JUMAPILI YA 4 YA PASAKA-A
JUMAPILI YA 4 YA PASAKA-A
Somo
I: Mdo 2:14a, 36-41
Zab: 23:1-3a, 3b-4, 5, 6
Somo
II: 1Pet 2:20b-25
Injili:
Yoh 10:1-10
Nukuu:
“Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa
jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha
Roho Mtakatifu,” Mdo 2:38.
“Kwa
kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio
mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie,” Mdo 2: 39.
“Akawashuhudia kwa maneno mengine mengi sana na kuwaonya,
akisema, Jiokoeni na kizazi hiki chenye ukaidi,” Mdo 2:40.
“Yesu
aliwaambia, Amin, amin, nawaambieni, Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la
kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni mnyang'anyi. Aingiaye mlangoni ni mchungaji wa kondoo,”
Yoh 10:1-2
“Mimi
ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata
malisho,”Yoh 10:9
“Lakini kustahimili,
mtendapo mema na kupata mateso, huu ndio wema hasa mbele za Mungu,” 1Pet 2:20b
“Kwa sababu ndio
mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo,
mfuate nyayo zake,” 1Pet 2:21
“Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana
kinywani mwake,” 1Pet 2:22
“Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa,
hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki,” 1Pet 2:23
“Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili
wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki;
na kwa kupigwa kwake mliponywa,” 1Pet 2:24
“Kwa maana mlikuwa mnapotea kama kondoo; lakini sasa
mmemrudia Mchungaji na Mwangalizi wa roho zenu,” 1Pet 2:25
TAFAKARI: “Wote
tumeitwa kama tulivyo; Kristo ndiye Mlango. tumrudie Mchungaji na Mwangalizi wa
roho zetu.”
Wapendwa wana wa Taifa
la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya nne ya mwaka “A” wa Kanisa. Masomo
yetu ya leo yanatualika kuyatafakari haya: “Wote tumeitwa kama tulivyo; Kristo
ndiye Mlango. Tumrudie Mchungaji na Mwangalizi wa roho zetu.” Hivyo, tendo la
ufufufuko wa Bwana Wetu Yesu Kristo, linatuwezesha na linakuwa neema na baraka
kwetu, hasa ule uwezo wa kupokea vipawa vya Roho Mtakatifu pale tu tunapofanya
toba ya kweli. Ni kwa dhambi zetu imekua sababu ya kifo cha Bwana wetu Yesu
Kristo, na ni kwa kupitia toba ya kweli kwa dhambi zetu twapokea neema na
baraka, na kuhesabiwa tena haki kuwa warithi na wana wa Mungu. Ni kwa sababu
hii, leo kwa namna ya pekee tutafakari juu ya neno hili, “Kwa Ufufuko wa Yesu
Kristo sote twahesabiwa haki kwa kufanya toba ya kweli; Naam, sote kwa upendo
wa Mungu twaitwa wana wake na yeye ni Mungu wetu.”
Mtume Petro, kwa
kujaliwa ujasiri na nguvu ya Kristo Mfufuka, haoni haya kuwaambia Wayahudi
ukweli kuhusu wokovu wao baada ya kufanya kosa la kumwua mwenye haki-Yesu
Kristo. Hata sasa Mtume Petro ananiambia mimi na wewe ambao twahitaji huruma na
neema ya Mungu. “Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu
Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho
Mtakatifu,” Mdo 2:38.
Ndugu
yangu, ni kwa jina la Yesu Kristo tu twaweza kupata msamaha wa dhambi, na
kupatanishwa tena na Mungu Baba. Na ni kwa njia ya ubatizo tunafia dhambi na
kuzaliwa wapya kama ishara halisi ya Ufufuko wa Yesu Kristo. “Naye alituokoa
katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa
pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi; naye ni
mfano wa Mungu alisiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” Kol 1:13-15.
Ili tufaidi neema za Ufufuko wa Bwana Yesu Kristo, ikiwa ni pamoja na vipawa
vya Roho Mtakatifu, yatupasa kufanya toba ya kweli, ikiambatana na kuzaliwa
upya kwa njia ya Roho Mtakatifu.
Toba
ya kweli ni kutambua kule kujikwaa kwetu, na kuyaacha maanguko hayo, huku
tukifuata njia iliyo sahihi. Yesu Kristo pasipo shaka yo yote, ndiye njia
sahihi ya kufuata, kwani kwa Ufufuko wake, yaliyo ya kale, na yasasa, na yajayo
yamekwisha eleweka. Tuendako sasa twakujua. “Yesu akamwambia.
Usinishike; kwa maana sijapaa kwenda kwa Baba. Lakini enenda kwa ndugu zangu
ukawaambie, Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu
naye ni Mungu wenu,” Yoh 20:17. Ili tupate
mastahili ya kumshika Kristo Mfufuka, yatupasa kufanya toba ya kweli kama
nilivyokwisha kusema. Yesu anamwambia Mariamu na kumbumbusha toba ya kweli. Huu
ni wito wa kujitakasa kwa yale mambo yanayotukwamisha kuiona sura ya Mungu.
Mastahili yetu baada ya kuhesabiwa haki kwa kufanya toba ya kweli, ni maisha ya
utakatifu.
Maisha mapya baada ya Ufufuko, ni maisha
ya Utakatifu kwa wote wanaoridhia njia ya Kristo. Kuridhia njia hii ni kufanya
toba ya kweli. Tendo hili la toba ya kweli ndani na katika Kristo, linatupa
mastahili sawa bila kujali historia zetu mbaya, makabila yetu, na hata utaifa
wetu. Tendo hili linatupa uhalali wa kuwa wana wa Mungu. “Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu,
na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu
wamjie,” Mdo 2: 39. Tendo hili ni
upendeleo mkubwa sana kwetu, na upendo wa Mungu wa ajabu. Je, watambua jambo
hilo? Je, wayajua mapungufu yako? Na je! waona umuhimu wa kupatanishwa na Mungu
Baba kupitia ushindi wa Mwanae dhidi ya uovu na dhambi?
Njia
na namna yetu ya kuishi baada ya Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo inatusukuma
kuishi upya katika kutenda na kunena. Ni maisha ya ushuhuda wa kweli. Kwa maana
hii, Mtume Petro anasema, “Jiokoeni na kizazi hiki chenye ukaidi,” Mdo 2:40.
Leo tunaisha katika kizazi chenye ukaidi uliokithiri. Leo walio wengi siyo
kwamba tu hawaamini, ila pia hawaoni umaana wa maisha yenye uhusiano na Mungu.
Wengi wamefikia hatua ya kuona historia nzima ya wokovu wetu kama hadithi za
kufikirika tu. Tupo kwenye wakati wa “ponda mali kifo chaja.” Kwa mtu yeyote na
hasa kiongozi akikosa hofu ya Mungu ndani yake, maisha na utu wa binadamu hauna
tofauti na bidhaa rahisi na isiyodumu kuwahi kutokea. Leo tunashuhudia mauaji
ya wazi na kikatili kuwahi kutokea, na hata watu kupotea.
Wapendwa
katika Kristo, tunamwitaji Kristo ambaye ndiye Mlango wa kwenda mbinguni.
Kristo akiwa nafsi ya pili ya Mungu, katika utendaji ndiye aliye mwokozi kwa
kile kilichoanguka. Nafsi hii inapokuwa katika utendaji haimaanishi kwamba kwa
wakati huo nafsi nyingine hazifanyi kazi, yaani Mungu Baba na Roho Mtakatifu.
Ni vile vile Roho Mtakatifu katika utendaji, uvitakatifuza vyote
vilivyokombolewa na Kristo, na kwa namna hiyo hiyo nafsi nyingine, yaani Mungu
Baba, na Mungu Mwana hufanya kazi pamoja. Na ndiyo maana Yesu anasema maneno
haya, “Amin, amin, nawaambieni, Yeye asiyeingia mlangoni
katika zizi la kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni
mnyang'anyi. Aingiaye mlangoni ni
mchungaji wa kondoo,” Yoh 10:1-2.
Kristo ndiye Mchungaji
wa kondoo na pia ndiye Mlango wenyewe. Kristo ndiye Mlango halisi wa kwenda
Mbinguni. “Basi Yesu aliwaambia tena, Amin,
amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo, Yoh 10:7. Anayempinga Kristo na
kutokufuata maagizo yake, ni kwa namna hiyo hiyo anajifungia mlango mwenyewe wa
kutokuiona Mbingu. Yesu anasema, “Mimi
ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata
malisho,”Yoh 10:9. Kukua kwetu kiroho kunategemea uhusiano wetu na Kristo, na
namno tunavyolishwa na neno lake. Ndugu yangu, malisho yako yako kwa nani?
Ingawa ni kweli kwamba
tumestahilishwa wokovu na uzima huo wa milele bila mastahili yetu, mimi na wewe
yatupasa kuishi upendo ule aliotufundisha Bwana wetu Yesu Kristo. Hivyo,
yatupasa “kustahimili, mtendapo mema na kupata mateso, huu ndio wema hasa mbele
za Mungu,” 1Pet 2:20b. Utendaji huu wa wema wapaswa kuendana na utimizaji wa
nyajibu tulizopewa na umma kwa uaminifu bila kubaguana kwa namna yoyote ile, “kwa
sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia
kielelezo, mfuate nyayo zake,” 1Pet 2:21. Kristo Yesu ndiye kielelezo chetu na
hitimisho ya yale yote tuyafanyayo leo na sasa. Kwa Kristo ipo njia, kweli, na
uzima, Yoh 14:6.
Kristo Yesu ndiye
kielezo na hitimisho la maisha yetu kama ifuatavyo: Moja, Yesu aliishi hali
yetu ya kibinadamu ikiwa ni pamoja na mahangaiko yetu ila “Yeye hakutenda
dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake,” 1Pet 2:22. Kwa mantiki hii,
Kristo Yesu ni mwalimu na kiongozi wa kufuata katika maisha mwili na roho.
Pili, licha ya kuishi hali yetu ya kibinadamu, hakusukumwa na hisia mbaya
katika kuona, kufikiri, kuamua, na kutenda. Kwa maana hiyo, “Yeye alipotukanwa,
hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye
ahukumuye kwa haki,” 1Pet 2:23. Kristo Yesu aliishinda hali ile ya kibinadamu
na kudhihirisha Umungu wake.
Tatu, Kristo kama
kielelezo na hitimisho la maisha yetu kwake Kristo wokovu na uponyaji upo na
unawezekana. Hivyo Kristo “…mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake
juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa
kupigwa kwake mliponywa,” 1Pet 2:24. Nne, ndani na katika Kristo tu salama kwa
sababu tunaye Mchungaji mwema. “Kwa maana mlikuwa mnapotea kama kondoo; lakini
sasa mmemrudia Mchungaji na Mwangalizi wa roho zenu,” 1Pet 2:25. Tendo hili, na
kweli hii, ni mwaliko kwetu wa kujisalimisha kwa Kristo bila kujibakiza.
Wapendwa katika Kristo
kama ilivyo kwa kila mmoja wetu yawezekana kuwa kajisalimisha kwa Kristo au
kitu fulani, Janeth Msomi alijisalimisha katika majivuno yake. Hivyo hakuhitaji
chochote kwa yeyote isipokuwa ufahamu wake.
Ikiwa ndiyo kwanza
tumeanza msimu wa mvua, yaani, masika, Janeth akiwa na gari yake aina ya “Prado
Land Cruizer” akielekea vijijini kwao, mvua zilikuwa zinanyesha bila kukatika.
Baada ya mwendo wa masaa mawili, Janeth alifika karibu na mto mkubwa na pale
daraja lilikuwa limevunjika na kuchukuliwa na maji.
Pembezoni mwa mto ule
walionekana wazee wawili wenye mitumbwi yao wakiwa wanaifanyia usafi. Hata
hivyo, baada ya kuona gari ile Prado, Mzee mmoja aliondoka na kutaka kujua kama
mwenye gari anahitaji masaada. Mzee yule aligonga dirisha la mlango, na Janeth
alishusha kioo. “Mwanangu pole kwa safari. Kwa bahati mbaya leo hutaweza kuvuka
mto huu kwa gari lako kwa sababu daraja limezombwa na mafuriko. Jambo la
kufanya ni hili; ‘waweza kuliacha gari lako nasi tukakuvusha kwa mtumbwi wetu.
Gari lako tunalilinda hadi utakaporudi huko uendapo,” Mzee yule alitoa ushauri
huo kwa upole.
“Ningehitaji ushauri
wako Mzee ningewafuata na kuwauliza. Hivyo, usiniambie kitu chochote kabla ya
kukuuliza,” Janeth alimjibu Mzee yule kwa jeuri huku akipandisha kio cha gari
lake nusura ya kuvibana vidole vya Mzee yule. Mzee yule aliondoka kwa upole na
kurudi kwenye mtumbwi wake.
Watu wengi walifika na magari yao. Waliyaacha
magari hayo, na kupakia mitumbwi na kuvushwa ng’ambo ya mto.
Ndugu yangu,
kuikamilisha safari yako ya maisha licha ya kufanikiwa kwa mambo mengi kwa
nyakati tofauti wahitaji mtumbwi. Mtumbwi huu wawezekana kuwa jirani yako, au
yeyote yule utakayekutana naye katika safari ya maisha yako. Ni vyema
kuusikiliza ushauri wao na kuepuka kuwahukumu kadiri ya mwono wao. Kristo Yesu kwetu
ni zaidi ya mtumbwi.
“Yeye
hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake,” 1Pet 2:22
Tusali:-Ee Yesu na Mchungaji wetu mwema, kwako twajisalimisha. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario