martes, 8 de septiembre de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 23 YA MWAKA-B

JUMATANO WIKI YA 23 YA MWAKA-B
9/9/2015
Somo: Kol 3:1-11
Zab: 144:2-3, 10-13
Injili: Lk 6:20-26
Nukuu:
Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi,” Kol 3:1-2 

Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu; kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu,” Kol 3:5-6

Mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba,” Kol 3:10 

Hapo hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote,” Kol 3:11

Heri ninyi watu watakapowachukia, na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu. Furahiwani siku ile na kuruka-ruka, kwa kuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni, maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo,” Lk 6:22-23

TAFAKARI: “Furaha ya kweli ni kuyapata yote ndani na katika Kristo.”

Wapendwa wana wa Mungu, licha ya kubatizwa kwetu na kuwa warithi halali wa ufalme wa Mungu, tunaishi katika changamoto nyingi kutekeleza kwa uaminifu mkubwa ahadi zetu za ubatizo. Changamoto hizi zinapotuzidi zinatuondolea ndoto ile ya furaha ya kweli ndani na katika Kristo. Hivyo kufikia lengo na makusudio ya furaha hii ya kweli ndani na katika Kristo, Mtume Paulo anatupa leo msingi wa kukabiliana na changamoto hizo za Imani pale tunapotaka kuishi vyema ahadi zetu za ubatizo. Naye anasema hivi, Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi,” Kol 3:1-2. Ndugu yangu unayesafiri na mimi katika tafakari hii, yatupasa kwanza kabisa kuyatafuta yaliyo juu Kristo aliko.

Ndugu yangu, mambo yaliyo juu aliko Kristo ni yale yote yanayotuongoza huko aliko, yaani ufalme wa mbinguni na umilele wake. Kwa maneno mengine ni kuvaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba,” Kol 3:10. Utu huu upya ni tendo la kupiga vita aina zote za dhambi kwa sababu dhambi ufifisha na kuzorotesha utu wetu wa ndani ambao ni nafsi na roho.

Jambo la pili na lenye maana kabisa katika maisha ya kiroho ni kufikiri muda wote yale yaliyo juu na siyo yaliyo katika nchi. Hapa Mtume Paulo anaongelea sana swala la nafsi ya mtu. Nafsi inapoegemea zaidi katika mwili matokea yake ni anguko kuu na mwisho wa matumaini yote ya kuurithi ufalme wa Mungu. Hapa ndipo binadamu anapoonekana mara zote kufikiri yaliyo katika nchi na yasiyo na umilele. Kuepukana na kadhia hii, Mtume Paulo anatoa angalisho kwa kusema,  Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu; kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu,” Kol 3:5-6. Ghadhabu ya Mungu hapa ni kuukosa ufalme wake na kuangamia milele pasipo kuwa na nuru yake.

 Ndugu yangu, pale nafsi inapoegemea roho, ndipo tunapojazwa tumaini jipya na kufanywa upya siku kwa siku. Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku,” 2Kor 4:16. Kuishi ukweli huu ndani na katika Kristo ni kuchuchumilia cheo chetu halisi, yaani UTAKATIFU WAKO! Cheo hiki kila mmoja wetu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu ndiyo stahili yake, na anaipata kwa kuishi kweli kwa mafundisho ya Kristo, na kutimiza ukweli huo kwa uaminifu. Hivyo hasili zetu katika maana ya mila na desturi zetu, familia zetu, koo zetu, makabila yetu, na utaifa wetu hazina uhalalisho wowote katika cheo hiki kama hatunaye Kristo katika maisha yetu ya kila siku. Ni kwa sababu hii Mtume Paulo anawapa angalisho watu wa nyakati zake, na sisi pia kwa kusema, hapo hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote,” Kol 3:11.

Wapendwa katika Kristo, angalisho la mtindo huo alilotoa Mtume Paulo na lenye kutuweka katika mstari sahihi kuelekea urithi tulioandaliwa na wenye hadhi ya cheo chetu, ndilo alilolikazia Yesu Krito katika injili ya leo anapozungumzia heri zile nne na ole zile nne. Maisha yetu ya leo na mahangaiko yake yamo katika haya anayoyakazia Bwana wetu Yesu Kristo katika injili ya leo. Kila heri moja huenenda na ole yake. Heri yao masikini kwa ajili ya Kristo, humpatia maskini huyo ufalme wa Mungu. Umaskini hapa ni uhitaji wa Kristo kila siku ya maisha yako. Hakuna anayeishi kwa ajili yake mwenyewe. Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,” Rum 14:8. Kinyume chake ole matajiri na walio na mali kwa walivyo kuwa navyo bila Kristo ni faraja ya leo na kesho tu, na mwisho wake ni kiama. Wote walio na njaa na kiu ya haki katika Kristo kamwe hawataona njaa, kwani Kristo atawashibisha daima kwa tendo hilo licha ya upinzani wake. Kinyume chake, ole walioshiba sasa kwa kuzikanyaka haki za wengine na wanyonge kwani wataona njaa ya milele.

Katika jamii yetu leo wapo watu wengi wanaolia kwa shida mbalimbali ili hali wapo wanaosheherekea na kutapanya vitu ovyo bila kuwajali wahitaji na wanyonge. Kristo anatuambia wanaotaabika sasa katika ulimwengu huu watacheka na kufurahi milele. Kwa upande wa pili, wote wanaocheka sasa na kuyafumba macho yao kwa kutokuona shida za wengine hao wataomboleza daima. Je, ndugu yangu kwa nini waandaa maombolezo ya kudumu katika umilele wote unaposhindwa kunyoosha mkono wa heri kwa mwitaji unayeishi naye katika familia yako, jumuiya yako ya kitawa, jumuiya yako ndogo ya Kikristo, ofisi moja ya kazi, kigango chako, na hata parokia yako?

Vile vile katika jamii yetu leo wapo wengi wanaochukiwa bila sababu ya msingi, wanaotengwa kutokana na misimamo yao katika kweli, wanaoshutumiwa na kunenewa uovu kwa sababu tu wanapenda kumuishi Kristo na kuwa pembeni ya kundi ovu linalopendwa na wengi. Hawa Kristo anasema thawabu yao ni kubwa mbinguni.Heri ninyi watu watakapowachukia, na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu. Furahiwani siku ile na kuruka-ruka, kwa kuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni, maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo,” Lk 6:22-23. Kinyume chake ni wake wanaopenda kuonwa wema na kusifiwa hata kama hawajafanya chochote. Hawa taji lao ni unabii wa uongo ambalo halina thamani yoyote mbele ya Mungu. Hawa ndio wale wanaopoteza muda na maisha yao kila siku. Ni sawa na parachuti lililojaa hewa na kuelea juu kabisa angani na mara hufikwa na kikomo linapokutana na ncha ndogo sana ya mwiba. Hewa yote hutoweka na kusinyaa.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU NITUMIE VYEMA KADIRI YA MPANGO WAKO KWANGU. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario