miércoles, 2 de septiembre de 2015

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 22 YA MWAKA-B

ALHAMISI WIKI YA 22 YA MWAKA-B
3/9/2015
Somo: Kol 1:9-14
Zab: 97
Injili: Lk 5:1-11
Nukuu:
mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu,” Kol 1:10

Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi,” Kol 1:13-14

Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simoni, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki,” Lk 5:4 

Simoni akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” Lk 5:5

Simoni Petro alipoona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana,” Lk 5:8

“Yesu akamwambia Simoni, Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu,” Lk 5:10b

TAFAKARI: “Kama ushakutana na Kristo katika Maisha yako lazima akubadili mwenendo wako.”

Wapendwa wana wa Mungu, yawezekana hadi leo licha ya kuingizwa katika urika wa wana wa Mungu na warithi wa ufalme wake kwa sakramenti ya ubatizo, bado haujawahi kukutana na Kristo katika maana ya kuguswa kuliko ndani kabisa ya maisha yako. Tunakutana na Kristo pale tu tunapoanza kuyachukulia maisha yetu na ufuasi wetu kwake kwa namna iliyo hai na ya kuguswa kwa yale yote tuyafanyayo ndani na katika Kristo Yesu. Mara tuifikiapo hatua na hali hii, tendo hili haliwi tena tendo au swala la kihisia, hadithi au simulizi fulani la kufikirika, bali maisha halisi.

Ndugu yangu, maisha halisi ndani na katika Kristo yanatuwajibisha kwa kila namna, tunapendezwa nayo, maisha hayo huzaa matunda mema, na mwisho maisha hayo utuongezea ufahamu juu ya Mungu. Ni kwa mantiki hii Mtume Paulo anawasihi Wakolosai nasi pia kwamba, tuenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu,” Kol 1:10. Tunawajibika kuuona ukweli huu tunapopima uzito wa dhambi na wokovu aliotupatia Kristo kwa sadaka ya Kifo chake pale msalabani. Hakika ni upendo mkubwa sana kwetu wanadamu. Kristo ndiye pekee anayetuweka huru kutoka nguvu za giza na kutuingiza katika ufalme wa Mungu kwa pendo lake, kwa sababu ni kwake tu kwenye ukombozi na msamaha wa dhambi zetu. Hivyo Kristo, alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi,” Kol 1:13-14. Je, ndugu yangu una sababu yoyote ya kuacha kumsamehe mwenzako kwa vigezo vyovyote vile  ulivyo navyo? Ukristo na ufuasi wangu kwake una maana gani ninapotazama tendo hili la msamaha? Nisipobadilika katika tendo hili hakika bado sijakutana na Kristo Yesu.

Ndugu zangu, mahangaiko katika maisha yetu ya kila siku yasiwe ukuta wa kutokuona uwepo na nguvu ya Kristo Yesu ndani ya yale tuyafanyayo hata kama tunauzoefu nayo. Kama kweli wasadiki Kristo ndiye Mwokozi, basi ni kwa namna hiyo hiyo huyaweza yote yaliyo chini ya miguu yake kwa sababu, “amevitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote,” Efe 1:22-23. Yesu Kristo analiweka jambo hili hadharani anapowakuta Simon Petro na wenzake waliokuwa mahodari wa kuvua samaki usiku kucha bila kupata chochote. Naye Yesu anamwambia Simoni, “Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki,” Lk 5:4. Kwa maana nyingine Yesu anamwambia Simoni Petro kwamba “jaribu tena pasipo kuwa na shaka na urushe kete yako ya mwisho katika ukamilifu wote.” Maneno haya ya Yesu yanamtia shaka kidogo Simoni Petro kutokana na uzoefu aliokuwa nao katika kuvua samaki. Hata hivyo Simoni anamwamini Yesu pasipo shaka na kufanya alivyoagizwa. Hivyo, Simoni akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” Lk 5:5. Ndugu zangu, “ni kwa neno lake Yesu, Simoni Petro anazishusha nyavu.” Ni kwa njia ya neno Mungu aliumba ulimwengu kutoka utupu. Hivyo ni kwa neno hili: Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika. Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu,” Yoh 1:3-4. Je, bado unamashaka na Neno wa Mungu, yaani Yesu Kristo?

Muujiza wa wingi wa samaki uliotokana na hali isiyoyakawaida kadiri ya ufahamu aliokuwa nao Simoni juu ya uvuvi unamfanya akutane na Kristo katika maisha halisi na kujiona alivyo kiroho. Hapa ndipo pale tunaposema kwamba unapokutana na Kristo ndani na katika yeye lazima akubadilishe. Kubadilishwa kwa Simoni kunajionyesha katika hali ya dhambi iliyoisuta nafsi yake. Hivyo katika mguso huu, Simoni Petro alipoona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana,” Lk 5:8. Je, ninapokutana na matendo makuu ya Mungu katika maisha yangu nauona udhaifu wangu? Je, matendo hayo makuu ya Mungu ni mastahili yangu yanayotokana na mafanikio yangu na juhudi zangu bila mkono wa Mungu?

Wapendwa wana wa Mungu, tunapokutana na Kristo katika uhalisia wa maisha yetu ya kila siku, hali hiyo hughubikwa na hofu kubwa kwa sababu tunajiona kama tulivyo kwani Kristo huwa kioo cha kujitazamia nafsi na roho yetu. Tupatapo hali hiyo, tusisahau kuwa Yesu anatuambia kama alivyo mwambia Simoni, “Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu,” Lk 5:10b. Maana yake yake, “usihofu kwani ninakuandaa kwa makubwa zaidi ya hayo niliyokutendea.” Mungu wetu mara zote utuwazia mambo makubwa zaidi ya yale tuyafanyayo kila siku, na neema na baraka anazotujalia pasipo mastahili yetu.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU MATENDO YAKO KWANGU NI YA AJABU SANA! UTUKUZWE NA KUHESHIMIWA MILELE. AMINA.

No hay comentarios:

Publicar un comentario