ALHAMISI
WIKI YA 8 YA MWAKA-B
28/5/2015
Somo: Ybs 42:15-25
Zab: 32:2-3, 4-5, 6-7, 8-9
Injili: Mk 10:46-52
Nukuu:
“Yeye huchunguza vilindi, na moya wa
binadamu, na kuyatambua mashauri yake ya siri; kwa maana Aliye juu amaizi yote
yaliyo ujuzi, naye hupenya ishara za ulimwengu,” Ybs 42:18
“Hakuna wazo asilolijua, wala hakuna
neno lolote ambalo limefichwa naye,” Ybs 42:20
“Vyote vinahitilafiana, wala hakufanya
chochote kisicho kamili; hata kimoja kinapita kingine kwa uzuri uzidio,” Ybs
42:24-25
“Yesu
akamjibu, akamwambia, Wataka nikufanyie nini? Yule kipofu akamwambia, Mwalimu
wangu, nataka nipate kuona,” Mk 10:51
TAFAKARI: Naye ni nani atakayekinai kwa kuutazama
utukufu wa Mungu?
Wapendwa wana wa Mungu, leo tutafakari uzuri
wa Mungu kwa vile alivyoviumba. Tunapotazama uzuri huu wa uumbaji wa Mungu,
tuanze kwa kutazama maajabu hayo katika uumaji wetu. Hakika tutazamapo uzuri
huo tunagundua kwamba, “vyote vinahitilafiana, wala hakufanya chochote kisicho
kamili; hata kimoja kinapita kingine kwa uzuri uzidio,” Ybs 42:24-25. Tazama
yote aliyokujalia Mungu na ulivyo wa pekee, na anavyokupenda kama ulivyo na
anavyotaka uwe kama alivyokuumba ili uwakilishe utukufu wake. Pamoja na
upendeleo huo kwako, Mungu anapenda kuuchunguza moyo wako kama unashukrani juu
ya upendeleo huo kwako.
Wapendwa, moyo usio na shukrani ukausha
mema yote. “Yeye huchunguza vilindi, na moyo wa binadamu, na kuyatambua
mashauri yake ya siri; kwa maana Aliye juu amaizi yote yaliyo ujuzi, naye
hupenya ishara za ulimwengu,” Ybs 42:18. Wengi wetu hatuoni sababu ya
kumshukuru Mungu kwa namna anavyotukirimia. Wengi wetu mara tuamkapo kitandani
kwa mfano; hatuwezi hata kufanya ishara ya msalaba, kwa kutambua tendo hili la
utukufu wa Mungu kwa kutupenda upeo. Mara tufanyapo tendo la Msaba kwa Imani na
sauti ya ndani, twatambua na kukiri haya juu ya msalaba: “huu ndio ule mti wa
msalaba ambao wokovu wetu umetukikwa juu yake.”
Hata baada ya kulindwa na kuepushwa na
majanga mengi katika maisha kwa upendeleo huu wa Mungu, bado hatuoni sababu ya
kusema neno asante. Giza lijapo twajirusha kitanbani kama mzingo usio na
mwenyewe tukijua tutaamka salama kama tulivyofanya tendo hilo siku ya jana. Je,
hatujawahi kusikia ‘alilala salama lakini hakuweza tena kuiona siku ya pili?’ Ndugu
yangu, “Hakuna wazo asilolijua, wala hakuna neno lolote ambalo limefichwa
naye,” Ybs 42:20. Mungu wetu ni mvumilivu sana. Ni mvumilivu kwa sababu Yeye ni
matumaini kwetu. Matumaini haya ni matokea ya upendo aliokuwa nao kwetu
usiokuwa na mfano.
Pamoja na upendeleo huo, Mungu kwa
kupitia mwanaye Mpendwa Yesu Kristo, yupo tayari kuyafanya yote ayatakayo Baba
yake ili utukukufu wake utawale daima. Tatizo kubwa kwetu sisi tu vipofu na
kushindwa kuona utukufu huo wa Mungu kwa vile alivyoviumba ikiwa ni pamoja na
wewe wenyewe. Ni mara ngapi tunashindwa kumshukuru Mungu kwa uzuri na mema
waliojaliwa rafiki na majirani zetu? Badala yake tumekuwa sababu na vielelezo
vikuu kuudhoofisha utukufu huo wa Mungu.
Kama tuna nia ya kubadilika ili tuone
vizuri kadiri ya utukufu wa Mungu, yatupasa kufanya hatua ya kwanza sisi
wenyewe kama alivyofanya yule mwombaji kipofu kwa kupaza sauti ili asikike na
kuponywa na Bwana Yesu. Nasi kutokana na udhaifu huo yanitupasa kusema toka
moyoni, ‘Yesu mwana wa Daudi, unirehemu.’ Haya ni majuto ya kweli. Hivyo Yesu
anamjibu na kumwambia, “Wataka nikufanyie nini? Yule kipofu
akamwambia, Mwalimu wangu, nataka nipate kuona,” Mk 10:51. Kwa tatizo alilokuwa
nalo mwombaji huyu kipofu alijibu kadiri ya tatizo lake, yaani anataka kuona.
Je, mimi na wewe swali la Yesu linatuhusu? Kama linatuhusu, je unajibu sahihi
kutokana na swali la Yesu? Mjibu Yesu tatizo lako na uwe huru kuudhihirisha
utukufu wa Mungu.
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU NATAKA KUONA.
AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario