martes, 13 de junio de 2017

TAFAKARI: SHEREHE YA UTATU MTAKATIFU


SHEREHE YA UTATU MTAKATIFU MWAKA-A

Somo I: Kut 34:4b-6, 8-9

Dan: 3:52, 53, 54, 55, 56 (52b)

Somo II: 2 Cor 13:11-14

Injili: Yoh 3:16-18

Nukuu:

“Bwana akapita mbele yake, akatangaza, Bwana, Bwana, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli,” Kut 34:6

“Akasema, Ikiwa sasa nimepata neema mbele zako, Bwana, nakuomba, Bwana, uende kati yetu, maana ni watu wenye shingo ngumu; ukasamehe uovu wetu na dhambi yetu, ukatutwae tuwe urithi wako,” Kut 34:9

“Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele,” Yoh 3:16

“Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu,” Yoh 3:18

“Hatimaye, ndugu, kwaherini; mtimilike, mfarijike, nieni mamoja, mkae katika amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi,” 2Kor 13:11

“Neema ya Bwana Yesu Kristo, na pendo la Mungu, na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote,” 2Kor 13:14

TAFAKARI: Tu ndani ya Neema ya Bwana Yesu Kristo, pendo la Mungu, na ushirika wa Roho Mtakatifu.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha sherehe ya Utatu Mtakatifu, ambao ni Mungu mmoja, nafsi tatu; Nafsi tatu Mungu mmoja. Ni Utatu Mtakatifu na Umoja usiogawanyika. Nazo ni Mungu Baba (Muumbaji), Mungu Mwana (Mkombozi), na Upendo wa Mungu Baba na Mwana, yaani, Roho Mtakatifu. Nafsi hizi tatu zinaonekana katika utendaji licha ya kwamba katika utendaji huo wa nafsi moja hautenganishi utendaji wa nafsi nyingine mbili. Kwa mantiki hii, alipo Mungu Baba yupo pia Mungu mwana na Roho Mtakatifu. Na ndivyo iliyo kwa Mungu mwana (Mungu Baba na Roho Mtakatifu), Roho Mtakatifu (Mungu Baba na Mungu Mwana) tokeo la upendo wa Mungu Baba na Mwana.

Kwa mtiririko huu katika utendaji ambao unatuwezesha kupata mwanga katika fumbo hili Takatifu, tunaona katika somo letu la kwanza utendaji wa Mungu Baba, yaani, sifa na utukufu wake. Ni “… Bwana, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli,” Kut 34:6. Ukweli huu ujajifunua katika historia nzima ya uumbaji na wokovu wa mwanadamu. Licha ya mwanadamu kukengeuka hapa na pale, Mungu hakuacha kuwa Mungu, yaani, mwingi wa rehema na upendo usio na kipimo. “…maana ni watu wenye shingo ngumu; ukasamehe uovu wetu na dhambi yetu, ukatutwae tuwe urithi wako,” Kut 34:9.

Ni katika safari hii ya wokovu wa mwanadamu twaona utendaji wa nafsi hii ya pili, yaani, Mungu Mwana. Kristo Yesu ndiye mwokozi. Hatuwezi kusimama katika kweli ndani ya Kristo kama hatumwamini Kristo. Na hatuwezi kumwamini Kristo kama tunamuishi Kristo wa Historia. Yesu Kristo katika maisha yetu na ufuasi wetu kwake ni Kristo aliye hai. Ni kristo tunayekutana naye kila siku ya maisha yetu. Ni Kristo tunayekutana naye katika mateso yetu na furaha yetu. Mateso na furaha kwa Mkristo yanamaana tu pale Kristo anapokuwa kielelezo cha mambo yote. Na hii ndiyo sababu ya Mungu kumtoa Mwanaye katika historia nzima ya wokovu wetu. “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele,” Yoh 3:16.

Wapendwa wana wa Mungu, Imani yetu juu ya Mwana wa Mungu ndiyo hukumu yetu. “Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu,” Yoh 3:18. Kuamini huku si kwa yale tu tuyapendayo kuyaona na kuyasikia katika maisha yetu, bali ni kuamini hata yale ambaye yapo juu ya uwezo wetu na mara nyingine hatuyaoni kwa uwezo wetu wa kibinadamu. Ni kuamini pia yote yawezekana kwa njia yake na kwa uwezo wake. Huku ndiko kuliamini jina pekee la Mwana wa Mungu. Jina hili lina mamlaka juu ya umilele wako na mimi. Kuamini huku huendana na kutenda kweli kadiri ya imani juu ya Kristo, Maandiko Matakatifu, Kanisa na Mapokea yake. Huwezi kuamini mtu fulani na kutenda kinyume cha imani iliyojenga juu ya mtu yule. Tunapofanya kinyume na imani ile ni wazi kwamba hatujui tunachoamini. Ni sawa na kuvaa miwani ya giza kuelekea usipokujua ili hali unaitaji mwanga. “Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu,” Yoh 3:21.

Roho Mtakatifu ambaye ndiye upendo wa Mungu Baba na Mwana, utendaji wake ni kuyatakatifuza yote yaliyoumbwa na kukombolewa. Nafsi hii, yaani, Roho huyu Mtakatifu kati ya kazi zake kubwa ni Umoja, mshikamano, na amani. Ndugu, “…nieni mamoja, mkae katika amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.” 2Kor 13:11. Hivyo salama yetu ipo ndani ya fumba zima hili yaani, Utatu Mtakatifu. Hivyo kama asemavyo Mtume Paulo, “Neema ya Bwana Yesu Kristo, na pendo la Mungu, na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote,” 2Kor 13:14. Amina

Tumsifu Yesu Kristo!

“Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu,” Yoh 3:18

Tusali:-Ewe fumbo la ajabu na uzuri wake, tujazwe neema, na upendo ndani yake. Usifiwe Utatu Mtakatifu, na Umoja usiogawanyika.

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario