lunes, 18 de mayo de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 7 YA PASAKA-B


JUMANNE WIKI YA 7 YA PASAKA-B

19/5/2015

Somo: Mdo 20:17-27
Zab: 67
Injili: Yoh 17:1-11a
Nukuu:                                                         
Basi sasa, angalieni, nashika njia kwenda Yerusalemu hali nimefungwa rohoni, nisiyajue mambo yatakayonikuta huko; isipokuwa Roho Mtakatifu mji kwa mji hunishuhudia akisema, ya kwamba vifungo na dhiki vyaningoja,” Mdo 20:22-23
Lakini siyahesabu maisha yangu kuwa kitu cha thamani kwangu kama kuumaliza mwendo wangu na huduma ile niliyopokea kwa Bwana Yesu, kuishuhudia Habari Njema ya neema ya Mungu,” Mdo 20:24
Kwa maana sikujiepusha na kuwahubiria habari ya kusudi lote la Mungu,” Mdo 20:27 
Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo,” Yoh 17:3
Mimi nawaombea hao; siuombei ulimwengu; bali hao ulionipa, kwa kuwa hao ni wako; na wote walio wangu ni wako, na walio wako ni wangu; nami nimetukuzwa ndani yao,” Yoh 17:9-10
Wala mimi simo tena ulimwenguni, lakini hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako,” Yoh 17:11a
TAFAKARI: “Uzima wa milele ndio huu; kumjua Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo.”
Wapendwa wana wa Mungu, kila mmoja wetu hapa duniani kaitwa kwa namna mbalimbali na ya pekee kadiri iliyompendeza Mungu. Kuitwa huku na Mungu kwa itaji mwitikio wetu. Hivyo kila mmoja wetu anavyoitikia bila kujibakiza ndivyo anavyojazwa uzima huo wa milele ambayo ni tayari katika hatua, na ambao bado katika utumilifu wake. Hapa haijalishi mwitikio huo umechukua taswira gani. Kwa maana nyingine haijalishi wewe ni mlei, matawa, au mkleri. Hivyo basi, mwitikio huu lazima ulenge kumjua Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo.
Ni katika  mwitikio huu kimaisha Mtume Paulo hajuutii kumjua na kumtumikia Mungu aliye hai, na Yesu Kristo. Hivyo Mtume Paulo yupo tayari kwa yote yatakayotokea kuhusu maisha yake na uhusiano wake na Mungu. Basi sasa, angalieni, nashika njia kwenda Yerusalemu hali nimefungwa rohoni, nisiyajue mambo yatakayonikuta huko; isipokuwa Roho Mtakatifu mji kwa mji hunishuhudia akisema, ya kwamba vifungo na dhiki vyaningoja,” Mdo 20:22-23
Mtume Paulo anajua wazi maamuzi yake aliyoyachukua katika maisha msingi wake ni Kristo mwenyewe, na hajuutii uamuzi wake huo. Siri yake ni kwamba, tunapojitoa kwake Kristo bila kujibakiza tunauhakika wa uzima wa milele, na safari yetu kuelekea katika utumilifu huo wa maisha ya umilele ni safari salama na yauhakika. Hivyo, siyahesabu maisha yangu kuwa kitu cha thamani kwangu kama kuumaliza mwendo wangu na huduma ile niliyopokea kwa Bwana Yesu, kuishuhudia Habari Njema ya neema ya Mungu,” Mdo 20:24.
Wapendwa wana wa Mungu, tufanyapo maamuzi haya katika maisha licha ya magumu tunayokumbana nayo, tunajua mbele yetu yupo Jemedari Mkuu Yesu Kristo aliyeyashinda yote, na asiyeshindwa kwa lolote. Mateso na magumu tunayokutakana nayo katika maisha Kristo anayajua, na ndiye yeye atakayetutoa kwenye mikwamo hiyo kiimani endapo tutaweka matumaini yetu yote kwake kama mweza wa vyote. Katika ukweli huu Yesu anasema, Mimi nawaombea hao; siuombei ulimwengu; bali hao ulionipa, kwa kuwa hao ni wako; na wote walio wangu ni wako, na walio wako ni wangu; nami nimetukuzwa ndani yao,” Yoh 17:9-10. Je, kwa nini Yesu hauombei ulimwengu? Ulimwengu huu ni kama tanuru la kufulia chuma. Kupata chuma bora na imara lazima kipite kwenye moto mkali sana. Nasi katika kuyashinda mateso haya hapa duniani ndivyo tunavyojiimarisha katika imani na kunyakua taji ile tuliyoandaliwa. Kwa hiyo ulimwengu kama ulivyo ni sehemu ya kukomaza Imani yetu na kukua Kiroho na kimwili.
Ndugu yangu, Je, mateso na maisha yako kwa ujumla yana mwelekeo huo wa uzima wa milele yaani kumjua Mungu wa kweli na Yesu Kristo?

Tumsifu Yesu Kristo!


EE MUNGU NIWEZESHE MAISHA YANGU YA LENGE KUKUJUA WEWE MUNGU WA KWELI NA YESU KRISTO MWANAO. 

No hay comentarios:

Publicar un comentario