JUMAMOSI
WIKI YA 8 YA MWAKA-B
30/5/2015
Somo:
Ybs 51:17-27
Zab:
18:8,9,10,11
Injili:
Mk 11:27-33
Nukuu:
“Enyi wajinga,
munikaribie, na kutua katika nyumba yangu ya mafundisho.” Ybs 51:23
Kwangu nira yake ikawa
utukufu, nami nitamshukuru Yeye aliyenifundisha,” Ybs 51:17
“wakamwambia,
Ni kwa mamlaka gani unatenda mambo haya? Naye ni nani aliyekupa mamlaka hii
uyatende haya?” Mk 11:28
“Ubatizo
wa Yohana ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu?” Mk 11:30a
TAFAKARI:
“Enyi wajinga, munikaribie, na kutua katika nyuma yangu ya mafundisho.” Ybs
51:23
Wapendwa wana wa Mungu,
umasikini mkubwa kwa binadamu wa nyakati zote ni kule kutokujua kwake. Kwa maana hiyo, ujinga wa mtu ni mateso yake,
na ndiyo umasikini wake. Mjinga ni yule asiyefahamu. Mtu huyu ili kuondokana na
karaha hii ya kutokufahamu, yampasa kujifunza. Hata hivyo hakuna binadamu
yeyote katika ulimwengu huu anayejua kila kitu. Kwa mizania halisi, hakuna
binadamu mwenye kujua moja ya kumi ya kila kitu hapa duniani. Kwa maana hii,
kila mmoja wetu ni mjinga wa kitu fulani na kiasi fulani. Je, tufanye nini ili
tuishi kwa amani na ufahamu wa kutosha?
Wapendwa wana wa Mungu,
jambo la kwanza na la msingi kabisa ni kuyajua mazingira yako. Mazingira kwa
maana halisi ya ufahamu, ni kuanzia hapo ulipo na hayo yanayokuzunguka. Je,
unaufahamu wa kutosha kuhusu hapo ulipo na mazingira yanayokuzunguka.
Usipolijua jambo hili, basi huo ndio umasikini wako mkubwa. Hali hii haijalishi
rasilimali na fursa ulizokuwa nazo, wala utajiri uliokuwa nao, iwe ni wako au
wakurithi. Waswahili katika hili wanasema, “mali bila daftari, huisha bila habari.”
Basi kama ni utajiri wa kurithi utatoweka mara. Ni mara ngapi tunasimuliwa
kwamba “familia hii wakati fulani walikuwa matajiri sana, leo ni masikini wa
kutupwa.”
Ni katika mtazamo na
mwono huu kibinadamu, kijamii, na kimazingira, nawaalika tutafakari neno hili;
“Enyi wajinga, munikaribie, na kutua katika nyumba ya mafundisho.” Ybs 51:23.
Baada ya kuona maana ya wajinga, sasa tuitazame nyumba ya mafundisho. Elimu
aisemayo Mungu kupitia kwa mtumishi wake Yoshua Bin Sira, siyo elimu ya
darasani katika tusomavyo leo. Nyumba ya mafundisho ni vile vyote
vinavyokuzunguka wewe. Hali ya hewa na mazingira unayoyaishi ni nyumba ya
mafundisho. Hali hii ya hewa itakufanya ujenge nyumba ya mtindo upi, uvae nguo
za mtindo upi, na hata ulime na kula vyakula vya mtindo upi. Kitu cha
kushangaza hata kwa hili ambalo lipo chini ya uwezo wetu hatuwezi kulifanya.
Matokeo yake tumebakia kudokolea macho mambo ya wengine na kuyaiga kama kasuku.
Vizuri vyote leo ni vile vinavyotoka nje. Lakini hapa wachina wamethibitisha si
kweli. Leo matibabu mazuri ni kutoka nje. Hata viongozi wetu wametusadikisha
hivyo, kwani hata mafua tu wanaenda nje kutibiwa.
Watu unaoishi nao ni nyumba ya mafundisho. Je,
upo tayari kujifunza kutoka kwa wenzako? Ukweli ni kwamba “anayekimbia mwenyewe
mara nyingi hufikiri kwamba yeye ni mkimbiaji bora kuliko wengine.” Yapo mambo
mengi tunayojifunza kwa wenzetu na hata kujisahihisha pale tuliposhindwa
kufanya vizuri. Maendeleo kwa ujumla wake ni tendo la kujifunza na ushindani.
Ila kiroho, ushindani huu huwa tunauchukulia kwa maana hii; “uwe na wifu wa
maendeleo.” Kama mwenzako kajenga nyumba na kaezeka bati, basi wewe fikiri juu
zaidi. Jenga nyumba yako ezeka vigae. Ushindani huu hata kwa mambo ya kiroho
pia twajifunza kwa wenzetu. Hii ndiyo sababu kubwa ya kuwaheshimu watakatifu.
Ila wapo pia kati yetu wanaoishi maisha ya utakatifu kiasi kwamba twataka kujua
siri ya mafanikio yao na hofu hiyo ya Mungu walio kuwa nayo. Ila cha
kushangaza, badala ya kujifunza mazuri kutoka kwa wenzetu kama changamoto ya
sisi kukua kiroho, tunakuwa sababu ya kuwaangamiza kabisa hata wasionekane
katika macho yetu. Neema na baraka Mungu azifanyazo kupitia wengine, hatuwezi
kamwe kuzifuta machoni mwa Mungu kwa hila zetu za kibinadamu. Roho huyu
Mtakatifu afanyaye kazi kupitia wenzetu na kuwatakasa, hatuwezi kumzuia kufanya
kazi hiyo kwa kujenga kuza za: wivu, visasi, kukomoana, vipingamizi na hata
chuki.
Wapendwa wana wa Mungu,
hatuishi kujifunza maovu kutoka kwa wenzetu ili tumwelekee Mungu. Wapo watu
wengi miongoni mwetu ni wezi, hasa wa mali za umma wamekuwa mfano wa kuoigwa na
kupigiwa debe. Leo vijana wengi wanavutiwa na watu waovu, na wanapenda kuwa
kama wao. Vijana wengi leo wanatumika kama njia na ngazi za watu waovu kufikia
tamaa zao iwe kisiasa, kijamii, kiuchumi na hata kidini. Ndugu yangu kwa nini
watumika vibaya? Hapa ndipo tunapozungumzia “UPUMBAVU.” Upumbavu wa mtu ni
saratani ya mtu. Saratani hii umtafuna taratibu, na mwisho wa siku hujikuta
hana namna nyingine ya kuishi zaidi ya dada MAUTI. Taifa letu na jamii yetu leo
ya Watanzania tunatafunwa na saratani hii-“UPUMBAVU.” Je, mpumbavu ni mtu gani?
Wapendwa, mpumbavu ni
yule anayejaribu kukusadikisha usalama wake mchana kweupe akiwa analikata tawi
alilokali akiwa juu ya mti mrefu. Kwa maana nyingine, ni mtu anayejifanya
anajua kumbe hajui kabisa. Ninapata shida sana, na hata nashindwa kuamini
inakuwaje mtu na ufahamu wake kwamba imethibitishwa mtu mfulani amejikoka
mabomu {wizi, rushwa, ufisadi, nk}, bado unaenda kumkumbatia na kutaka awe
msimamizi wa nyumba yako na shamba lako? Hapa kweli kuna nyumba ya mafundisho?
Jambo la kushangaza zaidi hata baadhi ya viongozi wa kidini hawaoni hatari hii
baada ya kupata mgao huu wa wizi.
Ndugu yangu, nyumba ya
mafundisho ni uwezo wa mtu kuzisoma alama za nyakati. Kuzisoma alama za nyakati
ni kufanya tathimini ya namna ulivyoishi jana, unavyoishi leo, na kutokana na
mang’amuzi hayo, upate dira ya kuishi kesho. Tulio wengi mtihani huu ni mgumu
sana. Ona tunavyojikanganya! Jana ulilaumu hali fulani ya masiha, leo hali ile
imejirudia, na kesho unayapigia debe maisha yale ambayo jana uliyalaumu, leo
yanakutesa, na kesho unataka yaendelee. Ni kuku tu mwenye ujasiri wa kuishi
maisha hayo. Ukitaka kujua ujasiri wa kuku mrushie nyanya utaona uwezo wake wa
kufikiri. Kuku anapoiona nyanya huanza kuidonoa ikijiviringisha upande wa pili,
kuku yule yule husahau kama ulishaitoboa upande mmoja, hivyo huanza tena
kuitoboa upande mwingine. Mungu hajatuumba tuwe kama kuku. Mungu ametuumba kwa
sura na mfano wake. Kwa nini basi tunapenda kuwa kuku? Kwa nini tunamshushia
Mungu hadhi yake?
Wapendwa wana wa Mungu,
tunapoyakubali mazingira ya kikuku kuku tunapoteza nira na utukufu wa Mungu.
Hatuwezi kusema maneno haya; “Kwangu nira yake ikawa utukufu, nami nitamshukuru
Yeye aliyenifundisha,” Ybs 51:17. Tunapopoteza nira hii na utukufu huu wa Mungu
ndani yetu, hatuwezi kamwe kupata yale tunayomwomba Mungu. Huku ni kuishi bila
Mungu, na mateso yake ni kuishi jangwani hadi tutakapotambua tulipoipoteza nira
na utukufu ule Mungu aliotupa kwa tendo la uumbaji wetu.
Katika njili ya leo
Yesu Kristo anakutana na Wapumbavu wengine. Pamoja na mambo yote aliyoyafanya
Yesu ikiwa ni pamoja na miujiza yake, na mafundisho yake yaliyojaa hekima na
nguvu ya kimaadili, bado hawajui ni kwa mamlaka gani anayafanya mambo hayo.
Wayahudi, na hasa nyakati za Yesu, walikwisha ichakachua Torati kiasi kwamba
walichokuwa wanakiishi na kukifuata ilikuwa ni tafsiri ya Torati na masimulizi
mbalimbali ya marabi-TALMUD. Hivyo kwa kuitupa Torati kapuni walikosa historia
nzima wa wokovu wa mwanadamu, na kilele chake katika fumbo zima la Kristo mwana
wa Mungu, akiwa ndiye ufunuo wa wazi kabisa wa Mungu. Hivyo wabishi na
“wapumbavu hawa,” wanahoji mamlaka ya Yesu kwa kumwambia, “Ni kwa mamlaka gani
unatenda mambo haya? Naye ni nani aliyekupa mamlaka hii uyatende haya?” Mk 11:28. Yesu hakuwapa jibu la moja kwa moja
kuhusu swali lao hili kwani mazingira yalisadifu kabisa kuelewa walicho uliza.
Yesu Kristo hana muda wa kujibizana na wapumbavu.
Yesu Kristo anao muda wa kuwafundisha wajinga/wasiofahamu, ili wafahamu siri ya
Mungu. Mastahili ya mpumbavu katika maana hii, ni laana na wala si baraka.
Wayahudi waliposhindwa kujibu swali alilouliza Yesu, “Ubatizo wa Yohana
ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu?” Mk 11:30a, kwa kujua mtego wake kwamba,
“tukisema, Ulitoka mbinguni, atasema, Mbona, basi, hamkumwamini? Ila tukisema,
Ulitoka kwa wanadamu, waliogopa watu; maana watu wote walimwona Yohana kuwa
nabii halisi,” na kusema hatujui, naye Yesu hakutoa jibu kwani jibu walikuwa
nalo. Huu ndiyo mtazamo wa mtu mpumbavu. Hujiaminisha kujua hata kama hajui.
Wapendwa wana wa Mungu,
wenye ufahamu wa kweli, na hofu ya Mungu, tuliombee sana Taifa letu. Taifa letu
sasa linaongowa na mihehuko ya wapumbavu ambao wengi sana. Ni sawa na kuwapa
vichaa rungu. Je, hapo unategemea nini? Kwa nini jamii yetu leo inawashabikia
wezi na mafisadi? Kwa nini wengi wetu leo wamekuwa wapumbavu? Hakika mwendelezo
wa upumbavu huu ni mwitikio wa laana ya Mungu. Tusipojikwamua katika mtego huu
wa upumbavu, tusishangae mateso makubwa huko tuendapo. Wayahudi walipotaka kuwa
na Mfalme kama mataifa mengine ya jirani zao, Mungu aliwapa licha ya kwamba
halikuwa chaguo lake. Wakamchagua Sauli. Mfalme Sauli aliwanyoosha vizuri wana
wa Israeli hadi pale Mungu alipowachagulia Mfalme Daudi. Je, nasi ndiko
tunapoelekea?
Tumsifu yesu Kristo!
EE YESU LITAZAME TAIFA
LAKO NA WATU WAKO. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario