sábado, 18 de julio de 2015

TAFAKARI: JUMAPILI YA 16 YA MWAKA-B

JUMAPILI  YA 16 YA MWAKA-B
19/7/2015
Somo I: Yer 23:1-6
Zab: 22:1-6
Somo II: Efe 2:13-18
Injili: Mk 6:30-34
Nukuu:
Kwa sababu hiyo Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, juu ya wachungaji wanaowalisha watu wangu, Mmetawanya kundi langu, na kuwafukuza, wala hamkwenda kuwatazama; angalieni, nitawapatiliza uovu wa matendo yenu, asema Bwana,” Yer 23:2 

Nami nitaweka juu yao wachungaji watakaowalisha; wala hawataona hofu tena, wala kufadhaika, wala hatapotea hata mmoja wao, asema Bwana,” Yer 23:4

Katika siku zake Yuda ataokolewa, na Israeli atakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, Bwana ni haki yetu,” Yer 23:6

Naye akiisha kuuondoa ule uadui kwa mwili wake; ndiyo sheria ya amri zilizo katika maagizo; ili afanye hao wawili kuwa mtu mpya mmoja ndani ya nafsi yake; akafanya  amani,” Efe 2:15

Akawapatanisha wote wawili na Mungu katika mwili mmoja, kwa njia ya msalaba, akiisha kuufisha ule uadui kwa huo msalaba,” Efe 2:16 

Kwa maana kwa yeye sisi sote tumepata njia ya kumkaribia Baba katika Roho mmoja,” Efe 2:18
Akawaambia, Njoni ninyi peke yenu kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo. Kwa sababu walikuwako watu wengi, wakija, wakienda, hata haikuwapo nafasi ya kula,” Mk 6:31 

TAFAKARI: “Makusudi ya Mungu: “asipotee hata mmoja wa wale aliowaumba kwa sura na mfano wake.”

Wapendwa wana wa Mungu, maisha yetu leo hapa duniani ni kulisadifu lile alilolianzisha Mungu na kulikusudia. Kwa maana hiyo, “Makusudi ya Mungu: “asipotee hata mmoja wa wale aliowaumba kwa sura na mfano wake.” Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, elewa kwamba maisha unayoishi kadiri ya wito wako, wewe ni kielelezo cha kusudio la Mungu katika uumbaji wake. Hapo ulipo, uwe mkleri, mtawa au mlei, uliokabidhiwa asipotee hata mmoja. Ni kosa kubwa sana kufanya hujuma kwa wale ambao Mungu ametukabidhi. Hivyo Mungu kwa kupitia Nabii Yeremia anasema, “juu ya wachungaji wanaowalisha watu wangu, Mmetawanya kundi langu, na kuwafukuza, wala hamkwenda kuwatazama; angalieni, nitawapatiliza uovu wa matendo yenu, asema Bwana,” Yer 23:2. Mpendwa katika Kristo, kama wewe ni kiongozi kwa ngazi yoyote ile, elewa kwamba wewe ni jalala la kila kitu. Hivyo yote uyapokeayo na kuambiwa na watu yachunguze kwa makini sana, na utoapo neno la mwisho lilenge katika kuwapata wale waliochini yako na siyo kuwapoteza.

Ndugu yangu, huyu tunayemwabudu na kumtumikia ni Mungu mwenye haki. Mungu wetu si Mungu wa visasi, bali ni Mungu anayetutaka tuishi katika haki na upendo.  Na Mungu anasema hivi; Katika siku zake Yuda ataokolewa, na Israeli atakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, Bwana ni haki yetu,” Yer 23:6. Yatupasa kuwa watu wa haki hata kama kwa kutenda haki tunaumizwa.

Wapendwa, Mungu wetu anatutakia mema siku zote, na hivyo kwa njia ya msalaba kupitia mwana wake mpezi, licha ya kwamba ni kifo cha aibu kutokea katika historia ya mwanadamu, anaonyesha upendo wake mkuu usio na kipimo kwetu. Naye akiisha kuuondoa ule uadui kwa mwili wake; ndiyo sheria ya amri zilizo katika maagizo; ili afanye hao wawili kuwa mtu mpya mmoja ndani ya nafsi yake; akafanya  amani,” Efe 2:15. Amani hii tuipatayo ni tunda la kifo cha msalaba wa bwana wetu Yesu Kristo, Ndugu yangu, maisha yako kama mfuasi wa Kristo hayawezi kutenganishwa na msalaba wa Bwana wetu Yesu. Ni katika msalaba tunapata utukufu. Hivyo, Akawapatanisha wote wawili na Mungu katika mwili mmoja, kwa njia ya msalaba, akiisha kuufisha ule uadui kwa huo msalaba,” Efe 2:16. Hakika Mungu anatupenda upeo!

Ndugu yangu, tunapoutambua ukweli huu, tujue kabisa tupo karibu na Roho wake Mtakatifu ambaye kwa kupita yeye tunapata maondoleo ya dhambi zetu, na kutufunulia yale yaliiojificha katika umilele wa Mungu. Kwa maana kwa yeye sisi sote tumepata njia ya kumkaribia Baba katika Roho mmoja,” Efe 2:18. Je, ni nani atakayetutenganisha na upende wake Kristo? Upendo haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika. Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu; lakini ijapo ile iliyo kamili, iliyo kwa sehemu itabatilika,” 1Kor 13:8-10. Upendo wa Mungu kati yetu hutufanya kile tulicho katika kweli na kile Mungu alichokusudia katika maisha yetu.

Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, Mungu anatutakia mema kila dakika. Na katika jambo hili ni vyema kuwa na muda wa kutosha katika kuyatafakari mambo makuu ya Mungu anayotutendea kila siku ya maisha yetu. Jiwekee utaratibu wa kuyatafakari makuu haya ya Mungu, hata mara moja kwa mwaka. Mfano wewe na mwenzi wako wa ndoa, wewe kama mkleri, na hata mtawa, nje ya utaratibu wa kawaida uwe na muda binafsi wa kuyatafakari hayo. Ikiwezekana hata kwa wiki moja ukiwa katika sehemu tulivu na  ya sala. Hivi ndiyo Bwana wetu Yesu Kristo awatakavyo wanafunzi wake wafanye. Akawaambia, Njoni ninyi peke yenu kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo. Kwa sababu walikuwako watu wengi, wakija, wakienda, hata haikuwapo nafasi ya kula,” Mk 6:31. Mara nyingi tumekuwa kama bomba lenye kumwaga maji na kujisahau lenyewe na kuleta ukavu pale liliposimikwa.

Ndugu yangu, naomba nikupe mfano huu: kuna aina nne za watu. Lakini leo nitasema aina moja ya watu inayoendana na injili na masomo yetu ya leo. Miongoni mwetu, wapo watu ambao wapo tayari kufanya jambo lolote la huruma kwa yeyote wanayemsikia bila kujibakiza.

Mtu wa mtindo huu namfananisha na bomba yetu ya kawaida ambayo ukitaka maji yakupasa kuifungua na kutoa maji kadiri ya kiwango utakacho. Bombo hilii la maji ni lile tuitumiayao mabafuni mwetu. Hutoa maji yake kwa mpango mzuri sana. Kitu cha kushangaza ni kwamba pamoja na umakini wake, juu ya bomba hii huwa pakavu sana. Hata kama tupo mstari wa mbele kwa kuwahudumia watu kadiri ya upendo na ukarimu wetu, yatupasa kujikumbuka wenyewe. Hatupaswi kujisahau nafsi zetu. “Ukarimu huanzia nyumbani.” Iweje nimwone Yesu kwa wengine na kumsahau Yesu kwa wale ninaoishi nao kila siku? Hivyo, pamoja na huduma tuzitoazo kwa watu wengine zisizokuwa na shaka yoyote, hatupaswi kujisahau wenyewe.

Tumsifu Yesu Kristo!


MUNGU ANAKUPENDA UPEO, NA KWA SABABU HIYO HAPENDI UPOTEE. AMINA.

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 15 YA MWAKA-B

JUMAMOSI WIKI YA 15 YA MWAKA-B
18/7/2015
Somo: Kut 12:37-42
Zab: 135:1, 10-15, 23-24
Injili: 12:14-21
Nukuu:
Basi wana wa Israeli kukaa kwao, maana, muda waliokaa ndani ya Misri, ulikuwa ni miaka mia nne na thelathini,” Kut 12:40

Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda,” Mt 12:20

Na jina lake Mataifa watalitumainia,” Mt 12:21

TAFAKARI: “Huyu ndiye Yesu.”

Wapendwa wana wa Mungu, haikua rahisi sana kwa wana wa Israeli kuupokea ujumbe ule waliopewa na Mungu kupitia mtumishi wake Musa, ya kwamba iliwapasa kutoka nchini Misri kwenye masufuria ya nyama na matango, na kwenda wasipopajua. Wana wa Israeli walikaa utumwani nchini Misri kwa muda wa kutosha. Basi wana wa Israeli kukaa kwao, maana, muda waliokaa ndani ya Misri, ulikuwa ni miaka mia nne na thelathini,” Kut 12:40. Kwa mtazamo huu, hata wale waliokuwepo katika mkakati wa kuondoka nchini Misri kuelekea nchi ya ahadi, hawakuona sababu ya kufanya hivyo, kwani walishaanza kuzoea mfumo wa maisha yale ya kitumwa. Hali hii ilimpatia Musa misukosuko mingi juu ya utayari wa wana wa Israeli. Lawama na manung’uniko yalikuwa mengi hasa pale walipopata taabu na dhiki nyingi nyikani.

Ni vigumu sana kuukataa mfumo wa maisha ambao kwayo tumeishi muda mrefu hata kama hauna tija. Wengi wetu huogopa sana kile tusichokijua kwa yale tuyatarajiayo. Ni ndani na katika Kristo tunapata uhakika wa kile tusichokijua na tusichokuwa nacho katika uhasilia wake licha ya shida na dhiki tuzipatazo kadiri ya wito wa kila mmoja wetu. Mungu anasema juu ya Yesu, yaani, uwezo na mamlaka aliyonayo, kwamba, Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda,” Mt 12:20. Huyu ndiye Yesu!

Wapendwa wana wa Mungu, ni kupitia jina lake Yesu Kristo twaponywa na twalitumainia milele yote. Ukweli huu si kwa sisi tu tafuasi wake, yaani wabatizwa, wakristo, bali kwa mataifa yote.Na jina lake Mataifa watalitumainia,” Mt 12:21. Kwa hiyo ndugu yangu, popote pale ulipo mfanye Yesu kuwa sababu ya ukweli ndani yako, njia ya maisha yako, na uhai wako.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU KUWA SABABU YA HIKI NILICHO. AMINA

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 15 YA MWAKA-B

IJUMAA WIKI YA 15 YA MWAKA-B
17/7/2015
Somo: Kut 11:10-12:14
Zab: 115:12-13, 15-18
Injili: Mt 12:1-8
Nukuu:
Musa na Haruni walifanya ajabu hizo zote mbele ya Farao; Bwana akaufanya moyo wa Farao kuwa mgumu, asiwape wana wa Israeli ruhusa watoke nchi yake,” Kut 11:10

Lakini nawaambieni, kwamba hapa yupo aliye mkuu kuliko hekalu,” Mt 12:6 

Lakini kama mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia,” Mt 12:7 

TAFAKARI: “Mungu anayathamini maisha yako kuliko kitu kingine chochote.”

Wapendwa wana wa Mungu, mara nyingi katika tafakari zangu nanyi nimekuwa nikikuambia kwamba wewe si bahati mbaya. Mungu wetu huyu, “anayathamini maisha yako kuliko kitu kingine chochote.” Mungu kwa kulifanya hili katika dhamiri iliyo safi, huthamini sana maisha yetu kwani yanachapa yake. Yeye ametuumba kwa sura na mfano wake. Hawezi kamwe kutupoteza kwa jambo lolote lile. Lakini kwa kutufundisha, mara nyingine husababisa ugumu wa kufikia lengo lile kwa kusababisha ugumu fulani. Mungu anachotaka tujifunze kutoka kwake ni hiki: “Maisha yako ni ya thamani kubwa sana. Maisha yako ndiyo utajiri wako. Huwezi kupanga wala kuwa karibu na Mungu wako kama maisha yako ni mgogoro. Ukiwa na afya njema waweza kusali vizuri na hata kuyaboresha maisha yako kama yamekwenda kombo.” Pili tunaimarishwa katika taabu na dhiki. Hivyo jambo hili linatokea kwa Musa. Musa na Haruni walifanya ajabu hizo zote mbele ya Farao; Bwana akaufanya moyo wa Farao kuwa mgumu, asiwape wana wa Israeli ruhusa watoke nchi yake,” Kut 11:10. Hapa kwa tendo hili, wana wa Israeli wanaandaliwa kwa lile lililo jema zaidi mbele ya safari.

Wapendwa wana wa Mungu, Mungu hapendi sadaka zetu zisizo na uhusiano wa maisha yetu na thamani yake. Mungu wetu hupenda rehema na neema anazotujalia pale tunapoziishi kuliko kile tumtoleacho kama sadaka. Yote tumtoleayo ni mali yake. Vyote vipo chini ya mamlaka yake. Hivyo Yesu anasema, Lakini kama mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia,” Mt 12:7. Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka kutokana na mila na desturi zetu, wakati fulani tulilazimika kufanya mitambiko na hata kutolea sadaka za kuteketezwa zisizo na uhusiano na imani yetu. Kwa kufanya hivi tunapoteza dira na mwelekeo wa Kimungu katika maisha yetu. Je, naweza kuwa huru hata kama naishi katika mila na desturi hizi?

Tumsifu Yesu Kristo.

EE YESU, TUWEZESHE TUYAONA MAISHA YETU KAMA MALI YA MUNGU NA ZAWADI YA MUNGU. AMINA


TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 15 YA MWAKA-B

ALHAMISI WIKI YA 15 YA MWAKA-B
16/7/2015
Somo: Kut 3:13-20
Zab: 104:1, 5, 8-9, 24-27
Injili: Mt 11:28-30
Nukuu:                              
Mungu akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO; akasema, Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli; MIMI NIKO amenituma kwenu,” Kut 3:14

Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha,” Mt 11:28 

Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu,” Mt 11:29 

kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:30

TAFAKARI: “Utulivu wa kweli twaupata ndani na katika Kristo.”

Wapendwa wana wa Mungu, kuzaliwa si lazima, ili kufa kama umeshazaliwa ni lazima. Ikiwa tupo hai na tunaishi, hatuwezi kudumu katika hali hiyo siku zote bila kuwa na mahangaiko. Binadamu huyapata mahangaiko yatokanayo na magonjwa, njaa, hali ya hewa, na hata hali mbaya ya siasa. Hali mbaya ya siasi huwa pia chanzo cha mahangaiko na kuwafanya watu kuwa wakimbizi katika inchi yao yenyewe, vifo vya watoto, akina mama na watu wasio na hatia yoyote.

Ndugu yangu, tunayaona mahangaiko pia kwa wana wa Israeli katika safari ya ukombozi kutoka inchi Misri. Hivyo Musa anapopewa majukumu la kuliongoza Taifa hili kutoka utumwani Misri, anataka kujua uhakika wa kile alichoambiwa na Mungu. Mungu akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO; akasema, Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli; MIMI NIKO amenituma kwenu,” Kut 3:14. Huyu ndiye Mungu hai tunayemwamini na kumwabudu.

Leo kwa yeyote yule mbatizwa na mwenye kumwamini Kristo, anapata kitulizo cha kweli ndani na katika Kristo. Ni kupitia Kristo wote twaweza kuiona nuru na kuishi katika nuru ya kweli. Hakuna jina lingine hapa dunia twaweza kuokolewa nalo nje ya jina hili, Yesu Kristo. Yesu ndiye njia, kweli na uzima wetu. Yesu anasema, Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha,” Mt 11:28. Kiboko cha mahangaiko yetu kama watu waaminio na wafuasi wa Kristo ni Yesu mwenyewe. Mizigo yetu na taabu zake zote ni Kristo mwenyewe anayeweza kutubebea tukiwa naye. Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha,” Mt 11:28. Hakuna pumzisho la kweli nje ya Kristo. Mwongozo wa kweli katika mahangaiko yetu ni Kristo mwenyewe. Mwongozo wake ni UPENDO, na hii ndiyo nira yake. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu,” Mt 11:29. Ndugu yangu kwa nini hupendi kupenda? Kwa nini humpendi huyo uliye weka mipaka naye? Je, Yesu angefanya hayo unayoyafanya?

Ndugu yangu, ukipenda katika kweli yote, yote huwa mepesi. Kipimo cha kupenda kinawiana na kipimo cha kusamehe. Usipo kuwa mwepesi wa kusamehe bado hujaijua kweli ya Mungu. Katika hili Yesu anasema, kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:30. Ndugu yangu, ni mzingo upi ulio nao ni mzito ambao Yesu atashindwa kuubeba?

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU KRISTO, TUJALIE IMANI YA KWELI. AMINA.

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 15 YA MWAKA-B

JUMATANO WIKI YA 15 YA MWAKA-B
15/7/2015
Somo: Kut 3:1-6, 9-12
Zab: 102:1-4, 6-7
Injili: Mt 11:25-27
Nukuu:
Naye akasema, Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu,” Kut 3:5

Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa,” Kut 3:9 

Tena akasema, Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu,” Kut 3:6

Musa akamwambia Mungu, Mimi ni nani, hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli watoke Misri?” Kut 3:11

Wakati ule Yesu akajibu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako,” Mt 11:25-26

TAFAKARI: “Mungu huyatenda makuu kwa wanyenyekevu wa Moyo.”

Wapendwa wana wa Mungu, tuitazamapo historia ya wokovu wetu, tunagundua kwamba Mungu hufanya kazi na wale wajishushao na wanyenyekevu wa Moyo. Licha ya tabia na mwono huu wa Kimungu, wale wate wanoshirikishwa mpango wa Mungu katika tendo la Kimungu, huwa ni watu wa kawaida sana, na mara nyingine huwa wale waliodharaulika na jamii husika. Mama Bikira Maria ni mmoja wa wale walioshiriki mambo makuu ya Mungu katika unyonge na unyenyekevu wake. Naye Bikira Maria analitambua jambo hili na kusema,  Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama, tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa,” Lk 1:48.  Bikira Maria anatambua pia kile kinachotendeka kwake ni upendeleo wa Mungu ndani mwake, na hivyo kinamakusudio makubwa kadiri ilivyompendeza Mungu. Naye anasema, Amewaangusha wakuu katika viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:52. Jambo hili linatokea pia kwa Musa ambaye anapokea misioni hiyo kama kiongozi wa wana Waisraeli kuwatoa kutoka utumwani Misri.

Kazi anayopewa Musa inamlazimu kuyaacha yote yale yaambatanayo katika maisha yake ambayo hayampendezi Mungu. Mungu anapompa majukumu haya mazito na muhuhi anampa angalisho na kusema, “Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu,” Kut 3:5. Wapendwa wana wa Mungu, kuvivua viatu ni kuenenda na kufanya katika hali halisi ya kile ulichotumwa kufanya bila kuwa na hisi fulani kama miwani ya kutazamia uhalisia wa mambo. Mara nyingi tumewahukumu watu na hata kuwatenda ndivyo sivyo kutokana na mang’amuzi yetu yasiyoendana na uhalisia wa jambo. Mara nyingi tumewahukumu watu kutokana na historia zetu mbaya. Na mara nyingine tumeenda mbali zaidi katika kutenda na kuhukumu kulikotokana na simulizi za chuki juu ya wale tunaoishi nao zisizo za kweli. Hivyo kuvivua viatu ni kuzama ndani kabisa katika mila na desturi za watu tuliotumwa kwao ili kujua ukweli wa mambo. Yatupasa kuweka kando nadhania zetu za vitu, na kuuona ukweli kama ulivyo. Hili ndilo jambo la msingi Musa ilimpasa kulijua kabla ya kulitenda lile Mungu alilotaka alitende juu ya watu wake.

Wapendwa, mara zote mjumbe hulifanya lile alilotumwa kulifanya na Bwana wake. Hatupaswi kubadili ujumbe ule kwa kujiinua nafsi zetu. Hivyo Mungu anamtaka Musa alitende lile aliloliona juu ya mateso ya Wana wa Israeli. Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa,” Kut 3:9. Agizo na mamlaka haya yanatoka kwa Mungu mwenye Mungu na aliye hai. Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu,” Kut 3:6. Neno hili ni lenye nguvu, na Mungu wetu ni Mungu mwenye wivu na kile alichokiumba kwa sura na mfano wake. Hata hivyo, kazi aliyopewa Musa haikuwa rahisi. Hivyo Musa anajipima nguvu na ushawishi aliokuwa nao kwa watu wake na mtesi wake, Farao, na kujiona mdogo na dhaifu. Naye akamwambia Mungu, Mimi ni nani, hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli watoke Misri?” Kut 3:11. Huu ndio unyenyevu wa Musa mbele ya Mungu. Ndugu yangu, yapo mambo mengi katika utume wetu kila mmoja kadiri ya wito wake, kwa nguvu zetu wenyewe hatuwezi kufikia malengo. Hivyo tunahitaji msaada wa Mungu.

Kujishusha huku na kuwa wanyenyekevu mbele ya Mungu mwenye kuyaweza yote, ndiko kunakotutafakarisha maneno na sala hii ya Yesu katika Injili ya leo: Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako,” Mt 11:25-26. Je, twatoa shukrani kwa Mungu hata kwa kile kidogo Mungu alichotuwezesha kukifanya? Je, mafanikio niyapatayo natambua ni mkono wa Mungu, au ni akili zangu na ujanja wangu? Ndugu yangu, ‘moyo usio na shukrani hukausha mema yote.’

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU NIJALIE FADHILA YA UNYENYEKEVU. AMINA.

lunes, 13 de julio de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 15 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 15 YA MWAKA-B
14/7/2015
Somo: Kut 2:1-15a
Zab: 68
Injili: Mt 11:20-24
Nukuu:
Mtoto akakua, naye akamleta kwa binti Farao, akawa mwanawe. Akamwita jina lake Musa, akasema, Ni kwa sababu nalimtoa majini,” Kut 2:10

Hata siku zile, Musa alipokuwa mtu mzima, akatoka kuwaendea ndugu zake, akatazama mizigo yao. Akamwona Mmisri anampiga Mwebrania, mmojawapo wa ndugu zake. Basi akatazama huko na huko, na alipoona ya kuwa hapana mtu, akampiga Mmisri yule, akamficha ndani ya mchanga,” Kut 2:11-12 

Basi Farao alipopata habari, akataka kumwua Musa; lakini Musa akakimbia mbele ya Farao, akakaa katika nchi ya Midiani; akaketi karibu na kisima,” Kut 2:15

“Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, wangalitubu zamani kwa kuvaa magunia na majivu,” Mt 11:21

Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe,” Mt 11:24 

TAFAKARI: “Sikio la kufa halisikii dawa.”

Wapendwa wana wa Mungu, msemo huu wa Kiswahili, “sikio la kufa halisikii dawa,” utusaidie katika tafakari yetu ya leo. Katika somo letu la kwanza tunaona namna ambavyo Musa anavyookolewa na kutunzwa kwa namna ya ajabu hadi kuwa mtu mzima na kuendeleza kazi ile ya ukombozi wa wana wa Israeli. Mtoto akakua, naye akamleta kwa binti Farao, akawa mwanawe. Akamwita jina lake Musa, akasema, Ni kwa sababu nalimtoa majini,” Kut 2:10. Mtoto huyu aliyeokolewa kutoka majini, Musa, anakuwa kielelezo na mkono wa Mungu. Hata hivyo Musa anapata upinzani kutoka kwa ndugu zake licha ya utetezi wake na juhudi zake kuliokoa Taifa lake. Hata siku zile, Musa alipokuwa mtu mzima, akatoka kuwaendea ndugu zake, akatazama mizigo yao. Akamwona Mmisri anampiga Mwebrania, mmojawapo wa ndugu zake. Basi akatazama huko na huko, na alipoona ya kuwa hapana mtu, akampiga Mmisri yule, akamficha ndani ya mchanga,” Kut 2:11-12 

Ni jambo gumu sana kuelewa ubaya wa kitu ndani ya mfumo wa kitu kile. Waisraeli wangetamani sana kuendelea katika mateso yale kuliko kujaribu upande wa pili wa maisha wasiyoyajua. Ni hali ya kawaida binadamu kuwa na hofu kwa kile asichokijua, hasa mambo yale yamtoayo kwenye mang’amuzi yake ya kila siku. Hapa ndipo tunaposema, “heri nusu shwari kuliko shwari nzima.” Musa anajaribu kuwaonyesha upande wa pili wa uhalisia wa mambo, lakini ndugu zake wanafanya upinzani juu ya ukweli ule.

Nasi leo tunaitaji kutoka kwenye utumwa wa fikra na kuyaona mambo kama yalivyo. Tumejawa hofu ya tusichokijua na           tumekuwa watumwa kwa hofu hii. Hatuwezi kwenda mbele kama hatupendi kufanya tofauti ya yale tuliyoyazoea kila siku, na miaka yote. Ujasiri ya Musa unamtia matatani. Habari za mauaji ya yule Mmisri zilizovujishwa na jamaa yake Musa inakuwa sababu ya Musa kutoroka na kuinusuru roho yake. Basi Farao alipopata habari, akataka kumwua Musa; lakini Musa akakimbia mbele ya Farao, akakaa katika nchi ya Midiani; akaketi karibu na kisima,” Kut 2:15

Mara zote tunapopambana na kweli, au kujikwamua kwenye shida fulani, mawazo pingamizi hayakosekani. Ugumu huu wakati mwingine husababishwa na kutokuwa na ufahamu wa kutosha wa jambo lile. Huku ndiko tunaposema kwamba sikio la kufa halisikii dawa. Jambo hili ndilo analolisema Yesu anapoitazama miji ile iliyokithiri kwa uovu. “Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, wangalitubu zamani kwa kuvaa magunia na majivu,” Mt 11:21. Ni mara ngapi tunaambiwa ukweli wa mambo lakini mara zote tunabakia na ushabiki usiokuwa na tija yoyote? Kwa nini hatupendi kuona ukweli kama ulivyo na badala yake tunaupindisha? Katika jambo hili, Yesu anatupa angalisho na kusema, Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe,” Mt 11:24.

Wapendwa, hawatashuka malaika kutoka mbinguni na kutuambia mambo haya zaidi ya watu wenye uelewa tunaoishi nao kila siku kutuambia kweli hiyo. Mungu utumia watu wake kulisemea lile lililo ovu. Watu wenye maadili mema na mwono chanya, walisemapo jambo yatupasa kusikia na kulipembua kwa kina. Je, yote yasemwayo kuhusu maisha yako, hali yako, na Taifa lako hayana ukweli? Je, unaridhika na hali hii? Umechukua hatua yo yote?

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU YAFUNGUE MACHO, MIOYO NA AKILI ZETU ILI TUYAONE MAMBO KAMA YALIVYO. AMINA

domingo, 12 de julio de 2015

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 15 YA MWAKA-B

JUMATATU WIKI YA 14 YA MWAKA-B
13/7/2015
Somo: Kut 1:8-14, 22
Zab: 123:1-8
Injili: Mt 10:34-11:1
Nukuu:
Kisha huyo Farao akawaagiza watu wake, akisema, Kila mtoto mwanamume atakayezaliwa mtamtupa mtoni, na kila mtoto mwanamke mtamhifadhi hai,” Kut 1:22

Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! Sikuja kuleta amani, bali upanga,” Mt 10:34

Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili,” Mt 10:37

Wala mtu asiyechukua msalaba wake akanifuata, hanistahili. Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataiona,” Mt 10:38-39

Ampokeaye nabii kwa kuwa ni nabii, atapata thawabu ya nabii; naye ampokeaye mwenye haki kwa kuwa ni mwenye haki, atapata thawabu ya mwenye haki,” Mt 10:41

TAFAKARI: “Yatupasa kujipambanua juu ya ufuasi wetu na Yesu.”

Wapendwa wana wa Mungu, mpango wa Mungu haufitiniki kwa hila za mwanadamu. Katika somo la kwanza tunaona ongezeko la Waisraeli utumwani  Misri linakuwa tishio kwa utawala wa Misri. Hofu hii inapelekea mauaji ya kimfumo kwa Waisraeli.Farao akawaagiza watu wake, akisema, Kila mtoto mwanamume atakayezaliwa mtamtupa mtoni, na kila mtoto mwanamke mtamhifadhi hai,” Kut 1:22. Pamoja na mauaji hayo ya kimfumo, mpango wa Mungu kwa watu wake hakuna binadamu awezaye kuubadilisha. Mateso yatakuwepo kwa wakati tu, na kupitia mateso hayo tunaimarishwa na kufanywa imara katika Imani ile tunayoiishi na kuishuhudia.

Kuiishi Imani ni changamoto kubwa sana. Yesu anaiona changamoto hii na anatupa angalisho. Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! Sikuja kuleta amani, bali upanga,” Mt 10:34. Kuiishi Imani yetu ni kufanya vita dhidi ya utawala wa giza. Mapambano haya lazima yazue sintofahamu nyingi; kifamilia, kiukoo, na hata kijamii.  Hivyo, Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili,” Mt 10:37. Ufuasi wetu katika Kristo, ni ufuasi wa kujikana nafsi kila siku. Mahangaiko yetu ya kila siku yasiwe ukuta wa kuiishi imani yetu. Ni katika mateso pia tunakutana na Kristo kwani kwa njia hiyo ya mateso Kristo kaushinda msalaba kwa kujipatia utukufu. Wala mtu asiyechukua msalaba wake akanifuata, hanistahili. Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataiona,” Mt 10:38-39. Hakuna utukufu pasipo msalaba.

Wapendwa wana wa Mungu, tuishi na kila mmoja wetu kwa upendo na amani. Tupokeane na kutabikiana kwa upendo. Tupokeane kwa upendo katika kweli. Ampokeaye nabii kwa kuwa ni nabii, atapata thawabu ya nabii; naye ampokeaye mwenye haki kwa kuwa ni mwenye haki, atapata thawabu ya mwenye haki,” Mt 10:41. Tuyaone mazuri kwa wenzetu, na mazuri hayo yawe kielelezo cha kuuona uzuri wa Mungu kwa yule aliyeumbwa na sura na mfano wake.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUPE UJASIRI WA KUTOSHA TUNAPOKUSHUHUDIA KILA SIKU KWA MAISHA YETU.