lunes, 13 de julio de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 15 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 15 YA MWAKA-B
14/7/2015
Somo: Kut 2:1-15a
Zab: 68
Injili: Mt 11:20-24
Nukuu:
Mtoto akakua, naye akamleta kwa binti Farao, akawa mwanawe. Akamwita jina lake Musa, akasema, Ni kwa sababu nalimtoa majini,” Kut 2:10

Hata siku zile, Musa alipokuwa mtu mzima, akatoka kuwaendea ndugu zake, akatazama mizigo yao. Akamwona Mmisri anampiga Mwebrania, mmojawapo wa ndugu zake. Basi akatazama huko na huko, na alipoona ya kuwa hapana mtu, akampiga Mmisri yule, akamficha ndani ya mchanga,” Kut 2:11-12 

Basi Farao alipopata habari, akataka kumwua Musa; lakini Musa akakimbia mbele ya Farao, akakaa katika nchi ya Midiani; akaketi karibu na kisima,” Kut 2:15

“Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, wangalitubu zamani kwa kuvaa magunia na majivu,” Mt 11:21

Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe,” Mt 11:24 

TAFAKARI: “Sikio la kufa halisikii dawa.”

Wapendwa wana wa Mungu, msemo huu wa Kiswahili, “sikio la kufa halisikii dawa,” utusaidie katika tafakari yetu ya leo. Katika somo letu la kwanza tunaona namna ambavyo Musa anavyookolewa na kutunzwa kwa namna ya ajabu hadi kuwa mtu mzima na kuendeleza kazi ile ya ukombozi wa wana wa Israeli. Mtoto akakua, naye akamleta kwa binti Farao, akawa mwanawe. Akamwita jina lake Musa, akasema, Ni kwa sababu nalimtoa majini,” Kut 2:10. Mtoto huyu aliyeokolewa kutoka majini, Musa, anakuwa kielelezo na mkono wa Mungu. Hata hivyo Musa anapata upinzani kutoka kwa ndugu zake licha ya utetezi wake na juhudi zake kuliokoa Taifa lake. Hata siku zile, Musa alipokuwa mtu mzima, akatoka kuwaendea ndugu zake, akatazama mizigo yao. Akamwona Mmisri anampiga Mwebrania, mmojawapo wa ndugu zake. Basi akatazama huko na huko, na alipoona ya kuwa hapana mtu, akampiga Mmisri yule, akamficha ndani ya mchanga,” Kut 2:11-12 

Ni jambo gumu sana kuelewa ubaya wa kitu ndani ya mfumo wa kitu kile. Waisraeli wangetamani sana kuendelea katika mateso yale kuliko kujaribu upande wa pili wa maisha wasiyoyajua. Ni hali ya kawaida binadamu kuwa na hofu kwa kile asichokijua, hasa mambo yale yamtoayo kwenye mang’amuzi yake ya kila siku. Hapa ndipo tunaposema, “heri nusu shwari kuliko shwari nzima.” Musa anajaribu kuwaonyesha upande wa pili wa uhalisia wa mambo, lakini ndugu zake wanafanya upinzani juu ya ukweli ule.

Nasi leo tunaitaji kutoka kwenye utumwa wa fikra na kuyaona mambo kama yalivyo. Tumejawa hofu ya tusichokijua na           tumekuwa watumwa kwa hofu hii. Hatuwezi kwenda mbele kama hatupendi kufanya tofauti ya yale tuliyoyazoea kila siku, na miaka yote. Ujasiri ya Musa unamtia matatani. Habari za mauaji ya yule Mmisri zilizovujishwa na jamaa yake Musa inakuwa sababu ya Musa kutoroka na kuinusuru roho yake. Basi Farao alipopata habari, akataka kumwua Musa; lakini Musa akakimbia mbele ya Farao, akakaa katika nchi ya Midiani; akaketi karibu na kisima,” Kut 2:15

Mara zote tunapopambana na kweli, au kujikwamua kwenye shida fulani, mawazo pingamizi hayakosekani. Ugumu huu wakati mwingine husababishwa na kutokuwa na ufahamu wa kutosha wa jambo lile. Huku ndiko tunaposema kwamba sikio la kufa halisikii dawa. Jambo hili ndilo analolisema Yesu anapoitazama miji ile iliyokithiri kwa uovu. “Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, wangalitubu zamani kwa kuvaa magunia na majivu,” Mt 11:21. Ni mara ngapi tunaambiwa ukweli wa mambo lakini mara zote tunabakia na ushabiki usiokuwa na tija yoyote? Kwa nini hatupendi kuona ukweli kama ulivyo na badala yake tunaupindisha? Katika jambo hili, Yesu anatupa angalisho na kusema, Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe,” Mt 11:24.

Wapendwa, hawatashuka malaika kutoka mbinguni na kutuambia mambo haya zaidi ya watu wenye uelewa tunaoishi nao kila siku kutuambia kweli hiyo. Mungu utumia watu wake kulisemea lile lililo ovu. Watu wenye maadili mema na mwono chanya, walisemapo jambo yatupasa kusikia na kulipembua kwa kina. Je, yote yasemwayo kuhusu maisha yako, hali yako, na Taifa lako hayana ukweli? Je, unaridhika na hali hii? Umechukua hatua yo yote?

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU YAFUNGUE MACHO, MIOYO NA AKILI ZETU ILI TUYAONE MAMBO KAMA YALIVYO. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario