jueves, 2 de julio de 2015

TAFAKARI: MTAKATIFU TOMASO, MTUME

MTAKATIFU TOMASO, MTUME
3/7/2015
Somo: Efe 2:19-22
Zab: 116
Injili: Yoh 20:24-29
Nukuu:
Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni,” Efe 2:20 

Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho,” Mt 2:22

Basi wanafunzi wengine wakamwambia, Tumemwona Bwana. Akawaambia, Mimi nisipoziona mikononi mwake kovu za misumari, na kutia kidole changu katika mahali pa misumari, na kutia mkono wangu katika ubavu wake, mimi sisadiki hata kidogo,” Yoh 20:25

Kisha akamwambia Tomaso, Lete hapa kidole chako; uitazame mikono yangu; ulete na mkono wako uutie ubavuni mwangu, wala usiwe asiyeamini, bali aaminiye,” Yoh 20:27

Tomaso akajibu, akamwambia, Bwana wangu na Mungu wangu!” Yoh 20:28 

Yesu akamwambia, Wewe, kwa kuwa umeniona, umesadiki; wa heri wale wasioona, wakasadiki,” Yoh 20:29

TAFAKARI: “Majeraha ya Utukufu ya Yesu, Tomaso aponywa majeraha yake ya ndani.”

Wapendwa wana wa Mungu, kanuni ya Imani ile ndefu tunakiri maneno haya na ndiyo msingi na mafundisho ya Kanisa: “Nasadiki kwa Kanisa moja, Takatifu, Katoliki, la Mitume.” Leo kutokana na siku hii maalumu ambapo Mama Kanisa anafanya kumbukumbu ya Tomaso Mtume, ni vyema katika tafakari yetu tukajikita kwenye hicho kipengele cha Mwisho, Mitume. Imani yetu ujengwa na kuelekezwa kwa mafundisho yenye kubeba mamlaka zifuatazo: Mamkala ya Kimungu, Mamlaka ya Kristo, Mamlaka ya Maandiko Matakatifu, Mamlaka ya Kanisa, Mamlaka ya Mitume (mamkaka fundishi ya Kanisa/magisterium). Mamlaka zote hizo chanzo chake ni Mamlaka ya Kimungu/Divine Authority. Tunapomtazama leo Tomaso tunamtazama katika mamlaka ya Mitume, ambayo iliwekwa na Yesu Mwenyewe na kuachwa katika uongozi wa Mitume, Petro akiwa ndiye kiongozi Mkuu.

Hivyo Kanisa letu, tena Katoliki limejengwa katika mamlaka hiyo ya Mitume. Mtume Paulo anatukumbusha jambo hilo kwa kusema, Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni,” Efe 2:20. Nasi leo katika Kristo Yesu, kwa sakramenti ya ubatizo , tumejengwa katika msingi huo wa mitume na kuwa maskani ya Mungu katika Roho. Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho,” Mt 2:22. Hivyo hatupaswa kuwa na shaka yo yote juu ya msingi huu wa Kanisa, na chini ya Mitume wake. Mtume Tomaso anajulikana sana kama Tomaso mwenye shaka. Tomaso mwenye shaka hakuamini ufufuko wa Yesu, hivyo anabakia na majeraha yake ya kutokupenda. Tomaso anaitaji uponyaji. Kujua hatua za uponyaji huu wa Tomaso yatupasa kuanza nyuma kidogo kuanzia ule mstari ya 19b, yaani Yoh 29:19b.

Jambo hili la kutokupenda kutokana na majeraha na kuumizwa kwetu, linaonekana wazi katika Injili ya leo ambapo tunaona watu wawili (Yesu Kristo Mfufuka na Mtume Tomaso) waliojeruhiwa, ambao mwisho wa siku mmoja wao (Yesu Kristo Mfufuka) anamponya mjeruhiwa mwenzake (Tomaso).

Uponyaji wa kwanza anaoutoa Yesu Kristo kwa wanafunzi wake ni kuiondoa hofu kwa salamu yake ya upendo, “Akaja Yesu, akasimama katikati, akawaambia, Amani iwe kwenu,” Yoh 20:19b. Tendo hili la kuwa na Amani ya kweli ndiyo mwanzo wa kuanza kupenda kuliko kwa kweli na furaha ya kweli. Wanafunzi wa Yesu wanaonyesha furaha hii, na kuanza kupenda tena, ingawa Mtume Tomaso hawakuwepo katika kundi. Naye Yesu baada ya salamu ya upendo iliyojaa matumaini mapya, “akawaonyesha mikono yake na ubavu wake. Basi wale wanafunzi wakafurahi walipomwona Bwana,” Yoh 20:20. Furaha hii inaendana na maagizo ya kufanya anayoyatoa Kristo kwa wanafunzi wake. Naye Kristo akawavuvia, akawaambia, “Pokeeni Roho Mtakatifu. Wowote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa,” Yoh 20:22-23. Kristo hapendi furaha ya kweli aliyotupatia tubaki nayo wenyewe. Hivyo furaha hii twapasa kuisambaza kwa wengine kila mmoja kadiri ya wito wake, vipaji vyake, dhamana na nafasi yake katika jamii anayoishi. Ndugu yangu ukiona hapo unapoishi hata mbwa wanakukimbia bila sababu, ujue wewe ni shiiiiida!

 Tomaso aliporejea anakokujua mwenyewe kwa kupoteza imani yake juu ya Kristo, anapoambiwa jambo hili la kuonekana kwa Kristo, hakuamini hata kidogo. Naye kwa ufahamu wake anatoa vigezo vya kutambua ukweli aliousikia kutoka kwa wenzake. Naye anatoa vigezo na masharti ambavyo lazima vizingatiwe. “Mimi nisipoziona mikononi mwake kovu za misumari, na kutia kidole changu katika mahali pa misumari, na kutia mkono wangu katika ubavu wake, mimi sisadiki hata kidogo,” Yoh 20:25. Kwa masharti haya na vigezo hivi tunaweza kuona ni kwa jinsi gani Tomaso alijeruhiwa na kusononeshwa kwa tukio la kifo cha Bwana wetu Yesu Kristo.

Wapendwa, baada ya siku nane, tunaona tukio la kukutana kwa wajeruhiwa hawa wawili, yaani Yesu Kristo Mfufuka na Mtume Tomaso. Mjeruhiwa wa kwanza ni Yesu Kristo. Yesu anamkuta Tomaso na kumwonyesha majeraha yake, na kusema, “Lete hapa kidole chako; uitazame mikono yangu; ulete na mkono wako uutie ubavuni mwangu, wala usiwe asiyeamini, bali aaminiye,” Yoh 20:27. Tendo hili la Yesu kumwonyesha Tomaso majeraha yake na kuumizwa kwake kunatoa picha ya majivuno ya Yesu na wakati mwingine kama kujigamba vile. Jambo hili lina ukweli wake kwa katika mtazamo huu wa majeraha na makovu aliyokuwa nayo Yesu. Majereha ya Kristo na maumivu yake hayakuwa majeraha ya kushindwa, bali majeraha ya UPENDO WA KWELI. Majeraha ya Kristo yalikuwa majeraha ya USHINDI uliotukuka. Hayakuwa majeraha ya kuuma, bali majeraha ya UTUKUFU. Ni majeraha ya UPENDO. Upendo ambao upo tayari kujitoa sadaka bila kipimo na kutojibakiza. Kristo anaonyesha ubavu wake na mikono yake ilivyotobolewa si kwa kujionyesha au kuhukumu, bali kuonyesha uzito na undani wa upendo wake kwa Mitume na kwetu sote.

Japokuwa Tomaso hakuwa na majereha kwenye ngozi yake, na hakuwa na kuvuja damu kutoka mwilini mwake, majeraha yake yalikuwa ndani ya moyo wake. Haya ni maumivu ya ndani. Moyo wake ulijeruhiwa kwa kusitikishwa na kifo cha Bwana wake. Alijisikia kudanganywa na Bwana wake Yesu Kristo. Alijisikia kushindwa baada ya kuyaweka matumaini yote kwa Kristo kwa sababu alifikiri Yesu Kristo ni Masiha, Mfalme, na kuhoji kwa nini Yesu afe kifo katili kama kile cha msalaba. Alifikiri Yesu Kristo angeikomboa Israeli kutoka kwenye dola ya Kirumi. Anajiuliza hivi, kwa nini hata yeye mwenye-Yesu ameshindwa kujinasua kutoka watesi wake? Mtume Tomasi alisikitishwa na kusijikia kusalitiwa na Yesu. Tomaso alishawishika kabisa kwamba alifanya uchaguzi usio sahihi kumfuata mseremala wa Galilaya. Kwa kweli Tomaso alikuwa na maumivu makubwa sana.

Wapendwa wana wa Mungu, maumivu na majeraha ya Moyo huchukua muda mrefu kupona. Majeraha haya na maumivu ya Moyo yanachukua kuda mrefu kupona kwa sababu twaweza kuyaficha na kujifanya hayapo. Twaweza kuongea na kutenda mambo yetu kama vile hakuna jambo lolote baya au upungufu wowote wetu. Wengi wetu twaweza kukaa katika hali hii kwa miaka mingi kwa kujivisha taswira nyingine na mwonekano mwingine ambao sio uhalisia wa kile kilicho ndani mwetu ingawa tunaendelea na mateso na maumivu hayo. Lakini ukweli ni kwamba hatuwezi kudumu katika hali hii kwa muda wote na nyakati zote. Mara tutaanza kujisikia vibaya na kujisikitikia na kufikiri marafiki zetu wametutenga na wapo mbali bila kutusikiliza maumivu yetu yanayotusonga moyoni. Mara tunajisikia kwamba hawajali na wanaubaridi kuhusu maumivu yetu, na hivyo kuwachukia pia.

Hivyo, katika kukutana kwa wawili hawa, mmoja wao yaani Yesu Kristo ana majeraha ya UTUKUFU, na mwingine yaani Tomaso ana majereha ya maumivu ya ndani. Yesu Kristo alikuwa tayari kujiponya kwa nguvu ya majeraha yake. Tomaso alihitaji kuponywa majeraha yake lakini hapakuwa na mtu wa kumponya. Hapa ndipo wanapokutana wajeruhiwa hawa wawili. Mjeruhiwa wa kwanza anamponya wa pili. Uponyaji huu unajionyesha kwa maneno ya Tomaso mwenyewe anapomjibu Kristo baada ya Kristo kumtaka kuvitia vidole vyake kwenye makovu na majeraha yake, akisema, “Bwana wangu na Mungu wangu!” Yoh 20:28. Mwisho wa kukutana huku, kila mmoja anapata majeraha ya UTUKUFU, na kuwa tayari kuponya wengine wenye maumivu.

Wapo maelfu ya watu wameumizwa na kujeruhiwa miongoni mwetu. Wengine wanabeba chuki kwa usiri mkubwa ndani ya mioyo yao kwa kusalitiwa  kulikotokana na kutokuwa na uaminifu kwa wenzi wake wa ndoa. Wengine wanabeba chuki dhidi ya wanaofisi wenzao kwa kuwaenezea umbea na uongo mitaani. Wengine pia wanabeba ndani ya mioyo yao chuki na manung’unika kwa milongo ya miaka iliyopita kwa kukosa sehemu ya kuponyeshwa na kusikilizwa. Wengine maumivu haya wanayabeba tangu kuzaliwa kwao hadi sasa kutokana na namna ya kutungwa mimba kwao kuliko kataliwa na kwa bahati mbaya au nzuri akazaliwa. Wengine wamesalitiwa na wapenzi wao na kuyabeba hayo hadi sasa hata kama wanaishi yao ya ndoa. Wapo wengi sana waliojeruhiwa na kuumizwa vibaya kwa namna tofauti tofauti. Jambo hili linaweza kutokea kwa yeyote yule, iwe mlei, mtawa na hata mtawa na mkleri.

Ndugu yangu, hata kama tutayaficha majereha na maumivu yetu, kwa binadamu itafika wakati lazima atayaonyesha tu wazi kwa kutafuta uponyaji. Ni njia mojawapo ya kurudisha mizania ya ndani katika uumbaji wetu. Ukweli ni kwamba walioumizwa kweli na kupata majeraha ya ndani hawawezi kuficha na kuvaa kinyago hicho kwa muda mrefu. Wanaweza kuwadanganya wanaowazunguka kwa wakati tu, ila hawawezi kujidanganya wenyewe na kuficha ukweli huu. Maumivu ya ndani ni vigumu sana kuyavumilia.

Watu hawa wanaitaji uponyaji. Wangepewa nafasi na uchaguzi wote wangependa kugusa majeraha ya Kristo. Wanapenda kujua kwa uhakika kama kuna mtu anayewapenda vya kutosha kwa kujeruhiwa kwao na mtu huyo yupo tayari kufa kwa kuwapenda. Tatizo kubwa ni kwamba hawawezi kumwona tena Kristo. Wanaweza tu kuwaona watu wanaojiita Wakristo. Wakristo ambao wanajulikana kwa kujinadi kulibeba jina la Kristo na siyo kumuishi Kristo. Swali ni hili: Je wakristo hawa wapo kweli kama Kristo? Je, wakristo leo wameumizwa vya kutosha kwa UPENDO kiasi kwamba wanaweza kuwaponya walioumizwa? Je, ni kweli wakristo leo wamefufuka kutoka kifo cha kujijali wenyewe, na ubinafsi, kwamba wanaweza kuwa matumaini na kielelezo cha kuwarudisha waliopotea kwenye kundi kwa kuumizwa kwao?

Ndugu yangu, kuurithi ufalme wa Mungu, ni kuishi vyema wito wako na vipaji alivyo kupa Mungu. Vipaji hivyo siyo mali yako bali viwafaidie wengine, na hasa katika kuyaponyesha majeraha na maumivu waliyokuwa nayo. Hiki ndicho kielelezo cha maisha yetu kama Wakriso na wafuasi wa Kristo Mfufuka. Jambo hili si katika kuangamizana, bali katika ufaidiana na kuongozana katika umilele ambao ndiyo makusudi ya Ufalme wa Mungu.

Wapendwa ulimwengu wa leo unamwitaji sana Kristo. Kama ulimwengu usipomwona Kristo kwa Wakristo wa leo, waliojerehiwa watajitoa kwa Mungu, na kubeba mioyo yao inayovuja damu na vidondo visivyoponyeka kwingine kusipo Mungu. Na wanavyojitoa huku ufikia mahali na kuinamisha vichwa vyao na kufikiri katika akili zao: “Mungu amekufa!”

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU, KWA MAJERAHA YA UTUKUFU WAKO NASI TWAPONA MAJEREHA YA MAUMIVU YETU YA NDANI. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario