ALHAMISI WIKI YA 10 YA MWAKA-I
Somo:
2 Kor 3:15-4:1, 3-6
Zab:
85:8ab-9, 10-11, 12-13
Injili:
Mt 5:20-26
Nukuu:
“Basi ndiye Roho; walakini alipo Roho wa Bwana,
hapo ndipo penye uhuru,” 2Kor 3:17
“Kwa maana hatujihubiri
wenyewe, bali Kristo Yesu ya kuwa ni Bwana; na sisi wenyewe kuwa tu watumishi
wenu kwa ajili ya Yesu,” 2Kor 4:5
“Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo
haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni,”
Mt 5:20
“Basi
ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno
juu yako, iache
sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha
urudi uitoe sadaka yako,” Mt 5:23
“Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye
njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa
askari, ukatupwa gerezani,” Mt 5:25
TAFAKARI:
“Patana na ndugu yako uwapo pamoja naye njiani.”
Wapendwa wana wa Mungu,
ni jambo la kawaida kuona ndugu wanagombana na mwisho wa siku wanaweka kando
tofauti zao na kuwa kitu kimoja. Hapa sina maana ya kuchochea ugomvi nikijua
kunakupatana, la hasha! Ninachosema ni kwamba ikitokea ndugu mmepishana kauli
si jambo jema mkaendelea kuzibeba tofauti zenu. Ukweli ni kwamba hata kama
umekosewa katika tofauti zenu, hakuna mshindi katika ugomvi huo kila mmoja
akibaki na tofauti zake. Ushindi wa kweli na wa roho ni kuchukua hatua na
kutafuta upatanisho hata kama wewe ndiwe uliyekosewa haki.
Ndugu yangu
tunayesafiri wote katika tafakari hii, usikubali hata mara moja kumbeba yeyote
katika moyo wako hasa kwa sintofahamu zilizotokana na ugomvi wenu. Kwa kukubali
kuishi kwa mtindo huo ni sawa na kuuza uhuru wako na kujifungia katika chumba
kidogo sana na kushindwa kutoka ilihali funguo za chumba hicho unazo mwenyewe.
Usijitengenezee gereza lako mwenyewe pasipo sababu. Roho wa Mungu uliyepewa
bure na kufanya makazi ndani yako unamtesa na hapo hapo unakosa neema. Toka
kwenye kifungo hicho na uwe huru, na hapo Roho wa Bwana atakuwa nawe na
kukupatia wingi wa neema zake. Ndugu yangu, “alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo
penye uhuru,” 2Kor 3:17.
Wapo wengi kati yetu huwa
wanajisifu kwa kutoshiriki sakramenti kwa kumkomesha ndugu yake au jirani yake
aliyemkosea. Utamsikia anasema kwa kujivuna, “nina mwaka mmoja na nuru si pokei
Ekaristi Takatifu kwa kumkomesha kwa sababu sina muda wa kupoteza kwa kuongea
naye.” Je, jambo hilo kwako ni habari njema? Ndugu yangu, huko ndiko
kujihubiria mwenyewe habari za kuzimu. Kwa nini unajijengea jehenamu yako
mwenyewe, tena kwa kupenda? Mtume Paulo anasema, “Kwa maana hatujihubiri
wenyewe, bali Kristo Yesu ya kuwa ni Bwana; na sisi wenyewe kuwa tu watumishi
wenu kwa ajili ya Yesu,” 2Kor 4:5. Yafanye maisha yako kuwa habari njema ya
wokovu kila mahali uendapo na kuishi na watu. Yafanye maisha yako kuwa barua ya
kusomwa na watu ili kwa kupitia kwako wamwone Kristo. “Ninyi ndinyi barua yetu,
iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote; mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya
Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye
hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama,”
2Kor 3:2-3.
Ndugu yangu, wapo wengi
pia kati yetu ni mabingwa sana wa sura mbili mbili. Nachotaka kusema ni kwamba,
wapo tunaoshiriki nao katika jumuiya ndogondogo, Kanisani, hata maisha yetu
utawani ambao muda wote umebeba zigo kubwa la chuki, visasi, hasira, wivu,
majivuno, na yale yote yanayofanana na haya na yasiyompendeza Mungu. Licha ya
zigo hilo kuulemea Moyo, hatupo tayari kuliweka chini. Kukiwa kwenye sehemu za
Ibadi huwa tunaliacha zigo hili mlangoni, na mara baada ya Ibada zigo hili
tunalikimbilia na kujitwisha na mara kunaondoka nalo. Tupo tayari kulibeba zigo
hili nyakati zote za majira ya mwaka, na ya Vipindi vyote vya Liturjia vya Mama
Kanisa. Leo Yesu anatupa angalizo: “Maana
nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo,
hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni,” Mt 5:20. Mbele za watu na jumuiya
tunazoishi twajionyesha sisi ni wema na hatuna tatizo na mtu, na wakati
mwingine twa tamani hata kwenda mbinguni kwa miguu yetu tukithibitisha
utakatifu wetu machoni pa watu.
Wapendwa
wana wa Mungu, ukitaka sala yako, na maombi yako yapate kibali mbele ya Mungu,
jipatanishe wewe mwenyewe, wewe na uliyekosana naye, na pia wewe na Mungu.
Hivyo “basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu
yako ana neno juu yako, iache
sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha
urudi uitoe sadaka yako,” Mt 5:23. Wengi na hasa wale tuliokosewa hupenda
kuyarefusha mambo sana, na wakati mwingine tungependa tunyunyuziwe ubani kwa
cheteso cha dhahabu ili tuwe tayari kwa kuyaongelea yale yaliyotutatiza.
Jambo
la muhumu kupita yote kama umekosana na ndugu yako au ye yote yule, patana naye
mngali injiani. Maana yake nini? Kupatana na ndugu yako mngali njiani ni
kufanya juu chini kupatana na ndugu yako angali yu hai. Wengi tumeshuhudia watu
hawapendi kupatana na kuishia kuapizana pasipo sababu. Wapo wengine hata baada
ya kuzidiwa wakiwa kitandani karibu ya kufa wanapoomba upatanisho na ndugu yake
kunakuwa na mkwamo bila mwitikio wowote na mwisho mtu huyo hufariki katika hali
ya majonzi makubwa. Hivi unajisikiaje ndugu yako kufa akikuomba upatane naye
nawe kwa kiburi chako hukusikia na hatimaye ndugu yako anafariki? Ndugu yangu, “Patana
na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije
akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani,” Mt
5:25. Je, kwa kutokupatana na ndugu yako angali hai, utajibu nini mbele ya
Kadhi-Mungu mwisho wa siku?
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Maana
nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo,
hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni,” Mt 5:20
Tusali:-Ee
Yesu uliyempatanishi wetu na Mungu Baba, tujalie moyo wa kusemehe na kusamehewa.
Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario