sábado, 18 de julio de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 15 YA MWAKA-B

IJUMAA WIKI YA 15 YA MWAKA-B
17/7/2015
Somo: Kut 11:10-12:14
Zab: 115:12-13, 15-18
Injili: Mt 12:1-8
Nukuu:
Musa na Haruni walifanya ajabu hizo zote mbele ya Farao; Bwana akaufanya moyo wa Farao kuwa mgumu, asiwape wana wa Israeli ruhusa watoke nchi yake,” Kut 11:10

Lakini nawaambieni, kwamba hapa yupo aliye mkuu kuliko hekalu,” Mt 12:6 

Lakini kama mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia,” Mt 12:7 

TAFAKARI: “Mungu anayathamini maisha yako kuliko kitu kingine chochote.”

Wapendwa wana wa Mungu, mara nyingi katika tafakari zangu nanyi nimekuwa nikikuambia kwamba wewe si bahati mbaya. Mungu wetu huyu, “anayathamini maisha yako kuliko kitu kingine chochote.” Mungu kwa kulifanya hili katika dhamiri iliyo safi, huthamini sana maisha yetu kwani yanachapa yake. Yeye ametuumba kwa sura na mfano wake. Hawezi kamwe kutupoteza kwa jambo lolote lile. Lakini kwa kutufundisha, mara nyingine husababisa ugumu wa kufikia lengo lile kwa kusababisha ugumu fulani. Mungu anachotaka tujifunze kutoka kwake ni hiki: “Maisha yako ni ya thamani kubwa sana. Maisha yako ndiyo utajiri wako. Huwezi kupanga wala kuwa karibu na Mungu wako kama maisha yako ni mgogoro. Ukiwa na afya njema waweza kusali vizuri na hata kuyaboresha maisha yako kama yamekwenda kombo.” Pili tunaimarishwa katika taabu na dhiki. Hivyo jambo hili linatokea kwa Musa. Musa na Haruni walifanya ajabu hizo zote mbele ya Farao; Bwana akaufanya moyo wa Farao kuwa mgumu, asiwape wana wa Israeli ruhusa watoke nchi yake,” Kut 11:10. Hapa kwa tendo hili, wana wa Israeli wanaandaliwa kwa lile lililo jema zaidi mbele ya safari.

Wapendwa wana wa Mungu, Mungu hapendi sadaka zetu zisizo na uhusiano wa maisha yetu na thamani yake. Mungu wetu hupenda rehema na neema anazotujalia pale tunapoziishi kuliko kile tumtoleacho kama sadaka. Yote tumtoleayo ni mali yake. Vyote vipo chini ya mamlaka yake. Hivyo Yesu anasema, Lakini kama mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia,” Mt 12:7. Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka kutokana na mila na desturi zetu, wakati fulani tulilazimika kufanya mitambiko na hata kutolea sadaka za kuteketezwa zisizo na uhusiano na imani yetu. Kwa kufanya hivi tunapoteza dira na mwelekeo wa Kimungu katika maisha yetu. Je, naweza kuwa huru hata kama naishi katika mila na desturi hizi?

Tumsifu Yesu Kristo.

EE YESU, TUWEZESHE TUYAONA MAISHA YETU KAMA MALI YA MUNGU NA ZAWADI YA MUNGU. AMINA


No hay comentarios:

Publicar un comentario