JUMATANO WIKI YA 14 YA MWAKA-B
8/7/2015
Somo: Mwa
41:55-57; 42:5-7,17-24a;
Zab: 32
Injili: Mt 10:1-7
Nukuu:
“Watu wa nchi zote wakaja Misri kwa Yusufu; ili wanunue
nafaka; kwa sababu njaa imekuwa nzito katika dunia yote,” Mwa 41:57
“Wana wa Israeli wakaja wanunue chakula miongoni mwao
waliokuja, kwa kuwa kulikuwa na njaa katika nchi ya Kanaani,” Mwa 42:5
“Yusufu akawaona nduguze, akawatambua, lakini alijifanya kama
mgeni kwao,” Mwa 42:7a
“Wakaambiana, Kweli sisi tulimkosa ndugu yetu, kwa kuwa
tuliona shida ya roho yake, alipotusihi, wala hatukusikia kwa hiyo shida hii
imetupata,” Mwa 42:21
“Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya
pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina,” Mt
10:1
“Simoni Mkananayo, na Yuda Iskariote, naye ndiye mwenye
kumsaliti,” Mt 10:4
“Hao Thenashara Yesu aliwatuma, akawaagiza, akisema, Katika
njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wo wote wa Wasamaria msiingie. Afadhali shikeni njia kuwaendea
kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli,” Mt 10:5-6
“Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa
mbinguni umekaribia,” Mt 10:7
TAFAKARI: “Na tushinde ovu kwa wema.”
Wapendwa
wana wa Mungu, ni wachetu tu kati yetu tunapotazama historia ya maisha yetu na
kuona kwamba hatujaumizwa, na wala hatuna maumivu ya ndani. Hata hivyo ili
chuma kiwe imara na thabiti katika kuhimili mishindo na mitikisiko ya hali
kimazingira, yakipasa chuma kile kiwe kipite katika moto mkali. Chuma kuwa
imara ni ishara kwamba chuma kile kimepita katika moto mkali sana ambao umekipa
chuma mwono huo.
Mfano huu
wa chuma imara hauna tofauti na maisha ya kiroho yenye ukomavu. Ukomavu wa
maisha ya kiroho ni utambuzi ule wa kuona mbele zaidi hasa kwenye uzuri na
malengo ya maisha yako na wale wanaokuzunguka. Ni kuelewa kwamba upo hapa
nduniani kwa malengo maalumu. Ni kuwa na ufahamu kwamba ulikuwepo jana, upo leo
na kesho, na siku zote za maisha yako hapa duniani kama ‘mmisionari.’ Unapo
fahamu jambo hili kwa kina chake, kamwe huwezi kuongozwa na vionjo wala
ulipizaji wa visasi ambavyo hapo mwanzo vilikutesa na kuwa sababu ya kutokuwa
na mwelekeo chanya wa maisha.
Tulitazamapo
somo letu la kwanza na kulitafakari tunaweza kugundua ni kwa namna gani Yusufu
alivyoumiazwa kwa kutoswa na ndugu zake ikiwa sababu kubwa ya maumivu hayo ni
wivu. Yusufu aliuzwa utumwani, na baadaya kuwa na nafasi kubwa ya kuwaudumia
watu kama leo cheo cha Waziri Mkuu. Tunaona tatizo la njaa linakuwa sababu ya
kukutana na ndugu zake. “Watu wa nchi zote wakaja Misri kwa Yusufu; ili wanunue
nafaka; kwa sababu njaa imekuwa nzito katika dunia yote,” Mwa 41:57. Hakika
kama waswahili wasemavyo njaa haina adabu, ndivyo ilivyotokea kwa ndugu zake.
Mara nyingi Mungu anapotufundisha tuushinde uovu kwa wema,
hutukutanisha na wenzetu kwenye matukio ya kuhusunisha kama vile kifo, majanga
ya asili, na matukio ya magonjwa tusiyoweza kuyamudu na wala kuyafahamu. Hivi
ndiyo Yusufu alivyo ushinda uovu kwa wema kwenye tukio la njaa lililotokea
nyakati zake. “Wana wa Israeli wakaja wanunue chakula miongoni mwao
waliokuja, kwa kuwa kulikuwa na njaa katika nchi ya Kanaani,” Mwa 42:5. Hakika
hii ilikuwa nafasi nzuri sana ya Yusufu kulipiza kisasi kwa kile ndugu zake
walichomtenda. Yusufu alichokifanya ni hiki: “Akawaona nduguze, akawatambua,
lakini alijifanya kama mgeni kwao,” Mwa 42:7a. Yusufu anakaa kimya kuwapa ndugu
zake nafasi ya kujirudi na kuzisoma alama za nyakati. Baada ya kuchomwa na
dhamiri zao, ndugu zake wanatambua walichokitenda kwa Yusufu na kusemezana
wenyewe kwa wenyewe: “Kweli sisi tulimkosa ndugu yetu, kwa kuwa tuliona shida
ya roho yake, alipotusihi, wala hatukusikia kwa hiyo shida hii imetupata,” Mwa
42:21. Je, waswahili walikosea waliposema kufanya kosa si kosa ila kurudia kosa
ni kosa?
Ni vizuri kutambua pale tulipowaumiza wenzetu, au mwenzako na
kujaribu kwa namna yoyote ile kupaponyesha. Hili ni jambo la muhimu sana
tunapoishi kama familia, au jumuiya yoyote ile ya Kikristo. Kutambua kosa na
kufanya juhudi ya kuleta uponyaji, kitendo hicho hutuponya pia. Agizo la Yesu
kwenye injili ya leo linatupa fursa ya kupambana na uovu bila kushindwa. Yesu “akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya
pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina,” Mt
10:1. Hapa pia tunaalikwa kuushinda uovu kwa kutenda mema. Kama asemavyo Mt.
Agustino; “ovu ni kutokuwa na mafaa,” kushinda lililo ovu ni kutenda lililo
jema.
Ndugu yangu unayesafiri nami sasa, ‘misioni’ yetu hapa
duniani kama watu wenye hofu ya Mungu ni kuwarudisha kundini wale waopotea au
kukwazika kutoka na utendaji wetu wa awali au sasa. Ni mwaliko pia wa
kujisahihisha pale tunapokosea. Yatupasa sana kuepuka kishawishi kile cha
kusema ‘mkubwa na mwenye madaraka au cheo hakosei.’ Kasumba hii ni saratani
mbaya sana katika utume wetu kama Kanisa mahalia. Kama sisi ni binadamu, na
ndivyo tulivyo, basi kukosea kupo. Kama kukosea kupo, kutambua na kujirekebisha
ndipo kunakotuhesabia haki mbele ya Mungu juu ya utendaji wetu na dhamana
tuliyopewa na Mungu mbele za watu na kondoo wa malisho yake. Hivyo Yesu
anawatuma, na kuwaagiza, akisema, “Katika
njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wo wote wa Wasamaria msiingie. Afadhali shikeni njia kuwaendea
kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli,” Mt 10:5-6. Yesu analifanya hili kwa
Thenashara wote ili hali akijua mmoja wao atamsaliti. Hivyo,“Simoni Mkananayo, na Yuda Iskariote, naye ndiye mwenye
kumsaliti,” Mt 10:4. Je, twaweza kuushinda uovu kwa kuzidi kutenda lililo jema
na hata kuendelea kuona uzuri kwa wenzetu hata kama tumegundua njama na hila
zao? Katika jambo hili bila shaka Yesu anatukumbusha thamani ya mtu na utu
wake. Mt. Agustino anasema hivi: “usimchukie mtu yeye, bali zichukie tabia zake
mbaya.”
Mwisho kauli mbiu yetu: jana, leo, na kesho na iwe kuhubiri
kusiko kikomo kwamba ufalme wa mbinguni umekaribia. Tunalisema hili iliwa ndiyo
kauli mbiu ya Kanisa kama sakramenti ya wokovu wetu. Tunalihubiri hili kwa
wengine tukijua kwamba ndani yetu na nafsini mwetu twauona na kuuonja ufalme
huo. “Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema,
Ufalme wa mbinguni umekaribia,” Mt 10:7
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU TUJALIE NEEMA YA KUSHINDA UOVU KWA
KUTENDA MEMA. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario