ALHAMISI WIKI YA 14 YA MWAKA-B
Somo: Mwa 44:18-21, 23b-29; 45:1-5
Zab: 104
Injili: Mt 10:7-15
Nukuu:
“Basi sasa, msihuzunike, wala msiudhike nafsi zenu, kwa
kuniuza huku; maana Mungu alinipeleka mbele yenu kuhifadhi maisha ya watu.” Mwa
45:5
“Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni
pepo; mmepata bure, toeni bure,” Mt 10:8
“Na mtu asipowakaribisha wala kuyasikiliza maneno yenu,
mtokapo ktika nyumba ile, au mji ule, kung’uteni mavumbi ya miguuni mwenu,” Mt
10:14
TAFAKARI: “Tusichoke kutenda lililo jema na lenye kumpendeza Mungu.”
Wapendwa wana wa Mungu, katika ulimwengu tunaoishi leo
unatutaka kufanya yale tu yanaotufurahisha moyo, na yale tu yanayotupa faida.
Nje ya mafao hayo ni vigumu kufanya yale yanayompendeza Mungu. Masomo ya leo
yanatufikarisha kuona furaha na umuhimu wa kufanya lililo jema na lenye
kumendeza Mungu, hata kama kwa macho yetu na mtazamo wetu itaonekana ovyo.
Yusufu analiona hilo na kuwaambia ndugu zake
maneno haya: “Basi sasa, msihuzunike, wala msiudhike nafsi zenu, kwa
kuniuza huku; maana Mungu alinipeleka mbele yenu kuhifadhi maisha ya watu.” Mwa
45:5. Ni kweli kwamba ndugu zake Yusufu walifanya kitendo kiovu sana kwa
kumuuza. Pamoja na maumivu haya, Yusufu haoni sababu ya kutosamehe na kuanza
upya katika kumtumikia Mungu.
Katika somo letu la Injili tunaona usia wa Yesu wa kuhimiza
maisha ya kutenda mara zote lile lililo jema na lenye kumpendeza Mungu kama
tutatenda bila kujibakiza. “Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye
ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni bure,” Mt 10:8. Jambo la msingi la
kuelewa juu ya ukweli huu ni kwamba tufanyacho ni kwa mkono wa Mungu nasi
twafanya tu kama watumishi wanaotimiza wajibu wao msingi.
Ndugu yangu, tuyafanyavyo mambo haya hatufanyi kwa
kumpendekeza mtu, bali twayafanya kwa kutimiza wajibu wetu na hasa kwa kufanya lile linalompendeza
Mungu. Hivyo, “Na mtu asipowakaribisha
wala kuyasikiliza maneno yenu, mtokapo katika nyumba ile, au mji ule,
kung’uteni mavumbi ya miguuni mwenu,” Mt 10:14. Kukung’uta mavumbi ya miguu ni
kutenda lililo jema na kutokutegemea shukrani yoyote. Kama wapo watakao beza
tendo hili la wema, adhabu yake ni hapa hapa duniani.
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU NIJALIE NEEMA YA KUTENDA LILILO JEMA SIKU ZOTE ZA
MAISHA YANGU. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario