sábado, 18 de julio de 2015

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 15 YA MWAKA-B

ALHAMISI WIKI YA 15 YA MWAKA-B
16/7/2015
Somo: Kut 3:13-20
Zab: 104:1, 5, 8-9, 24-27
Injili: Mt 11:28-30
Nukuu:                              
Mungu akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO; akasema, Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli; MIMI NIKO amenituma kwenu,” Kut 3:14

Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha,” Mt 11:28 

Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu,” Mt 11:29 

kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:30

TAFAKARI: “Utulivu wa kweli twaupata ndani na katika Kristo.”

Wapendwa wana wa Mungu, kuzaliwa si lazima, ili kufa kama umeshazaliwa ni lazima. Ikiwa tupo hai na tunaishi, hatuwezi kudumu katika hali hiyo siku zote bila kuwa na mahangaiko. Binadamu huyapata mahangaiko yatokanayo na magonjwa, njaa, hali ya hewa, na hata hali mbaya ya siasa. Hali mbaya ya siasi huwa pia chanzo cha mahangaiko na kuwafanya watu kuwa wakimbizi katika inchi yao yenyewe, vifo vya watoto, akina mama na watu wasio na hatia yoyote.

Ndugu yangu, tunayaona mahangaiko pia kwa wana wa Israeli katika safari ya ukombozi kutoka inchi Misri. Hivyo Musa anapopewa majukumu la kuliongoza Taifa hili kutoka utumwani Misri, anataka kujua uhakika wa kile alichoambiwa na Mungu. Mungu akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO; akasema, Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli; MIMI NIKO amenituma kwenu,” Kut 3:14. Huyu ndiye Mungu hai tunayemwamini na kumwabudu.

Leo kwa yeyote yule mbatizwa na mwenye kumwamini Kristo, anapata kitulizo cha kweli ndani na katika Kristo. Ni kupitia Kristo wote twaweza kuiona nuru na kuishi katika nuru ya kweli. Hakuna jina lingine hapa dunia twaweza kuokolewa nalo nje ya jina hili, Yesu Kristo. Yesu ndiye njia, kweli na uzima wetu. Yesu anasema, Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha,” Mt 11:28. Kiboko cha mahangaiko yetu kama watu waaminio na wafuasi wa Kristo ni Yesu mwenyewe. Mizigo yetu na taabu zake zote ni Kristo mwenyewe anayeweza kutubebea tukiwa naye. Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha,” Mt 11:28. Hakuna pumzisho la kweli nje ya Kristo. Mwongozo wa kweli katika mahangaiko yetu ni Kristo mwenyewe. Mwongozo wake ni UPENDO, na hii ndiyo nira yake. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu,” Mt 11:29. Ndugu yangu kwa nini hupendi kupenda? Kwa nini humpendi huyo uliye weka mipaka naye? Je, Yesu angefanya hayo unayoyafanya?

Ndugu yangu, ukipenda katika kweli yote, yote huwa mepesi. Kipimo cha kupenda kinawiana na kipimo cha kusamehe. Usipo kuwa mwepesi wa kusamehe bado hujaijua kweli ya Mungu. Katika hili Yesu anasema, kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:30. Ndugu yangu, ni mzingo upi ulio nao ni mzito ambao Yesu atashindwa kuubeba?

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU KRISTO, TUJALIE IMANI YA KWELI. AMINA.

No hay comentarios:

Publicar un comentario