JUMAPILI YA 6 YA PASAKA-A
Somo
I: Mdo 8:5-8, 14-17
Zab: 66:1-3, 4-5, 6-7,
16, 20
Somo
II: 1Pet 3:15-18
Injili:
Yoh 14:15-21
Nukuu:
“Kwa maana pepo
wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi
waliopooza, na viwete, wakaponywa,” Mdo 8:7
“wakawapelekea Petro na Yohana; ambao waliposhuka, wakawaombea
wampokee Roho Mtakatifu,” Mdo 8:14b-15
“kwa maana bado hajawashukia hata mmoja wao, ila wamebatizwa
tu kwa jina lake Bwana Yesu,” Mdo 8:16
“Ndipo wakaweka mikono yao juu yao, nao wakampokea Roho
Mtakatifu,” Mdo 8:17
“Mkinipenda, mtazishika
amri zangu,” Yoh 14:15
“Nami nitamwomba Baba,
naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele,” Yoh 14:16
“ndiye Roho wa kweli;
ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali
ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu,” Yoh 14:17
“Sitawaacha ninyi
yatima; naja kwenu,” Yoh 14:18
“Bado kitambo kidogo na
ulimwengu haunioni tena; bali ninyi mnaniona. Na kwa sababu mimi ni hai, ninyi
nanyi mtakuwa hai,” Yoh 14:19
“Siku ile ninyi
mtatambua ya kuwa mimi ni ndani ya Baba yangu, nanyi ndani yangu, nami ndani
yenu,” Yoh 14:20
“Yeye aliye na amri
zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba
yangu; nami nitampenda na kujidhihirisha kwake,” Yoh 14:21
“Mwe tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari
za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu,” 1Pet 3:15
“Nanyi
mwe na dhamiri njema, ili katika neno lile mnalosingiziwa, watahayarishwe wale
wautukanao mwenendo wenu mwema katika Kristo,” 1Pet 3:16
“Maana ni
afadhali kuteswa kwa kutenda mema, ikiwa ndiyo mapenzi ya Mungu, kuliko kwa
kutenda mabaya,” 1Pet 3:17
“Kwa
maana Kristo naye aliteswa mara moja kwa ajili ya dhambi, mwenye haki kwa ajili
yao wasio haki, ili atulete kwa Mungu; mwili wake akauawa, bali roho yake
akahuishwa,” 1Pet 3:18
TAFAKARI:
“Mkinipenda, mtazishika amri zangu,” Yoh 14:15
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya sita ya Pasaka ya mwaka “A” wa Kanisa.
Leo Yesu anaweka wazi neno hili: “Mkinipenda, mtazishika amri zangu.” Upendo
ndiyo msukumo hai wa maisha ya jumuiya, na sote kama wakristo. Ingawa waweza
kutoa bila kupenda, huwezi kupenda ukaacha kutoa. Hali na mtazamo huu ndiyo
sura halisi ya jumuiya ile ya kwanza ya wakristo.
Wapendwa wana wa Mungu,
ni kweli pasipo shaka yoyote kwamba kila mmoja wetu kuna kitu ambacho
kinaongoza na kuyasukuma maisha yake. Kitu hicho ndiyo dira na sababu ya mtu
kufanya afanyavyo na kuishi aishivyo. Msukumo huo ndiyo unaotufanya kama
tulivyo. Msukumo huyo ndio unaotupa furaha na matumaini kwa yale
tunayoyatarajia. Msukumo huo wa maisha ndio unaotupa moyo wa kuendelea kufanya
tunayoyafanya. Na kwa upande mwingine, msukumo huo wa maisha huwa sababu ya
huzuni yetu ya kudumu.
Hivyo ndugu yangu
tunayesafiri pamoja katika tafakari hii, Mtume Paulo anasema jambo hili
kuonyesha kile kinachosukuma maisha yake. “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na
Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,”
Kol 3:1. Huu ndiyo msukumo sahihi wa maisha yetu ya ufufuko, maisha mapya na
Kristo. Ni maisha ya kuutafuta ufalmwe wa Mungu kwa yale yote tuyafanyayo. Ni
kumwona Kristo kwa kila unayekutana naye, ishi naye, na kuwajibika kwako kwao
kadiri ya wito wako, nafasi yako, na vipaji na uwezo aliokujalia Mungu. Na
jambo hili linawezekana pale tu upendo wa kweli unapotawala mioyoni mwa
wanajumuiya.
Wapendwa wana wa Mungu,
msukumo huu wa maisha (maisha ya ufufuko yenye kusukumwa na upendo wa kweli)
ndiyo sababu ya kifo dini na shahidi cha Stefano. Jumuiya ya kwanza ya Wakristo
inahujumiwa na Sauli na kutawanyika. Mitume wakisukumwa na Kristo aliye sababu
ya maisha yao, na Roho Mtakatifu, wanabaki Yerusalemu wakitoa ushuhuda wa
Kristo hadi toni la mwisho licha ya machafuko yaliyotokea kwa sababu ya kifo
cha Shahidi Stefano. Ni nguvu katika umoja wa Roho huyu Mtakatifu inafanya kazi
kama Kristo alivyokwisha wahaidia kabwa ya kupaa kwake, kwamba, “nami nitamwomba
Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele,” Yoh 14:16.
Na huyu “ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa
haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye
atakuwa ndani yenu,” Yoh 14:17
Ndugu yangu, ni nguvu
ya Roho huyu Mtakatifu waliyemwamini wa Kristo wa kwanza na Mitume, na
kuongozwa naye kwamba hata “siku ile kukatukia
adha kuu ya Kanisa lililokuwa katika Yerusalemu; wote wakatawanyika katika nchi
ya Uyahudi na Samaria, isipokuwa hao Mitume,” Mdo 8:1. Hata wale waliotawanyika
kutokana na hujuma hii, hawakukoma kulitangaza na kulihubiri jina hili
lililopita majina yote, Yesu Kristo Mnazareti. “Lakini wale waliotawanyika
wakaenda huko na huko wakilihubiri neno,” Mdo 8:4. Miongoni mwa watu hawa ni Filipo.
Filipo analihubiri
Jina la Yesu na wengi wanaona mwanga, kweli, na uzima kwa kuponywa na kuwa
huru. “Kwa maana pepo wachafu wakawatoka
wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na
viwete, wakaponywa,” Mdo 8:7. Haya ndiyo mambo makuu ya Mungu kwa wale wanao
mwamini na kumtegemea. Haya ndiyo mambo makuu Mungu huyafanya kwa wale
wasiokuwa na shaka naye na uwezo wake. Mungu huyatenda makuu hayo kwa wale
wasiokatishwa tamaa na vipingamizi dhidi ya kile wanachoamini.
Wapendwa
katika Kristo, ndani na katika Kristo kuna uzima na ufufuo siku ya mwisho.
Maisha ya kweli na Kristo, ndiyo njia sahihi ya kuufikia umilele ambao ndiyo
makusudi ya uumbaji wetu. Kazi kubwa ya Kristo ni kuhakikisha walio mridhia
hawapotei hata mmoja. Ulizi ndani ya Kristo ni salama kuliko linzi nyingine
zote unazoweza kufikiria. Ni ulinzi, si tu katika usalama wa miili yetu na mali
zetu, ila roho zetu katika hali ya ufufuo na uzima wa milele. Naye Yesu
anatuhakikishia jambo hili na kusema, “Wote anipao Baba
watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe,” Yoh 6:37.
Kristo aliyeishinda mauti na yu hai sasa
ndiye huyo huyo anayetupa matumaini hai na ya kweli kwa kusema, “Sitawaacha
ninyi yatima; naja kwenu,” Yoh 14:18. Leo Kristo yupo na anakuja kwetu kila
tunaposhiriki sakramenti zake pasipo hatia. Tunatiwa uzima kwa kushiriki Mwili
na Damu ya Kristo pasipo na hatia, na kunaponywa majeraha yetu yaliyotokana na
dhambi zetu kwa sakramenti ya kitubio.
Wewe na mimi kama
wafuasi wake Kristo tu mashahidi na watoa ushuhuda wa kweli kuhusu Kristo Yesu
aliye yote katika yote. Na hivyo Yesu anatuambia hivi, “Bado kitambo kidogo na
ulimwengu haunioni tena; bali ninyi mnaniona. Na kwa sababu mimi ni hai, ninyi
nanyi mtakuwa hai,” Yoh 14:19. Bila Kristo Yesu hatuwezi fanya lolote, liwe
kubwa au dogo, Yoh 15:5. Ila tukiwa ndani na katika Kristo, Yeye mwenyewe
anatuambia, “Siku ile ninyi mtatambua ya kuwa mimi ni ndani ya Baba yangu,
nanyi ndani yangu, nami ndani yenu,” Yoh 14:20. Na haya yote yatafanyika pale
tu tunapopendana na kuishi upendo wa kweli kati yetu bila kubaguana. Na huku
ndiko kuzishika amri zake. Naye Yesu anasema, “Yeye aliye na amri zangu, na
kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami
nitampenda na kujidhihirisha kwake,” Yoh 14:21
Pamoja na hayo yote swali la kujiuliza
ni hili; Ndugu yangu maisha yako umeyawekeza kwa nani? Je, kwenye utajiri wako?
Je, kwa marafiki zako? Je, akili na ujanja wako? Je, katika maisha yako ya
kijanja kijanja? Je, kwenye kadi zako za benk ya “life security?” Yote hayo
utayaacha na kuondoka na Roho yako tu. Je, mbele ya Mungu utajitetea na nini?
Njia salama ni kuwekeza kwa Kristo kupitia Benk yake-ni “ROHO YAKO.”
Ndugu yangu na Mkristo mwenzangu, pamoja
na changamoto tunazokutana nazo ikiwa ni pamoja na imani yetu kama Wakristo
Wakatoliki, Mtume Petro anatupa namna ya kufanya na kuishi, yaani, tuwe “tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za
tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu,” 1Pet 3:15. Kwa maana
nyingine ni wito wetu leo kutoa ushuhuda wa ukimya pale tulipo, na ushuhuda huo
ubebe uhalisia wa maisha yetu kama wafuasi wake Kristo na wenye hofu ya Mungu.
Katika kweli hii, Mtume Petro anasema, tuwe “…na dhamiri njema, ili katika neno
lile mnalosingiziwa, watahayarishwe wale wautukanao mwenendo wenu mwema katika
Kristo,” 1Pet 3:16.
Kuongozwa
na dhamiri njema ni wito vile vile wa kuona uhalisia wa jambo kama ulivyo, na
siyo kama nilivyo. Tatizo kubwa la jamii yetu leo, Watanzania, tumeingiwa na
woga pasipo woga, na tokeo lake ni nidhamu ya woga iliyojengeka katika
mazingira ya unafiki. Tumekuwa watu wa tabasamu pasipo tabasamu, na wapiga
makofi pasipo pongezi. Tumepoteza uthubutu wa kuhoji: ‘kwa nini twafanya kama
tunavyofanya,’ na mwisho tumebaki kuwa kile tusicho.
Ndugu
yangu, Mtume Petro anakuambia wewe na mimi kwamba, “Maana ni afadhali kuteswa
kwa kutenda mema, ikiwa ndiyo mapenzi ya Mungu, kuliko kwa kutenda mabaya,”
1Pet 3:17. Kweli hii inatupeleka karibu kabisa na tafakari juu ya msalaba.
Ingawa penye msalaba kuna utukufu, hakuna utukufu pasipo msalaba.
“Kwa maana Kristo naye aliteswa mara moja kwa ajili
ya dhambi, mwenye haki kwa ajili yao wasio haki, ili atulete kwa Mungu; mwili
wake akauawa, bali roho yake akahuishwa,” 1Pet
3:18. Leo wengi wetu twapenda utukufu, na hata kuitwa watukufu bila msalaba. Historia
ni mwalimu mzuri sana. Ni punde tu historia itatuweka mahali pake.
Ndugu yangu nikuache na
changamoto hii. Maisha yetu ni changamoto kubwa sana kama ilivyo giza na
mwanga. Kumbe tunapohitaji mwanga kuliondoa giza, tujifunze kutoka mshumaa.
Mshumaa unaotoa mwanga kulifukuza giza, na kwa tendo hilo haliuachi mshumaa
katika umbo lake. Na ndivyo ilivyo kwa wapigania haki na amani katika jamii
yetu, na wale wote wanaojitoa bila kujibakiza kwa upendo. Na katika kweli hii
Yesu anasema, “Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi,
ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi,” Yoh
12:24. UKIPENDA UTAFANYA YOTE, Mt. Augustino wa Hippo.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Maana ni afadhali
kuteswa kwa kutenda mema, ikiwa ndiyo mapenzi ya Mungu, kuliko kwa kutenda
mabaya,” 1Pet 3:17
No hay comentarios:
Publicar un comentario