jueves, 28 de mayo de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 8 YA MWAKA-B

IJUMAA YA WIKI YA 8 YA MWAKA-B
29/5/2015
Somo: Ybs 44:1,9-12
Zab: 149: 1-2, 3-4, 5-6a, 9b
Injili: Mk 11:11-26
Nukuu:
“Wema wao utawadumia wazao wao, na urithi wao una wana wa wana. Wazao wao wanashikamana na agano, na watoto wao kwa ajili yao,” Ybs 44:11-12
Hata asubuhi yake walipotoka Bethania aliona njaa,” Mk 11:12
14 Akajibu, akauambia, Tangu leo hata milele mtu asile matunda kwako,” Mk 11.14a
Akafundisha, akasema, Je! Haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi,” Mk 11:17
Yesu akajibu, akamwambia, Mwaminini Mungu,” Mk 11:22
Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu,” Mk 11:24
Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu,” Mk 11:26
TAFAKARI: “Mwaminini Mungu.”
Wapendwa wana wa Mungu, kwa kubatizwa kwetu na leo kuitwa Wakristo bila kuishi Imani hiyo hakusadifu chochote. Hata hivyo, imani ya mtu si tu kwa kile anachokiamini kwa nadharia fulani, bali ni kuwa na imani, na imani hiyo ijionyeshe katika maisha mazima yako ya kila siku. Kwa maana hiyo, leo tutafakari neno hili; “mwaminini Mungu.” Maneno haya anayatamka Yesu kwa wanafunzi wake baada ya Petro kumkumbusha kukauka kwa ule mti aliyoulaani kwa kukosa kuzaa matunda kwa wakati wake.
Maneno haya ya Yesu yanatufundisha kwamba, maisha yetu tunayoyaishi yanapoendana na Imani yetu, neema na baraka zitakuwepo na Mungu atajidhihirisha mara zote kwa yale tunayoyaamini. Hivyo tunapoamini kuliko kwa dhati, tutastajabia mengi katika maisha. Mfumo wa maisha ulio kielelezo cha imani thabiti, ndiyo njia pekee ya kurizishana kizazi hata kizazi. Pamoja na utajiri ambao tunaweza kuwaachia watoto zetu na hata wale tunaoishi nao ni pamoja na Imani iliyo thabiti. Kwa imani hii kizazi kitaendele kumcha Mungu na kuneemeka kwa baraka zake. Hivyo, “Wema wao utawadumia wazao wao, na urithi wao una wana wa wana. Wazao wao wanashikamana na agano, na watoto wao kwa ajili yao,” Ybs 44:11-12. Huu ndio urithi utakao tuwezesha kuuona uso wa Mungu.
Wapendwa, Bwana wetu Yesu Kristo kama Mungu na Mwanadamu; aliona njaa kama mwanadamu, hivyo ilimpasa kula. Kama Mungu alijua ni sahihi kabisa kwa kipindi kila na majira yale ya Mwaka, Mtini ule ulipaswa kuwa na matunda. Badala yake hakupata tunda hata moja. Hivyo anaulaani mtini ule kwa kusema, “Tangu leo hata milele mtu asile matunda kwako,” Mk 11.14a. Kulaaniwa kwa mtini huu kunatupa angalisho kwa maisha yetu ya Kiroho. Je, tunatumia fursa tulizokuwa nazo vizuri kukua kiroho?
Wapendwa tendo hili la kulaaniwa kwa mtini huu kwa kutokuzaa matunda wa wakati wake, kunanikumbusha aina fulani ya mawe yajulikanayo kama “songoro,” kwa kichangga. Mawe haya hupatikana mitoni na kwa uhasilia wake huteleza kutokana na kukaa kwenye maji kwa muda mrefu. Kitu cha kushangaza kwa mawe haya pamoja na kukaa muda mrefu kwenye maji kwa maisha yote ya mto huo, ulipasuapo jiwe hili ndani yake ni kavu sana. Hakuna dalili ya unyevunyevu wa maji. Hii ndiyo laana ambayo tunapata kwa kutotumia fursa tuliyonayo na mazingira tuliyonayo kukua kiroho.
Ni katika mtindo huo huo miili yetu kama hekalu la Roho Mtakatifu, tunaona Yesu akiwatawanya waliokuwa wanalinajisi Hekalu la Mungu kama sehemu ya kumsifu, kumwabudu na kuomba wanapolifanya pango la wanyang’anyi kama sehemu ya biashara. “Je! Haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi,” Mk 11:17. Hatuwezi kumsifu, kumwabudu Mungu na kusali kwa utulivu kama hatuna utulivu ndani yetu. Kumbe kukaa na kumsikiliza Mungu ni kuwa na utulivu ndani yetu. Na siyo tujitawanya kimawazo.
Zaidi ya hayo, tunasali kwa sababu tunaimani kwa kile tunachokiomba. Kama tunasali kwa sababu ni utaratibu wa familia, jumuiya na kikundi chetu cha sala, sala hiyo haina uhai. Huku ni kupotea kiimani na muda pia. Ndani na katika Kristo tunasali kwa sababu tunaamini tumekwisha pata kile tunachokiomba kwa sababu Kristo ni yote katika yote. Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu,” Mk 11:24. Tufanyapo tendo hili kiimani, yatupasa kuwa katika hali ya usafi kimwili na kiroho. Yatupasa kujitakasa kabla ya kutakaswa na kutiwa nguvu na neema kwa yale tuyaombayo. Hivyo hatuwezi kujongea mbele ya Mungu tukiwa na hatia. Yatupasa kujipatanisha na nafsi zetu, wenzetu, na Mungu. Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu,” Mk 11:26.
Wengi wetu, twajipendekeza kwa Mungu, kwa kutimiza ratiba yote kila siku tukisema tuna mpa Mungu haki yake huku upande wa pili hatuishi vyema na ndugu zetu, na jirani zetu. Kusamehe kwa Mkristo ni AMRI. “Utusamehe makosa yetu kama tunavyo wasamehe walio tukosea.”  Maneno haya katika sala ya Baba yetu, yatukumbushe wajibu wetu wa kusamehe.

Tumsifu Yesu Kristo!


NA TUSAMEHANE KILA WAKATI. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario