martes, 13 de junio de 2017

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 10 YA MWAKA-I


jumanne wiki ya 10 ya mwaka-I

Somo: 2Kor 1:18-22

Zab: 119:129, 130, 131, 132, 133, 135

Injili: Mt 5:13-16

Nukuu:

Maana ahadi zote za Mungu zilizopo katika yeye ni Ndiyo; tena kwa hiyo katika yeye ni Amin; Mungu apate kutukuzwa kwa sisi,” 2Kor 1:20

Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 5:16

TAFAKARI: “Ninyi ni chumvu ya dunia, na nuru ya ulimwengu: matendo yenu yamtukuze Baba yenu aliye Mbinguni.”

Wapendwa wana wa Mungu, swala ya imani halina mbadala, yaani kubadilika badilika kama kinyonga. Kwa maana nyingine ni heri kuwa moto au baridi kuliko kuwa viguvugu. Hatumwendei Mungu kwa hali ya kusitasita. Hivyo kujitoa kwa Mungu asilimia tisini na tano haitoshi na hiyo siyo imani ya kweli. Hatumwendei Mungu katika hali ya mashaka huku tukitamka kwa vinywa vyetu “Mungu ni mweza wa vyote.” Basi niwaombe nyote tusafiri pamoja katika neno hili; “Ninyi ni chumvu ya dunia, na nuru ya ulimwengu: matendo yenu yamtukuze Baba yenu aliye Mbinguni.” Ndugu yangu waamini jambo hili?

Mtume Paulo anaelezea Imani ya kweli ni kusimama katika NDIYO itokayo ndani yako. Bila shaka wote tunamfahamu vizuri “chura.” Nina swala moja kwako, Je, unapomtazama chura kasimama au kachuchumaa? Usicheke! Fanya utafiti unipe jibu. Kwa upande wangu hadi leo sielewi pozi la chura ni “mwamko/kusimama” au “mchuchumao/kuchuchumaa.” Hatupaswi kupata ugumu wa kimtazamo na kiimani kama tuupatao kwenye pozi la chura. Hivyo imani yetu yapaswa kuwa NDIYO ya herufi kubwa. “Maana ahadi zote za Mungu zilizopo katika yeye ni Ndiyo; tena kwa hiyo katika yeye ni Amin; Mungu apate kutukuzwa kwa sisi,” 2Kor 1:20. Kama tunataka Mungu atukuzwe kupitia sisi, twapaswa kusimama imara na kuamini kile tunachokisimamia.

Kati yetu tupo ambao ni mabingwa wa kuhama Kanisa moja na kwenda lingine kama walivyo wachezaji wa mpira maarufu ulimwenguni. Tunapoishi Imani yetu hatuna lengo la kumfurahisha mtu fulani au watu fulani. Lengo ni kumtukuza Mungu, na tendo hilo libakie kuwa shuhuda kwa wengine. Mshangao huu na ushuhuda huu ndiyo unaotuelekeza kumtangaza mtu kuwa kwenye heri au Mtakatifu. Ukilenga kumpendezesha mtu, au kundi la watu, utaambulia huzuni na masikitiko kwa sababu yale yote yatupayo furaha ya leo na sasa hayana umilele. Ipo siku yatachuja au kupitwa na wakati.

John Masifa alikuwa mchezaji mzuri sana wa mpira wa mikono. Kwa kupitia kwake, timu yake ya chuo ilipata vikombe vingi sana, na hivyo kulipamba jengo lile la utawala la Chuo kwa tunzo hizo. Hivyo John Masifa aliweka nia ya dhati kabisa mara baada ya kumaliza masomo yake angependa kurudi chuoni pale awe mkufunzi.

Kwa vile Mungu si Edgar, yote yaliwezekana na akarudi Chuoni pale baada ya miaka mitano kama Mkufunzi na mkuu wa chuo. Lakini jambo la kusikitisha hakuviona vile vikombe katika jengo lile la utawala. Hivyo alianza kuvitafuta.

Siku mmoja akiwa anatafuta kipande cha mbao katika moja ya stoo za zamani aliona pipa kumbwa lililosheheni kila aina ya uchafu pembezoni kwa ukuta. Pipa hili lilimvutia, na hivyo alikwenda na kuona kilichoko ndani yake. “Ha! Kumbe vikombe vyote na zile picha zangu vimetupwa huku?” John Masifa alisema kwa masikitiko.

Ndugu yangu, kwa uhakika Imani yetu msingi wake haujengwi kwa yale tu yatufurahishayo moyo kwa wakati fulani katika maisha. Mambo hayo hayana umilele kwa yenyewe. Mwanafalsafa Plato anatusaidia katika jambo hili. Plato anasema yote haya tunayoyaona na hata kuyafanya ni kivuli tu cha uhalisia wa kitu kile kilichopo katika ulimwengu wa mafaa-“good.” Je, kwa nini sana unapoteza muda wako wote na kuweka roho yako kwenye uvuli wa vitu?

Wapendwa wana wa Mungu, Yesu anatupa mpango mzima wa thamani yetu mbele ya Mungu. Sisi tu chumvi ya dunia, na nuru ya ulimwengu. Je, nini maana ya maneno haya? Bila shaka tu chumvi ya ulimwengu kimtindo wa maisha, namna ya kuishi na wenzetu katika jamii. Yatupasa kuchanganyika na watu kwa matendo yetu mema ili tuwe kikolezo kama ilivyo kazi ya chumvi. Pamoja na matumizi mengi ya chumvi, chumvu hutumika kuhifadhi vyakula visiharibike, kukoleza na kuleta ladha ya chakula, na chumvi pia utumika kuyeyusha barafu. Basi kuchanganyika huku katika jamii kwa matendo yetu mema mfano wa chumvi, yaani kuhifadhi tunu njema za jamii/maadili na kuruhusu uwepo wa Mungu kama hofu yetu. Kama chumvu, tuwe kikolezo cha upendo pasipo na upendo, furaha pasipo na furana, haki pasipo na haki, na uwajibikaji palipo na uzembe. Mwisho kama chumvi, yatupasa kuyeyusha barafu ya chuki na visasi katika jamii, kuyeyusha maovu wanayofanyiwa wazee, walemavu wa ngozi na wanyonge wasio na watetezi.

Wapendwa tusisahau sisi pia ni nuru ya ulimwengu. Kana nuru maisha yetu ya lenge katika maadili mema. Tutambulike mbele ya jamii tunayoishi kwa maadili mema na kupitia kwetu kama barua zinazosomwa, tuwe kielelezo cha wengine kuona nuru hiyo, kuifuata, na kubadilika. “Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 5:16. Taifa letu leo linaangamia kwa mmomonyoko wa maadili. Kumbe haitoshi tu kusema, bali mabadiliko haya yaanzie kwangu mwenyewe.

Tanzania yetu ya leo inanitia hofu kubwa sana. Ni jana tu mtu kashitakiwa na kuhukumiwa kwa kosa la wizi wa mali ya umma kwa uthibitisho wa kutosha. Mtu huyo huyo jana usiku kasafishwa kosa lake na wezi wenzake waliovalia ngozi ya kondoo, na leo asubuhi mtu huyo anaomba ridhaa yetu tumkabidi mali ile aliyotuibia jana. Tunashawishika kwa ubwabwa wa maharage na soda ya Pepsi na kuuza uhuru wetu na watoto wetu. Hakika Tanzania kama ni mwili basi saratani imeshakuwa “cronic.” Tuyafungue macho na mioyo yetu kuuona ukweli huu.

Wapendwa katika Kristo, si lengo langu kuongelea siasa kisiasa, bali ninaongelea siasa kama sehemu muhimu ya maisha kijamii ambapo mimi na wewe tunaoufanya mwili wa Kristo, yaani Kanisa ni sehemu ya jamii hiyo. Ni kosa kubwa kwa Mkristo kusema siasa haimuhusu. Au tusichanganye siasa na dini. Kwa kukana ukweli huu ni kutenda siasa. Leo katika Kanisa moja ya mambo muhimu katika masomo ya “fundamental Theology,” ni kuhusu “Political Theology.” Huwezi kumtenganisha binadamu na jamii yake anayoishi. Kufanya hivyo ni kuishi katika ndoto za kugushi mchana kweupeeee! Embu tujikumbushe ile sala ya Bwana wetu Yesu Kristo, “Wala mimi simo tena ulimwenguni, lakini hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako. Baba mtakatifu, kwa jina lako ulilonipa uwalinde hawa, ili wawe na umoja kama sisi tulivyo. Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli,” Yoh 17:11, 15-17. Je, sala hii ya Yesu inasema nini juu ya maisha yako kijamii?

Ndugu yangu, bado tupo ulimwenguni, na inatupasa kuufanya ulimwengu huu kuwa sehemu salama ya kuishi kila mmoja wetu bila kujali itikadi za vyama na wafuasi wake. Kama Watanzania jukumu la kuilinda amani si kwa kundi fulani la watu waliojihesabia haki ya kuongoza milele, bali ni jukumu la kila mmoja wetu. Mambo yatakapo haribika hakuna atakayekutambua wewe kwa dhehebu lako. Kuilinda Amani ni kufanya tendo la siasa kwa sababu linagusa jamii na sisi wote si visiwa wala milima, bali ni sehemu ya jamii hiyo.

Tusifu Yesu Kristo!

Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 5:16

Tusali: Ee Yesu uliye njia, kweli na uzima, tufanye chumvi ya dunia na nuru ya ulimwengu. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario