JUMAPILI YA 5 YA PASAKA-A
Somo
I: Mdo 6:1-7
Zab: 33:1-2, 4-5, 18-19
Somo
II: 1Pet 2:4-9
Injili:
Yoh 14:1-12
Nukuu:
“Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu
na kuhudumu mezani,” Mdo 6:2
“Ambao wakawaweka mbele ya mitume, na
walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao,”Mdo 6:6.
“Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na
mimi,” Yoh 14:1.
“Basi mimi
nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo
mimi, nanyi mwepo,” Yoh 14:3.
“Mmwendee yeye, jiwe
lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye
heshima,” 1Pet 2:4.
“Bali ninyi ni mzao
mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate
kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake
ya ajabu,” 1Pet 2:9.
TAFAKARI:
“Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya nne ya Pasaka ya Mwaka “A” wa Kanisa. Jumuiya ya kwanza ya wakristo kadiri
ya somo la kwanza leo, wanaingiwa hofu kutokana na jumuiya hiyo kuongezeka, na
huduma kutokwenda sawa. “Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu
na kuhudumu mezani,” Mdo 6:2. Hivyo wanaona ipo hatari ya kuacha
kulihubiri neno wakabaki kutatua matatizo yanayotokana na manung’uniko kati ya Wayahudi
wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma
ya kila siku.
Jumuiya hii kwa
kuongozwa na nguvu ya Kimaadili, Unyenyekevu, na Roho Mtakatifu, wanakabiliana
na hofu hii kwa kufanya uteuzi wa watu saba “Mashemasi,” kutatua tatizo hilo.
Mitume wanatoa agizo na vigezo vya kuwachagua wasaidizi hao na kusema, “basi
ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye
kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na
kulihudumia lile Neno,” Mdo 6:3-4.
Baada ya vigenzo na
masharti kuzingatiwa, wateule hawa wanawekwa wakfu kwa tendo “ambao wakawaweka
mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao,” Mdo 6:6. Tendo hili linamsisitizo wa umoja
wa Mitume ambao leo tungesema umoja wa maaskofu, “Collegiality of Bishops.”
Umoja huu ni muhimu sana leo katika Kanisa letu. Tunapoona mmoja katika kundi
hili akitamka yake kama anavyojisikia, ni wazi taasisi hii muhimu na fundishi
inaingiliwa. Tulio wengi tunajiuliza, hilo alinenalo kalitoa wapi, na kwa
baraka ya nani? Na kama jambo hilo asemalo linaukweli, Je, ni kwa manufaa ya
nani?
Wapendwa wana wa Mungu,
ingawa upo uwezekano wa mtu yeyote kuupata wokovu na kuifikia Mbingu kutokana
na msukumo wa maisha yake yenye kuongozwa na dhamiri yake njema na hofu ya
Mungu hata kama hakuwahi kusikia habari njema za Kristo Yesu, wewe na mimi
tuyeunganishwa na Kristo kwa Sakramenti ya Ubatizo, Kristo hubaki kuwa njia,
kweli, na uzima katika usahihi wake. Kwa wale ambao bado hawajafikiwa na habari
njema ya wokovu ila wanaishi kwa dhamiri zao njema, Kanisa kupitia Mamlaka yake
fundishi-Magisterium, linasema hivi juu ya wokovu wao; -Mafundisho ya Kanisa hasa tunaposoma Katekisimu ya Kanisa Katoliki,
namba 847 inafundisha juu ya dhamiri hai na safi ambapo hata wale wasiomjua
Kristo ndiyo ponya yao.
Ukweli
huu pia umefafanuliwa vizuri katika mafundisho ya Mtaguso wa Pili wa Vatikano,
Konstitusio ya Kichungaji juu ya Kanisa katika Ulimwengu wa leo, “Gaudium Et
Spesteaches,” “Furaha na Matumaini,” inaelezea ukweli huu kama ifuatavyo; “Jambo hilo haliwahusu wakristo tu bali pia wanadamu wote
wenye mapenzi mema, ambao neema ya Mungu hufanya kazi mioyoni mwao, kwa namna
isiyoonekana. Maana Kristo alikufa kwa ajili ya watu wote na wito halisi wa binadamu ndio mmoja, ule
wa kimungu. Kwa hiyo lazima tuwe na wazo kwamba Roho Mtakatifu anawajalia watu
wote uwezekano wa kushiriki fumbo la kipasaka, kwa jinsi anayoijua Mungu,” (no.
22)
Pamoja na ukweli huo,
ikiwa wewe na mimi tumeunganishwa na Kristo kwa Sakramenti ya Ubatizo na kuwa
warithi wa ufalme wa mbinguni, yatupasa kuishi ndani na katika Kristo. Hivyo ni
wajibu wangu leo na daima kumjua Kristo, kumpenda, kumtumikia–(kupitia wote
wale walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, Mwa 1:27), na mwisho ni Yeye tu
atakaye nihesabia haki mbele ya kiti chake cha uzima wa milele mbinguni. Masomo
yetu ya leo yamefafanua kwa undani kweli hii.
Wapendwa wana wa Mungu,
ikiwa wewe ni mfuasi wa Kristo na Mungu aliye hai, katika maana ya kuziishi
vyema na kwa uaminifu ahadi zako za ubatizo, yakupasa kuelewa ukweli huu juu ya
Kristo Yesu. Ukweli ni kwamba, bila Kristo hatuwezi kufanya lo lote, liwe dogo
au kubwa. Kama Kristo ni Mzabibu nasi tu matawi yake, twawezaje basi kushamiri
na kupata uhai pasipo shina lenyewe? Kitendawili hiki kinateguliwa na Kristo
mwenyewe. Naye anasema, “Mimi ni mzabibu;
ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana
pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:5.
Ndugu yangu na Mbatizwa
mwenzangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, kwa weledi wako na yote
uliyonayo, Je, waweza kutoboa mbingu bila Kristo Yesu? Na kama vile haitoshi,
Yesu anaenda mbali zaidi na kujifananisha yeye na Mlango. Ndugu yangu na
Mbatizwa mwenzangu, Kristo tu ndiye Mlango wa kufikia huo upande wa pili,
yaani, Mbingu. Naye Yesu anatuambia hivi, “Amin,
amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo. Mimi ndimi mlango; mtu akiingia
kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata malisho,” Yoh 10:7, 9.
Upekee wa Kristo kama ndiyo Mlango sahihi umebebwa na maneno haya mazito ya
Yesu. Naye anasema hivi, “Wote walionitangulia ni wevi na wanyang'anyi; lakini
kondoo hawakuwasikia,” Yoh 10:8.
Maana yake ni kwamba, kama hapo-“wakati
fulani” iliwezekana wachache kwa ujanja ujanja wao kupita, au waliojitangazia
na hata kujiinua kwamba wao ni “milango,” hawakuwa sahihi, na hata leo kama
wapo si milango au mlango sahihi. Habari Njema kwa sasa ni kwamba Yeye mwenyewe-Yesu
Kristo ndiyo HABARI NJEMA HIYO, na ndiyo MLANGO SAHIHI na wa KWELI.
Mpendwa katika Kristo,
hapana shaka yoyote kwamba msukumo wa maisha ya Mtume Paulo ulipata msingi
imara katika fundisho hili la Mtume Petro, kwamba “Wala
hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini
ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo-Yesu Kristo,” Mdo
4:12. Ufahamu huu ndio, yaani, ‘Kristo ndiye kila kitu katika maisha yetu,’
ndio unaotupeleka kuyafahamu maneno ya Yesu katika Injili ya leo. Naye Yesu anasema, “Mimi
ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh
14:6. Yesu Kristo ni njia kama ulivyo Mlango
pekee wa kuufikia uzima wa milele. Na njia aliyoichagua Yesu ni Msalaba. Kwa
kuibeba misalaba yetu na kuchukulia kindugu katika misalaba ya wenzetu kwa
uaminifu na hofu ya Mungu tunakutana naye Kristo katika hali na mazingira hayo.
Yesu Kristo ni kweli halisi. Kweli hii tunakutana nayo katika neno lake hasa
pale tunapokuwa tayari kulisikia neno, kulipokea neno, kulitafakari neno,
kulishirikisha neno, na mwisho kuwa shahidi wa neno.
Na Yesu Kristo ni
uzima halisi. Kristo ni uzima halisi tunaposhiriki Ekaristi Takatifu katika
mastahili yake. Yesu anatuambia, “Mimi
ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye
hataona kiu kamwe” Yoh 6:35. Ni katika kula chakula hiki-mwili na damu yake, Yesu
anahaidi mambo mawili makuu: Moja, ni ufufuko siku ya mwisho. Naye anasema, “Aulaye
mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya
mwisho,” Yoh 6:54. Na katika kula chakula hiki-mwili na damu yake, Kristo hukaa
ndani yetu. Naye anasema, “Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani
yangu, nami hukaa ndani yake,” Yoh 6:56.
Hata
hivyo Mtume Paulo anatupa angalizo la chakula hiki cha uzima. Naye anasema, “Basi
kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili,
atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana,” 1Kor 11:27. Yatupasa
kuijongea Meza ya Bwana tukiwa na mastahili ya kufanya hivyo-usafi wa mwili na
roho, yaani, pasipo hatia yoyote. Zaidi ya hapo ni kuikufuru Meza ya Bwana.
Wapendwa wana wa Mungu,
kwa kupitia Sakramenti ya kitubio tunapatanishwa tena na Kristo kutoka katika
hatia zote. “Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa
nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera,
zitakuwa kama sufu,” Isa 1:18. Hakuna sababu ya kufa moyo pale ambapo mambo
huenda ndivyo sivyo. Mungu aliye Upendo na Huruma uanza upya nasi pale
tunapokuwa tayari kufanya hivyo. Hivyo ndani na katika Kristo hakuna sababu ya
kuwa na hofu. Tumwamini Kristo na tuziamini kazi zake na hasa kupitia
Masakramenti yake. “Msifadhaike mioyoni mwenu;
mnamwamini Mungu, niaminini na mimi,” Yoh 14:1.
Ndani na Katika
Kristo kunautulivu wa kweli, naye kesha tuandalia makao ya milele. Duniani hapa
ndugu yangu tunapita tu. Ulimwenguni hapa ni sehemu ya maandalizi ya huo
umilele. Mbinguni ndipo kwenye nafasi ya kila mmoja wetu, na ndiyo makao ya
milele. “Nyumbani mwa Baba
yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia
mahali,” Yoh 14:2. Lengo la Kristo ni kumpata kila mmoja wetu. Hili ndilo pia
lengo msingi la Kanisa. Lilipo Kanisa katika maana ya Mwili wa Kristo nasi
tukiwa viungo hai vyake, Kanisa huwa Sakramenti ya Wokovu kwa sababu Kristo yu
hai mahali hapo. “Basi mimi nikienda
na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi,
nanyi mwepo,” Yoh 14:3. Ndungu yangu, je, hu kiungo hai cha mwili wa Kristo,
yaani Kanisa?
Wapendwa wana wa Mungu,
msingi wa haya yote tunayoyaona kutoka jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo
yanatokana na msingi wa imani waliyokuwa nayo juu ya Yesu Kristo na yale
aliyoyafundisha. Ni ukweli usiotia shaka kwamba jumuiya hii ya kwanza ya
Wakristo waliamini barabara yule wamfuatao na kumshuhudia mbele za watu. Mtume
Filipo anapomwuliza Yesu tuonyeshe Baba nayo yatosha kumwamini, Yesu anamjibu
na kusema, “Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku
hizi zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba; basi wewe
wasemaje, Utuonyeshe Baba?” Yoh 14:9. Kristo
anafumbua ukweli wa kumwilishwa kwake, si tu kwa Filipo, hata kwetu pia.
Kumwilishwa huku kwa Yesu Kristo ni ukweli wa Mungu mwenyewe katika fumbo na
umbo hili la kibidamu kama sisi ila utofauti wake ni kwamba hakutenda dhambi
kama mwanadamu. Yesu Kristo anakazia ukweli huu na kusema, “Hayo maneno
niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu
huzifanya kazi zake,” Yoh 14:10b. Ufunuo huu wa Mungu kupitia Yesu Kristo ni wa
wazi na wakati mwingine wakujificha. Ila hapana shaka hata kidogo kwa umungu wa
Kristo kunakojieleza kwa yale aliyoyafanya yaani kazi zake.
Wapendwa
wana wa Mungu, Kristo analifumbua jambo hili pale tunapokuwa na shaka juu yake
kwa kusema, “La! Hamsadiki hivyo, sadikini kwa sababu ya kazi zenyewe,” Yoh
14:11b. Imani ya kweli juu ya Kristo ndiyo inayotufanya kuishi na kutenda kama
alivyofanya Yesu Kristo. Ukweli huu anausema Kristo mwenyewe, na wale wote
waliouishi ukweli huu, Kristo amefanya makuu kupitia kwao kwa mkono wake. “Yeye
aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa
kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba,” Yoh 14:12. Matendo makuu
hufanyika kwa mtu huyu aaminiye juu ya Kristo si kwa faida yake binafsi, ila
kwa kupitia mtu huyu Mungu anatukuzwe na kuabudiwa milele ndani ya Yesu Kristo
mwanaye. “Nanyi mkiomba lo lote kwa jina
langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana,” Yoh 14:13. Je,
ndugu yangu, hupendi kuwa sababu ya utukufu huu wa Mungu kupitia mwanaye Yesu
Kristo?
Wapendwa,
jibu la swali hili ndilo kiini cha Imani yetu, na maisha yetu kama Wakristo na
Wafuasi wa Kristo leo katika dunia hii tunayoishi: “KUWA SABABU YA UTUKUFU WA
MUNGU KUPITIA MWANAYE YESU KRISTO, na si vinginevyo.
Ndugu yangu, unapopata
kuona njia kwa macho ya kiroho ni sawa na kuzaliwa upya. Ni kushibishwa nuru
ile iangazayo katika kweli halisi. Ni msukumo wa neema ndani yako unaoangaza na
kuyaona yale yaliyo juu ya uwezo wako kiakili kama wanadamu. Neema ya Mungu
ndani na kwa njia yake Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai, utuwezesha na
kutuongoza kuyafikia yale Mungu anayotamani sote siku moja kuyafikia. Hivyo
ndugu yangu, “Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali
kwa Mungu ni teule, lenye heshima,” 1Pet 2:4. Jiwe hili ndilo Kristo Yesu Mwana
wa Mungu aliye hai.
Kwa Sakramenti ya
Ubatizo miili yetu inakuwa Hekalu la Roho Mtakatifu, na viungo wa Kristo kama
Kanisa. Kwa Sakramenti ya Ubatizo tunashirikishwa ukuhani wa kawaida wa Yesu
Kristo. “Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo
hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho,
zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo,” 1Pet 2:5. Licha ya kuwa
makuhani wa kawaida wa Kristo, kwa Sakramenti ya Ubatizo, tu wa milki ya Mungu
katika nuru ya ajabu-wana wa Mungu aliye Mtakatifu. “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa
kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake
yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu,” 1Pet 2:9. Tu
wana wa nuru na kwa sababu hiyo ndicho alichokijia Yesu. “Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila
mtu aniaminiye mimi asikae gizani,” Yoh 12:46.
Ndugu
yangu, bila shaka ulishakutana na mdudu huyu (kwa Kichaga hujulikana
kama-“Kirombocho”). Mdudu huyu husukuma kinyesi cha ng’ombe kwa kutumia miguu
yake ya nyuma kutwa kuchwa, kila siku. Hufanya kazi hii kwa bidii kubwa sana,
na hasa pale anapokisukuma kinyesi hiki kuelekea mlimani.
Jambo
la kushangaza mara afikapo kileleni, kwake siyo mwisho wa kazi, safari, wala
pumziko. Kinyesi hiki huweza kumponyoka na kuporomoka tena hadi chini kabisa,
mwanzoni, pale alipoianza safari, na kazi huanza tena.
Kwa
mwono wa kujishughulisha kama sera, mdudu huyu anaitendea haki. Ila kwa upande
wa “maisha yenye kuongozwa na malengo,” mdudu huyu yupo nje ya sera.
Bila
shaka wewe na mimi tusipo ishi maisha yenye ‘kuongozwa na malengo,’ na Kristo
akiwa kielelezo chetu kama ‘Njia, Kweli, na Uzima,’ tutaishia kuwa kama mdudu
huyu “Kirombocho.”
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Mmwendee yeye, jiwe lililo hai,
lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima,” 1Pet 2:4.
Tusali:
Ee Yesu, tuongoze kuishi maisha yenye malengo na mwisho tuufikie ule uzima wa
milele.
No hay comentarios:
Publicar un comentario