domingo, 12 de julio de 2015

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 15 YA MWAKA-B

JUMATATU WIKI YA 14 YA MWAKA-B
13/7/2015
Somo: Kut 1:8-14, 22
Zab: 123:1-8
Injili: Mt 10:34-11:1
Nukuu:
Kisha huyo Farao akawaagiza watu wake, akisema, Kila mtoto mwanamume atakayezaliwa mtamtupa mtoni, na kila mtoto mwanamke mtamhifadhi hai,” Kut 1:22

Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! Sikuja kuleta amani, bali upanga,” Mt 10:34

Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili,” Mt 10:37

Wala mtu asiyechukua msalaba wake akanifuata, hanistahili. Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataiona,” Mt 10:38-39

Ampokeaye nabii kwa kuwa ni nabii, atapata thawabu ya nabii; naye ampokeaye mwenye haki kwa kuwa ni mwenye haki, atapata thawabu ya mwenye haki,” Mt 10:41

TAFAKARI: “Yatupasa kujipambanua juu ya ufuasi wetu na Yesu.”

Wapendwa wana wa Mungu, mpango wa Mungu haufitiniki kwa hila za mwanadamu. Katika somo la kwanza tunaona ongezeko la Waisraeli utumwani  Misri linakuwa tishio kwa utawala wa Misri. Hofu hii inapelekea mauaji ya kimfumo kwa Waisraeli.Farao akawaagiza watu wake, akisema, Kila mtoto mwanamume atakayezaliwa mtamtupa mtoni, na kila mtoto mwanamke mtamhifadhi hai,” Kut 1:22. Pamoja na mauaji hayo ya kimfumo, mpango wa Mungu kwa watu wake hakuna binadamu awezaye kuubadilisha. Mateso yatakuwepo kwa wakati tu, na kupitia mateso hayo tunaimarishwa na kufanywa imara katika Imani ile tunayoiishi na kuishuhudia.

Kuiishi Imani ni changamoto kubwa sana. Yesu anaiona changamoto hii na anatupa angalisho. Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! Sikuja kuleta amani, bali upanga,” Mt 10:34. Kuiishi Imani yetu ni kufanya vita dhidi ya utawala wa giza. Mapambano haya lazima yazue sintofahamu nyingi; kifamilia, kiukoo, na hata kijamii.  Hivyo, Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili,” Mt 10:37. Ufuasi wetu katika Kristo, ni ufuasi wa kujikana nafsi kila siku. Mahangaiko yetu ya kila siku yasiwe ukuta wa kuiishi imani yetu. Ni katika mateso pia tunakutana na Kristo kwani kwa njia hiyo ya mateso Kristo kaushinda msalaba kwa kujipatia utukufu. Wala mtu asiyechukua msalaba wake akanifuata, hanistahili. Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataiona,” Mt 10:38-39. Hakuna utukufu pasipo msalaba.

Wapendwa wana wa Mungu, tuishi na kila mmoja wetu kwa upendo na amani. Tupokeane na kutabikiana kwa upendo. Tupokeane kwa upendo katika kweli. Ampokeaye nabii kwa kuwa ni nabii, atapata thawabu ya nabii; naye ampokeaye mwenye haki kwa kuwa ni mwenye haki, atapata thawabu ya mwenye haki,” Mt 10:41. Tuyaone mazuri kwa wenzetu, na mazuri hayo yawe kielelezo cha kuuona uzuri wa Mungu kwa yule aliyeumbwa na sura na mfano wake.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUPE UJASIRI WA KUTOSHA TUNAPOKUSHUHUDIA KILA SIKU KWA MAISHA YETU.

No hay comentarios:

Publicar un comentario