jueves, 1 de junio de 2017

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 7 YA PASAKA


IJUMAA WIKI YA 7 YA PASAKA

Somo: Mdo 25:13-21

Zab: 103:1-2, 11-12, 19-20ab

Injili: Yoh 21:15-19

Nukuu:

Na wale waliomshitaki waliposimama hawakuleta neno lo lote baya, kama nilivyodhani, bali walikuwa na maswali mengine mengine juu yake katika dini yao wenyewe, na katika habari ya mtu mmoja Yesu, aliyekuwa amekwisha kufa, ambaye Paulo alikaza kusema kwamba yu hai,” Mdo 25:18-19

Nami nikaona shaka jinsi ya kutafuta hakika ya habari hii, nikamwuliza kama anataka kwenda Yerusalemu ahukumiwe huko katika mambo haya,” Mdo 25:20

Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu,” Yoh 21:17

Akasema, Amin, amin, nakuambia, Wakati ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga mwenyewe na kwenda utakako; lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka,” Yoh 21:18

TAFAKARI: “Lisha, Chunga, Lisha Kondoo Wangu.”

Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na Mtume Petro kumkana Yesu mara tatu, leo Petro anatambua kosa lake, analikiri kosa lake, na yupo tayari kufuata maagizo na mfano wa Kristo kama mchungaji mwema. Petro anaulizwa swali mara matatu, kama kumkumbusha alivyomkana Kristo na Bwana wake mara tatu. Mtume Petro kuulizwa kwa swali hili mara ya kwanza kunabeba msingi wa muulizo wa mara nyingine mbili zilizobaki. Yesu anamuuliza Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Neno “hawa” limebeba ujumbe mzito sana katika maisha ya kiroho.

Kumpenda Kristo kuliko “hawa” kwa maanisha kumpenda Yesu Kristo kuliko vitu vingine vyote. Kumpenda Kristo kusiko fananishwa na yale tuyaonayo na hata kuyagusa. Ni kumfanya Kristo kuwa ndiyo njia ya kweli, uzima wa kweli, na ukweli usiotia shaka katika maisha yetu ya kila siku. Ni kutokuwa na mashaka kabisa tunapokuwa katika mikono yake. Ni kumfanya Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wako. Swali hili aliloulizwa Petro, nasi tunaulizwa kila siku tunapoenenda katika njia yake.

Wapendwa wana wa Mungu, jibu la Petro lilikuwa, “ndiyo Bwana, wewe wajua nakupenda.” Maneno haya ayasemayo Mtume Petro yanamsingi wake kiimani. Mtume Petro hayatamki tu kwa kumpendezesha Kristo, licha kwamba alimkana kuwa hamjui. Wakati Yesu anafundisha kuhusu fumbo la mwili na damu yake kuwa ni chakula cha uzima, wengi wa wanafunzi wake walimwacha kwa sababu fundisho lile lilikuwa gumu. Mafundisho haya yalikuwa mzito sana. Hivyo Yesu aliwauliza wale Thenashara, “Je! Ninyi nanyi mwataka kuondoka?” Yoh 6:67. Mitume wote walikuwa kimya kama wamepigwa ganzi vile. Ni Mtume Petro tu kwa ujasiri wake aliweza kumjibu Kristo, tena kwa kile kilichokuwa kimeujaza moyo wake na kusema, “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu,” Yoh 6:68-69. Huu ndiyo msingi wa jibu la Petro kwamba, “Ndiyo Bwana, wewe wajua nakupenda.”

Hata hivyo baada ya kujibu kuwa anampenda Kristo, Mtume Petro anapewa majukumu ya jibu lile alilolitoa. Mtume Petro anawajibishwa kutumika kama alivyomkiri Kristo na kusema, “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai,” Mt 16:16. Maagizo ya Kristo kwa Petro ni kulisha kondoo zake, kuwalinda, na kuwalisha. Kazi hapa ni kulisha, kulinda, na kulisha. Hii ndiyo maana ya Jina lake ‘Petro,’ “Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda. Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni,” Mt 16:18-19. Mtume Petro anarudishiwa mamlaka yake aliyopewa na Kristo.

Wapendwa wana wa Mungu, tendo hili la Kristo analolionyesha kwa Mtume Petro, ni tendo la upendo wa hali ya juu, na hata sisi hasa pale tunapojenga uhusiano naye tena baada ya kumwasi. Yesu yupo tayari kutupokea kama tulivyo ili mradi tujirudi na kufanya toba ya kweli. Kristo hakuvunja ahadi yake aliyokwisho isema juu ya Petro licha ya udhaifu aliyouonyesha siku ile ya kukamatwa Yesu Kristo. Tendo hili linatukumbusha pia simulizi lile la mwana mpotevu. Upendo huu wa kibaba ndiyo upendo wa Mungu kwetu. Mungu anasema na mtu mwovu, “Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu,” Isa 1:18. Hii ndiyo huruma ya Mungu kwetu. Mtume Petro anarudishiwa mamlaka yake na kupewa kazi ya kulisha, kulinda, na kulisha daima kondo wake Kristo.

Wajibu huu aliopewa Petro, nasi tumepewa kwa njia ya ubatizo wetu na kushiriki ukuhani wa Kristo ulio wa kawaida. Hivyo twawajibika kufanya kazi hii ya kulisha kondoo zake, hasa kwa matendo yetu mema pale tulipo. Tuwe mfano kwa matendo yetu na kuwa barua za kusomwa na wegine. “Ninyi ndinyi barua yetu, iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote; mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama,” 2Kor 3:2-3. Kuishi katika ukweli huu, kutatugharibu maisha yetu kama mshumaa uwakavyo nakutoa mwanga ndivyo hivyo unavyokufa. Kwa wajibu huu wa kuwa barua za kusomwa na wengine kwa matendo yetu mema, Yesu anamwambia Petro, “Amin, amin, nakuambia, Wakati ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga mwenyewe na kwenda utakako; lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka,” Yoh 21:18. Mtiririko wa ukweli huu ndiyo unaomkuta Mtume Paulo anavyohukumiwa na kwenda kifungoni huko Roma. Mwisho wa siku Mtume Petro, na Paulo waliyatoa maisha yao na kufa kifo dini kumshuhudia Kristo. Ndugu yangu, palipo Msalaba wa Kristo ndipo ulipo Utukufu wake. Hii ndiyo njia yetu sote kama wafuasi wake kila mmoja kadiri ya wito wake.

Tumsifu Yesu Kristo

“Lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka,” Yoh 21:18b

Tusali:-Yesu Mwema, tufanye barua iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye hai. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario