JUMATANO WIKI YA 15 YA MWAKA-B
15/7/2015
Somo: Kut 3:1-6, 9-12
Zab: 102:1-4, 6-7
Injili: Mt 11:25-27
Nukuu:
“Naye akasema,
Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama
ni nchi takatifu,” Kut 3:5
“Basi, tazama, kilio
cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri
wanawatesa,” Kut 3:9
“Tena akasema, Mimi ni
Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa
akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu,” Kut 3:6
“Musa akamwambia
Mungu, Mimi ni nani, hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli watoke
Misri?” Kut 3:11
“Wakati ule Yesu akajibu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana
wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia
watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako,” Mt
11:25-26
TAFAKARI: “Mungu
huyatenda makuu kwa wanyenyekevu wa Moyo.”
Wapendwa
wana wa Mungu, tuitazamapo historia ya wokovu wetu, tunagundua kwamba Mungu
hufanya kazi na wale wajishushao na wanyenyekevu wa Moyo. Licha ya tabia na
mwono huu wa Kimungu, wale wate wanoshirikishwa mpango wa Mungu katika tendo la
Kimungu, huwa ni watu wa kawaida sana, na mara nyingine huwa wale
waliodharaulika na jamii husika. Mama Bikira Maria ni mmoja wa wale
walioshiriki mambo makuu ya Mungu katika unyonge na unyenyekevu wake. Naye
Bikira Maria analitambua jambo hili na kusema,
“Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama,
tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa,” Lk 1:48. Bikira Maria anatambua pia kile
kinachotendeka kwake ni upendeleo wa Mungu ndani mwake, na hivyo kinamakusudio
makubwa kadiri ilivyompendeza Mungu. Naye anasema, “Amewaangusha wakuu katika
viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:52. Jambo hili linatokea pia
kwa Musa ambaye anapokea misioni hiyo kama kiongozi wa wana Waisraeli kuwatoa
kutoka utumwani Misri.
Kazi
anayopewa Musa inamlazimu kuyaacha yote yale yaambatanayo katika maisha yake
ambayo hayampendezi Mungu. Mungu anapompa majukumu haya mazito na muhuhi anampa
angalisho na kusema, “Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana
mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu,” Kut 3:5. Wapendwa wana wa Mungu,
kuvivua viatu ni kuenenda na kufanya katika hali halisi ya kile ulichotumwa kufanya
bila kuwa na hisi fulani kama miwani ya kutazamia uhalisia wa mambo. Mara
nyingi tumewahukumu watu na hata kuwatenda ndivyo sivyo kutokana na mang’amuzi
yetu yasiyoendana na uhalisia wa jambo. Mara nyingi tumewahukumu watu kutokana
na historia zetu mbaya. Na mara nyingine tumeenda mbali zaidi katika kutenda na
kuhukumu kulikotokana na simulizi za chuki juu ya wale tunaoishi nao zisizo za
kweli. Hivyo kuvivua viatu ni kuzama ndani kabisa katika mila na desturi za
watu tuliotumwa kwao ili kujua ukweli wa mambo. Yatupasa kuweka kando nadhania
zetu za vitu, na kuuona ukweli kama ulivyo. Hili ndilo jambo la msingi Musa
ilimpasa kulijua kabla ya kulitenda lile Mungu alilotaka alitende juu ya watu
wake.
Wapendwa,
mara zote mjumbe hulifanya lile alilotumwa kulifanya na Bwana wake. Hatupaswi
kubadili ujumbe ule kwa kujiinua nafsi zetu. Hivyo Mungu anamtaka Musa alitende
lile aliloliona juu ya mateso ya Wana wa Israeli. “Basi, tazama, kilio
cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri
wanawatesa,” Kut 3:9. Agizo na mamlaka haya yanatoka kwa Mungu mwenye Mungu na
aliye hai. “Mimi ni Mungu wa baba
yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso
wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu,” Kut 3:6. Neno hili ni lenye nguvu,
na Mungu wetu ni Mungu mwenye wivu na kile alichokiumba kwa sura na mfano wake.
Hata hivyo, kazi aliyopewa Musa haikuwa rahisi. Hivyo Musa anajipima nguvu na
ushawishi aliokuwa nao kwa watu wake na mtesi wake, Farao, na kujiona mdogo na
dhaifu. Naye akamwambia Mungu, “Mimi ni nani, hata
niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli watoke Misri?” Kut 3:11. Huu ndio unyenyevu wa Musa mbele ya
Mungu. Ndugu yangu, yapo mambo mengi katika utume wetu kila mmoja kadiri ya
wito wake, kwa nguvu zetu wenyewe hatuwezi kufikia malengo. Hivyo tunahitaji
msaada wa Mungu.
Kujishusha huku na kuwa
wanyenyekevu mbele ya Mungu mwenye kuyaweza yote, ndiko kunakotutafakarisha
maneno na sala hii ya Yesu katika Injili ya leo: “Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi,
kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto
wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako,” Mt
11:25-26. Je, twatoa shukrani kwa Mungu hata kwa kile kidogo Mungu
alichotuwezesha kukifanya? Je, mafanikio niyapatayo natambua ni mkono wa Mungu,
au ni akili zangu na ujanja wangu? Ndugu yangu, ‘moyo usio na shukrani hukausha
mema yote.’
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU NIJALIE FADHILA YA UNYENYEKEVU. AMINA.
No hay comentarios:
Publicar un comentario