IJUMAA YA OKTAVA YA PASAKA
Somo: Mdo 4:1-12
Zab: 118:1-2, 4,
22-24, 25-27a
Injili: Yoh 21:1-14
Nukuu:
“Wakawakamata, wakawaweka gerezani hata asubuhi; kwa kuwa
imekwisha kuwa jioni,” Mdo 4:3
“Walipowaweka katikati wakawauliza, Kwa nguvu gani na kwa
jina la nani ninyi mmefanya,” Mdo 4:7
“Jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina
la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua
katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu,” Mdo 4:10
“Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana
hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi
kuokolewa kwalo,” Mdo 12
“Simoni Petro
aliwaambia, Naenda kuvua samaki. Nao wakamwambia, Sisi nasi tutakwenda nawe. Basi
wakaondoka, wakapanda chomboni; ila usiku ule hawakupata kitu,” Yoh 21:3
“Basi Yesu akawaambia,
Wanangu, mna kitoweo? Wakamjibu, La,” Yoh 21:5
“Akawaambia, Litupeni
jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata. Basi wakatupa; wala sasa
hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki,” Yoh 21:6
“Basi yule mwanafunzi
ambaye Yesu alimpenda akamwambia Petro, Ndiye Bwana,” Yoh 21:7
“Naye
Simoni Petro, aliposikia ya kwamba ni Bwana, akajifunga vazi lake, (maana
alikuwa uchi), akajitupa baharini,” Yoh 21:7b
“Basi Simoni Petro
akapanda chomboni, akalivuta jarife pwani, limejaa samaki wakubwa, mia hamsini
na watatu; na ijapokuwa ni wengi namna hiyo, jarife halikupasuka,” Yoh 21:11
TAFAKARI: “Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata.”
Wapendwa wa Mungu, Tumsifuni Yesu Kristo kwa wingi wa neema na
baraka zake anazotujalia kila siku tunapo tafakari neno lake. Wapendwa leo kwa
namna ya pekee tuyatafakari naneno haya ya Bwana wetu Yesu Kristo, “Litupeni
jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata.” Neno hili Yesu anawaambia
wanafunzi wake ambao wameshinda usiku kucha wakivua samaki, na kutoka wakavu
kabisa. Neno hili la Yesu Kristo limejaa neema na maarifa, limejaa upyaisho na
mwelekeo mpya, limejaa nguvu na matumaini, limejaa uthaminishwaji katika
kutenda vyema tena. Sababu kubwa na neno hili ni UPANDE WA KUUME liliko
elekezwa lile JARIFE. Ni upande walioheri na salama. Ni upande wenye baraka.
Neno hili ndiyo siri kubwa ya uinjilishaji wa kina, chini ya
msukumo wa Roho Mtakatifu wa Kanisa la jumuiya ya kwanza ya Wakristo. Roho huyu
Mtakatifu, ndiye kichocheo kikubwa cha ushupafu waliokuwa nao Mitume, licha ya
kuhujumiwa mara kwa mara kwa sababu la JINA LlLE KUU LA BWANA WETU YESU KRISTO
MNAZARETI. Mitume baada ya ufufuko wa Kristo, walisongwa sana, kwa sababu tu
walishuhudia ufufuko wa Kristo. “Wakawakamata, wakawaweka gerezani hata asubuhi; kwa kuwa
imekwisha kuwa jioni,” Mdo 4:3. Misukosuko hii tunayoiona leo katika zama zetu,
inakishindo kikuu sana. Leo, Wakristo wengi uharabuni, Iran, na baadhi ya nchi
za Afrika kama Nigeria, Somalia, Sudani ya Kaskazini, Tanzania Visiwani yetu ya
leo; wanateswa na hata kuuwawa kwa sababu tu wao ni Wakristo.
Pamoja na hali hiyo, Mtume Petro kama kiongozi hakusita
kusema iliyo kweli mbele ya macho ya hawa wahujumu wa Kanisa la Kristo.
Wanapohojiwa ni kwa mamlaka gani wanafundisha kuhusu JINA LILE-YESU KRISTO, na
Imani hiyo, Mitume hawasiti kusimama kwa lililo kweli. Petro bila kupepesa
macho anasema, “Jueni
ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa
Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina
hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu,” Mdo 4:10. Kiongozi wa dini leo
ambaye anapenda kupata sifa na kupendwa na wote, na hasa wanasiasa ambao kwao
rushwa ni sifa ya utumishi bora, hakika mbele ya JINA HILI, kiongozi huyu
atakuwa na swali kubwa la kujibu.
Petro kama walivyokuwa Mitume wengine hawakuwa na elimu ya
ajabu sana zaidi ya stadi za kupambana na maisha ya kila siku. Petro Mtume kama
walivyo wengine katika kundi hili la Mitume, walikuwa wavuvi. Watu hawa kwa
mang’amuzi yao ya maisha, ilikuwa ni jambo la ajabu kutoa elimu hii ya wokovu
juu ya siri ile kubwa ya Ufalme wa Mungu na Uzima wa milele kwa wale waliokuwa
wamebobea kwenye uwanja huo kama Waandishi, Mafarisayo na Masadukayo. Jambo
hili linatupa ukweli wa nguvu na mwongozo wa Roho Mtakatifu kwa Kanisa hili la
Mwanzo. Leo, tunamwitaji sana huyu Roho Mtakatifu katika Kanisa, na siyo majina
na vyeo visivyokuwa na uhusiano wa moja kwa moja na maisha yetu ya Imani na ya
Kiroho. Wapendwa huu ndio ukweli kwamba, “Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana
hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi
kuokolewa kwalo,” Mdo 12.
Tunapojaribu kuchenga ukweli huu, tunakuwa nje ya kweli
mzima ya mafundisho ya Kristo na lengo zima la umilele wa maisha haya
tunayoyaishi. Mara kwa mara kunakuwa na vishawisha vya kurudi nyuma na kufanya
yale tuliyoyazoea. Hata Mitume hawakuweza kukwepa hali hiyo, kwani maisha yao
na ukuuaji wao wa Imani ulilandana sana na maisha na mazingira yao. Hivyo Mtume
Simon Petro anawaambia wenzake, “Naenda kuvua samaki.
Nao wakamwambia, Sisi nasi tutakwenda nawe. Basi wakaondoka, wakapanda
chomboni; ila usiku ule hawakupata kitu,” Yoh 21:3.
Wapendwa
wana wa Mungu, tunapokuwa nje ya mpango mzima wa Mungu, na hasa kwa wale
tuliopewa thamana hiyo, mafanikio ya yale tuyatamaniyo huwa hewa na kutoweka
kabisa. Kumhubiri Kristo na kumshuhudia kwa maneno na matendo ni kazi ya kila aliyebatizwa na kuimarishwa. Hivyo basi,
yatupasa kulifanya tendo hilo pasipo shaka. Kristo hachoki tukumbusha
tunapokengeuka kuhusu ukweli huu. Kristo aweza kutumia njia mbalimbali
kuwakilisha ujumbe wa kweli hii. Kwa upendo wake, Kristo mara zote anapenda
kujua mahangaiko yetu, na kuturudisha katika mstari. Katika hali ya kuchoka na
uchovu mwingi kwa kupigika usiku kucha bila kupata samaki, anawaambia wanafunzi
wake, “Wanangu, mna kitoweo? Wakamjibu, La,” Yoh 21:5. Kwa maana
nyingine Yesu anataka kutuambia, Je, mnapozifuata njia zenu na kuacha maagizo
yangu mnapata mafanikio?
Kuonyesha
ukweli wa jambo hili, Yesu Kristo, anawafundisha njia na maagizo yake yaliyo
kweli na sahihi kwa uzima wa mwili na roho. “Akawaambia, Litupeni
jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata. Basi wakatupa; wala sasa
hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki,” Yoh 21:6.
Wapendwa
katika Kristo, yawezekana ushapigana sana na maisha kiasi kwamba kila siku ni
aheri ya jana. Jambo la kwanza usitafuta mchawi wala kwenda kwa waganga, au kusafisha
nyota kama tunavyosikia wengi wakidanganywa. Jambo la kwanza chunguza uhusiano
wako na Mungu. Je, umelitupa jarife hilo upande wa kuume wa chombo chako yaani,
maisha yake? Je, unaisha kadiri ya matakwa ya Mungu? Kama hapana, Je,
unaridhika na hali hiyo? Kama siyo, Je, ni kitu gani kinachokukwamisha
kurejesha uhusiano huo? Kama uhusiano wako na Mungu ni mzuri na bado unapigika
sana na maisha, jambo hilo unalichukuliaje? Je, walichukulia kama kusahauliwa
na Mungu, au kutokutendewa haki na Mungu? Je, unaelewaje subura ya Mungu kwa
yale uyaombayo na kuyatamani?
Ndugu
yangu, hakuna jambo lolote tuombalo Mungu aache kutupatia. Kama itatokea kwa
hapa duniani hatukulipata basi jua umeandaliwa jambo hilo kwa umilele wake,
mara baada ya maisha haya ya hapa duniani. Kamwe Mungu hamtupi mja wake. Kwa
wale ambao Mungu ametukirimia zaidi na hata kupita mahitaji yetu,
tunachukuliaje jambo hilo? Je, tunamtambua Mungu katika mali na utajiri wetu?
Ukweli ni kwamba kamwe hatutaweza mtambua Mungu kwa yale tuliyonayo, kama
hatuna upendo na Mungu. Yohane Mtume anamtambua Kristo kwa sababu alikuwa na
upendo wa dhati kwa Kristo na Kristo alikuwa anampenda kwa namna ya pekee. Na
hivi ndiyo Injili inavyotuambia, “Basi yule mwanafunzi
ambaye Yesu alimpenda akamwambia Petro, Ndiye Bwana,” Yoh 21:7.
Kumtambua
huku Kristo, Yohani habaki na hali hiyo mwenyewe. Anamwambia na Petro pia. Je,
tunapoguswa na upendo wa Kristo na Mungu tupo tayari kuushirikisha kwa wenzetu
nao wapate wokovu huo? Tunaona baada ya Petro Mtume, kusikia habari hiyo,
anajitosa kwenye maji maana alikuwa uchi. “Naye Simoni Petro, aliposikia ya
kwamba ni Bwana, akajifunga vazi lake, (maana alikuwa uchi), akajitupa
baharini,” Yoh 21:7b. Mpendwa tunayesafari wote katika tafakari hii, Petro kuwa
uchi hapa kunamaanisha kwa upande mwingine kwamba anatambua kujikwaa kwake
kunakotokana na kutokuyafanya yale aliyopaswa kufanywa kama kiongozi, kama
niliyoeleza hapo mwanzo.
Mara
baada ya Petro kujitambua, anaingia chomboni na hapa tunaona maajabu haya. “Basi Simoni Petro akapanda chomboni, akalivuta jarife pwani,
limejaa samaki wakubwa, mia hamsini na watatu; na ijapokuwa ni wengi namna
hiyo, jarife halikupasuka,” Yoh 21:11. Ndugu yangu, jarife hili halina tofauti
na Kanisa kama chombo cha wokovu ambacho kazi yake kubwa ni kuwavuta watu kwa
Kristo na kuwapeleka kwake wakiwa salama. Usalamu huu ni idadi inayotolewa ya
samaki hawa. Tutajulikana kwa idadi yetu mbele za Mwanakondoo. Nasi tukifika
mbele ya uso wa Mungu tutajulikana kwa idadi, na wale tuliopewa kazi hiyo
yatupasa tutoe hesaba ya idadi tulioifikisha mbele ya Mungu na Mwanakondo.
Hata
hivyo tunasikia jarife hili-Mtego huu, haukupasuka licha ya wingi wa samaki
wale. Jibu ni kwamba mtego haukupasuka kwa sababu u imara. Mtego, yaani Jarife
kama Kanisa, na Sakramenti ya wokovu wetu, uimara wake unatokana na uwepo wa
nguvu ya Roho Mtakatifu, ambaye uyaratibisha yote kadiri ya mahitaji ya Kanisa
lake kwa nyakati zote. Tumruhusu Roho Mtakatifu huyu afanye kazi yake, na siyo
Roho Mtakavitu. Roho Mtakavitu atalipasua JARIFE-KANISA. Roho Mtakavitu huyu
ni: SIFA, CHEO, KUJULIKANA KULIKO BINAFSI, MAMLAKA MBELE ZA WATU, NA MBAYA
ZAIDI KWA VIONGOZI WALA RUSHWA. Tusichoke kuhubiri na kuishi kwa vitendo Huruma
ya Mungu kwa sababu hata hawa viongozi wala rushwa, wote wasio na hofu ya Mungu ndani yao, na
sisi sote kwa ujumla wetu kama Kanisa na wabatizwa tunahitaji huruma hiyo na
wokovu wa Mungu.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana
jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa
kwalo,” Mdo 12
Ee Yesu na Mwokozi
wetu, tujalie mara zote kuutafuta uso wako wa Huruma ili tuufikie uzima ule wa
milele uliyotuhaidia. Amina