domingo, 7 de mayo de 2017


JUMATATU WIKI YA 4 YA PASAKA

Somo: Mdo 11:1-18

Zab: 42:2-3; 43:3, 4

Injili: Yoh 10:11-18

Nukuu:

“Basi mitume na ndugu waliokuwako katika Uyahudi wakapata habari ya kwamba watu wa Mataifa nao wamelipokea neno la Mungu,” Mdo 11:1

“Sauti ikanijibu mara ya pili kutoka mbinguni, Alivyovitakasa Mungu, usivinene wewe najisi,” Mdo 11:9

“Ikawa nilipoanza kunena, Roho Mtakatifu akawashukia kama alivyotushukia sisi mwanzo,” Mdo 11:15

“Basi ikiwa Mwenyezi Mungu amewapa wao karama ile ile aliyotupa sisi tuliomwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani niweze kumpinga Mungu?” Mdo 11:17

Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:11

“Mtu wa mshahara, wala si mchungaji, ambaye kondoo si mali yake, humwona mbwa-mwitu anakuja, akawaacha kondoo na kukimbia; na mbwa-mwitu huwakamata na kuwatawanya,” Yoh 10:12

“Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:14-15

“Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja,” Yoh 10:16

“Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena,” Yoh 10:18a

TAFAKARI: Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.”

Wapendwa wana wa Mungu, Jumuiya ya kwanza ya Wakristo inaanza kukua na kuenea maeneo tofauti tofauti nje ya Yerusalemu. Uwezo na Nguvu hizi unatoka na kazi ya Roho Mtakatifu Mwenyewe ambaye jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo wamemridhia. Jumuiya ile ya Yerusalemu inapigwa mshangao kuona hata watu wa mataifa wamelipokea nano la Mungu. “Basi mitume na ndugu waliokuwako katika Uyahudi wakapata habari ya kwamba watu wa Mataifa nao wamelipokea neno la Mungu,” Mdo 11:1. Ukweli ni kwamba, kazi ya Roho Mtakatifu ni kutuunganisha sote kuwa kitu kimoja mbele ya Mungu. Namna ya maisha yetu, mwelekeo wa kijiografia, na ukabila, havina nafasi katika Kanisa la Mungu. Sote kwa Sakramenti ya ubatizo tunafanywa wana wa Mungu, na warithi wa Ufalme wa Mungu. Ukweli huu unafunuliwa kwa njia ya maono kupitia Mtume Petro. Sauti ikanijibu mara ya pili kutoka mbinguni, Alivyovitakasa Mungu, usivinene wewe najisi,” Mdo 11:9. Vilivyoumbwa na Mungu na kutakaswa naye si najisi. Nasi mbele za Mungu, kwa kuumbwa kwa sura na mfano wake, sote tunamastahili sawa.

Kwa mastahili haya mbele za Mungu, hatuwezi kumwekea ukuta Roho Mtakatifu kuzitenda kazi zake. Ukweli huu unamtokea Mtume Petro, na kusema, “Ikawa nilipoanza kunena, Roho Mtakatifu akawashukia kama alivyotushukia sisi mwanzo,” Mdo 11:15. Hakuna mwenye hati miliki ya Roho Mtakatifu, bali tunapewa haki hiyo kadiri Mungu apendavyo kugawa karama zake, na kadiri pia ya Roho Mtakatifu huyu apendavyo. Basi ikiwa Mwenyezi Mungu amewapa wao karama ile ile aliyotupa sisi tuliomwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani niweze kumpinga Mungu?” Mdo 11:17

Pamoja na nguvu hizi za Roho Mtakatifu, hatuwezi kutenganisha mahusiano haya na nafsi nyingine katika umoja hasa ule wa kitendaji. Tunamwitaji Kristo ambaye ndiye Mlango wa kwenda mbinguni. Kristo akiwa nafsi ya pili ya Mungu, katika utendaji ndiye aliye mwokozi kwa kile kilichoanguka. Nafsi hii inapokuwa katika utendaji haimaanishi kwamba kwa wakati huo nafsi nyingine hazifanyi kazi, yaani Mungu Baba na Roho Mtakatifu. Ni vile vile Roho Mtakatifu katika utendaji, uvitakatifuza vyote vilivyokombolewa na Kristo, na kwa namna hiyo hiyo nafsi nyingine, yaani Mungu Baba, na Mungu Mwana hufanya kazi pamoja. Na ndiyo maana Yesu anasema maneno haya, “Amin, amin, nawaambieni, Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni mnyang'anyi. Aingiaye mlangoni ni mchungaji wa kondoo,” Yoh 10:1-2.

Furaha yetu ni kwamba tunaye mchungaji mwema anayetuthamini na kutujua si tu kwa majina yetu, bali hata mahitaji yetu. Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:11. Ameutoa uhai wake kwetu na anautoa kila mara tunapoisikia sauti yake. Kristo hatotuacha kamwe wala kujitenga nasi yatakatopotokea majangwa kwetu tukiwa na imani naye na katika  njia pamoja naye. Mtu wa mshahara, wala si mchungaji, ambaye kondoo si mali yake, humwona mbwa-mwitu anakuja, akawaacha kondoo na kukimbia; na mbwa-mwitu huwakamata na kuwatawanya,” Yoh 10:12. Yesu Kristo kwetu si mtu wa mshahara wala mwajiriwa fulani ambaye huliwa kwa kazi yake.

Kristo kwetu ni yote na katika yote. Anatupenda kama tulivyo na amekubali na yupo nasi muda wote ili tufahamu upendo wake kwetu. “Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:14-15. Taswira ya upendo huu wa Kristo kwetu ndiyo kielelezo cha uchungaji wake kwetu. Uchangaji huu wa Kristo haubagui wale wasiopenda ulishaji wake. Huduma anayotoa Kristo habagui hata wale wanaompinga. Hivyo yupo kwa ajili ya wote kwa wakati wote. Kujitenga na Kristo ni kukataa upendo wake anaotupa bure wakati wote. Kristo analitambua jambo hilo na anasema, “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja,” Yoh 10:16. Ni mara ngapi tunawatenga wale ambao wanapingana na mawazo yetu hata ikiwa kwa nia nzuri?

Wapendwa, haya yote Kristo anafanya si kwa kulazimishwa na yeyote au na nguvu yoyote ile, bali anayafanya kwa upendo wake Mkubwa. Haoni shaka wala shida kufa kwa ajili yako. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena,” Yoh 10:18a. Upendo huu wa Kristo kwetu ni wapekee sana.

“Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena,” Yoh 10:18a

Tusali: Ee Yesu Mchungaji Mwema, tufanye wachungaji wema kila mmoja wetu kadiri ya nafasi na wito wake.

No hay comentarios:

Publicar un comentario