martes, 13 de junio de 2017

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 10 YA MWAKA-I


 
JUMATATU WIKI YA 10 YA MWAKA-I
Somo: 2Kor 1:1-7
Zab: 34:2-3, 4-5, 6-7, 8-9
Injili: Mt 5:1-12
Nukuu:
“Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote ili nasi tupate kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote, kwa faraja hizo, tunazofarijiwa na Mungu,” 2Kor 1:3-4
“Kwa kuwa kama vile mateso ya Kristo yanavyozidi kwetu, vivyo hivyo faraja yetu inazidi kwa njia ya Kristo,” 2Kor 1:5
“Na tumaini letu kwa ajili yenu ni imara, tukijua ya kuwa kama vile mlivyo washiriki wa yale mateso, vivyo hivyo mmekuwa washiriki wa zile faraja,” 2Kor 1:7
Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao,” Mt 5:3
TAFAKARI: “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.
Wapendwa wana wa Mungu, kila kazi au taaluma fulani hapa duniani ina maadili yake ambayo huendana na taaluma ile. Mfano: Kama wewe ni tabibu wa afya ya binadamu jamii inategemea uwe na maadili ya taaluma yako hiyo, na kutokana na uwanja wako huo, jamii inategemea kwa uhakika wote uwe mtetezi wa uhai. Kadhalika nasi kama Wakristo, wafuasi wake Bwana wetu Yesu Kristo, yatupasa pasipo shaka kuyaisha maadili yanayoendana na Imani yetu. Maadili hayo hatakama yangekuwa na uzuri gani, na faida gani katika kuyaishi, yanaupande wake wa pili, yaani, mapaswa yake. Kuishi ukweli huo kutakudai sana kujitoa sadaka ili dhima yake ikamilika na kuonekana.
Sehemu hii ya pili, yaani, sadaka itupasayo kuitoa kwa kuyaishi maadili hayo kama wafuasi wa Kristo, ndiyo Mtume Paulo anayoizungumzia katika somo hili la kwanza, mwanzoni mwa waraka wa pili wa Mtume Paulo kwa Wakorintho. Kwa vile Bwana wetu Yesu Kristo aliona inafaa na kumpendeza Baba wa Mbinguni kupitia njia ya mateso ili mimi na wewe tuwe huru kutoka utumwa wa dhambi, ni kwa namna hiyo hiyo tunaalikwa kuyapokea mateso yetu kwa furaha ndani na katika Kristo kwa sababu ni katika Yesu Kristo mateso hayo hupata maana. Kwa mantiki hii, “Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote ili nasi tupate kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote, kwa faraja hizo, tunazofarijiwa na Mungu,” 2Kor 1:3-4. Hivyo ndani na katika Kristo mateso hutufariji na kuwa sababu ya furaha yetu.
Mtazamo huu wa Kiimani tunapoyakabili mateso yetu, hautushawishi kufikia hitimisho la mateso hayo kwa nguvu zetu wenyewe. Ni ukweli usiopingika kwamba kwa mabaji yake saba aliyotukirimia na anayozidi kutukirimia Roho Mtakatifu yanatusaidia kuyakabili yale yatuzungukayo. Hata hivyo hatuwezi kukwepa ukweli huu kwamba yote huwa hivyo na kufanyika hivyo kwa huruama na matakwa yake Mungu kwetu. Hapa ndipo twaweza kuona maana ya mateso na kile kinachotokana na mateso yetu ndani na katika Kristo-UTAKATIFU. Hivyo tumaini letu katika mateso ni hili: “Kwa kuwa kama vile mateso ya Kristo yanavyozidi kwetu, vivyo hivyo faraja yetu inazidi kwa njia ya Kristo,” 2Kor 1:5. Kwa mantiki hii ni kosa kubwa la kiimani kukata tamaa kama tunamwamini Kristo.
Wapendwa wana wa Mungu, kama wewe ni mdau wa mateso ndani na katika Kristo, yakupasa kuwa FARAJA kwa wale wote wenye mateso, na hasa yale yasiyo na majibu ya moja kwa moja na ya kueleweka. Wewe uijuaye siri hii ya teso lenye uhusiano wake na teso la Kristo, ndiye unayechukua nafasi ya Kristo katika tendo hili la kuwafariji wengine wenye mateso. Hivyo, “Na tumaini letu kwa ajili yenu ni imara, tukijua ya kuwa kama vile mlivyo washiriki wa yale mateso, vivyo hivyo mmekuwa washiriki wa zile faraja,” 2Kor 1:7. Ninaamini pasipo shaka kwamba mateso yetu ndani na katika Kristo yanasababu yake katika wokovu wako/wangu.
Injili yetu ya leo inatuelezea sehemu ya kwanza ya sababu ya kile tulicho na tupasacho kukiishi. Hiki siyo kitu kingine bali ni maadali ya kile tunachopaswa kukiishi kama wafuasi wake Kristo. Maadili haya kwa maneno mengine ni zile HERI ZA MUNGU. Tuelewe kwamba tumeumbwa ili tumjue, tumpende, tumtumikie na mwisho turudi kwake mbinguni. Kuyafanya haya kwa ukamilifu wake kunatutaka kuyaishi maadili hayo, yaani hizi heri za Mungu kwa uaminifu.
Wapendwa katika Kristo, heri hii ya kwanza, yaani, “HERI WALIO MASIKINI WA ROHO,” “MAANA UFALME WA MBINGUNI NI WAO,” ndio msingi wa heri nyingine zote. Pasipo kuwa na umaskini wa roho, yaani kuwa na nafasi ya kutosha ya Mungu ndani yako, huwezi kuziishi kikamilifu heri nyinge zote. Uhusiano wetu na Mungu ni sehemu muhimu sana kuona sababu ya kuyafanya hayo yote kuelekea katika hitimisho letu, yaani, uzima wa milele. Hivyo umasikini huu wa kiroho hutufanya tuone sababu ya haya yafuatayo; kujua ukweli huo, kufanya jambo hilo, na kuona thamani ya kile tukifanyacho hata kama matokeo yake hatutayaona katika uhasilia wake kwa muda mfupi tunaoishi hapa duniani. Masikini wa roho ni Mkristo yule mwenye hofu ya Mungu, na wale ambao kwa dhamiri zao njema huongozwa na hofu hii ya Mungu ndani yao na kutenda kadiri ya mwono wa kimungu hata kama hawamjui Kristo au Mungu tunayemwanini na kumwabudu.
Hivyo ni yule mwenye umasikini wa roho katika maana niliyoizungumzia hapo juu atakaye ona huzuni za wengine kwa sababu hali hiyo imo ndani mwake, na hivyo ufarijika na kufarijiwa kwa kutenda tendo hilo la huzuni. Upole wa mtu nje ya hali ya kuzaliwa nayo, ni tabia ile aijengayo mtu, na kumwona mwingine zaidi ya mahitaji yake mwenyewe. Ni hali ya kujali zaidi wengine, kuliko kujionea huruma mwenyewe kuliko pitiliza. Msingi huu ni ule ule wa umasikini wa roho. Kuirithi nchi wa wale wapole ni kuwa wahenga. Mtu huwa mhenga kwa sababu ameacha kitu cha kujifunza au kuigwa na wengine. Kinyume cha kuwa Mhenga ni kuwa Lihoko-roho isiyo salama/bad spirit.
Mpendwa ukiwa maskini wa Roho utawajali wenye njaa, na kutenda haki kwa kila mmoja. Ni kwa kufanya tendo hili bila kujibakiza nasi tutakidhiwa mahitaji yetu na Mungu kwa kipimo hicho hicho. Hivyo, “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa,” Lk 6:38. Huku ndiko kushibishwa na Mungu kuliko kwa haki.
Mwenye hofu ya Mungu ndani mwake ambao msingi wake umetokana na umasikini wake wa roho, hujazwa rehema (nguvu ya pekee katika kutenda) kwa sababu ndani mwake kuna nafasi ya Mungu, malipo yake ni neema juu ya neema. Hivyo neema hufuata palipo na neema. “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Tazama Kristo anavyokupenda!
Usafi wa moyo ni hali ile yakutokuyabeba yasiyoendana na hali na tabia ya Mungu. Makazi ya Mungu na hasa Roho Mtakatifu ni kwenye mahekalu-miili iye isiyo kuwa na hatia yo yote. Uwepo wa Mungu ndani ya mahekalu haya ni fursa ya kumwona Mungu. Roho huyu Mtakatifu hawezi kupata makazi yake kwenye mahekalu yasiyo na nafasi. Hivyo ni wale tu walio masikini wa roho wenye nafasi ya Mungu ndani ya mioyo yao, na hivyo watamwona Mungu. Mioyo safi ni hakikisho la kumwona Mungu muda wote kwani mtu huyu kesha jianda kwa lolote.
Ni katika umasikini wetu wa roho twaona na kujali wengine wawe na utulivu wa ndani kama tulio nao sisi. Wito huu unatusukuma pasipo hiyana kuwa wapatanishi pale amani ile inapokosekana. Kristo akiwa ndiye mpatanishi wetu kwa Baba yake wa Mbinguni, nasi kwa kufanya tendo hilo la upatanishi kwa wengine twahesabiwa haki ya kuwa wana wa Mungu. Ni maskini wa roho pasipo shaka yoyote aishie bila makuu, na ambaye kwa hali hiyo yupo tayari kuifia haki katika kweli. Hawa ndiyo wafia dini wa nyakati zetu ambao wapo tayari kufa kwa ajili ya wanyonge waminywao haki zako na matajiri katika jamii tunayoishi sasa. Ukweli ni kwamba wanapoifia haki hii, ufalme wa mbinguni ni wao. Huku ni kuishi katika hali ya watoto wadogo, wafanyayo yote katika yote bila kujibakiza kwa sababu hawana shaka na baba /mama yao.” Waacheni watoto wadogo waje kwangu, msiwazuie; kwa maana watoto kama hawa ufalme wa Mungu ni wao,” Mk 10:14
Masikini wa roho, mwenye nafasi ya Mungu ndani yake, hawezi ogoba shutuma zitolewazo juu yake kwa ajili ya haki au kutenda haki. Haki na Wema ni baadhi ya sifa na asili ya Mungu. Hapa ndipo kwenye furaha ya kweli tunapoifia haki tukijua mtetezi wetu ndiye chanzo na ukamilifu wa furaha ya kweli ndani yetu. Yesu anatukumbusha jambo hili na kutupa angalizo kwa kusema, “kwa kuwa itamfaidi mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake?” Mk 8:36.
Wapendwa wana wa Mungu, jambo la kushangaza badala ya kuishi maadili haya ya Ukristo wetu, yaani,  heri hizi za Mungu, tumekuwa tunaishi kwa nyakati zote na mitindo tofauti tofauti ya  HERI NANE ZA SHETANI kama ifuatavyo;
1.     Heri yao waliochoka sana, waliobanwa na shughuli na kukosa muda wa kukutana na wakristo wenzao Jumapili, na shughuli za Jumuiya kila wiki. Kwa maana hao ni wafuasi wangu waaminifu.
2.     Heri yao wanaofurahia kutambua tabia, udhaifu wa makleri na mapungufu ya watumishi wa Mungu. Kwa maana hao ndio vitendea kazi vyangu.
3.     Heri yao Walei na Watawa na Makleri wanaosubiri kuambiwa kufanya kitu na kutegemea kupongezwa hata kama hawakufanya kitu. Hakika hao naweza kuwatumia vyema.
4.     Heri wanaoguswa na kukwazika kwa vitu vidogovidogo na kuacha Ukristo wao; kwa kutokwenda Kanisani, kutoshiriki masakramenti na kuacha kusali. Kwa maana hao ni wamisionari wangu.
5.     Heri yao hao wanaojitangaza au kudai kuwa wanampenda Mungu na wakati mwingine wanawachukia jirani zao na ndugu zao. Hakika  hao ni mali yangu  Milele.
6.     Heri yao watenganishi na waletao fujo na chuki. Wataitwa wana wangu.
7.     Heri yao wasiokuwa na muda wa kusali kabisa, na kuzisadifikisha kazi na majukumu yako kuwa ndiyo sala. Maana hao wananiombea mimi.
8.     Heri yako wewe unayesoma haya na wewe unayeyasikia haya na kufikiri ni kwa ajili ya watu wengine na siyo wewe mwenyewe. Hakika  nimeshakupata tayari.
Tumsifu Yesu Kristo!
Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao,” Mt 5:3
Tusali:-Ee Yesu uliye yashinda mateso, nijalie furaha na shangilio katika mateso ndani na katika Wewe; kwa kuwa kwako thawabu kubwa ipo mbinguni. Amina
 
 

No hay comentarios:

Publicar un comentario