jueves, 2 de julio de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 13 YA MWAKA-B

IJUMAA WIKI YA 13 YA MWAKA-B
3/7/2015
Somo: Mwa 23:1-4, 19; 24:1-8, 62-67
Zab: 105:1-2, 3-4a, 4b-5
Injili: Mt 9:9-13
Nukuu:
Bwana, Mungu wa mbingu, aliyenitoa katika nyumba ya babangu, na kusema nami katika nchi niliyozaliwa, aliniapia akisema, Nitawapa uzao wako nchi hii; yeye atampeleka malaika wake mbele yako, nawe utamtwalia mwanangu mke tokea huko; na yule mwanamke asipokubali kufuatana nawe, basi, utafunguliwa kiapo changu hiki; lakini usimrudishe mwanangu huko,” Mwa 24:7-8

Isaka akamwingiza Rebeka katika hema ya mama yake, Sara, akamtwaa Rebeka, akawa mkewe, akampenda; Isaka akafarijika kwa ajili ya kufa kwa mamake,” Mwa 24:67

Naye Yesu alipokuwa akipita kutoka huko aliona mtu ameketi forodhani, aitwaye Mathayo, akamwambia, Nifuate. Akaondoka, akamfuata,” Mt 9:9

Naye aliposikia, aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi,” Mt 9:12

Lakini nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka; kwa maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi,” Mt 9:13

TAFAKARI: “Nawe umeitwa kutukumika kwa ajili ya ufalme wa Mungu.”

Wapendwa wana wa Mungu, kwa namna ya pekee tujikumbushe sababu ya kuumbwa kwetu, kadiri ya katekesi tuliyoipata katika hatua za awali za ukristo wetu. Mafundisho haya ya Kanisa yanatufundisha kwamba “tumeumbwa ili tumjue, tumpende, tumtumikie na mwisho turudi kwake mbinguni.” Hii ndiyo sababu ya kuumbwa kwetu, na ndiyo sababu ya uwepo wetu hata dunia.

Ibrahimu anafahamu vizuri sababu ya kuumbwa kwake na ahadi zote Mungu alizofanya naye katika maisha yake yote. Pamoja na umri wake kusongea, Ibrahimu kamwe hakuweza kusahau maagano ya Mungu. Mke wake keshafariki, nawe amebaki na mwanawe Isaka. Isaka umri wa kuwa na mji wake umewadia. Ibrahimu kama Mzazi anayejali na kuwajibiki, anakuwa makini sana kumtafutia mtoto wake mke. Ibrahimu anayafanya haya yote kwa kutambua sababu ya uwepo wake. Naye anasema, Bwana, Mungu wa mbingu, aliyenitoa katika nyumba ya babangu, na kusema nami katika nchi niliyozaliwa, aliniapia akisema, Nitawapa uzao wako nchi hii; yeye atampeleka malaika wake mbele yako, nawe utamtwalia mwanangu mke tokea huko; na yule mwanamke asipokubali kufuatana nawe, basi, utafunguliwa kiapo changu hiki; lakini usimrudishe mwanangu huko,” Mwa 24:7-8. Hii ni changamoto kubwa kwa wazazi wetu wa leo. Familia zetu leo zinajiendea zenyewe kama saa za “SEIKO,” yaani ukishaijaza ufunguo unaiacha ijiendee yenyewe. Je, wewe kama Baba au Mama katika familia unakaa na watoto wako waliopevuka na kujua mahangaiko yao? Ni vyema kama mzazi ukatumia angalau nusu saa kila wiki kwa kuongea tu na watoto wako. Ni vizuri watoto wako kutofahamu ratiba hii. Yakupasa kama mzazi kuongelea mambo yale ya kawaida tena yanayozunguka jamii yako.

Isaka anapata jiko na huzuni aliyokuwa nayo kuhusu kufariki kwa mama yake Sara inatoweka. Isaka akamwingiza Rebeka katika hema ya mama yake, Sara, akamtwaa Rebeka, akawa mkewe, akampenda; Isaka akafarijika kwa ajili ya kufa kwa mamake,” Mwa 24:67. Huu ndiyo ule mkamilishano tunaouona katika fumbo la ndoa. Adamu akasema, Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume. Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja,” Mwa 2:23-24

Wapendwa wana wa Taifa ya Mungu, kila mmoja wetu kadiri ya wito wake, anapoishi hapa duniani yampasa kujua sababu ya kuumbwa kwake. Tunapojua sababu ya kuumbwa kwetu ni kwa namna hiyo twafahamu kuwa maisha ya kila mmoja wetu ni wito maalumu. Maisha kama wito, yanatudai kujitoa sadaka kwa kile tulichochagua kuishi kwa kuwezeshwa na Mungu mwenyewe. Leo katika Injili tunaona namna Mathayo alivyochaguliwa na mara kuacha mpangilia wa maisha yake ya zamani. Kuujua wito wako ni kuanza mpangilia mpya wa maisha yako. Hivyo,Naye Yesu alipokuwa akipita kutoka huko aliona mtu ameketi forodhani, aitwaye Mathayo, akamwambia, Nifuate. Akaondoka, akamfuata,” Mt 9:9. Ukweli ni kwamba tendo hili la kumfuata Yesu katika mazingira aliyokuwa nayo Mathayo, linamlazimu muhusika kujimamanua kutoka yale aliyojifungamanisha nayo. Mathayo anaamua kuiacha kazi yake ya ukarani na kumfuata Yesu ambaye hana chochote katika maisha linganishi, ila uzima wa milele. Yesu anasema, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake,” Lk 9:58. Kumfuata Yesu kwa ukaribu na uthabiti, kunatualika kuitafakari changamoto hii.

Kitendo cha Yesu kumchagua Mathayo kuwa mmoja wa Mitume wake na kula pamoja na wenye dhambi kinawakasirisha sana Mafarisayo. Yesu anawajibu Mafarisayo kwa kulenga sababu ya uwepo wake hapa duniani: Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi,” Mt 9:12. Yesu amekuja kwa sababu ya wale wenye uhitaji wa mwili na roho. Yesu amekuja kwa ajili ya wadhambi na wale wote wenye moyo wa hofu ya Mungu. Hili ndilo fumbo tunalotakiwa kulitafakari kila siku. Pili, ni Mungu peke yake wenye kutuhesabia haki. Hivyo, Lakini nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka; kwa maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi,” Mt 9:13. Ndugu yangu, embu ona Yesu anavyokupenda kupita upeo. Kuuthaminisha upendo huu ni kuishi kadiri ya mpango wa Mungu na yale yote Mwanaye Mpendwa aliyotufundisha.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU, NIONGOZE NA KUNILINDA KATIKA WITO ULIONIITIA.

No hay comentarios:

Publicar un comentario