kwa maana watu wangu ni wapumbavu, hawanijui; ni watoto waliopungukiwa na akili, wala hawana ufahamu; ni wenye akili katika kutenda mabaya, bali katika kutenda mema hawana maarifa,” Yer 4:22. Wapendwa wana wa Mungu, yatupasa kuyatafakari maneno haya mazito ya Mungu kama Taifa. Yawezekana chanzo cha mahangaiko yetu kama Taifa kipo juu ya upumbavu wetu. Wana wa Israeli wanakiri upumbavu wao kwa kusema, tangu siku za baba zetu tumekuwa na hatia kupita kiasi hata leo; na kwa sababu ya maovu yetu sisi, na wafalme wetu, na makuhani wetu, tumetiwa katika mikono ya wafalme wa nchi hizi, tumepigwa kwa upanga, tumechukuliwa mateka, tumenyang'anywa mali zetu, tumetiwa haya nyuso zetu, kama hivi leo,” Ezr 9:7. Hivi kweli Taifa letu pamoja na utajiri wake ni laana kwetu? Kwa nini basi kila kukichwa hatuishi kulalama kama mayatima!

Wapendwa wana wa Mungu lazima tukiri kwa dhati kwamba wakati fulani na watu fulani katika Taifa hili wametufikisha hapa tulipo. Je, tuendelee kulalama ilihali Mungu anakuonyesha neema yake kupitia matukio mbalimbali ya sasa? Je, tunayo nafasi ya kujinasua kutoka katika mtego huu wa uovu? Hatima ya wana wa Israeli ilikuwa chini ya mikono yao ama kusuka au kunyoa. Vile vile hatima ya Taifa letu ipo chini ya mikono yetu. Kila mmoja wetu itampasa kuona, kutathimini na kuchukua hatua. Kila Taifa lina utaratibu wake wa kujinusuru kutoka mikono ya waovu na uovu. Bila shaka kwa upande wetu wa Tanzania huu ndio wakati wa kuona, kutathimini na kuchukua hatua. Wana wa Israeli walipo ona nuru ya Mungu katika mahangaiko yao walisema kwa pamoja, Na sasa kwa muda kidogo tumeneemeshwa na Bwana, Mungu wetu, hata akatuachia mabaki yaokoke, akatupa msumari katika mahali pake patakatifu. Mungu wetu atutie nuru machoni mwetu, tuburudike kidogo katika kufungwa kwetu,” Ezr 9:8. Je, twahitaji Mungu kushuka na kutuambia haya ili hali tumefunuliwa ukweli na kupewa nuru ya Mungu? Kama hata upande ule wa uovu unalalamika kuhusu uovu, Je, hiyo haitoshi kuona kwamba mimi na wewe yatupasa kuchukuwa hatua sahihi tusije angamia katika uovu moja kwa moja? Kwa upande wangu binafsi naliamini sana neno hili, na ninaona huu ndio wakati wakujinasua kutoka mzimu huu wa uovu na maovu.

Wapendwa wana wa Mungu, maisha haya tunayoishi leo kama Taifa siyo makusudi ya Mungu na uumbaji wake. Tuelewa kwamba tumeumbwa na Mungu ili tumjua, tumpende, tumtumikie na mwisho turudi kwake mbinguni. Je, twawezaji kuyafanya hayo yote katika hali hii ya dhiki na machafuko? Yatupasa kufanya kitu. Wana wa Israeli walivyojitambua walisema haya ya moyoni, “hijapokuwa sisi tu watumwa; lakini Mungu wetu hakutuacha katika utumwa wetu, bali ametufikilizia rehema zake, mbele ya wafalme wa Uajemi, ili kutuburudisha, kuisimamisha nyumba ya Mungu wetu, na kuitengeneza palipobomoka, atupe ukuta katika Yuda na Yerusalemu,” Ezr 9:9. Tanzania kama Taifa letu na nyumba, imebomoka. Taifa linahitaji wajenzi wapya na wenye moyo na uchungu na siyo wababaishaji wenye kutumia wimbo ule ule wenye kulevya, na baada ya ulevi huo mateso na mahangaiko yapo pale pale.

Wapendwa wana wa Mungu, kila mmoja wetu ni sababu ya uzuri wa Taifa letu. Uzuri huo upo ndani yetu tangu kuumbwa kwetu. Tunaye chapa ya Mungu ambaye ndiye ukamilisho wa uzuri wote kwa yale yanayoonekana na yasiyoonekana. Hivyo Yesu anamtuma kila mmoja wetu kupambana na yaliyomaovu. Naye akawatuma wautangaze ufalme wa Mungu, na kupoza wagonjwa,” Lk 9:2. Ufalme wa Mungu ni ufalme wa amani, upendo, umoja, haki na kweli. Tunapoona hakuna amani, upendo, umoja, haki na kweli, Mungu hayupo nasi. Ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha mambo hayo yapo na yanadumu. Katika vita hii, Yesu anawaasa wanafunzi wake na sisi pia kwa kusema, “msichukue kitu kwa safari yenu, fimbo, wala mkoba, wala mkate, wala fedha, wala mmoja wenu asiwe na kanzu mbili,” Lk 9:3. Maana yake nini? Kwa hali ilivyo sasa yatupasa kupigania hili ambalo halipo na ni nadra kupatikana katika ufalme wa Mungu, yaani, amani, upendo, umoja, haki na kweli katika Taifa letu. Mada na mahitaji mengine ya ziada nje ya ukweli huu hayana umuhimu hata kama yanahitajika.

Wapendwa wana wa Mungu, katika safari hii tuelewe kwamba mambo siyo rahisi. Kurudisha ufalme wa amani, upendo, umoja, haki na kweli pale ambapo hayo mambo yalisahaulika na kuwa faida kwa wachache waliojineemesha na kuhodhi mamlaka, haitakuwa jambo rahisi kwao kukubali ukweli huu licha ya kwamba hakuna njia nyingine. Siri ya ushindi ni hii anayotuambia Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba, na nyumba yo yote mtakayoingia kaeni humo, mpaka mtoke mjini,” Lk 9:4. Kukaa ndani ya nyumba ile ile ni kusimama katika kweli hata kama itatulazimu kufa kwa ajili ya kweli. “Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” Yoh 8:32. Asiye pokea kweli hii na akapenda kung’ang’ana na uongo na upotoshaji, hakuna muda wa kupoteza katika vita juu ya uovu. Naye Yesu anasema, na wale wasiowakaribisha, mtokapo katika mji huo, yakung'uteni hata mavumbi ya miguuni mwenu, kuwa ushuhuda juu yao,” Lk 9:5. Ni swala la wakati tu kwamba historia ndiyo itakayo kuwa hukumu kwa wale wote walioukataa ukweli, na ukweli ule ule walioukataa utasimama daima.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUSIMAMA NASI KATIKA VITA HIVI DHIDI YA UOVU KATIKA TAIFA LETU. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario