martes, 26 de mayo de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 8 MWAKA-B

JUMATANO WIKI YA 8 YA MWAKA-B
27/5/2015
Somo: Ybs 36;1-2a, 5-6, 13-19
Zab: 78
Injili: Mk 10:32-45
Nukuu:                                                         
Ee Bwana, uisikilize sala yao wakuombao, sawasawa na kibali chako kwa watu wako. Na wote wakaao duniani watajua ya kwamba Wewe ndiwe Bwana, Mungu wa milele,” Ybs 36:16-17
Yesu akawaambia, Hamjui mnaloliomba. Mwaweza kunywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi?” Mk 36:38
“Yesu akawaambia, Kikombe ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; lakini habari ya kuketi mkono wangu wa kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa tayari,” Mk 10:39b-40
Yesu akawaita, akawaambia, Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha,” Mk 10:42 
Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote,” Mk 10:43-44
Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mk 10:45 
TAFAKARI: “Hamjui mnaloliomba”
Wapendwa wana wa Mungu, sala na maisha ya sala ni vitu viwili tofauti, ila hatuwezi kuvitenganisha tunapozama katika mahusiano na Mungu yaliyo ya karibu na ya kweli. Kwa ufupi, sala ni mwitikio wa ndani ya mtu ulio wa kweli na usio na shaka yoyote kwa Mungu aliye yote katika yote. Mwitikio huu ni tokeo la kiufahamu unaoweka wazi ubinadamu wetu na mipaka yake, na Umungu katika ukamilifu wake. Hivyo, mwitikio huu hujidhihirisha katika namna mbalimbali kadiri ya mguso wa ndani wa mtu juu ya mahusiano haya ya kipekee baina yake na Mungu. Mguso huu wa ndani hujionyesha nje ya mtu kama: Maombi, kusifu, kushukuru, kuambudu/kujisalimisha na ukimya wa kujizamisha ndani ya mafumbo na maajabu wa Mungu.
Hivyo basi, tukiwa na uelewa huu tutafahamu kile/lile tunachokiomba, tunachokisifu, tunaloshukuru, tunachokiabudu, na kule tunapozama katika mafumbo na maajabu ya Mungu. Leo tuelekeze tafakari yetu katika maneno haya ya Yesu, “hamjui mnaloliomba.” Maneno haya Yesu anayatamka kwa Yakobo na Yohana wana wa Zebedayo, ambao walimwomba Yesu wakae mmoja mkono wake wa kushoto na mwingine mkono wake wa kuli. Sala kama maombi, haitoshi tu kuweka mbele matamanio yetu binafsi, bali maombi yetu yawezeshwe kadiri ya mapenzi ya Mungu aliye yote katika yote. Yakobo na Yohana wanatanguliza matamanio yao na ubinafsi wao. Hawakuweza hata kuwakumbuka Mitume wenzao waliobaki, yaani wale kumi. Haya ni maombi yasiyo na ukomavu kiimani. Ni mara baada ya kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo, Yakobo anatambua maana ya maombi, na kusema, “Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu” Yak 4:3. Huyu sana ni Yakobo Mtume aliyekomaa kiimani. Kwa sasa anajua kile aombacho.
Wapendwa wana wa Mungu, Yesu ndiye anayetufundisha uhusiano wa maombi yetu na matakwa ya Mungu katika sala yake kule Bustanini Getsemani. “Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, akapiga magoti akaomba, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke,” Lk 22:41-42. Tuliombalo licha ya kwamba latupendeza na tunalihitaji, yatupasa kujisalimisha kwake yeye aliye yote katika yote, naye atupe kadiri ya hitaji letu na mapenzi yake. Huku ndiko Yesu alikomaanisha, kunywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi” Mk 36:38.
Hivyo Mungu aliye Baba yetu Mwema na anayetujua sisi watoto wake atatupa kadiri ya upendo wake. Hivyo, “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa nyoka? Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?” Mt 7:7-11. Hii ndiyo maana halisi ya kile tuombacho na matakwa ya Mungu kwa yale tuyaombayo. Kuhesabiwa haki kwa yale tuyaombayo baada ya kupitia taratibu zote; ni juu ya Mungu mwenyewe kutupa kadiri ya hitaji letu na mapenzi yake. Hivyo, “Yesu akawaambia, Kikombe ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; lakini habari ya kuketi mkono wangu wa kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa tayari,” Mk 10:39b-40. Mungu pekee ndiye anayetuhesabia haki.
Wapendwa, kwa kujua ukweli wa jambo hili juu ya namna ya kuomba, twaweza kuyatamka maneno haya kutoka kitabu cha Yoshua Bin Sira, “Ee Bwana, uisikilize sala yao wakuombao, sawasawa na kibali chako kwa watu wako. Na wote wakaao duniani watajua ya kwamba Wewe ndiwe Bwana, Mungu wa milele,” Ybs 36:16-17. Bila kuyafahamu mahusiano yetu na Mungu, na hali yetu ya ubinadamu, sala kama nilivyoelezea hapo juu ubakia katika hali ya ukavu.
Udadisi wa Yohana na Yakobo kutaka sehemu ya pekee kwa Yesu Kristo, kunazua mzozo miongoni mwa Mitume kwa kauli yao hiyo. Ni kama leo tunaposikia baadhi ya Viongozi wakitangaza nia zao za kutaka kugombea urahisi kabla ya wakati. Yesu analiona hili na kulikemea moja kwa moja kabla halijawa tatizo. Kristo hapa anaonyesha ukomavu katika uongozi na anawataka nao Mitume waige mfano huo. Yesu akawaita, akawaambia, Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha,” Mk 10:42. Kwa upande wa Mitume hawapaswi kufanya hivyo na wala kuwa hivyo. Mitume wameshafunuliwa siri ya umilele, hivyo waishi katika mwono huo wa umilele. Nasi pia kwa ubatizo wetu tumeshafunuliwa siri hiyo ya umilele, na hivyo yatupasa kuishi kadiri ya mwelekeo huo wa umilele. Naye Yesu anatuambia, Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote,” Mk 10:43-44. Maisha ya Mkristo ni kutumika vyema kwa ajili ya ufalme wa Mungu.
Wapendwa wana wa Mungu, kielelezo cha  kutumika vyema ni Kristo mwenyewe aliyekuwa mfano hai kwetu na bado ndiye mfano hali kati yetu hasa pale tunapoona ndugu zetu katika jumuiya na familia wanavyojitoa bila kujibakiza na kuwa mfano wa Kristo aliye hai. Katika ukweli huu Yesu anatukumbusha kupitia maisha yake mwenyewe, akisema, kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mk 10:45. Basi, nitumike vyema katika familia yangu kadiri ya nafasi yangu, nitumike vyema katika jumuiya yangu ya kitawa kadiri ya nafasi yangu, na nitumike vyema katika jamii ninayoishi kadiri ya nafasi yangu.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUFUNDISHE NAMNA YA KUOMBA. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario