domingo, 14 de mayo de 2017

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 5 YA PASAKA


JUMATATU WIKI YA 5 YA PASAKA

Somo: Mdo 14:5-17

Zab: 115: 1-2, 3-4, 15-16

Injili: Yoh 14:21-26

Nukuu:                                                               

Na makutano walipoona aliyoyafanya Paulo wakapaza sauti zao, wakisema kwa Kilikaonia, Miungu wametushukia kwa mifano ya wanadamu. Wakamwita Barnaba, Zeu, na Paulo, Herme, kwa sababu ndiye aliyekuwa mnenaji,” Mdo 14:11-12

Walakini mitume Barnaba na Paulo, walipopata habari, wakararua nguo zao, wakaenda mbio wakaingia katika makutano, wakipiga kelele, wakisema, Akina bwana, mbona mnafanya haya? Sisi nasi tu wanadamu hali moja na ninyi; twawahubiri habari njema, ili mgeuke na kuyaacha mambo haya ya ubatili na kumwelekea Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; ambaye zamani zilizopita aliwaacha mataifa yote waende katika njia zao wenyewe,” Mdo 14:14-16

Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami nitampenda na kujidhihirisha kwake,” Yoh 14:21

Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka,” Yoh 14:24

Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia,” Yoh 14:26

TAFAKARI: “Na tuwe kile kilicho kadiri ya makusudio ya Mungu katika uumbaji wake, sisi kama wanadamu.”

Wapendwa wana wa Mungu, siku yetu hii ya leo na tulitafakari neno hili kadiri ya masomo yetu ya leo, “na tuwe kile kilicho kadiri ya makusudi ya Mungu katika uumbaji wake, sisi kama wanadamu.” Mungu kutuumba sisi kama tulivyo, yaani wanadamu anasababu kubwa sana katika historia nzima ya wokovu wetu. Moja ya sababu kubwa ya kutuumba kama tulivyo wanadamu ni kuwa na uwezekano wa kutushirikisha yale yaliyo ya kimungu [yake], na kuyafanya kama yalivyo tukiwa wawakilishi wake halisi. Bila shaka hii ndiyo sababu kubwa ya kutuumba kwa sura na mfano wake.

Pamoja na kutokukubalika kwa Mtume Paulo na wenzake na Wayahudi kutokana na ujumbe waliokuwa wakiutoa ikiwa ni mwendelezo wa kazi ya Kristo, wanakimbilia Listra na Derbe kupata hifadhi. Mtume Paulo na Barnaba wanafanya mambo makuu kwa mkono wa Mungu, na kuleta tafrani kubwa. Tendo hili la uponyaji wa mtu mwenye udhaifu wa miguu, kiwete tangu tumboni mwa mamaye, linaibua hisia za watu hawa wa Likaonia na kuwaona Paulo na Barnaba kama miungu ya kuabudiwa. Na makutano walipoona aliyoyafanya Paulo wakapaza sauti zao, wakisema kwa Kilikaonia, Miungu wametushukia kwa mifano ya wanadamu. Wakamwita Barnaba, Zeu, na Paulo, Herme, kwa sababu ndiye aliyekuwa mnenaji,” Mdo 14:11-12. Hakika, tendo hili ni moja ya mambo hatari sana katika utume wetu. Ukiona hali hii ndani mwa watu inajitokeza na kuacha kumwabudu Mungu na kuanza kukuambudu wewe kama mchungaji wao, ujue wazi ufanyacho si matakwa ya Mungu bali shetani amechukua mkondo wake.

Ni ukweli usiopingika kwamba, tunastahili pongezi kwa yale tuyafanyayo na hata wakati mwingine kuthaminiwa hasa kwa kuitambua kazi tunayoifanya. Ila mtazamo na mwelekeo huu wa kuthaminishwa na kutambulika kwa yale tuyafanyayo usichukue kamwa nafasi ya Kristo na Mungu. Hivyo kwa kutambua kasoro hii, Mtume Paulo na Barnaba wanatoa angalizo kwa Walikaonia na kusema, “Akina bwana, mbona mnafanya haya? Sisi nasi tu wanadamu hali moja na ninyi; twawahubiri habari njema, ili mgeuke na kuyaacha mambo haya ya ubatili na kumwelekea Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; ambaye zamani zilizopita aliwaacha mataifa yote waende katika njia zao wenyewe,” Mdo 14:14-16. Hatari kubwa katika jambo hili ni kwamba, binadamu anapoukataa ubinadamu wake, anajeuka kuwa mbaya kuliko shetani, kwani shatani alishaukubali ushetani wake pale alipomwasi Mungu.

Ndugu yangu, kuukubali ubinadamu wetu ni pamoja na kujitambua na kuzishika amri za Mungu kwani twataka kuongozwa na Mungu na kuwa watoto wa Mungu. Hivyo Yesu anasema, “Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami nitampenda na kujidhihirisha kwake,” Yoh 14:21. Nani asiyependa kutambuliwa na Mungu? Embu fikiri yote uyafanyayo leo kadiri ya wito wako mwisho wa siku yanakosa kibali mbele ya Mungu. Kumpenda Mungu ni kushika amri zake. Kristo kesha tuambia ni amri ipi iliyo kubwa kuliko zote. Je, neno UPENDO ni geni kwako? Yesu anasema, “Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka,” Yoh 14:24. Hata Bwana wetu Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani hakujifanyia mambo yake kadiri atakavyo. Alikuwa makini sana kutimiza mapenzi ya yule alimpeleka yaani Mungu Baba. Swali la kujiuliza mara zote ni hili, je, hapa nilipo na kadiri ya maagano yangu kimaisha ninayafanya mapenzi ya Mungu? Kama jibu ni hapana, Je, nimejiandaaje kujibu swali hili siku ya mwisho?

Ndugu yangu, mpango wa Mungu kwetu na hasa swala zima la maisha ya umilele limeratibishwa vizuri sana. Nafasi uliyokuwa nayo leo na “mawezekano ya kimaisha,” “life opportunities” hayapo kwa bahati mbaya kwako au upendeleo. Yote haya yanasababu kubwa kuhusu maisha yako ya sasa na wale wanaokuzunguka, na hatma  yake, yaani, umilele. Hata hivyo, kwa kutusaidia, Yesu Kristo anatukumbusha jambo muhimu sana ndugu zangu. Naye anasema, “Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia,” Yoh 14:26. Hivi kama tumefundishwa yote na kukumbushwa yote tunayosababu ya kushindwa mtihani ulio mbele yetu? Ni katika maana hii Yesu anatuambia mwisho wa kiama jambo hili litatokea kwa hakika. “Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno, mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje,” Lk 13:28. Neno hili “kusaga meno” limesemwa mara sita Injili ya Matayo, mara moja Injili ya Marko na mara moja Injili ya Luka. Maana yake ni kwamba hakutakuwa na nafasi ya kujitetea kwani nafasi ya kufanya vema ni leo na sasa.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami nitampenda na kujidhihirisha kwake,” Yoh 14:21

Tusali:-Ee Yesu, tufanye kile tulicho na tuishi kadiri ya mango wa Mungu maishani mwetu. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario