JUMANNE
WIKI YA 8 YA MWAKA-B
26/5/2015
Somo:
Ybs 35:1-15
Zab:
49
Injili:
Mk 10:28-31
Nukuu:
“Umheshimu Bwana kwa
jicho la ukarimu, wala usimtolee malimbuko ya kazi za mikono yako kwa ubahili.
Kwa kila kitolewacho uonyeshe ukunjufu wa uso, hata sehemu ya kumi uiweke wakfu
kwa changamko. Mpe Mungu kama alivyokupa wewe, na kama mkono wako ulivyopata,
utoe kwa ukarimu,” Ybs 35: 7-9
“Amhurumiaye maskini
humkopesha Bwana, naye ni nani awezaye kulipa isipokuwa ni Yeye; kwa kuwa Bwana
hulipa, naye atakulipa wewe mara saba,” Ybs 35:10
“Yesu
akasema, Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au
ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa
ajili ya Injili, ila atapewa mara mia
sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na
mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele,” Mk
10:29-30
TAFAKARI:
“Faida ya kutumika VYEMA kwa ajili ya ufalme wa Mungu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo tutafakari neno hili; “faida ya kutumika VYEMA kwa ajili ya ufalme wa
Mungu.” Kwa ulimwengu huu tunaoishi leo wenye mtazamo wa kupata tu FAIDA na
kuishi katika hali ya USHINDANI, kwa haraka haraka huwezi ona faida ya kutumika
VYEMA kwa ajili ya ufalme wa Mungu. Tupo kwenye ulimwengu usioguswa na hofu ya
Mungu, na hivyo waliowengi siyo tu kwamba hawaamini uwepo wa Mungu, bali pia
hawataki kusikia habari zake.
Ndugu yangu kuna faida
kubwa sana kutumika vyema kwa ajili ya ufalme wa Mungu. Kuzipata na kuzifikia
faida hizi kwa urahisi yakupasa kuzishika amri zake kisawasawa. Kuzishika amri
hizi si kwa ajiali ya kuwakonga watu nyoyo zao, bali kuona ni sehemu ya umilele
wako, na amri za Mungu kuzishika kwa ufahamu, kutakuongoza katika njia iliyo
kweli.
Jambo la pili, ni
kuweka amri hizo katika matendo. Na kwa namna ya pekee, Bwana wetu Yesu Kristo
amezifupisha amri zote kwa kuziweka katika mihimili miwili, yaani Mpende Mungu
wako kwa moyo wako wote, akili zake zote, na nguvu zako zote. Na muhimili wa
pili Mpende jirani yako kama nafsi yako. Hivyo ukimpenda Mungu kwa kile chote
ulicho utafanya haya kadiri ya somo letu la leo; “Umheshimu Bwana kwa jicho la
ukarimu, wala usimtolee malimbuko ya kazi za mikono yako kwa ubahili. Kwa kila
kitolewacho uonyeshe ukunjufu wa uso, hata sehemu ya kumi uiweke wakfu kwa
changamko. Mpe Mungu kama alivyokupa wewe, na kama mkono wako ulivyopata, utoe
kwa ukarimu,” Ybs 35: 7-9. Jambo hili litakupa wajibu wako mbele ya Mungu. Na
utawajibika kumrudishia Mungu kilicho chake. Mara nyingi tunamrudishia Mungu
mabaki ya kazi za mikono yetu. Elewa vitu vyote ni mali yake MUNGU.
Mhimuli wa pili wa amri
za Mungu ni kumpenda jirani yako kama unavyojipenda wewe MWENYEWE. Hapa
utatambua wajibu wako kwa jirani na hasa wahitaji. Utatambua ubinadamu wako na
umuhimu wa binadamu mwingine, hasa wale wasiokuwa na fursa katika jamii
kutokana na mambo mbalimbali. Hivyo, “Amhurumiaye maskini humkopesha Bwana,
naye ni nani awezaye kulipa isipokuwa ni Yeye; kwa kuwa Bwana hulipa, naye atakulipa
wewe mara saba,” Ybs 35:10. Wajibu huu ni muhimu sana kuishi katika hofu ya
Mungu. Masikini tunao wengi sana. Kabla ya kuanza kuwatafuta masikini mitaani,
masikini hawa tunao kwenye familia zetu, jumuiya zetu za kitawa, jumiya zetu
ndogondogo, vigangoni mwetu, na hata parokiani mwetu. Masikini katika hali ya
uuitaji wapo wengi sana. Wengine wengependa tu wasikilizwe hiyo ndiyo kiu yao.
Wengine wengependa wakusikie tu, hiyo ndiyo kiu yao. Na wengine wangeitaji
ufahamu wako katika kuchambua mambo kwa haki na busara.
Wapendwa wana wa Mungu,
katika kuyafanya mambo hayo kulingana na miimili hii miwili, hatupotezi
chochote zaidi ya kufaidika kwa kutumika vyema. Hakuna anayepoteza muda wake
kwa kufanya yale yanayohusu ufalme wa Mungu. Ni furaha kubwa sana mbele za
Mungu akiona umewapeleka wengi kwake. Hivyo Yesu anatuambia tunapoyaacha yale
ambayo yangetujengea umaarufu hapa dunia usiodumu, kwa namna hiyo hiyo
tunajaliwa mengi katika ufalme weke. Hivyo, “Yesu
anakasema, Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au
ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa
ajili ya Injili, ila atapewa mara mia
sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba,
pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele,” Mk 10:29-30. Je,
bado unamashaka kwa utume unaoutoa kwa ajili ya ufalme wa Mungu? Kwa nini hauna
furaha katika utume wake? Kwa nini utume wako unawadumaza watu badala ya
kuwakuza na kufurahia ufalme wa Mungu? Kwa nini unakuwa sababa ya watu
kumchukia Mungu na kuasi njia zake?
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU TUJALIE
TUTUMIKE VYEMA KWA AJILI YA UFALME WAKO. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario