miércoles, 23 de septiembre de 2015

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 25 YA MWAKA-B

ALHAMISI YA WIKI YA 25 YA MWAKA-B
24/9/2015
Somo: Hag 1:1-8
Zab: 149:1-6, 9
Injili: Lk 9:7-9
Nukuu:
Ndipo neno la Bwana lilikuja kwa kinywa cha nabii Hagai, kusema, Je! Huu ndio wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenye mapambo ya mbao, iwapo nyumba hii inakaa hali ya kuharibika?” Hag 1:3-4

Basi sasa, Bwana wa majeshi asema hivi, Zitafakarini njia zenu,” Hag 1:5

Mmepanda mbegu nyingi mkavuna kidogo; mnakula lakini hamshibi; mnakunywa lakini hamkujazwa na vinywaji; mnajivika nguo lakini hapana aonaye moto; na yeye apataye mshahara apata mshahara ili kuutia katika mfuko uliotoboka-toboka,” Hag 1:6

Pandeni milimani, mkalete miti, mkaijenge nyumba; nami nitaifurahia, nami nitatukuzwa, asema Bwana,” Hag 1:8

Lakini Herode akasema, Yohana nilimkata kichwa; basi ni nani huyu ambaye ninasikia mambo haya juu yake? Akataka kumwona,” Lk 9:9

TAFAKARI: “Natuzitafakari  njia zenu asema Bwana wa Majeshi.”

Wapendwa wana wa Mungu, mafanikio ya mtu katika nyanja zote zile  hayatofautiani sana na utaratibu mzima wa maisha ya mtu. Mfano; afya njema ya mwili wa mtu hutegemea sana chakula anachokula. Ukitaka kujua ufahamu wa mtu kiakili na kitaalumu, tazama mambo anayoyasoma. Ukitaka kujua hofu ya Mungu ya mtu, tazama uhusiano wake na Mungu, uhusiano wake na watu, na uhusiano wake na mazingira yanayomzunguka. Ni ukweli usiotia shaka kwamba hatuwezi kutoa kile tusichokuwa nacho. Hivyo basi, kitu cho chote afanyacho mwanadamu ni msukumo wa kitu fulani kilichokwishwa kuwepo kutokana na mpangilio mzima wa maisha yake. Binadamu aweza kuwa cho chote kile kwa sababu kaumbwa na kuwezeshwa “kuwa-potential” na mwenyezi Mungu. Hivyo basi, tunapokuwa nje ya ukweli huu niliouelezea kwa kifupi, yatupasa kuzifakari vyema njia zetu ikiwa ndilo agizo la Bwana wetu wa Majeshi.

Jamii yoyote ile na hasa inayoongozwa na mambo ya kiroho, mafanikio yao na kudondoka kwao hutokana na kutokuzingatia kwa undani mahusiano yao kimwili na kiroho. Kujua mahusiano haya bayana ni kuweka vipaumbele vyako wazi katika maisha unayoishi. Wengi wetu kutambua jambo hili tunasaidiwa sana na mafungo ya mara kwa mara. Vipauambele vyetu ndiyo dira inayoongoza maisha yetu. Kwa mantiki hii, Wayahudi walikuwa na vipauambele vitatu, ambavyo kwayo vilileta karibu uhusiano wao na Mungu. Kipauambele namba moja ni uwepo wa Hekalu ambapo waliweza kumsifu Mungu, kumwabudu Mungu, na kumtolea sadaka na shukruni. Hivyo popote pale walipokuwa, iwe huru au utumwani, uwepo wa Hekalu uliwaunganisha na Muumba wao.

Kipauambele namba mbili ni ardhi. Hapa waliweza kupata mahitaji yao ya mwili, na mwisho wa siku kumtolea Mungu sadaka zao za kuteketeza kama shukrani kubwa kwa Mungu. Uwepo wa ardhi na umuhimu wake tunaweza kuuona hata leo katika migogoro mingi kati ya Taifa hili la kiyahudi-Isreaeli, na majirani zake.

Kipauambele namba tatu ni uongozi imara utakao simamia haki na kweli kwa kila raia wake wote. Tunaona jambo hili pale wayahudi walipomwomba Mungu kupitia Nabii Samweli wawe na Mfalme kama yalivyokuwa mataifa mengine yaliyowazunguka. Hivyo Mungu anawapa angalisho na mwisho anawapatia Mfalme Sauli. “Bwana akamwambia Samweli, Isikilize sauti ya watu hawa katika kila neno watakalokuambia; kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi, ili nisiwe mfalme juu yao. Basi sasa, isikilize sauti yao; walakini, uwaonye sana, na kuwaonyesha desturi ya mfalme atakayewamiliki. Akasema, Mfalme atakayewamiliki ninyi atakuwa na desturi hii; atatwaa wana wenu na kuwaweka kwake, kwa magari yake, na kuwa wapanda farasi wake; nao watapiga mbio mbele ya magari yake.” ISam 8:7, 9, 11. Mfululizo wa mstari wa 12 hadi ule wa 18 unaelezea desturi ya mfalme huyo na ukatili wake. Ila sikio la kufa halisikii dawa. Wana wa Israeli kwa kiburi chao wakamjibu Nabii Samweli na kusema, “sivyo hivyo; lakini tunataka kuwa na mfalme juu yetu; ili sisi nasi tufanane na mataifa yote; tena ili mfalme wetu atuamue, tena atoke mbele yetu na kutupigia vita vyetu.” 1 Sam 8:19-20.

Wapendwa wana wa Mungu, mambo hayo matatu yalikuwa muhimu sana kwa wana wa Israeli. Ukweli huu, na hasa kipaumbele cha kwanza kinajionyesha katika somo letu la leo kutoka kitabu cha Nabii Haggai 1:1-8. Ndipo neno la Bwana lilikuja kwa kinywa cha nabii Hagai, kusema, Je! Huu ndio wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenye mapambo ya mbao, iwapo nyumba hii inakaa hali ya kuharibika?” Hag 1:3-4. Ni kweli kabisa mara baada ya kutoka utumwani au uhamisho wa Babeli mwaka 520 Kabla ya Kristo, wana wa Israeli walijisahau katika wajibu wao huu mkubwa wa kulijenga Hekalu la Mungu. Haggai Nabii anaanzisha kipindi cha mwisho cha unabii katika Israeli. Wana wa Israeli wanajikuta kutokusonga mbele kimaendeleo, mwili na roho kwa kutokulitenda jambo hili muhimu. Nabii Haggai anawapa sababu ya mkwamo wao na kusema, Mmepanda mbegu nyingi mkavuna kidogo; mnakula lakini hamshibi; mnakunywa lakini hamkujazwa na vinywaji; mnajivika nguo lakini hapana aonaye moto; na yeye apataye mshahara apata mshahara ili kuutia katika mfuko uliotoboka-toboka,” Hag 1:6. Ndugu yangu unaye safiri nami katika tafakari hii ulishawahi kuzitafakari njia zako katika mikwamo yako kimaisha? Wengi wetu tusipokaa na pesa ingawa tunafanya kazi na kulipwa mishahara hufikiria tumewekewa kitu kinachoitwa “kichuma pesa.” Wengine hata kila tunapolima hatupati mazao yenye tija kabisa. Je, umejiuliza vyema utoaji wako wa zaka? Wengi wetu tunachofanya ni kumwibia Mungu kila wakati.

Wapendwa wana wa Mungu, Zaka yako ni kama ifuatavyo: Zaka ya fungu la kumi ni mujibu wa mwenye ardhi na mashamba, na hata waajiriwa katika mtazamo wa kileo. Usiache kutoa zaka ya fungu la kumi katika maongeo yote ya mbegu zako, yatokayo shamba mwaka baada ya mwaka,” kumb, 14:22. Ni lazima kumtolea Mungu zaka hiyo, kwa sababu yeye ni Bwana wa ardhi yote ya Nchi Takatifu. Ni  wajibu kutoa zaka hiyo kwa mazao yote ya ardhi na kuyapeleka patakatifu. Huko ndiko kumcha Mungu kuliko kwa kweli na haki. Nawe utakula mbele za Bwana, Mungu wako, mahali atakapochagua apakalishe jina lake, zaka ya nafaka zako, na divai yako, na mafuta yako, na wazaliwa wa kwanza wa makundi yako ya ng'ombe na ya kondoo; ili upate kujifunza kumcha Bwana, Mungu wako, daima,” Kumb 14:23.

Kila mwaka wa tatu zaka hiyo inachukuliwa na fukara. Hiyo ni sheria ya kitabu cha tano cha Musa. (Hes 18:21-32) inatazama fungu la kumi kama kodi ya kuwalipia Walawi.  Nao Walawi  walilazimishwa kutoa fungu la kumi la kodi hiyo kwa makuhani kama sadaka ya kuinuliwa kwao kwa Bwana. Iliwapasa pia kulipa fungu la kumi la mifugo. Tena zaka yote ya nchi, kama ni mbegu ya nchi, au kama ni matunda ya nchi, ni ya Bwana; ni takatifu kwa Bwana. “Na kama mtu akitaka kukomboa cho chote cha zaka yake, ataongeza sehemu yake ya tano juu yake. Tena zaka yote ya ng'ombe, au ya kondoo, kila apitaye chini ya fimbo; sehemu ya kumi watakuwa ni watakatifu kwa Bwana,” Law 27:30-32. Fedha nazo zinaruhusiwa kutolewa badala ya sadaka yenyewe.  “Ndipo uzibadili ziwe fedha, na kufunga zile fedha uende nazo mkononi mwako, hata mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako. Na kama mtu akitaka kukomboa cho chote cha zaka yake, ataongeza sehemu yake ya tano juu yake,” Kumb 14:25, Law 27:31

Mwisho kabisa, katika kutafakari njia zetu yatupasa kuhoji ukaribu wetu na Mwana wa Mungu. Herode anaingiwa na hofu baada ya kusikia habari za Yesu kwa sababu alifikiri baada ya kumwangamiza Yohane Mbatizaji kwa kumkata kichwa siku ya sherehe ya kuzaliwa kwake-Herode, angeendelea kuisalimisha dhamiri yake mbaya katika uovu. Herode anataka kumwona Yesu si kwa sababu anataka kuanzisha uhusiano mzuri naye, bali bila shaka kutafuta namna ya kumwangamiza ili asiwe tishio kwake. Hivyo anawajibu wale waliomletea habari juu ya Yesu na kusema, “Yohana nilimkata kichwa; basi ni nani huyu ambaye ninasikia mambo haya juu yake? Akataka kumwona,” Lk 9:9. Tukitaka kuwa na amani ya kweli ndani yetu lazima tupatanishwe na Kristo. “Huyu manabii wote humshuhudia, ya kwamba kwa jina lake kila amwaminiye atapata ondoleo la dhambi,” Mdo 10:43.

Tumsifu Yesu Kristo!


Pandeni milimani, mkalete miti, mkaijenge nyumba; nami nitaifurahia, nami nitatukuzwa, asema Bwana,” Hag 1:8

No hay comentarios:

Publicar un comentario