viernes, 7 de agosto de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 18 YA MWAKA-B

IJUMAA WIKI YA 18 YA MWAKA-B
7/8/2015
Somo: Kumb 4:32-40
Zab: 76:12-16, 21
Injili: Mt 16:24-28

Nukuu:
Basi, zishike sheria zake, na amri zake, ninazokuamuru leo, upate kufanikiwa, wewe na watoto wako baada yako, na siku zako ziwe nyingi katika nchi ile akupayo Bwana, Mungu wako, milele,” Kum 4:40

Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate,” Mt 16:24

Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona,” Mt 16:25

Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake?” Mt 16:26

TAFAKARI: “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate.”

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna aliye kati yetu anayeishi kwa ajili yake mwenyewe. Ni kwa ukweli huu kwamba hakuna kati yetu na aliye hai leo katika ulimwengu huu, yupo kwa bahati mbaya. Kila mmoja wetu na kwa namna alivyo kadiri ya wito wake ni kusudi la Mungu. Mungu ana mpango wa pekee na maisha yako hapa duniani. Hivyo kuishi katika mpango huu wa Mungu yatupasa kufuata matakwa ya Mungu. Jambo hili si rahisi sana kulipokea na kulikubali kwa sababu kadiri ya ufahamu wetu kibinadamu, itatupasa kwenda kinyume na matakwa yetu na ufahamu wetu wa mambo na vitu.

 Ni kwa namna hii tunaona kwamba baada ya wana wa Israeli kukombolewa kutoka utumwana Misri inawapasa kuishi kadiri ya mpango wa Mungu ili wapate kufanikiwa, na siku zao ziwe nyingi katika inchi ile aliyowapa wairithi. Kuishi mpango wa Mungu ni pamoja na kuzishika sheria zake. Basi, zishike sheria zake, na amri zake, ninazokuamuru leo, upate kufanikiwa, wewe na watoto wako baada yako, na siku zako ziwe nyingi katika nchi ile akupayo Bwana, Mungu wako, milele,” Kum 4:40. Kuishi katika ukweli huu yatupasa kuwa watii na waaminifu kila siku ya maisha yetu. Kwa upande mwingine, mafanikio yetu katika maisha ni matokeo ya kuushinda ubinadamu wetu kila siku kwa neema zake Mungu.

Katika agano jipya la Mungu na watu wake, chini ya mwanaye mpenzi Yesu Kristo, ili kuurithi uzima huu wa milele, kila mmoja wetu yampasa kuishi njia hii ya uzima wa kweli kama Mwanaye Yesu Kristo anavyotuwasa katika injili ya leo: “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate,” Mt 16:24. Tunamfuata Yesu kwa sababu ‘Yeye ndiye njia, kweli na uzima,’ Yoh 14:6. Katika ufuasi wetu kwa Kristo, haya mambo matatu ni muhumu sana: KUJIKANA NAFSI, KUJITWIKA MSALABA, NA KUMFUATA YESU. Kujikana nafsi ni tendo la kujisalimisha na kuwa tayari kufanya kadiri ya mapenzi yake Mungu, na siyo tutakavyo sisi au tuonavyo. Ni tendo la kusalimisha utashi wako kwa Mungu, na kuwa tayari kutumika kadiri ya mpango wa Mungu. Unafanya tendo hili na kuwa sehemu ya maisha yako kwa kuyachuchumilia yale ya umilele ukilinganisha na haya ya leo na sasa tu. Ni kuishi ulimwenguni pasipo kubebwa na malimwengu.

Kujitwika msalaba ni kukubali kuwa hapana utukufu pasipo msalaba. Maisha tunayoyaishi kila mmoja kadiri ya wito wake, si maisha rahisi. Kuna wakati katika maisha hayo itakupasa kutoa sadaka kubwa ili kuufia umilele ule aliotuandalia Mungu. Hivyo kujitwika msalaba ni kupokea mateso pasipo shaka yoyote na bila manung’uniko. Mambo hayo yanaweza kuwa magonjwa, ulemavu, mahangaiko katika maagano yetu, mfano: ndoa, maisha ya wakfu, aka. Ni kuona utukufu wa Mungu katika mateso na mahangaiko yetu ya kila siku tunapokabiliana nayo. Msalaba huo katika maisha utusukume kuubeba kila siku na kusafiri nao hadi golgota alipowambwa Bwana wetu Yesu Kristo. Ni kuyapokea mateso yote na kuyabeba mpaka mwisho bila kumwasi Mungu na mwanaye Yesu Kristo. Tukifanya hivi pasipo shaka yoyote ndipo tutakapo hesabiwa haki na kuushinda mateso hayo. Mateso hubadilika kuwa ushindi, na msalaba huwa kielelezo cha ushindi huo. Hapa ndipo tunapoweza kuiokoa nafsi yetu katika majaribu. Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona,” Mt 16:25. Je, upo tayari kuipoteza nafsi yako katika umilele wote?

Kumfuata Yesu ni mwito na matokeo ya kujikana nafsi, na kujitwika msalaba pasipo shaka. Kumfuata Yesu ni kusafiri naye pasipo shaka tukijua na kuamini kabisa kuwa ni yeye tu njia ya umelele, ukweli wa umilele, na uzima wa umilele. Ni kufahamu pasipo shaka na kuamini maneno haya aliyosema Yesu: Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:28-30. Hivyo kitulizo cha mahangaiko na mateso yetu ni YESU TU. Tunapojikana nafsi na kujitwika msalaba wetu bila kufuatana na Yesu alioshinda mateso na maumivu ya msalaba ni bure na kupoteza muda. Katika mahangaiko yote tuyapitiayo kamwe tusimwache Yesu.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU NI KWAKO TU TUNAPOPATA FURAHA YA KWELI. TUJALIE FURAHA HIYO DAIMA. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario